Aina ya Watu Wanaokubaliwa Kuingia Katika Taratibu Mpya ya Mungu
1. Ingawa tunaona mapema mwisho mbaya sana wa taratibu ya kale, kwa sababu gani hatuna haja ya kufadhaishwa na tumaini la kuja kwa hali zisizopendeza wakati huo?
WATU wanaoamini kabisa kwamba karibuni taratibu ya kale iliyopo leo itatoweka wamepaswa kuwa wakijitayarisha kuingia katika Taratibu Mpya ya Mungu. Wanaona mapema mwisho mbaya sana wa “mbingu” za sasa, ambazo ni serikali, na wa “dunia” ya sasa iliyo chini yazo, ambayo ni jamii ya watu. Tumaini hilo haliwaogofishi. Kutokana na Biblia Takatifu wanafahamu “mwisho” hasa una maana gani, wanafahamu jinsi utakavyokuja na wanafahamu kusudi lake. Wanataka sana na kutazamia kwa hakika “mbingu mpya na dunia mpya” zilizoahidiwa na Mungu. Hii inawafanya wasiwaze kabisa juu ya hali zisizopendeza duniani ambazo lazima zije pamoja na mwisho wa taratibu ya kale. Kwa kufaa sana wanamkumbuka Nuhu na jamaa yake. Wakati ‘ulimwengu wa kale’ wa “watu wasiomcha Mungu” ulipokuwa ukimalizwa kwa gharika, huenda hali za maisha ndani ya safina yenye kupakiwa wanyama na ndege zikawa hazikuwa za kupendeza sana kwa Nuhu na jamaa yake waliokaa humo kwa zaidi ya mwaka mzima wa miezi mifupi. Hata hivyo nafsi nane hizo za kibinadamu ziliokoka. Hivyo waliweza kuipa jamaa ya kibinadamu mwanzo mpya wenye haki.
2. (a) Kwa sababu gani sasa si mapema mno Kwetu kuanza kujitayarisha kwa ajili ya taratibu mpya ya Mungu? (b) Ni wakati tunapofanya mambo gani tusipopaswa kuogopa kufika kwa “siku” ya Yehova?
2 Taratibu mpya ya Mungu, inayofananishwa na “mbingu mpya na dunia mpya” ambamo haki itakaa, ni jambo linalostahili kungojewa mpaka wakati wa Mungu alioweka wa kuianza utakapofika. (2 Pet. 3:13, NW) Sasa si mapema mno kwetu waamini kuanza kujitayarisha kwa ajili ya taratibu hiyo, ili tuhesabiwe kustahili kuiingia kwa faida na furaha yetu ya milele. Mtume Petro atukumbusha uhitaji wa kuwa tayari, hasa kwa kuwa “siku ya Yehova” itakuja kama mwivi usiku, iharibu taratibu ya kale ya mambo. Petro asema hivi: “Kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, inawapasa ninyi kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na matendo ya utawa, mnapongojea na kukumbuka sana kukaribia kwa kuwapo kwa siku ya Yehova.” (2 Pet. 3:10-12, NW) Tukiogopa kufika kwa siku ya Yehova pamoja na mambo yote ya kuogofya yatakayokuja pamoja nayo, tutakuwa tukionyesha kwa njia hiyo hatuingojei wala kuikumbuka sana, bali tutakuwa tukionyesha tunataka kuiahirisha ije wakati ujao usiojulikana tutakapokuwa hatuko hai, wakati “kizazi hiki” kitakapokuwa kimepita. Ikiwa tunafanya “matendo matakatifu ya mwenendo na matendo ya utawa,” hatuna haja ya kuogopa kwamba itakuja katika wakati wetu.
3. Katika toba yetu kwa Mungu wa Taratibu Mpya tumefanya nini, nasi twataka nini tofauti na taratibu ya kale isiyo haki?
3 Je! sisi tu “watu wa namna” hiyo? Toba ya kweli kwa Mungu, ambaye ameiahidi taratibu mpya yenye haki, imepaswa kuwa imekwisha kutufanya watu wa namna hiyo, wenye matendo yanayostahili toba. Kwa kumtubia Mungu tumejiweka wakf kwake kupitia kwa Kristo tukaonyesha wakf huo kwa kubatizwa majini. Tumefanya hivyo kwa sababu twampenda sana Yehova Mungu na twaipenda haki ambayo Yeye asimamia. Tunataka kustahili kuingia katika taratibu Yake mpya ya mambo. Kwa sababu taratibu hiyo ya mambo iliyo tofauti italeta mwungano wa “mbingu mpya na dunia mpya,” sisi twaipenda haki itakayokaa katika mambo hayo mapya. Kwa moyo wote twataka tukubaliwe kuingia katika taratibu mpya hiyo iliyo safi. Hatufurahishwi wala kutoshelezwa na uovu wa taratibu ya mambo isiyo kamilifu, yenye upotovu na iliyohukumiwa maangamizi.
4. (a) Ni kwa njia gani ulimwengu utajaribu kutuondoa katika ‘matendo yetu matakatifu ya mwenendo na matendo ya utawa’? (b) Sisi tutakataa kukubaliana na ulimwengu hata chini ya hali gani zinazokuja?
4 Sisi tumejitoa sana tuwe wa Muumba wa “mbingu mpya” na “dunia mpya” hata twadharau hali ya kupendwa sana na kujulikana sana na “ulimwengu wa watu wasiomcha Mungu” na twatafuta kibali yake. Ulimwengu utajaribu kutuogofya tuyaache “matendo matakatifu ya mwenendo na matendo ya utawa” kwa kutufanyia mzaha au kututisha-tisha; njia hiyo isipofaulu, ulimwengu utajaribu kutunasa tutoke katika mwendo wetu wenye haki unaoulaumu ulimwengu wenyewe kuwa usiopatana na Mungu. Lakini kwa kuendelea kuelekeza nyuso zetu kwenye taratibu mpya ya Mungu ya maisha yenye haki hatujiachi tuvutwe na mambo yanayoweza kutolewa na taratibu ya mambo iliyohukumiwa maangamizi. Tunajikaza tukisonga mbele katika njia takatifu ambayo Mungu ametuonyesha. Hatuwezi kujiunga kamwe na Jumuiya ya Wakristo, ‘rafiki ya ulimwengu’ apendwaye sana. (Yak. 4:4) Tena wakati Ukristo wa jina tu, au Jumuiya ya Wakristo, utakapogeukiwa na wapenzi wake wa kisiasa na kuharibiwa pamoja na sehemu nyingine yote ya Babeli Mkuu wa kidini, sisi hatutafikiria kamwe kufanya mkataba wa kukubaliana na waharabu hao wa kisiasa wa dini ya uongo.
5. Ni nani peke yao watakaookoka “dhiki kubwa” inayokuja waingie katika taratibu mpya ya Mungu iliyo bora?
5 Twajua kwamba “dhiki kubwa” isiyo na kifani katika historia ya kibinadamu iko mbele tu ya Babeli Mkuu na waharabu wake wa kisiasa. (Mt. 24:3-22, 37-39) Dhiki hiyo ya dunia yote imekusudiwa kuwaharibu wao, si sisi, kwa maana itatoka kwa Mungu tunayeabudu. Itaziharibu “mbingu na dunia zilizopo sasa” za mfano, taratibu hii ya kale. (2 Pet. 3:7) Hata hivyo, itafuatana na jaribu lililo kubwa zaidi la imani yetu katika Mungu na uaminifu wetu kwake. Mashahidi wa Kikristo wa Yehova ambao watafaulu kulipita jaribu hilo ndio watakaookoka peke yao watokee wakiwa kama dhahabu iliyoondolewa uchafu kwa moto wapate kutumiwa na Mungu katika taratibu yake mpya iliyo bora.
6. Mwishoni mwa “dhiki kubwa,” bado Mungu atakuwa na nini duniani kama ukumbusho wa ushindi wake?
6 Mungu hataki wale wanaomjia kwa kutubu na kuwa wanafunzi waliobatizwa wa Yesu Kristo wapatwe na uharibifu wa milele katika “dhiki kubwa” ya “siku ile kuu” yake, ‘siku ya Yehova itishayo.’ (Ufu. 16:14; Yoeli 2:31) Yeye anakusudia kurudia kufanya alilofanya siku za Nuhu, yaani, kupitisha waabudu wake waaminifu waliojaribiwa katika mwisho wa “ulimwengu wa watu wasiomcha Mungu.” (2 Pet. 2:5, NW) Shambulio linalokuja lililotabiriwa zamani la “Gogu, wa nchi ya Magogu” ya mfano litashindwa kufutilia mbali waabudu wa Yehova waliokusanywa tena watoke duniani, nao washambuliaji watafadhaishwa, watasagwa na kushindwa kwa njia yenye aibu. (Eze. 38:1 mpaka 39:26) “Dhiki kubwa” yenye kuogofya itakapokuwa imekwisha kabisa, bado kutakuwa na waabudu wa Mungu Mwenye Nguvu Zote duniani watakaohifadhiwa wawe kama ukumbusho wa ushindi wake mtukufu!
7. Kulingana na aliyosema Petro, tunaweza kuwa sehemu ya ukumbusho wa ushindi wa Mungu ikitegemea kama Yeye atatukuta tukiwa katika hali gani mwishowe?
7 Lo! litakuwa pendeleo kubwa namna gani kwa ye yote kuwa sehemu ya ukumbusho huo ulio hai wa kushuhudia ushindi wa Yehova katika “siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” penye Har–Magedoni! (Ufu. 16:14, 16) Sisi tunaweza kupewa pendeleo hilo ikitegemea Mungu atatukuta tukiwa “watu wa namna gani” ‘siku hiyo ya Yehova’ itakayoubadili ulimwengu. Mtume Petro aeleza waziwazi takwa hilo la lazima kwa Wakristo wa kweli ambao wangependa kuuokoka mwisho wa taratibu ya kale iliyohukumiwa maangamizi, anaposema hivi: “Kwa hiyo, wapendwa, kwa kuwa mnayatazamia mambo haya, fanyeni yote mwezayo ili mwishowe mwonekane naye bila doa na bila waa na katika amani. Tena, ioneni saburi ya Bwana wetu kama wokovu, kama vile ndugu yetu mpendwa Paulo alivyowaandikia pia kulingana na hekima aliyopewa.” (2 Pet. 3:14, 15, NW) Basi, twawezaje kuonekana tukiwa na hali hiyo iliyokubaliwa?
“BILA DOA NA BILA WAA”
8, 9. (a) Ni wakati gani inakuwa aibu kwa mtu kuonekana na doa mwilini mwake? (b) Kulingana na Yakobo 1:26, 27, dini ya mtu inawezaje kuwa na doa?
8 Doa lenye kuonekana katika mwili wa mtu laweza kuharibu sura yake. Ikiwa mtu amelipata doa hilo akifanya kwa bidii kazi nzuri, doa hilo haliaibishi. Hata hivyo, mtu huyo angependa kulisafisha doa hilo lisilopendeza kabla hajajitokeza mbele ya kusanyiko la watu safi. Lakini, ikiwa mtu amelipata doa hilo akifanya kazi isiyo ya kuheshimika, doa lenyewe linamletea sifa mbaya. Ni aibu tena laonyesha mwenye kuonekana nalo hafai. Kwaweza kuwa na madoa ya aina hiyo ya pili juu ya dini ya mtu, namna ya ibada ya mtu. Je! dini yetu au namna ya ibada yetu ina madoa ya namna hiyo? Ikiwa inayo, basi haimpendezi wala haikubaliwi na Mungu. Kwa kuhakikisha hilo, twasoma hivi:
9 “Mtu akidhani ya kuwa anayo dini [au, akidhani ni mfuata dini], wala hauzuii ulimi wake kwa hatamu, hali akijidanganya moyo wake, dini yake mtu huyo haifai. Dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.”—Yak. 1:26, 27.
10. Kwa sababu gani dini ya Jumuiya ya Wakristo haiwezi kuonwa kamwe ‘kuwa safi na isiyo na taka’ mbele za Mungu?
10 Jumuiya ya Wakristo, pamoja na Ukristo inayojidai kuwa nao, imefunikwa na madoa ya ulimwengu. Kati ya dini zote, matendo yake ndiyo mabaya zaidi. Huenda ikajisifia kuangalia yatima na wajane katika nyumba za yatima na maskini, lakini hiyo haifichi uhakika wa kwamba imetokeza mamilioni ya yatima na wajane. Je! mtu auliza ni kwa njia gani imefanya hivyo? Jibu ni jepesi: Ni kwa kuendeleza mapigano na vita vitakatifu, kuviongeza na kuviunga mkono kwa kuvibariki, kutoa sala juu ya vita hivyo na kusaidia kwa vifaa vyake yenyewe vya vita. Inajulikana sana kuwa yenye sifa mbaya kwa kujiingiza katika siasa za kilimwengu na hata wanasiasa wengi wanaichukia. Haikuzuia ulimi wake kwa hatamu, bali imefundisha mafundisho ya uongo ya namna zote, ya Kibabeli, kwa kuyaficha ikisingizia ni ya Kikristo, nayo imesema mambo mabaya sana ya uongo juu ya Mungu wa kweli ikaletea jina lake takatifu suto la ajabu, tena imelaumu waabudu wake wa kweli kwa njia ya uongo. Basi, mvurugo wa namna zake za ibada wawezaje kuwa ‘safi na usio na taka’ mbele za Mungu? Hauwezi kamwe!
11. Wale wanaotaka kuzoea dini ‘iliyo safi na isiyo na taka’ wanakataa kujipanga upande wa nani, naye Mungu anatoa amri gani leo juu ya jambo hilo?
11 Watu wanaotaka kuonekana “bila doa” na Yehova Mungu siku yake ya kufikiliza hukumu ifikapo hawawezi kujipanga upande wa sehemu yenye kujidai kuwa ya Kikristo ya Babeli Mkuu ya kidini, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Ili watu wawe bila doa katika habari hii, imewapasa wafuate amri ya Mungu anayotoa leo: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake.” (Ufu. 18:4, 5) Kwa sababu ya unafiki wake wa kutumia jina la Mungu na la Kristo wake, Jumuiya ya Wakristo ndiye mshiriki mwenye lawama zaidi wa kahaba huyo wa mataifa yote, Babeli Mkuu. Ye yote kati yetu asiendelee kuwa na madoa na kushiriki dhambi zake mbele za Mungu!
12. Jumuiya ya Wakristo haijatubia uzinzi gani wa kiroho, nao washirika wake wa kilimwengu hawatubii nini?
12 Acheni tutambue kwamba Jumuiya ya Wakristo imehukumiwa maangamizi, pamoja na sehemu nyingine yote ya Babeli Mkuu. Imekataa kutubia mwendo wake wa kidini wa ufisadi na uzinzi, urafiki wake na ulimwengu huu. (Yak. 4:4) Iko kama ulimwengu mwingine wote usiomcha Mungu, hata baada ya Mashahidi wa Yehova wa Kikristo kutangaza waziwazi hukumu ya Mungu iliyo karibu kuipata. Kwa unabii, Ufunuo 9:20, 21 husema hivi juu ya watu hao wenye kushupazwa na dhambi: “Na wanadamu waliosalia, wasiouawa kwa mapigo hayo, hawakuzitubia zile kazi za mikono yao, hata wasiwasujudie mashetani, na sanamu za dhahabu na za fedha na za shaba na za mawe na za miti, zisizoweza kusikia wala kuenenda. Wala hawakuutubia uuaji wao, wala uchawi wao, wala uasherati wao, wala wivi wao.”—Tazama pia Ufunuo 18:9, 11.
13. Kulingana na 2 Petro 2:20-22, ni nani walio kama madoa kundini, na lazima madoa hayo yaondolewe kwa njia gani?
13 Washiriki wote wa kundi la kweli la Kikristo wanataka sana kuendelea kuliweka tengenezo bila doa katika namna ya ibada yake. Hatutaki kuwa na washirika wenye kuweka madoa katika tengenezo. Mtume Petro anasema juu ya aina hiyo ya watu wasiotakiwa katika kundi la Kikristo, akinena hivi: “Wao ni madoa na mawaa, wakijitia na kupendezwa bila kujizuia katika mafundisho yao ya udanganyifu huku wakifanya karamu pamoja nanyi.” (2 Pet. 2:13, NW) Wasipotubu kwa unyofu na kuondoka katika mafundisho ya udanganyifu, watu hao walio kama madoa wamepaswa kufukuzwa katika kundi ili kulinda wale wazoeao ibada ya kweli ya Mungu. Ama sivyo, wao ni suto kwa kundi, zaidi ya kuwa hatari kwa kondoo za Mungu.—2 Pet. 2:20-22.
14, 15. Yuda 22, 23 yasema lazima wenye mashaka wafanyiwe nini pamoja na wale walio na hatia ya tendo la uasherati?
14 Huenda matukio ya kushangaza ulimwenguni leo yakatia mashaka katika akili za wengine kundini. Huenda bado kukawa na wengine wenye kufanya tendo la uasherati, kwa sababu wamekuwa dhaifu au wazembe. Mwandikaji wa Biblia Yuda aeleza kundi jinsi ya kushughulika na washiriki hao, akisema hivi: “Wahurumieni wengine walio na shaka, na wengine waokoeni kwa kuwanyakua katika moto; na wengine wahurumieni kwa hofu, mkilichukia hata vazi lililotiwa uchafu [au, madoa] na mwili.”—Yuda 22, 23.
15 Hapo The New English Bible yasema hivi: “Wako wengine ambao huruma yenu kwa ajili yao lazima ichanganywe na woga; lichukieni vazi lenyewe lililochafuliwa na nyege.” The New American Bible yasema hivi: “Hata wale mnaohurumia jihadharini nao; chukieni sana vazi lao lenye madoa ya mwili.” An American Translation yasema hivi: “Nanyi tazameni wengine kwa huruma ikichanganywa na woga, mkikirihi hata mavazi ambayo yametiwa madoa na hali yenye tamaa nyingi za mwili.” Lazima kundi litii onyo hilo.
16. Kwa sababu gani lazima kundi liwe na busara linapohurumia mtenda dhambi mwenye kutubu ambaye amefanya tendo la uasherati?
16 Kundi haliwezi kuachilia uasherati ikiwa linataka kuonekana na Yehova bila doa siku yake ya kufikiliza hukumu. Linaweza kurehemu na kuhurumia washiriki wanaofanya tendo la ufisadi kwa sababu ya udhaifu wa mwili au maongozi mengine. Lakini lazima watoe ushuhuda wa toba ya kweli. Hata hivyo, lazima kundi liwaonyeshe rehema na kuwasamehe wenye kutubu kwa busara nyingi, sikuzote likijihadhari, kwa maana halitaki kudhoofika katika msimamo wake wa haki katikati ya kizazi cha watu wasiomcha Mungu ambacho kimedidimia katika ufisadi kama ule uliofanya Yehova alete hukumu za moto juu ya miji ya kale ya Sodoma na Gomora,—Yuda 7;2 Pet. 2:6-8, 1 Pet. 4:3, 4.
17. Kundi linapochunguza ushuhuda wa kuonyesha hatia ya uasherati kwa upande wa mshiriki wake, limepaswa kutendaje likiuona ushuhuda huo?
17 Lazima kundi liendelee kujawa na roho takatifu ya Mungu na kusitawisha matunda yake, na tunda mojawapo ni kujiweza kwa adili. (Efe. 5:18; Gal. 5:22, 23, NW) Kwa kupatana, lazima lijitenge mbali na uasherati wa namna zote. Halitachunguza vazi la ndani lenye ushuhuda wa madoa ya uchafu wa ngono wa mwenye vazi hilo huku likifurahi na likiwa na nyege kama za mtu huyo. Badala yake, litachukia, kukirihi, kutaka kutapika kwa sababu ya kitambaa chenye kuonyesha hatia ya kosa kinachopaswa kufuliwa uchafu wake wa ngono. Kwa njia hiyo litakuwa imara katika kupenda usafi. Kwa hiyo, haliwezi kutazama vitabu wala sinema wala televisheni zenye kuonyesha picha za umalaya ndiyo lichochee nyege zalo.—Linganisha Mambo ya Walawi 15:16, 17.
18. Imewapasa wazee au waangalizi wathamini maneno gani ya kutia moyo yaliyotolewa katika 1 Timotheo 6:11-14?
18 Lazima washiriki wa kundi wajihadhari pia wasiwe na doa kwa jinsi wanavyoshika amri ambazo Mungu amewapa wafuasi wa Kristo. Imewapasa wazee au waangalizi wanaomwiga mwangalizi Timotheo wa karne ya kwanza wathamini mambo ambayo mtume Paulo alimwandikia Timotheo juu ya mwenendo wa Kikristo, yaani: “Bali wewe, mtu wa Mungu, uyakimbie mambo hayo [matokeo yenye msiba ya kufuatia vitu vya kimwili]; ukafuate haki, utauwa, imani, upendo, saburi, upole. Piga vita vile vizuri vya imani; shika uzima ule wa milele ulioitiwa, ukaungama maungamo mazuri mbele ya mashahidi wengi. Nakuagiza mbele za Mungu anayevihifadhi hai vitu vyote, na mbele za Kristo Yesu, aliyeyaungama maungamo mazuri yale mbele ya Pontio Pilato, kwamba uilinde amri hii pasipo mawaa, pasipo lawama, hata kufunuliwa kwake Bwana wetu Yesu Kristo.”—1 Tim. 6:11-14.
19. Kwa hiyo, hatutaki kumbukumbu letu la utii na matendo yetu yaweje?
19 Imetupasa tutake kutii amri hiyo iliyopewa kwa Wakristo kwa njia ‘isiyo na mawaa wala lawama’ mbele za Yehova Mungu. Hatutaki kumbukumbu letu la utii liwe na madoa, liwe na alama nyeusi nyeusi za kuliharibu, wala hatutaki kuonekana wenye makosa mengi kwa jinsi tunavyofanya mambo. Imetupasa tufanye yote tuwezayo kuonyesha tamaa yetu ya unyofu ya kuwa watii nyakati zote. Imetupasa tujiangalie tutembee pamoja na Mungu wetu bila lawama, kama alivyofanya Nuhu mjenzi wa safina “wakati wa mwisho” wa taratibu ya mambo iliyotangulia Gharika.—Mwa. 6:3, 9.
JINSI GANI “BILA WAA”?
20. Pana tofauti gani kati ya waa na doa katika mwili wa mtu, nasi tusemeje juu ya Yesu Kristo katika habari hii?
20 Imetupasa tuonekane mwishowe na Yehova Mungu, si “bila doa” tu bali pia “bila waa” wakati “siku” Yake itakapofika. (2 Pet. 3:14, NW) Twajua kwamba waa hushika zaidi kuliko doa. Doa ni la juu-juu nalo laweza kufutwa au kusafishwa, lakini sivyo waa lilivyo. Waa ni kasoro, kitu chenye kuharibu ubora wa mwili wa kitu kingine. Waa huonyesha kwamba kitu fulani ni kibaya kwa ndani, kina kasoro. Yesu Kristo alikuwa mkamilifu kabisa kabisa, na kwa hiyo angeweza kujitoa awe dhabihu ya ukombozi kwa wanadamu, kama “mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa.”—1 Pet. 1:18,19; Ebr. 9:14.
21. Ni katika upande gani tunajaribu kuwa bila waa mbele za Mungu, kama tunavyotiwa moyo katika Wafilipi 2:14-16?
21 Bila shaka, sisi wazao wa Adamu mwenye dhambi hatuwezi kuwa na miili mikamilifu, isiyo na waa la aina yo yote. Lakini namna gani utu wetu na makusudi ya mioyo yetu? Kwa kufaa, tunajitahidi sana kujiweka ‘bila mawaa ya dunia,’ lakini pia tunajaribu kusitawisha utu kama wa Kristo tukiwa na mioyo safi. Tusiwe kamwe kamwe na kasoro katika unyofu wetu wa kumwiga Bwana Yesu Kristo. Hatutaki kuwa kama mnyama maskini aliyetolewa katika madhabahu ya Mungu apate kuwa dhabihu Yake kisha akakataliwa na kuhani wa hekalu kwa sababu ‘alikuwa na waa.’ Maneno ya mtume Paulo ya karne kumi na tisa zilizopita yanatuhusu sawa na yalivyohusu siku hizo: “Yatendeni mambo yote pasipo manung’uniko wala mashindano, mpate kuwa wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu, wasio na ila kati ya kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka; ambao kati ya hao mnaonekane kuwa kama mianga katika ulimwengu, mkishika [sana] neno la uzima.”—Flp. 2:14-16.
22, 23. Mungu ataendeleaje kuiangaza nuru inayotolewa na watoto wake duniani wasio na waa wala hatia, kujapokuwa na shambulio la majeshi ya giza?
22 Je! huo si mradi mzuri sana unaostahili tujaribu kufikia, yaani, kuwa “wana wa Mungu wasio na lawama [au, “waa,” NW]”? Tukiwa watoto Wake wa aina hiyo, yeye hatakuwa na la kuaibikia wala la kuonyesha chuki. Ataendelea kuiangaza nuru tunayoitoa tukiwa kama mianga.
23 Hatutazimishwa kamwe tusitoe nuru! Sisi tutakuwa kama yeye ambaye nyayo zake twafuata, Logos au Neno la Mungu. Imeandikwa hivi juu yake: “Ndani yake ndimo ulimokuwa uzima, nao ule uzima ulikuwa nuru ya watu. Nayo nuru yang’aa gizani, wala giza halikuiweza.” (Yohana 1:4, 5) Tunatazamia kwamba Jumuiya ya Wakristo, ambayo imesingizia Mungu na Kristo, itaharibiwa karibuni, na kwamba nuru ya ‘wana wa Mungu wasio na waa’ itaendelea kulipenya giza linaloongezeka duniani. Halafu, wakati majeshi ya “Gogu, wa nchi ya Magogu” ya mfano yasiyofuata dini yatakapojiondokea yote pamoja yakashambulie mianga hii ya kiroho, “kama wingu kuifunika nchi,” majeshi hayo ya giza yatashindwa kuimaliza nuru yao. (Eze. 38:16-19) Mungu hataacha kamwe watoto wake ‘wasio na lawama wala udanganyifu, watoweke duniani!
“NA KATIKA AMANI”
24. Wakati wa kufumuliwa kwa taratibu ya kale, Yehova hatafanya nini kwa watu wake walioratibishwa duniani, na kwa sababu gani?
24 Hivyo, wakati ukiwa umepita sana katika mambo ya kibinadamu, matukio ya ulimwengu yakiwa yamekwisha elekea sana katika mwendo wa uharibifu, huu sio wakati wetu wa kusahau yatakayotukia karibuni. Yaani, kufumuliwa, kuvunjwa-vunjwa, kwa “mbingu” za kale na “dunia” ya kale. Kwa hiyo tusiache kamwe kujiongoza kupatana na uhakika huo wenye kuogofya. Katika 2 Petro 3:11, The New English Bible yaeleza jambo hilo kwa maneno haya: “Kwa kuwa ulimwengu wote utavunjika hivyo, ebu wazieni imewapasa kuwa watu wa namna gani, imewapasa kuishi maisha za utawa na wakf namna gani!” Ikiwa mvunjo huo wa ulimwengu wote uko mbele, Yehova Mungu Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Ndiye atakayeuleta kupitia kwa Mwanawe wa kifalme, Yesu Kristo. Mbingu za kale za mfano na dunia ya kale zitafumuliwa kweli kweli, zitavunjwa-vunjwa kabisa. Lakini wakati wote wa kufumuliwa kwa moto kwa taratibu ya kale ya mambo, Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu hatafumua wala hatavunja ushikamano wa watu wake walioratibishwa duniani. Yeye atawakuta wakitenda “matendo matakatifu ya mwenendo na matendo ya utawa.” Ukaguzi wake utawaonyesha kuwa “bila doa na bila waa.”—2 Pet. 3:11, 14 NW.
25. “Kuwapo kwa siku ya Yehova” kutakapofika, kutakuwa na tofauti gani kati ya wale wanaopendelea taratibu mpya ya Mungu na wale wanaounga mkono taratibu ya kale?
25 Paradiso ya kiroho ambamo waabudu hawa waliokubaliwa wa Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu wamejikuta tangu mwaka wa 1919 W.K. itaendelea kuwako bila kuharibiwa wakati ufumuzi ulio mkubwa zaidi wa taratibu ya kale ya kilimwengu utakapotokea ukisababishwa na joto lenye kuwaka la hasira ya Mungu. Kwa waabudu wake waaminifu huo utakuwa kama wakati Nuhu na jamaa yake walipokuwa wamekwisha ingia katika safina iliyomalizwa kujengwa, yenye kufaa kuingia baharini na wakati Yehova Mungu alipokwisha kufungia waliokuwa salama ndani kwa kutumia mlango ule mmoja tu, awalinde na nguvu za asili alizofungulia ziumwagikie ‘ulimwengu wa kale’ wa watu wasiomcha Mungu. (Mwa. 7:16) Lakini damu ya ulimwengu wa wanadamu wasiotii itapatwa na baridi ya kushtuka watambuapo kwamba “kuwapo kwa siku ya Yehova” wasiyoiamini kumewafikilia! Wataliona umbo la taratibu yao ya kale likiumbuka, kama tufe la theluji linalotupwa katika tanuru lenye kuwaka kweli kweli. Umoja wa jamii ya kibinadamu utavunjika-vunjika, hata mkono wa kila mtu utakuwa juu ya ndugu yake. Looo! jinsi itakavyokuwa tofauti kwa wenye kuunga mkono wakati huo taratibu mpya yenye haki ya Yehova!
26. Itawapasa mawakili wa Taratibu Mpya wazuie mikazo ya kutaka wafanye nini, na kwa sababu gani upendo kama wa Kristo utawasaidia?
26 Sheria na utengemano zitakapokuwa zikiharibiwa ulimwenguni pote na wenye kuunga mkono taratibu ya kale, mawakili wa taratibu mpya ya Mungu watapaswa kuzuia mikazo ya kuwafanya walete machafuko. Itawapasa kuendelea kushikamana kama watu walioratibishwa na Mungu, wakiendeleza umoja wa kweli wa Kikristo. Hiyo itawataka wawe wenye amani wao kwa wao. Kwa kuonyeshwa yaliyoko mbele na Mungu mtume Petro ametuonya kwa upole kwamba, wakati siku ya Yehova ya kufikiliza hukumu yake itakapofika kwa ghafula kama mwivi, lazima sisi tusio na doa wala waa tuonekane tukiwa “katika amani” pia. Kwa maana kwa muda mrefu tumekuwa tukisitawisha upendo kama wa Kristo, ambao “ndio kifungo cha ukamilifu.” (Kol. 3:14) Lakini hata hivyo, kuna nguvu zaidi ya moja ya kufunganisha.
27. Ni aina gani nyingine za umoja zitakazowasaidia wakati wa ufumuzi wa “dhiki kubwa”?
27 Iko pia ile nguvu ambayo upendo ndilo tunda kubwa lake, na hiyo ndiyo roho takatifu ya Mungu. Kwa hiyo lazima tuwe na umoja wa roho. Tena, kuna umoja wa imani, umoja wa utendaji wa Kikristo wa kuhubiri na kufanya wanafunzi, na umoja pamoja na Mungu mmoja aliye hai na wa kweli Yehova kupitia kwa Mwanawe Yesu Kristo. Mambo hayo yenye nguvu huleta mapatano na amani ndani ya tengenezo la mashahidi wa Yehova wa Kikristo. Mambo hayo yenye kuleta amani yatawasaidia wakati wa “dhiki kubwa” inayokaribia itakayoyeyusha taratibu ya kale ya kilimwengu itoweke kabisa.
28. Ili amani iwe kifungo cha umoja, tuna mambo gani yenye kupatanisha yaliyoandikwa katika Waefeso 4:3-6?
28 Muda wote huo, “wakati wa mwisho” huu ulioanza mwaka wa 1914 W.K., mawakili waliojitoa wa taratibu mpya ya Yehova yenye haki wamekuwa wakijitahidi sana kufanya vile mtume Paulo anavyotutia moyo tufanye: “Kujitahidi kuuhifadhi umoja wa [roho] katika kifungo cha amani. Mwili mmoja, na [roho moja], kama na mlivyoitwa katika tumaini moja la wito wenu, Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja. Mungu mmoja, naye ni Baba wa wote, aliye juu ya yote na katika yote na ndani ya yote.”—Efe. 4:3-6.
29. Sisi tu umoja pia katika kungojea nini, na kwa hiyo imetupasa tuendelee kufanya jambo gani analotuagiza Petro?
29 Mwishowe, sisi tu umoja katika kungojea ufumuzi utakaotokea karibuni wa taratibu hii ya kale ya mambo inayoelekea kufa. Basi, tutaendelea kufanya nini mpaka “kuwapo kwa siku ya Yehova” kutakapofika kama mwivi? Mtume Petro atuagiza sisi tunaotaka kujihakikisha tunastahili kuingia katika taratibu mpya ya Mungu jambo la kufanya: “Fanyeni yote mwezayo ili mwishowe mwonekane naye bila doa na bila waa na katika amani.”—2 Pet. 3:10-14, NW.—Kutoka The Watchtower, Dec. 15, 1975.