Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 7/15 kur. 315-319
  • Nimepooza—Lakini Nafurahia Maisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nimepooza—Lakini Nafurahia Maisha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUJIFUNZA KUMTEGEMEA YEHOVA
  • BARAKA ZA KWANZA KUTOKA KWA YEHOVA
  • UGONJWA WA KUSHANGAZA
  • MSAADA WA KUPAMBANA NA HALI YENYE KUHARIBIKA ZAIDI
  • DAWA BORA NI KUENDELEA KUWA NA SHUGULI
  • JARIBU GUMU KUPITA YOTE
  • THAWABU AMBAZO NIMEKWISHA POKEA
  • Yehova Amenipa Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • ‘Nitapanda Juu Kama Vile Paa Anavyofanya’
    Amkeni!—2006
  • Nashukuru kwa Ajili ya Utegemezo wa Yehova Usioshindwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Nina nguvu ingawa mimi ni dhaifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 7/15 kur. 315-319

Nimepooza​—Lakini Nafurahia Maisha

Imesimuliwa na Rodolfo Barin katika visiwa vya Philippines

MIAKA minane iliyopita nilikuwa naweza kusimama na kutembea bila kusaidiwa. Miaka sita iliyopita nilikuwa bado naweza kuandika jina langu na kujilisha, lakini miaka miwili iliyopita hata kazi ndogo hizo siwezi kuzifanya. Nisomapo, inakuwa lazima mtu anifungulie kurasa, nami nikiinamia mbele mno katika kiti changu cha kutembelea, kichwa changu huanguka kifuani pangu nisiweze kukiinua tena bila ya kusaidiwa. Nimepoozeshwa na ugonjwa unaoitwa multiple sclerosis.

Kwa maana nilikuwa mtu mwenye maungo na mwenye afya nilipopatwa mara ya kwanza na ugonjwa huo nikiwa wa miaka 37, huenda ukashangaa jinsi nimeweza kuendelea kuwa mchangamfu na mwenye bidii. Nimepambanaje na huzuni ya kuvunjika moyo miaka hiyo kumi na miwili ya kupatwa na adui yangu asiyenihurumia? Jibu lapatikana kwa kurudi huko nyuma mwaka 1957, nilipoamua kuweka maisha yangu wakf nimtumikie Muumba wetu, Yehova Mungu.

KUJIFUNZA KUMTEGEMEA YEHOVA

Ingawa ilinichukua zaidi ya miaka miwili nikijifunza na Mashahidi wa Yehova kabla sijasadiki kabisa kweli ya Biblia, mara niliposadiki nilijitahidi kufanya mabadiliko katika maisha yangu. Nilikuwa na jumba la kunywea pombe hata wakati wa usiku, lenye kuniletea pesa nyingi, nami nilikuwa mlevi halisi na mvuta sigareti asiyechoka. Lakini baada ya kufikiria shauri la Biblia katika 2 Wakorintho 7:1 kwamba “tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho,” niliyaacha mazoea yangu mabaya. Nililiuza jumba la kunywea pombe kwa bei ya chini nikajaribu kusadikisha wasichana waliokuwa wakifanya kazi humo wabadili maisha zao kwa kutumia mashauri ya Mungu. Wengine walikubali wakaacha kufanya kazi katika jumba hilo. Huo ulikuwa uamuzi mwema, kwa maana miaka mingi baadaye hali yao ilikuwa afadhali zaidi kuliko ya wasichana waliobaki.

Nilipokuwa nikitumia kanuni za Biblia bila kukubaliana na wasiotaka nifanye hivyo, karibuni nilitendwa mabaya ya namna zote na rafiki wenzangu. Ingawa nilikuwa na cheo kikubwa katika shirika kubwa la kutengeneza vitu katika Manila, marafiki walikuwa wakinilaumu-laumu kwa sababu nilikataa kushiriki katika mazoea ya biashara yenye kuvunja Neno la Mungu. Hali yao iliniudhi, hata hivyo ninapotazama nyuma, naona kwamba nilimkaribia zaidi Yehova nikapata nguvu kwa kumtegemea. Nguvu hizo za kiroho zikawa za maana sana katika siku zenye huzuni zilizokuwa mbele yangu.

Baadaye, niliiacha kazi yangu ya kimwili nikaanza kazi yangu mwenyewe ya kutangaza bidhaa, nayo mwishowe ilifanikiwa ikahusu taifa lote. Sasa yaajiri watu 80 kwa kawaida, na nyakati nyingine hesabu hiyo huwa maradufu. Karibu 90 kwa mia kati ya wafanya kazi wangu ni Mashahidi wa Yehova.

Ingawa afisi yangu ni ndogo ikilinganishwa na nyingine, hiyo ndiyo imepewa mara nyingi kazi zinazohitaji uangalifu zaidi na shirika lenye kutusaidia. Shirika letu ndilo limepewa sikuzote madaraka ya kutangaza bidhaa za pesa nyingi zaidi. Hiyo si kwa sababu sisi twaziuza kwa bei nafuu, bali kwa sababu wafanya kazi wetu wanajulikana kuwa waaminifu kupita watu wengine kwa sababu ya dini yao, nami naonea hilo fahari. Hivyo wasimamizi wa shirika lenye kutusaidia hutuomba sikuzote tuwape kazi Mashahidi wa Yehova.

Lakini, kama inavyotazamiwa, kushikamana sana na sheria na kanuni za Yehova kumeniletea majaribu pia. Nilipokataa kutangaza sabuni ambayo watu wangepewa wakinunua vitu vya kidini kama misalaba, picha na sanamu, mmojawapo wajumbe wa shirika alinikasirikia akaniuliza, “Sababu gani wakataa kushughulika na bidhaa za kidini zinazovutia wanunuzi?”

Nikasema, “Mungu huchukia sanamu zinapotumiwa, kwa hiyo sisi hatuzigusi.”

Aliponikunjia uso na kuniambia tulikuwa watu wa dini tofauti, nilijibu: “Hata hivyo, kama ningalikuwa wa dini yako, ingalinipasa kukataa hata zaidi. Bila shaka nisingedharau Mungu wangu kwa kumpa mtu picha yake ati ndiyo anunue vifurushi vichache vya sabuni.” Hatukuzungumza tena jambo hilo.

Lakini nilipatwa na mambo mengine kama hayo. Wakati mmoja, sikujua kwamba tikiti za bahati nasibu zilitiwa ndani ya bidhaa fulani ziwe kama zawadi. Nilipojua hivyo baadaye, nililikataa jambo hilo mara moja, nikaelezwa mkataba niliofanya ungevunjwa nifanyiwe kesi mahakmani. Lakini, nilisimama pale pale, nikawaeleza nilikuwa na nia ya kupatwa na lo lote. Ikawaje? Walinyamaza wakaziondoa tikiti.

Wakati mwingine, nilipokuwa katika shughuli ya utangazaji kusini ya Phillippines, wafanya kazi wangu ambao ni Mashahidi waliniomba ruhusa ya kuhudhuria kusanyiko la wilaya la siku nne. Nilikubali bila kusitasita. Shirika lenye kutusaidia lilipofahamu hivyo walikasirika sana, wakasema wasingevumilia tena kusumbuliwa hivyo. Nilitumia nafasi hiyo kuwaeleza kwamba Mashahidi wasingekubali kutohudhuria makusanyiko yao hata kama ningetaka wasiyahudhurie. Niliwakumbusha pia kwamba shirika hupendelea zaidi kufanyiwa kazi na watu wetu kwa sababu ni waaminifu, wenye bidii na nadhifu. Nikawaonyesha kwamba, kwa kuwa ni katika makusanyiko hayo wafanya kazi wetu hupata ujuzi na roho inayowafanya wawe walivyo, shirika lingepata hasara likiwazuia wasihudhurie. Kwa mara nyingine tulishinda katika msimamo wetu.

BARAKA ZA KWANZA KUTOKA KWA YEHOVA

Lakini si majaribu ya imani yangu peke yake yaliyonitia nguvu. Yehova Mungu alinibariki kwa kunipa mapendeleo mengi kati ya watu wake, kama kwamba alikuwa akinitayarisha kuukabili ugonjwa wangu wenye kunidhoofisha. Niliwekwa niwe mwangalizi katika kundi lililoundwa majuzi lililoitwa Roosevelt Congregation katika Quezon City, karibu sana na afisi ya tawi ya Philippine ya Watch Tower Society, baada ya mwaka mmoja tu tangu nilipojiweka wakf na kubatizwa. Ingawa niliona kazi hiyo ilikuwa kubwa kunizidi, nilitiwa moyo na ndugu zangu Wakristo, na vilevile na mwangalizi wa tawi, aliyekuwa akishirikiana na kundi hilo wakati huo. Nilifurahi sana kuliona kundi likikua miaka michache iliyofuata! Mwaka 1964 iliwezekana kuanza kundi jipya katika kiunga cha mbali cha Quezon City ili kuangalia watu kumi na wawili, waliotatizwa kuhudhuria mikutano. Niliwekwa niwe mwangalizi wa kundi hili jipya la Novaliches.

Kwa kuwa nilikuwa nikikaa karibu kilomita 25 kutoka lilikokuwa kundi hilo (maili 151/2), niliamua kuhamia Novaliches daima ili niwe karibu na kundi jipya hilo. Kwa kuwa miaka iliyofuata lilikua kutoka wahubiri kumi na wawili wa kwanza likawa na jumla ya wahubiri wa Ufalme 200, nilikuwa na pendeleo la kusaidia kujenga Jumba la Ufalme kubwa katika uwanja uliokuwa pale pale karibu na nyumba yangu.

Karibu miezi mitatu baada ya kuundwa kundi jipya hili ndipo niliposumbuliwa kwanza na ugonjwa wangu, Juni 1964.

UGONJWA WA KUSHANGAZA

Nilianza kuona vitu kama kwamba vilikuwa zaidi ya kimoja, nikawa nikikazika macho kwa sababu misuli ya macho ililegea. Hilo lilipotukia nikawa nikishikwa na kizunguzungu muda mrefu. Baada ya kupatwa na hilo mchana kutwa afisini, nililazimika kuita daktari, akanipa maagizo juu ya nitakalofanya. Siku zilipita bila badiliko kubwa. Nilianza kushuka moyo. Nilihuzunika sana kufikiria kwamba ugonjwa huu ungenizuia nisifanye utendaji wangu wa Kikristo.

Ili nipunguze kizunguzungu kilichotokana na kuona vitu kama kwamba vilikuwa zaidi ya kimoja, nilifunga jicho moja, nikalifungua, kisha nikatumia lile jingine na kuendelea kufanya hivyo. Hivyo niliweza kutimiza wajibu wangu wa kundi na wa jamaa, ingawa yalikuwako magumu. Baada ya miezi miwili nilianza kuona kama kawaida, nami nashukuru kwamba naweza bado kuona vizuri. Walakini, tatizo la macho yangu lilikuwa mwanzo tu wa ugonjwa wenyewe. Karibuni nilianza kujisikia nikiwa dhaifu katika mguu wangu wa kushoto, ukawa ukifa ganzi. Badala ya kutembea sasa nilikuwa nikiyumbayumba, nami niliweza kushinda tatizo hilo kwa kutumia fimbo.

Niliwaendea madaktari mbalimbali, lakini uchunguzi wao ulitofautiana kama vile madaktari wenyewe walivyotofautiana. Miezi iliposonga mbele ugonjwa wangu ukakosa kujulikana, nilizidi kumtegemea Mponyaji mkuu na Mpaji uzima, Yehova Mungu. Niliamua kwa imara nisiache woga uingie moyoni mwangu, tena nilifarijiwa sana na andiko lililoongozwa na Mungu katika Zaburi 55:22: “Umtwike [Yehova] mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.”

Kufika mwaka 1966 ugonjwa huo ulikuwa umeongezeka sana hata mguu wa kuume ukaanza kuugua, hata sehemu za chini za miguu yangu zikawa kavu. Kufika mwaka 1968 sikuweza tena kutembea hata kwa kutumia fimbo, nikalazimika kutumia kiti cha kutembelea. Sasa nilikuwa kama kilema nikahuzunika sana.

Kabla ya kupatwa na ugonjwa huo, nilikuwa mwenye nguvu na bidii nyingi, hata ilikuwa ajabu sana uliponipata. Nilifikiria jinsi majuzi tu kazi ya kuzihubiri habari njema nyumba kwa nyumba ilivyokuwa ikinifurahisha na kunifaidi. Nilikumbuka sana nilivyofurahi kupata watu wenye nia ya haki nikawapa imani mpya juu ya Mungu wa pekee anayeahidi taratibu mpya kabisa ya mambo!

MSAADA WA KUPAMBANA NA HALI YENYE KUHARIBIKA ZAIDI

Baadaye daktari mmoja mashuhuri alichunguza ugonjwa wangu akajua kwamba ni multiple sclerosis (kukauka-kauka kwa sehemu fulani za ubongo au za uti wa mgongo). Kinacholeta ugonjwa huu hakijulikani, na haiwezi kujulikana mapema jinsi utakavyokuwa kwa maana hauwezi kuponywa. Ingawa vipindi fulani ulipungua, nilipojiacha nipigwe na baridi au nilipopatwa na ugonjwa wa namna nyingine, au hata nilipohuzunika, ugonjwa huo ulirudi ukiwa mbaya zaidi. Nilikuwa na wasiwasi sana kwa sababu sikujua ugonjwa huo utaniletea nini baada ya hapo. Lakini nilimtumaini Yehova, nami nimejiondolea huzuni nyingi iliyoletwa na kulemaa kwangu, kwa kusali daima. Nilifarijiwa na maneno ya Zaburi 46:1, 2: “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa.” Sikuzote maneno hayo yamenitia nguvu ninapojitahidi nisivunjike moyo na kufadhaika.

Wakati huo wote hali yangu ya kimwili iliendelea kuharibika. Kufika mwaka 1970 mikono yangu ilidhoofika sana hata sikuweza tena kujisukuma katika kiti cha kutembelea. Kufika mwaka 1974 vidole vyangu vilikuwa vimelegea kabisa, nisiweze tena kusoma, kuandika wala kujilisha. Mbu akiniuma, naweza kumsikia akiniuma, lakini sina nguvu za kumchapa. Sasa ugonjwa huo umeanza kushika misuli ya shingo yangu hivi kwamba, nikiwa peke yangu kisha kichwa changu kianguke upande wa mbele, siwezi kujizuia nisianguke kutoka katika kiti changu cha kutembelea.

Naam, nina mambo mengi ya kupigia asante. Kwanza, nashukuru kwamba bado akili yangu ni nzuri na yafanya kazi, ijapokuwa misuli ya mwili wangu imeharibika. Pili, nashukuru kwamba macho yangu hayajaharibiwa na ugonjwa huo tangu mara ya kwanza nilipoona vitu kama kwamba vilikuwa zaidi ya kimoja, miaka kumi na mmoja iliyopita. Kwa hiyo naweza kusoma mtu akinifungulia kurasa. Vilevile, ingawa sauti yangu imedhoofika, bado inasikika waziwazi. Hiyo imeniwezesha niendelee kuwa mzee kundini, kutoa hotuba za Biblia za watu wote katika Jumba la Ufalme na katika makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Hivyo naweza bado kufundisha wengine makusudi ya Mungu.

Hata naweza kukubali mapendeleo zaidi katika tengenezo la Kikristo, kama kuwa mwangalizi wa kusanyiko katika mzunguko wetu wa Mashahidi wa Yehova. Mimi hutumikia kama mwangalizi wa kupakua chakula pia katika makusanyiko makubwa zaidi ya wilaya yanayofanywa mjini. Mimi hufurahia sana kutumiwa hivyo ijapokuwa nimelemaa.

Mke wangu na watoto wetu wanne wamenitia sana nguvu na moyo, wakanihurumia wakati huu wenye magumu. Sijapata kamwe kujisikia niko peke yangu. Mwana wangu mkubwa zaidi amekuwa akinifanyia mambo mengi ambayo ningalifanya kama mikono na miguu yangu ingalikuwa mizuri. Washiriki wa jamaa yangu ndio wameniandikia hadithi hii huku mimi nikiwaeleza mambo watakayoandika.

Sisi tuna gari kubwa lenye kiti cha pekee kinachopepewa hewa, nacho huniwezesha kutembeatembea kidogo. Wanangu ndio huniinua kutoka kiti cha kutembelea na kuniingiza garini, kisha hukunja kiti cha kutembelea na kukiweka nyuma. Tafrija ninayopenda zaidi ni kusafiri, nasi husafiri maili mia moja (kilomita 160) au zaidi, kutembelea Mashahidi wenzetu katika majimbo mengine.

DAWA BORA NI KUENDELEA KUWA NA SHUGULI

Napenda kuwa na mambo mengi ya kufanya. Mimi huamka saa 10:30 alfajiri na mapema, na wakati huo mimi hukandwa-kandwa mwilini. Nahitaji kukandwa kabla ya kulala na niamkapo, ili misuli ya miguu na mikono isikauke. Saa 12:00 asubuhi naenda na watoto wangu wawili wa mwisho katika shule zao mbalimbali, kisha napelekwa afisini kwangu, kwa gari. Nafanya kazi mpaka adhuhuri. Alasiri ya kila siku ya pili nafundisha wafanya kazi wenzangu Biblia. Jumla ya wafanya kazi saba wanajifunza Biblia sasa pamoja nami, wote wakiwa pamoja. Kisha naenda nyumbani, ambao ni mwendo wa karibu saa moja kwa gari, kutoka afisini kwangu.

Kila jioni ya Jumanne naongoza funzo la kundi la Biblia. Jioni za Jumatano nazungumza habari za Biblia na jamaa yangu yenye washiriki wanne. Jioni za Alhamisi nafundisha kikundi cha jamaa tatu Biblia, nao wanaishi kilomita kumi na saba (maili 101/2) kutoka nyumbani kwangu. Sasa kikundi hicho kinakuwa na mikutano ya kawaida ya kundi na huenda karibuni kikastahili kuwa kundi la watu wa Mungu. Jioni za Ijumaa tunakuwa na mikutano yetu ya kawaida ya kundi inayoitwa Shule ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi.

Asubuhi za Jumamosi mimi huenda na ndugu zangu Wakristo katika gari langu kubwa nikashiriki kuhubiri hadharani. Ijapokuwa siwezi kwenda nyumba kwa nyumba nikiwa na kiti changu cha kutembelea kwa sababu barabara na vijia vya mashambani si laini, mara nyingi akina ndugu huniweka mahali palipo na watu wengi nami huanza kuongea nao. Au mimi huketi ndani ya gari na kuita watu wanaopita karibu niwaeleze habari za tumaini nililopata katika Biblia. Alasiri za Jumamosi mimi huwa nikitayarisha mambo ya mikutano ya kundi na hotuba za Biblia. Asubuhi za Jumapili hujiunga na Mashahidi wenzangu kuhubiri, na alasiri tunakuwa na hotuba yetu ya kawaida ya watu wote, ya Biblia, na funzo la Biblia la kutumia Mnara wa Mlinzi.

Nyakati nyingine watu wenye nia nzuri hunijia na kunishauri kwamba najiumiza sana kwa kufanya mambo mengi hivyo. Sikuzote mimi hujibu kwamba sitaacha mapendeleo yo yote ya Kikristo niliyo nayo maadamu naweza kuyatimiza. Mapendeleo na madaraka ayo hayo ndiyo yameniwezesha nisiwe nikijisikitikia. Yamenisahaulisha ugonjwa wangu, na hiyo ndiyo imekuwa dawa bora kwangu.

JARIBU GUMU KUPITA YOTE

Nadhani jaribu lililokuwa gumu kupita yote lilinipata siku moja mwaka 1972 nilipoona maumivu makali sana katika misuli ya uso. Sikuweza kusema hata neno moja. Nilikuwa nimepatwa na neuralgia (ugonjwa wa kuwasha neva). Nilipopatwa nao mara ya kwanza, sikuweza kusema muda wa siku mbili. Niliumwa kweli kweli nilipojaribu kufungua kinywa kidogo tu. Nashindwa kueleza jinsi nilivyohuzunika. Hakuna kitu kingeweza kunihuzunisha zaidi kuliko kuona nikipoteza kipawa changu cha kusema. Nilivunjika moyo kweli kweli; kwa muda moyo wangu ukashuka.

Nilisali kwa unyamavu, nikamsihi sana Yehova anirudishie usemi niweze kuendelea kutaja sifa zake. Nilishukuru kwamba nilirudiwa tena na uwezo wa kusema baada ya muda mfupi, ingawa nimekuwa nikiumwa neva mara kwa mara. Nimezidi kujisikia kwamba Yehova yupo nami, nao ugonjwa huu wa majuzi ulinifanya nimkaribie hata zaidi.

THAWABU AMBAZO NIMEKWISHA POKEA

Nina hakika sasa umekwisha jua kile ambacho kimenisaidia nisivunjike moyo na kuvumilia udhaifu wangu wa mwili. Naam, ni uhusiano wa karibu na Yehova Mungu na tumaini langu imara juu ya taratibu mpya yake yenye haki, na vilevile kupendwa na kusaidiwa na jamaa yangu na ndugu na dada Wakristo. Nimesaidika kujisikia kwamba nahitajiwa bado na kwamba nina faida, kwamba naweza kusaidia wengine, kwa kuwa na kazi nyingi ya Bwana. Wakati wo wote nivunjikapo moyo, jambo linalonifurahisha zaidi ni kutembelea rafiki na ndugu zangu na kuzungumza nao Neno la Mungu.

Hakuna furaha duniani inayoweza kulingana na pendeleo ambalo nimekuwa nalo kusaidia watu wengine wapate kumpenda Yehova na kumtumikia. Majuzi jamaa moja niliyosaidia, yenye washiriki sita, iliweka maisha zao wakf kumtumikia Yehova na wote walibatizwa pamoja! Wengi ambao nimesaidia walikuwa wadadisi tu, kwa kuona udhaifu wangu. Lakini walivutwa sana na mambo mapya, mazuri sana, waliyokuwa wakijifunza katika Neno la Mungu, wakasahau hali yangu. Baadaye walikuwa wakiniambia kwamba juhudi na uhakika niliotumia kuongea nao ndiyo mambo yaliyowafanya waanze kupendezwa. Niliposikia hilo, nilimshukuru Yehova kwa unyamavu kwa sababu ya kunithawabisha na kunitia moyo hivyo.

Furaha ya utumishi wa Mungu yashinda sana maumivu ya mwili niliyo nayo. Nifikiriapo mambo ambayo nimependelewa kutimiza kwa msaada wa Yehova, nasaidika nifurahie maisha, nisijisikitikie kama mtu aliyepooza awezavyo kufanya. Kwa kusaidiwa hivyo na Yehova, siwezi kamwe kuzuiwa na maumivu, kupooza wala ugonjwa wa kuwashwa neva, nisilisifu jina lake kuu lenye utukufu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki