Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 6/15 kur. 273-280
  • Kujihakikisha Tunastahili Kuingia Katika Taratibu Mpya ya Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujihakikisha Tunastahili Kuingia Katika Taratibu Mpya ya Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • LAZIMA YA KALE IONDOKEE MPYA
  • MWISHO WA TARATIBU YA KALE WATAZAMIWA KWANZA
  • MAELEKEO YA KIMUNGU KWENYE SIKU YA HUKUMU HAYAKAWII
  • Mfano wa Unabii Uliofananisha Wokovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Je! Wewe Walaani Vikali Ulimwengu Kupitia Imani Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Ulimwengu Ulioharibiwa
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Ukombozi Wakaribia kwa Ajili ya Watu wa Ujitoaji Kimungu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 6/15 kur. 273-280

Kujihakikisha Tunastahili Kuingia Katika Taratibu Mpya ya Mungu

“Kwa kuwa mnayatazamia mambo haya, fanyeni yote mwezayo ili mwishowe mwonekane naye bila doa na bila waa na katika amani.”​—2 Pet. 3:14, NW.

1. Kutotosheka na taratibu ya kale hakuwezi kuifanyia nini, lakini Mungu aweza kufanya nini?

DUNIANI pote watu hawatosheki na taratibu ya kale ya mambo. Watu wengi wenye kutaka mapinduzi wanateta wakiipinga. Wengi wao wanataka kuiharibu. Lakini, wanajikuta bila kitu cha kufaa kukiweka badala yake. Hawawezi kutengeneza kitu kipya kilicho bora cha kuwako badala yake. Wakiiharibu taratibu ya kale iliyosimamishwa, hawataweza kuleta nyingine mpya. Linalofurahisha ni kwamba, kuna mtu aliye juu zaidi ya mwanadamu asiyetosheka pia na taratibu ya kale iliyo duniani. Yeye aweza kuiharibu kabisa taratibu ya kale, na pia kuweka mahali pake taratibu mpya kabisa kwa ajili ya wanadamu. Yeye ndiye Mungu Mwenye Nguvu Zote, Muumba mbingu na dunia.

2. Huyu Mungu Mwenye Nguvu Zote ameahidi kuifanyia nini, nasi twaona ahadi yake imeandikwa wapi?

2 Mungu uyu huyu ameahidi kwamba taratibu ya kale yenye uonezi na yenye kufisha itaondolewa duniani kisha taratibu mpya ya haki yenye kutoa uzima isimamishwe itakayotosheleza mahitaji na matakwa yanayofaa ya wanadamu wote. Twaona ahadi ya kimungu juu ya badiliko hilo zuri sana imeandikwa katika Kitabu ambacho kiliandikwa na Mungu, Biblia Takatifu. Mwandikaji mmoja wa Biblia wa karne ya kwanza aliitaja ahadi hiyo nzuri sana alipoandika hivi: “Lakini kuna mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizi haki itakaa.”​—2 Pet. 3:13, NW.

3, 4. (a) Ni ulizo gani linalotokea juu ya ahadi hiyo ya kimungu? (b) Wanadamu wataonaje watakapotimiziwa yaliyoandikwa katika Ufunuo 21:3-5?

3 Wasomaji wa karne ya kwanza wa maneno hayo hakika ya mtume Petro wa Kikristo walikuwa kweli wakingojea kwa shauku “mbingu mpya na dunia mpya” zilizoahidiwa na Mungu asiyesema uongo. Ahadi yake yaendelea kuwa kweli hata leo! Kwa hiyo, ulizo ndilo hili, Je! sisi pia twaiamini ahadi hiyo? Ikiwa twajidai kuiamini, je! sisi pia tunayangojea mambo hayo ‘mapya’ yenye haki? Inatupasa kuwa tukifanya hivyo, kwa kumpa sifa Mungu ambaye ahadi yake haikosi kutimia kamwe. (Yos. 21:45; 23:14; Tito 1:2) Kwa kweli, imetupasa kufurahi sana, kwa sababu “mbingu mpya na dunia mpya” hizo zimetukaribia sana! Kwa hakika tunazihitaji sasa kuliko wakati mwingine wo wote uliotangulia! Vitu vipya hivyo vinafananisha taratibu mpya ya Mungu yenye haki. Itakuwa “mpya” kweli kweli. Mpaka sasa wanadamu hawajapata kuona kitu kama hicho. Bila shaka wanadamu watashangaa kuona jambo wasilopata kuliona wakati maneno yaliyo mwishoni mwa Biblia yatakapotimizwa:

4 “Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita. Na yeye aketiye juu ya kile kiti cha enzi akasema, Tazama, nayafanya yote kuwa mapya. Akaniambia, Andika ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.”​—⁠Ufu. 21:3-5.

5. Ahadi za wanasiasa huwaje tofauti na ahadi za Mungu?

5 Wanadamu wameona kwa njia yenye huzuni kwamba ahadi za kujitakia makuu za wanasiasa wenye kugombea uchaguzi ni za upuzi, ni maneno matupu, ni za kutiwa chumvi, hazitimizwi wala hazistahili kuaminiwa wala kutumainiwa. Tofauti kabisa na ahadi hizo, ahadi za Muumba wa “mbingu mpya na dunia mpya” zitakuwa “amini na kweli.” Tunaweza kungojea mambo aliyoahidi bila ya kuwa na matumaini ya bure.

LAZIMA YA KALE IONDOKEE MPYA

6, 7. Watu wengine huaminije kwa njia ya dini ya taratibu ya kale, nao hawajui Kitabu kipi pamoja na Mwandishi wacho?

6 Kwa maelfu ya miaka sasa taratibu ya kale ya mambo imekuwa ikitawala dunia. Huo umekuwa wakati mrefu kufanya watu waichukie na kuchoshwa nayo. Mamilioni yasiyohesabika ya wanadamu yanaamini kwa njia ya dini kwamba mwanadamu aliandikiwa awe na taratibu hiyo ya kale, na kwamba haiwezi kubadilika. Wanajiachilia waongozwe nayo bila ya kujua la kufanya. Wanadini hao hawaijui Biblia Takatifu. Hawamjui Mwandishi wa kimungu wa Biblia. Linaloshangaza ni kwamba wengi hata hawalijui jina lake. Wanayajua majina ya kipekee ya miungu isiyo ya Kibiblia ambayo wamefundishwa kuiabudu, lakini jina la kipekee la Mungu wa Biblia hawalijui. Hata hivyo, jina Lake limo katika Kitabu hicho. Ili walione, wamepaswa kuchukua tu tafsiri ya Kiswahili inayojulikana sana ya Biblia Takatifu, Union Version, na kufungua Kutoka (kitabu cha pili cha Biblia), sura ya sita, mistari ya pili na tatu. Humo watasoma hivi:

7 “Kisha Mungu akasema na Musa, akamwambia, Mimi ni YEHOVA; nami nilimtokea Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo, kama Mungu Mwenyezi, bali kwa jina langu YEHOVA sikujulikana kwao.”

8, 9. Jina la ‘aliye juu, juu ya nchi yote’ ni nani, na ni kwa njia gani na kwa sababu gani tunaweza kulitumia jina lake la kipekee?

8 Ikiwa hawatosheki na mfano mmoja huu wa jina la kimungu katika nakala yao wenyewe ya Biblia, wanaweza kufungua Zaburi 83, mstari wa kumi na nane, na humo watasoma hivi: “Wajue ya kuwa Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” Wanaweza pia kufungua Isaya 12:2 na 26:4.

9 Kwa hiyo jina la kipekee la Yeye ambaye ni Mungu ‘aliye juu, juu ya nchi yote’ ni Yehova. Katika Maandiko ya Kiebrania ya asili, ambayo kwa kawaida huitwa Agano la Kale,. jina hilo la kipekee la kimungu huonekana karibu mara elfu saba nalo huendelezwa kwa herufi bubu (konsonanti) nne za Kiebrania. Kwa kuwa jina la Mungu mwenyewe la kipekee hutumiwa mara nyingi sana katika maandishi ya Biblia, sisi leo twaruhusiwa kulitumia jina hilo kwa heshima tu, si kulitaja bure. Hivyo tunaweza kuonyesha Mungu tunayemaanisha, Mungu wa Biblia. Jina lake la kipekee ni tofauti na lile la Mwanawe mpendwa, Yesu, ambalo humaanisha “Yehova Ni Wokovu.”

10. (a) Ahadi ya Mungu ya mbingu mpya na dunia mpya ilimaanisha nini kwa taratibu ya kale ya mambo? (b) Ingawa Petro hakuruhusiwa aishi mpaka kuja kwa vitu ‘vipya’ vilivyoahidiwa, aliwatia moyo wasomaji wake wafanye nini?

10 Baba wa kimbinguni, Yehova, Ndiye ameahidi kuleta Taratibu Mpya, yenye “mbingu mpya na dunia mpya.” Alipokwisha tu kutaja mbingu mpya na dunia mpya, hiyo ilimaanisha kwamba taratibu ya kale ya mambo, ambayo haikutoka kamwe kwa Yehova Mungu, ilihukumiwa kupita. Je! si habari njema hizo? (Linganisha Waebrania 8:13.) Tangu kutolewa kwa ahadi hiyo ya kimungu, watu wenye imani ya kweli katika Mtoaji wa ahadi hiyo wamemtazamia kwa shauku ailete taratibu mpya hiyo. Mtume Petro na makundi ya Wakristo alioandikia barua yake walikuwa kati ya wasioona mambo ya sasa peke yake bali wenye kungojea kwa matumaini kusimamishwa kwa “mbingu” mpya ambazo ni serikali yenye haki na “dunia” mpya ambayo ni jamii ya watu wenye haki. Petro mwenyewe hakutazamia kuishi mpaka siku hiyo yenye baraka duniani itakapotokea, kwa sababu ya aliyokuwa ameambiwa na Bwana wake, Yesu Kristo. (Yohana 21:18, 19; 2 Pet. 1:13-15) Lakini aliwatia moyo wasomaji wake wangojee kuingia katika taratibu mpya yenye haki. Maneno yenye kutia moyo ya Petro yaliyoongozwa na Mungu yanatuhusu sisi sasa, karne kumi na tisa baadaye.

MWISHO WA TARATIBU YA KALE WATAZAMIWA KWANZA

11. Lazima nini kiondolewe duniani kwanza, na ilionyeshwaje kwamba si kazi ngumu mno kwa Muumba kufanya hivyo?

11 Hata hivyo, lazima kwanza tutazamie mwisho wa taratibu ya kale isiyomcha Mungu. Taratibu mbovu ya kale imejiimarisha duniani tangu muda mfupi baada ya gharika ya ulimwenguni pote iliyogharikisha dunia siku za nabii Nuhu, zaidi ya miaka 4,300 iliyopita. Kwa hiyo haikusudii kuondoka vyepesi, bila kujipigania. Kupigana na nani? Bila shaka na Mwanzishaji wa Taratibu Mpya, Muumba wa “mbingu mpya na dunia mpya.” Lakini si kazi ngumu mno kwa Mungu Mwenye Nguvu Zote kuing’oa taratibu ya kale. Siku za Nuhu Mungu huyu aliuonyesha uwezo wake wa kuharibu ulimwengu mzima kwa pigo moja, ‘kazi moja ya Mungu’ ambayo haikujitokea tu. Muda mrefu mapema, siku ya pili ya juma Yake ya uumbaji, aligawanya maji hata maji yaliyo mengi yakaning’inia katika anga la dunia yote, kukiwa na eneo la hewa katikati. (Mwa. 1:6-8) Katika wakati aliouweka Yeye aliyaangusha duniani maji hayo yenye kuning’inia. Kukawa na gharika ya dunia yote iliyoua wanadamu wote duniani isipokuwa nafsi zile nane za kibinadamu zilizokuwamo katika safina ya Nuhu.​—1 Pet. 3:20.

12. Ni kwa kipindi kisichopungua muda gani Mungu alijizuia asilete gharika, nayo gharika iliharibu nini?

12 Gharika hiyo ya dunia yote ilikuwa adhabu kutoka, kwa Yehova Mungu. Alikuwa amejizuia kwa saburi asitoe adhabu hiyo kwa miaka isiyopungua 120. (Mwa. 6:1-3) Hasa mtume Petro alionyesha vile Mungu alivyojizuia, alipoandika hivi: “Hakuuachilia ulimwengu wa kale, bali alimhifadhi Nuhu, mjumbe wa haki, na watu wengine saba, hapo alipoleta Gharika juu ya ulimwengu wa wasiomcha Mungu.” Mtume Petro atia mkazo tena kwamba huo ulikuwa uharibifu wa ulimwengu anapoendelea kusema hivi: “Kwa hayo dunia [ulimwengu, NW] ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.”​—2 Pet. 2:5; 3:6.

13. ‘Ulimwengu wa kale’ na ulimwengu wa sasa, au jamii ya kibinadamu, zinalinganaje ustahimilivu wa Mungu unapofikiriwa?

13 Hivyo ‘ulimwengu wa kale,’ jamii ya kwanza ya wanadamu, iliendelea kuwako kwa karibu miaka 1,656 baada ya kuumbwa kwa mwanadamu. Lakini Mungu ameusubiri ‘ulimwengu’ wa sasa, au jamii ya kibinadamu, kwa muda mrefu zaidi, kwa karibu karne 42 au tangu ilipofanywa “kazi ya Mungu” ya kuvuruga lugha ya wajenzi wa mnara wa Babeli. (Mwa. 10:8-10; 11:1-9) ‘Ulimwengu wa kale’ wa siku za Nuhu uligharikishwa kwa sababu ulikuwa ‘haumchi Mungu.’ Ulikuwa umejaza dunia jeuri. Ulikuwa ukiharibu dunia wala haukuwa ukiiletea uzuri wa kiparadiso. ‘Maovu ya mwanadamu yalikuwa makubwa duniani.’ (Mwa. 6:5-9, 12, 13) Yalistahili kuharibiwa.

14. Kwa sababu gani Nuhu na jamaa yake walihesabiwa kuwa wanastahili kuiokoka gharika?

14 Kwa sababu gani basi Nuhu na jamaa yake walihesabiwa kuwa wanastahili kuokolewa wapite gharika na kuingia katika kipindi kilichofuata? Ni kwa sababu Nuhu aliongoza jamaa yake ‘wakatembea pamoja na Mungu wa kweli,’ si na ulimwengu usiomcha Mungu. Mungu alimwona Nuhu kuwa mwenye haki, “mkamilifu katika vizazi vyake.” Alikuwa ‘mhubiri wa haki.’ Alikuwa na imani nyingi katika Mungu. Ndiyo sababu aliijenga safina ya kuhifadhia jamaa yake kwa utii.​—⁠Mwa. 6:9 mpaka 7:1; Ebr. 11:7.

15, 16. (a) Ni somo gani tunalopaswa Kujifunza hapa leo? (b) Yesu alitabirije mwisho wa ulimwengu mzima?

15 Na tusikose kuliona somo linaloonyeshwa hapa: Kwamba inawezekana kwa Yehova Mungu kuleta mwisho wa ulimwengu mzima wa jamii mbaya ya kibinadamu na, zaidi ya hilo, kuhifadhi wanadamu mmoja mmoja wenye kukubaliwa waokoke mwisho kama huo wa ulimwengu. (2 Pet. 2:9, 10) Vivyo hivyo huko mbele yetu kutakuwa na mwisho wa ulimwengu mzima. Mwana wa Mungu mwenyewe, Yesu Kristo mwenyewe aliutabiri, akisema:

16 “Na kama ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo itakavyokuwa katika siku zake Mwana wa Adamu. Walikuwa wakila na kunywa, walikuwa wakioa na kuolewa, hata siku ile Nuhu aliyoingia katika safina, gharika ikashuka ikawaangamiza wote. . . . Hivyo ndivyo itakavyokuwa siku ile atakayofunuliwa Mwana wa Adamu.”​—⁠Luka 17:26-30; Mt. 24:37-39.

17, 18. Kwa sababu gani ‘ulimwengu wa kale’ haukutii onyo la Mungu alilotoa kupitia kwa Nuhu, na hukumu ya kimungu ilifunuliwa lini?

17 Huko nyuma mwaka wa 2370 K.W.K., watu wasiomcha Mungu hawakuuamini ushuhuda waliouona kwamba mwisho wa ‘ulimwengu wao wa kale’ ulikuwa umekaribia sana. Wao walidhani mwisho huo haukuelekea kuja, ulikuwa hauwezekani kutokea! Waliona kwamba mtu yule Nuhu alikuwa akiwaonya juu ya msiba wa asili uliokuwa mkubwa mno kwao kutoweza kuamini. Kwa hiyo sababu gani wawe na wasiwasi?

18 Mpaka wakati huo maisha yalikuwa yameendelea kuwa ya kawaida tu kwao, wakila, kunywa, kuoa na kuolewa ili wazae kizazi kitakachofuata. Hawakufikiri kwamba kutakuwa na siku yo yote ya kutoa hesabu mbele za Mungu kwa ubaya wao wote, kwa jeuri waliyokuwa wakiijaza dunia, na jinsi walivyokuwa wakiiharibu dunia, na njia yao ya choyo duniani. Hata Nuhu alipomaliza kujenga safina na kuingiza humo aina za msingi za ndege na wanyama hiyo haikuwafanya waone uzito wa onyo la Nuhu kwao. Walikosa imani. Kwa hiyo walikuwa wenye laana machoni pa Mungu, wakiwa tofauti na Nuhu mwenye imani yenye kutegemezwa na matendo. Mwishowe, siku ya kumi na saba ya mwezi mfupi wa pili (inaelekea kuwa ni mwezi wa Bul, unaomaanisha “Mvua”) wa mwaka wa 2370 K.W.K. ilifika. Ndipo hukumu ya uharibifu iliyoletwa na Mungu wa Nuhu ilipofunuliwa kwa ‘ulimwengu huo wa watu wasiomcha Mungu.’​—⁠Mwa. 7:11-17; 2 Pet. 2:5.

19. Ikiwa tunataka kuokoka mwisho wa ulimwengu kama Nuhu, ni nini zaidi yanayotakiwa kuliko kutaka tu kuepuka kuharibiwa pamoja na taratibu hii ya mambo?

19 Je! sisi leo tunataka kuwa kama Nuhu na jamaa yake kwa kuuokoka mwisho wa ulimwengu na kuingia katika taratibu mpya yenye haki, tukafurahie “mbingu mpya na dunia mpya”? Ili tuhesabiwe kuwa tunastahili kupata pendeleo hilo, kutaka tu kuuokoka uharibifu utakaoipata ‘taratibu mbovu iliyopo sasa’ hakutoshi. (Gal. 1:4) Lazima tufuate mfano wa jamaa ya Nuhu, ‘mhubiri wa haki,’ tufanye kama walivyokuwa wakifanya siku zao kabla ya gharika ya dunia yote. Ilimpasa Nuhu kufanya matendo ya imani zaidi ya kuhubiri haki na kutangaza onyo la uharibifu wa ulimwengu. Je! nasi pia hatutazamiwi kufanya hivyo, sisi ambao sasa twajikuta katika “mwisho wa taratibu ya mambo,” kulingana na masimulizi ya. unabii ya Yesu juu ya kipindi chenye kujawa na matukio ambamo tumepitia tangu mwaka wa 1914 W.K.? Sivyo! Sivyo kwa maana lazima kilichofananishwa na mfano wa kale wa siku za Nuhu kitukie.​—⁠Mt. 24:3-39.

20. Anapotukumbusha tunalopaswa kufanya, Petro anatumia hoja gani juu ya uwezo wa Mungu wa kushughulika na watu wenye haki na wasio haki?

20 Tunalopaswa kufanya ni jambo lile lile ambalo mtume Petro akumbusha wasomaji wa barua yake ya pili aliyoandikia waamini Wakristo. Akitoa hoja (au sababu) juu ya kufikiliza kwa Mungu hukumu juu ya malaika na wanadamu waovu, Petro aandika hivi: “Hakuuachilia ulimwengu wa kale, bali alimhifadhi Nuhu, mjumbe wa haki, na watu wengine saba, hapo alipoleta Gharika juu ya ulimwengu wa wasiomcha Mungu; . . . basi, Bwana ajua kuwaokoa watauwa na majaribu, na kuwaweka wasio haki katika hali ya adhabu hata siku ya hukumu; na hasa wale waufuatao mwili katika tamaa ya mambo machafu, na kudharau mamlaka [“Mamlaka za kimbinguni,” Moffatt].”​—2 Pet. 2:5-10.

MAELEKEO YA KIMUNGU KWENYE SIKU YA HUKUMU HAYAKAWII

21. Kwa sababu gani kizazi hiki kinadhani kwamba uharibifu wake unakawia na kwamba Mungu ni mkawivu wa kufikiliza hukumu?

21 Karibu na mwisho wa miaka mia mbili baada ya gharika ya siku za Nuhu, wazao wa Nuhu kwa ujumla walianza kusahau kwamba Mungu alifikiliza hukumu ulimwenguni pote juu ya watu wasiomcha Yeye. Ndipo walipokuza jamii ya kibinadamii hiyo ya kibinadamu yenye kumdharau Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote. Mji mbaya wenye kujulikana sana ulioitwa Babeli (au, Babiloni) ukawa mfano wa jamii hiyo kibinadamu yenye kumdharau Mungu. (Mwa. 10:8-10) Hiyo ilikuwa maelfu ya miaka yaliyopita. Kwa hiyo ulimwengu huu wa wanadamu unaompuza Mwamuzi Mkuu Zaidi ya wote, aliyeleta gharika juu ya ‘ulimwengu wa kale,’ umeruhusiwa kuwako muda mrefu sasa. Ni muda mrefu hata unapopimwa kutoka kuanzishwa kwa Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) siku za Mfalme Konstantino Mkuu, katika karne ya nne ya Wakati wetu wa Kawaida. Tena, katika kizazi chetu wenyewe, miaka 62 imekwisha pita tayari tangu kuanza kwa “wakati wa mwisho” mwaka wa 1914 W.K. (Dan. 12:1-4) Kwa hiyo, wanadini wanafiki wa Jumuiya ya Wakristo huenda wakaelekea kudhani kwamba hukumu ya Mungu inakawia kufikilizwa na kwamba kuharibiwa kwao kunakawia. Wanafikiri kwamba, ijapokuwa wao wana unafiki wa kidini juu ya Mungu wa Biblia, yeye hatarudia kazi yake ya kuharibu ulimwengu mzima wa wanadamu waasi.

22. Ni kulingana na mifano gani ya zamani ya kushughulika na watu Mungu hataachilia ulimwengu wa sasa wa wanadamu?

22 Leo, ni hekima kwetu kuyathamini maneno yaliyoongozwa na Mungu ya mtume Petro: “Hukumu yao tangu zamani haikawii, wala uvunjifu wao hausinzii.” (2 Pet. 2:3) Kulingana na ushuhuda wote unaoonekana kulingana na Maandiko yaliyoongozwa na Mungu, wakati umepita sana. Ustahimilivu wa Mungu unakaribia upeo wake. Kama vile hasa asivyoachilia malaika waliokosa kutii miaka iliyotangulia gharika, na kama vile hasa asivyouachilia ulimwengu wa wanadamu wasiomcha Mungu wenye kufuatia na kuamini vitu vya kimwili tu siku za Nuhu, na kama vile hasa asivyoiachilia miji yenye ufisadi ya Sodoma na Gomora siku za Ibrahimu na mpwa wake Lutu, vivyo hivyo ndivyo Mungu huyu mwenye kanuni zisizobadilika hataachilia ulimwengu wa sasa wa watu wasio na imani, wenye kufikiria yao tu.

23, 24. (a) Kwa sababu gani haitupasi kukata maneno kwamba Mungu hana wakati alioweka usiobadilika wa kufanya hivyo? (b) Ustahimilivu wa Mungu siku za Nuhu uliwezesha nini?

23 Sababu tu ulimwengu huu haukuambiwa katika Biblia siku na saa yenyewe hasa ya “Mhukumu ulimwengu wote” kufikiliza hukumu yake ya uharibifu juu ya taratibu hii ya mambo, haionyeshi Yeye hakuweka wakati usiobadilika wa kufanya hivyo.​—⁠Mwa. 18:25.

24 Hiyo haionyeshi hukumu inakawia, kama katika baraza za sheria za kisasa. Haionyeshi kwamba Mungu anasinzia-sinzia akiwa amekalia kiti chake cha hukumu wala hakulala fofofo, kwa habari ya kuleta uharibifu juu ya “taratibu mbovu ya mambo iliyopo sasa.” (Gal. 1:4, NW) Wakati wake alioweka haujafika mpaka sasa kwa sababu Yeye amekuwa mstahimilivu, “si mwepesi wa hasira.” (Kut. 34:6) sote leo twaweza kuwa wenye furaha kwa sababu ya Mungu kuhesabu hivyo wakati wa kutukia kwa mambo! Kwa sababu gani? Kwa sababu nzuri ya kwamba hiyo inafanya iwezekane tuokoke. Ni kama katika siku za Nuhu, wakati Nuhu na mkewe walipopata nafasi ya kuzaa wana watatu waliokua kisha wakaoa wasichana watatu halafu wote wanane wakaungana kujenga safina na kuingiza humo viumbe vingine vipate kuokoka, kwa sababu Mungu aliruhusu ipite miaka 120 kabla gharika haijatokea.​—⁠Mwa. 6:3 mpaka 7:10; Zab. 103:8.

25. Watu wa taratibu ya kale na wale wanaotaka taratibu mpya ya Mungu wanatumiaje ustahimilivu wake?

25 Ulimwengu usiomcha Mungu wa leo unatumia nafasi ya ustahimilivu wa Mungu kufurahia anasa za kichoyo katika taratibu hii potovu ya kale. Wale wanaotamani sana taratibu mpya ya Mungu yenye haki wanatumia ‘kutokuwa kwake mwepesi wa hasira’ kwa kutubia matendo yao yenye kufisha na kuhakikisha wanastahili kuokoka waingie katika taratibu mpya Yake. Wanafuata maoni anayoonyesha mtume Petro anaposema hivi: “Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.”​—2 Pet. 3:9.

26, 27. (a) Toba inayotajwa hapa inahusu nini? (b) Yesu alionyeshaje kwamba hii ndiyo aina ya toba aliyokuwa akimaanisha?

26 Je! sisi tumefikia toba? Tunapouliza hivyo, hatumaanishi kutubu kule kwa kawaida kama kule kunakohusu ubaya uliotendwa, kama wakati Yesu alipotaja mtu mwenye kukosea-kosea mwingine, akisema: “Kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe.” (Luka 17:4) Bali, toba inayotajwa katika 2 Petro 3:9 inahusu mwendo wa mtu wa kutenda juu ya ufalme wa Mungu, serikali ambamo Yesu Kristo amepewa mgawo wa kuwa Mfalme juu ya wanadamu wote.

27 Toba hiyo inayohusu ufalme wa Mungu wa kimbinguni wa Kimasihi ndiyo aliyokuwa akimaanisha Yesu, kulingana na yaliyoandikwa katika Mathayo 4:17, ambapo twasoma hivi: “Tokea wakati huo Yesu alianza kuhubiri, na kusema, Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Tazama pia Marko 1:14, 15; Mathayo 3:1, 2.) Kupatana na maandishi hayo Yesu Kristo aliwatuma mitume wake kumi na wawili, wawili wawili, wakahubiri kama yeye mwenyewe kwamba, “Ufalme wa mbinguni umekaribia.” Kwa hiyo, “wakatoka, wakahubiri kwamba watu watubu.”​—⁠Mt. 10:1-15; Marko 6:7-12.

28. Petro na Paulo walionyeshaje lilikuwa jambo la haraka kutubu kuhusu ufalme wa Mungu wa Kimasihi?

28 Huko nyuma lilikuwa jambo la haraka kwa Wayahudi kutubu kuhusu ufalme wa Kimasihi. Kwa hiyo, Yesu aliwaambia hivi: “Msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo.” (Luka 13:1-4) Siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., mtume Petro aliwaambia hivi maelfu ya Wayahudi wenye maulizo: “Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu.” (Matendo 2:1-38) Baadaye, Petro aliwapa Wayahudi mashauri kama hayo katika hekalu la Yerusalemu, kulingana na Matendo 3:19-23. Mtume Paulo pia alitia mkazo juu ya kutubu kuhusu ufalme wa Mungu wa Kimasihi. Kwa mfano, katika Athene, Ugiriki, baada ya ‘kuhubiri habari za Yesu na ufufuo,’ Paulo aliiambia hivi Baraza ya Areopago juu ya Mlima Mars: “Zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu. [Kwa sababu gani?] Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kumfufua katika wafu.”​—⁠Matendo 17:16-31. Tazama pia Matendo 26:20; Warumi 2:4.

29. (a) Kwa hiyo hatua yetu ya kwanza ya kujihakikisha tunastahili kuingia katika taratibu mpya ya Mungu ni nini? (b) Kulingana na aliyosema Petro, kutubu kunatosha?

29 Kwa hiyo, hakuna shaka juu ya jambo hilo: Hatua yetu ya kwanza ya kujihakikisha tunastahili kuingia katika taratibu mpya ya Mungu yenye haki ni kutubu kuhusu ufalme wa Mungu wa Kimasihi. Ni kupitia kwa mfalme aliyewekwa na Mungu awe wa serikali hiyo, Yesu Kristo, watu wanaotubu wanaweza kusamehewa na Mungu dhambi zao. (Matendo 2:38) Kupitia kwa ufalme huo wa Kimasihi Mungu atashuhudia enzi kuu yake ya ulimwengu wote, na wanadamu watapaswa kutubu juu ya kuwa kwao hapo kwanza chini ya enzi kuu ya Adui mkuu wa Mungu, Shetani Ibilisi. Je! sisi sote tumefikia toba hiyo kupatana na takwa la Mungu kwetu? Ikiwa twaweza kujibu Ndiyo, basi kulingana na aliyosema mtume Petro, imetupasa kufanya yaliyobaki ikiwa tunataka kupata kibali ya mwisho ya Mungu. Tunaweza kutumia kwa faida ustahimilivu wake wa mwisho anaoonyesha taratibu hii mbovu ya kale ya mambo. Hivyo tunaweza kuwa na hakika ya kupata kibali Yake ya mwisho. Kwa sababu hiyo tutapata wokovu.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 276]

Nuhu aliongoza jamaa yake katika ibada

Alikuwa ‘mhubiri wa haki’

Aliijenga safina kwa utii

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki