Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 8/15 kur. 371-376
  • Rafiki ya Yehova au Rafiki ya Ulimwengu—Jambo Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Rafiki ya Yehova au Rafiki ya Ulimwengu—Jambo Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SI RAFIKI ZA ULIMWENGU
  • USEMI NA MWENENDO WETU
  • URAFIKI KATATI YA NDUGU
  • KUENDELEZA URAFIKI NA MUNGU
  • Jinsi Unavyoweza Kupata Marafiki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Unaweza Kuwa Rafiki ya Yehova
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Wataka Rafiki za Namna Gani?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Lazima Waokokaji Wawe “Si Sehemu ya Ulimwengu”
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 8/15 kur. 371-376

Rafiki ya Yehova au Rafiki ya Ulimwengu​—Jambo Gani?

“Hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu?”​—Yak. 4:4.

1. Rafiki aelezwa kuwa nani, na lazima mambo gani yafikiriwe wakati wa kuchagua rafiki?

WATU wengi huwa waangalifu sana wanapochagua rafiki. Rafiki anaelezwa kuwa ni “mtu anayeshikamanishwa na mwingine na shauku ya upendo au heshima,” “mshirika wa karibu sana.” Je! wewe ungechagua mtu unayechukia tabia zake, ambaye mawazo na maoni yake sikuzote yanapingana na yako, ambaye angeshirikiana au kuunga mkono adui zako, ndiye awe rafiki yako wa karibu sana? Kwa kuwa sisi huchagua rafiki kwa uangalifu sana, yatupasa tumtazamie Mungu Aliye Mkuu Zaidi wa ulimwengu wote afanye hivyo pia. Kwa hiyo, ni lazima tujue namna ya kuwa rafiki za Mungu, Yehova, na namna ya kuendeleza urafiki naye.

2. Je! Mungu amezuia wanadamu wasiwe rafiki zake? Ni kwa njia gani asivyochagua rafiki wo wote tu?

2 Yehova hakuzuia taifa la kibinadamu lisiwe rafiki zake. Kwa kweli, upendo wake kwa wanadamu ndio uliomwongoza kumtoa ‘Mwanawe mzaliwa wa pekee mwenye thamani nyingi, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.’ (Yohana 3:16) Lakini tusidhani kwamba Yehova atakuwa rafiki ya mtu ye yote tu. Katika Zaburi 5:4 twajulishwa nia na mwenendo ambao Yehova hawezi kuachilia rafiki zake wawe nao: “Maana huwi Mungu apendezwaye na ubaya; mtu mwovu hatakaa kwako.”

3. Yesu na Yakobo wanasema nini juu ya kuchangamana na walimwengu?

3 Wafuasi wa Yesu wanajua kwamba lazima wajitenge na ulimwengu na uharibifu wake. (2 Pet. 1:4) Ni kama vile Yesu alivyojulisha katika Yohana 17:16: “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” Ndugu mzazi mmoja na Yesu Yakobo alionyesha matokeo mabaya ya kutojitenga hivyo aliposema hivi: “Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? basi kila atakaye kuwa rafiki wa dunia hujifanya kuwa adui wa Mungu.”​—Yak. 4:4.

SI RAFIKI ZA ULIMWENGU

4. (a) Maana yake nini kuwa rafiki ya ulimwengu? (b) Matendo ya mwili ni nini, nayo matokeo ya kufuata matendo hayo ni nini?

4 Maana yake nini kuwa rafiki ya ulimwengu? Maana yake ni kuwa kama ulimwengu, kuwaza kama ulimwengu, kushiriki katika tamaa zake, kuweka moyoni mambo yake ya kutaka makuu, kuonyesha chuki zake zisizo na msingi. Mtu aliye rafiki ya ulimwengu hufuata nia kuu inayoonyeshwa na jamii ya watu wa ulimwengu. Mtume Paulo aliitaja kama “roho inayotenda kazi sasa katika wana wa kutokutii.” (Efe. 2:2, NW) Roho hiyo inaweza kufanya mtu ajitie katika mazoea ya kilimwengu yanayotajwa katika Wagalatia 5:19-21: “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo.” Matokeo ya kufuata njia hizo za kilimwengu ni nini? Twaonywa kwamba “watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.”

5. Yampasa Mkristo afuate mwendo gani, na ni matunda gani yanayompendeza Yehova?

5 Basi, ni wazi kwamba tukijitia katika mazoea hayo yanayochukiwa na Yehova, tutakuwa tukijitenga naye. Kwa hiyo, lazima tufuate mwendo mwema kwa kuonyesha roho na nia ya Mungu. Paulo atuambia kwamba “matunda ya roho ni upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza . . . wale walio wa Kristo Yesu waliutundika mwili pamoja na tamaa na nyege zake.” (Gal. 5:22-24, NW) Hivyo, tukionyesha matunda hayo tutakuwa tukimpendeza Mungu wala si ulimwengu.

6. (a) Miradi ya ulimwengu na ya Wakristo inatofautianaje? (b) Yesu alitia wafuasi wake moyo wapateje riziki?

6 Kumbuka kwamba ulimwengu una miradi tofauti na ile ya Mkristo. Miradi ya ulimwengu ni ya kutafuta vitu vya kimwili. Ulimwengu haujali hata ukiacha kanuni za haki ndio uendeleze faida zake wenyewe, hata ikiwa utaumiza rafiki wa karibu kwa kufanya hivyo. Unawaza kwamba kila mtu apaswa kuongeza mali zake. Ulimwengu unahangaikia utakachokula, kunywa na kuvaa. (Mt. 6:25-30) Yatupasa tuamini kwamba Yehova atawaruzuku watu wake ili tuepuke kufuata maoni ayo hayo ya kutafuta vitu vya kimwili tu. Lazima tuamini kwamba yeye aweza kuzibariki jitihada zetu na kwamba atazibariki tupate riziki yetu. Yesu, Bwana wetu, hakuwa na mahali pa kulaza kichwa chake, lakini Baba yake alimpa. (Luka 9:58) Vivyo hivyo, Yesu aliwatia wafuasi wake moyo wasiwe na wasiwasi wa kujipatia riziki. Baada ya kusimulia habari ya kuthibitisha alilokuwa amesema katika Mathayo, sura ya 6, mistari 25 mpaka 30, Yesu aliwahakikishia hivi wafuasi wake: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”​—Mt. 6:31-33.

7. Yatupasa tuepuke maoni gani ya kilimwengu, na ni maandiko gani yanayotusaidia kufanya hivyo?

7 Ni jambo la lazima kwetu kuepuka kutegwa na “masumbufu ya maisha,” tukitamani kupata yanayoonwa na ulimwengu kama ‘maisha ya starehe.’ (Luka 21:34) Katika mfano wake wa mpanzi, Yesu alisema kwamba “shughuli za dunia, na udanganyifu wa mali hulisonga lile neno.” (Mt. 13:22) Maneno yake yaliyo katika Luka 12:15 ni ya kweli sana: “Uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.” Yakobo aonyesha vizuri ujinga wa kutumia wakati wetu tukikusanya mali tuwe na maisha ya starehe. Alisema hivi: “Jua huchomoza kwa hari, huyakausha majani; ua lake huanguka, uzuri wa umbo lake hupotea; vivyo hivyo naye tajiri atanyauka katika njia zake.” (Yak. 1:11) Baadaye, anaonyesha mashaka ya maisha anapoeleza hivi: “Ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka.” Kwa hiyo, badala ya kutumainia mipango yetu, yatupasa kusema: “[Yehova] akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.” (Yak. 4:13-15) Ni wazi sana kutokana na maandiko haya kwamba kusitawisha urafiki na Mungu ndiko kwa maana zaidi kuliko kujitahidi kuwa na maisha ya starehe kwa kukusanya lundo la vitu vya kimwili.

8, 9. (a) Ulimwengu huwaonaje watu mashuhuri, lakini yawapasa vijana na watu wazima wakumbuke nini? (b) Yatupasa tuige mifano gani ya rafiki za Mungu, tukiwa na mradi gani?

8 Nia yetu ni nini juu ya watu wenye kupigiwa vifijo na vigelegele na walio mashuhuri wa ulimwengu​—wale wanaofurahisha kwa michezo, sayansi au kwa njia nyingineyo? Wanaume na wanawake hao huheshimiwa sana na ulimwengu. Kwa sababu ya umashuhuri wao, watu wazima na watoto pia huwaabudu na kuiga mienendo na njia zao. Walakini, lazima rafiki ya Yehova ajiangalie asianze kufuata kielelezo hicho cha ulimwengu. Kumbuka, mawazo na njia za wanaume na wanawake hao hazilingani na njia za Yehova. Wao ni washirika wakubwa wa ulimwengu. Kwa hiyo, tukifanya maisha zetu na mwenendo wetu uwe sawa na usemi, mavazi, mapambo na mwenendo wao tutakuwa tukijifanya rafiki zao badala ya kuwa rafiki za Mungu.

9 Yawapasa nyie vijana hasa mjiangalie msiige watu hao kwa kuwa maelekeo yenu ya asili ni kuiga wakubwa wenu. Lakini watu hao mashuhuri ni viumbe wa kibinadamu wasiokamilika watakaokufa katika Har–​Magedoni, wasipobadili mwendo wao na kujipatanisha na kanuni za Yehova. Basi, je! lingekuwa jambo la hekima kutembea na watu hao kwa kufuata njia zao? Je! isingekuwa afadhali kwenu vijana, na vilevile watu wazima, kuwaheshimu sana wale ambao wamejihakikisha kuwa rafiki za Mungu​—watu kama Musa, Yoshua, Daudi, Baraka, Yeftha na Yesu? Wengine, pia, kama Ruthu, Rahabu, Debora na wengine wengi sana, wameendeleza urafiki wao na Yehova nao wanastahili kweli kusifiwa na kuheshimiwa sana nasi. (Ebr. 11:4-38) Namna gani juu ya mifano ya kisasa ya wale ambao wameendelea kuwa rafiki za Mungu? Je! wewe usingetaka kuiga uaminifu na uvumilivu wa ndugu zako waliovumilia walipolemezwa na tawala zenye kutumia nguvu kama utawala wa Nazi wa Hitler au tawala za Kikomunisti, kwa sababu walikataa kuacha urafiki wao na Yehova? Watu hao na wengine wasiohesabika ambao wametembea na Mungu nyakati zote watakuwa hai baada ya “dhiki kubwa,” lakini rafiki wakubwa wa ulimwengu huu watatoweka milele.​—Zab. 37:10, 34, 38; Mt. 24:21, 22.

USEMI NA MWENENDO WETU

10, 11. (a) Je! tukishirikiana na ulimwengu usemi wetu waweza kuharibiwa? Eleza. (b) Biblia yasema nini juu ya mwenendo na mavazi, na kwaweza kuwa na matokeo gani tusipotii 1 Wakorintho 15:33?

10 Tena, rafiki za Mungu wanaonywa kwa upole wajenge wengine kwa usemi wao. Paulo aandika hivi: “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia.” (Efe. 4:29) Je! twaweza kusema kwamba rafiki za ulimwengu huyatii maneno haya? Je! wao hujenga wengine kwa usemi wao? Je! ‘huwafaa wenye kusikia’? Yakobo alisema mengi juu ya ulimi: “Katika kinywa kile kile hutoka baraka na laana. Ndugu zangu, haifai mambo hayo kuwa hivyo.” (Yak. 3:2-12) Basi, je! lingekuwa jambo la hekima kushirikiana na walimwengu, na pengine kuwa na ulimi wa namna inayoelezwa na Yakobo?

11 Vilevile, namna gani mwenendo wetu? Je! unapatana na wa ulimwengu au ni “mzuri kati ya Mataifa,” kama Petro anavyopendekeza? (1 Pet. 2:12) Namna gani mavazi yetu? Je! twajaribu kufuata mitindo ya karibuni? Je! twaweza kufanya hivyo tukavaa kwa “adabu nzuri, na moyo wa kiasi,” kama Paulo alivyotutia moyo tufanye? (1 Tim. 2:9; Mit. 11:2; Mik. 6:8) Tusijipumbaze. Paulo alisema hivi kwa mkazo: “Mashirika mabaya yanaharibu mazoea mazuri.” (1 Kor. 15:33, NW) Kwa hiyo, katika pande tulizoangalia, ni wazi kwamba hatuwezi kufurahia ushirika wa ulimwengu kwa mawazo na matendo yetu tukatazamia kuendelea kuwa rafiki za Mungu.

12. Petro asema nini katika 2 Petro 3:11-14, na nyingine za tabia na mwenendo tunaoweza kufuata ni nini?

12 Ili tuendelee kuwa rafiki za Mungu, lazima tuyatii maneno ya Petro yaliyoongozwa na Mungu: “Kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa!” (2 Pet. 3:11-14) Nyingine za tabia hizo ni kushiriki kuzihubiri habari njema, kuhudhuria mikutano ya watu wa Mungu na vilevile “kujilinda na dunia pasipo mawaa.” (Mt. 24:14; Ebr. 10:25; Yak. 1:27) Tukiwa na “mwenendo mtakatifu” huo na ‘utawa’ tutajishughulisha sana hata tusiwe na wakati wa kujichanganya na ulimwengu wala kufikiria njia zake. Hilo ni jambo la lazima ili tuwe rafiki za Mungu.

URAFIKI KATATI YA NDUGU

13. (a) Ni kwa njia gani huenda tukaonyesha nia ya kilimwengu juu ya ndugu yetu, na 1 Yohana 4:20 yasema nini juu ya hilo? (b) Yesu alitutia moyo tufanye nini na ndugu yetu, na kwa sababu gani?

13 Liko jambo jingine pia ambalo lazima lifikiriwe. Nia yako ni nini juu ya ndugu zako? Je! unawapenda? Je! unahakikisha unawapenda kwa kushirikiana nao? Je! wewe huongea na wote kwa hiari? Au umekosa kusema na mtu fulani kwa miaka mingi kwa sababu ya kutoelewana kidogo? Au unaepuka watu fulani kwa sababu hii au ile? Huenda ukatumia wakati mwingi katika kazi ya kuhubiri. Huenda ukatoa maelezo katika mikutano yote kwa hiari. Huenda ukawa unajitahidi sana katika kazi zote za kundi. Lakini, hata hivyo, je! wewe kweli ni rafiki ya Mungu na hali wamwepuka ndugu yako? Mungu asema nini? “Mtu akisema, Nampenda Mungu, naye anamchukia ndugu yake, ni mwongo; kwa maana asiyempenda ndugu yake ambaye amemwona, hawezi kumpenda Mungu ambaye hakumwona.” (1 Yohana 4:20) Kwa hiyo, ni jambo la lazima “upatane kwanza na ndugu yako,” kama Yesu alivyoonya kwa upoe, kwa kuwa kumwonyesha nia isiyo ya upendo kwaonyesha wazi sisi si rafiki za Yehova.​—Mt. 5:23, 24; 1 Pet. 1:22.

14. (a) Je! yatupasa kufuata nia ya ulimwengu juu ya wengine, na kwa sababu gani? (b) Ni nini kitakachotusaidia tuachilie au kusahau kutokamilika kwa wengine?

14 Tabia nyingine ya walimwengu ni kutokuwa wenye huruma na kutosamehe rafiki zao. Je! hawadharau watu wengine, kuwalaumu-laumu, kuwalalamikia na kuwaharibia sifa yao? Biblia yasema hivi juu yao: “Mtu asiyefaa kitu huchimba shimo la madhara; katika midomo yake mna moto uteketezao.” (Mit. 16:27) Walakini, haiwapasi rafiki za Yehova kutenda hivyo. Sisi tu tofauti kwa sababu tunaachilia udhaifu na makosa madogo ya wengine. Sisi tu wenye nia ya kusamehe. Kwa sababu gani? Je! kwani si Yehova anayetuwekea mfano? Daudi atukumbusha hivi katika Zaburi 103:9: “Yeye hatateta sikuzote, wala hatashika hasira yake milele.” Nao mstari wa 14 wasema hivi: “Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” Huo ni mfano mwema tunaopaswa kufuata. Kwa hiyo, ndugu yetu apungukiwapo, tufanye nini? Tutafanya sawa na vile Yehova angefanya. Tutamsamehe! Ili kutusaidia kufanya hivyo, twaweza kujiuliza maulizo kadha. Je! amefanya hivyo kwa sababu ya kutokamilika kwake? Je! amefanya hivyo kwa sababu hakufikiri? Twaweza kuuona udhia wake kama jambo dogo? Sababu gani tusiliache jambo lenyewe kwa sababu hatujui kwa nini amelitenda? Ingekuwa afadhali kuwa na “juhudi nyingi katika kupendana,” kwa maana “upendano husitiri wingi wa dhambi.” (1 Pet. 4:8; Efe. 4:32; Kol. 3:13; 1 Pet. 3:8, 9) Tukifanya hivyo twaonyesha kwamba sisi ni rafiki za Mungu wala si rafiki za ulimwengu.

KUENDELEZA URAFIKI NA MUNGU

15. Ibilisi anatumia nini kuvunja urafiki wetu na Mungu, nasi twawezaje kuepuka kunaswa katika njia zake?

15 Ulimwengu huu mkatili usio na urafiki hukaza sana rafiki za Mungu leo. Ni lazima wajitahidi sana kuendelea kuwa rafiki Zake. Ibilisi anajaribu sana kuuvunja urafiki huo. Afanya hivyo kwa kuufanya ulimwengu uonekane wa kuvutia sana. Angalia yanayosemwa na 1 Yohana 2:16: “Kila kilichomo duniani,” kisha Yohana aonyesha mambo yale matatu makubwa yanayotokana na ulimwengu na yanayotumiwa na Shetani​—“tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, [“na kujionyesha kwa mtu mali yake,” NW].” Aonyesha kwa usahihi sana vile ulivyo ulimwengu ambao yatupasa kuupinga ikiwa hatutaki kunaswa katika njia zake na kuacha kutambuliwa kama rafiki za Mungu.

16. Yesu alimpingaje Shetani, nasi twawezaje kufanya vivyo hivyo?

16 Lazima Mkristo achukue hatua za hakika kumpinga ‘mtawala wa ulimwengu huu,’ Shetani, na washirika wake. (Efe. 6:10-18; Yak. 4:7) Kwa njia gani? Yesu alifanya nini aliposhawishwa nyakati tatu mbalimbali jangwani? Alijibu akasema: “Imeandikwa.” (Mt. 4:1-11) Mtu huyo mkamilifu aliyaacha maneno ya Mungu yakauongoza mwendo wake wa maisha, nasi twapaswa kumfuata kwa maana alituwekea mfano. Mtunga zaburi alisema: “Neno lako ni taa ya miguu yangu.” (Zab. 119:105) Hivyo, kwa kuacha Neno la Mungu liongoze kila hatua yetu ya kumpinga Shetani, tunaweza kuimarisha uhusiano wetu na rafiki yetu, Yehova.

17. Twahitaji nini ndio tushinde majaribu yaliyoko mbele, nasi tungepoteza nini kwa kufuata tamaa mbaya?

17 Kati ya sasa na mwisho wa taratibu hii, hatutaweza kushinda vita yetu na Ibilisi kwa nguvu zetu wenyewe. Twauhitaji msaada wa Mungu. Lazima tumwombe Yeye hekima na uongozi wa kupambana na majaribu na vishawishi vitakavyotukabili. (Yak. 1:5) Hakuna wo wote kati yetu wasioweza kujaribiwa kwa hila za Ibilisi. Yeye anakesha ili atutie tamaa mbaya tushindwe na mikazo ya ulimwengu wake. Walakini, tukizifuata tutaupoteza urafiki wenye thamani nyingi pamoja na Mungu, na tutakufa milele. (Yak. 1:14, 15) Je! ni sawa tufuate mwendo huo?

18. Mungu amefanya jambo gani jingine asaidie rafiki zake, nasi tumepaswa kuwaonaje wazee?

18 Vilevile, Yehova amechukua hatua zaidi kwa kuweka wazee ili atie moyo na kusaidia rafiki Zake wazuie tamaa za kichoyo. Lingekuwa jambo la hekima kuitikia mashauri yao. Paulo ashauri hivi: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya [nafsi] zenu, kama watu watakaotoa hesabu.” (Ebr. 13:17; Gal. 6:1) Pindi kwa pindi, huenda tusipendezwe na wanayotuambia. Huenda wakatuambia mambo yaliyo kinyume cha tunayotaka kusikia. Lakini, ili tuwe rafiki za Mungu, yatupasa kuwasikiliza na kutumia mashauri yao kwa unyenyekevu. Mtunga zaburi asema: “Njia ya mpumbavu imenyoka machoni pake mwenyewe; bali yeye aliye na hekima husikiliza shauri.”​—Mit, 12:15.

19. Je! mtu akitenda kosa zito hana tumaini kabisa? Eleza.

19 Namna gani mtu akiwa “mpumbavu” na kufanya kosa zito? Je! hana tumaini lo lote? Sivyo, maana Yakobo atukumbusha hivi: “Ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa. Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa.” (Yak. 5:13-16) Kwa hiyo, uombe msaada wa wazee uwaache wakusaidie uache mwendo wako wenye dhambi. (Mit. 28:13) Lo! inafariji namna gani kujua kwamba mtu aweza kupoteza urafiki na Mungu kwa muda, na bado arudi kuwa rafiki mwenye kutumainiwa kwa kutubu na kufuata mwendo unaopatana na njia zake!​—Isa. 55:7.

20. (a) Je! faida zinazopatikana katika ulimwengu ni za kudumu? (b) Ni nani aliyetuwekea mfano mwema, na kwa sababu gani alifuata mwendo huo?

20 Urafiki na ulimwengu unaweza kuleta faida fulani lakini ni raha ya dhambi ya muda tu. Ni ya kitambo tu. Ni maisha yasiyo na wakati ujao. Inaweza kuendelea kwa muda mchache tu uliobaki kwa ulimwengu huu wa kale. Je! isingekuwa afadhali kufuata mfano mwema wa Musa? Biblia yasema hivi juu yake: “Kwa imani Musa alipokuwa mtu mzima, akakataa kuitwa mwana wa binti Farao; akaona ni afadhali kupata mateso pamoja na watu wa Mungu kuliko kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo; akihesabu ya kuwa kushutumiwa kwake Kristo ni utajiri mkuu kuliko hazina za Misri; kwa kuwa aliyatazamia hayo malipo.” (Ebr. 11:24-26) Musa alikataa toleo la kuwa rafiki ya ulimwengu huo, pamoja na mali na vitu vyake vyenye kuvutia, kwa sababu alitaka kupata thawabu kutoka kwa Yehova. Thawabu hiyo ilikuwa nini? Alijua kwamba kwa kuendelea kuwa rafiki ya Mungu angekumbukwa na Mungu na kufufuliwa katika taratibu mpya yenye haki.

21. (a) Lazima tufanye nini tupate thawabu waliyowekewa rafiki za Mungu? (b) Tutapata thawabu gani?

21 Imani yetu na tumaini letu na liwe lenye nguvu kama la Musa. Katika njia zote za maisha, na tuendelee kuwa ‘bila madoa’ ya ulimwengu na rafiki zake. Mawazo na matendo yetu na yawe juu ya rafiki yetu wa karibu, Yehova. Mioyo yetu na itake kuendelea kujishikamanisha naye kwa shauku ya upendo kama rafiki mkubwa sana. Tuwe kati ya “watiwa mafuta wa Bwana” au kati ya “mkutano mkubwa,” tukifanya hivyo tutapata baraka nyingi SASA, lakini pia tutaipata thawabu iliyo kubwa zaidi ya uzima wa milele katika taratibu mpya yenye haki itakayokaliwa na rafiki za Yehova peke yao.​—1 Tim. 4:8.

[Picha katika ukurasa wa 373]

Kama vile ua hunyauka juani ndivyo mtu anayejitahidi kuwa tajiri “atanyauka katika njia zake”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki