Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 7/1 kur. 311-312
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Habari Zinazolingana
  • Mungu Aliumba Mwanamume na Mwanamke wa Kwanza
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
  • Ikiwa Adamu Alikuwa Mkamilifu, Angeweza Jinsi Gani Kufanya Dhambi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Adui wa Mwisho, Kifo, Aangamizwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Adamu na Hawa
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 7/1 kur. 311-312

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

● Je! Adamu alikuwa na ngozi nyekundu, kama wengine wanavyosema jina lake laonyesha?

Hakuna mtu aliye duniani leo awezaye kutaja kwa uhakika rangi ya ngozi ya Adamu. Lakini, twajua kwamba yeye ndiye aliyekuwa mzazi wa wanadamu wote wenye rangi mbalimbali za ngozi. Lakini kwa sababu gani kumetokea wazo la kwamba labda ngozi ya Adamu ilikuwa nyekundu?

Neno la Kiebrania adam limetafsiriwa kuwa “Adamu.” Zaidi ya kuwa jina, lamaanisha na kutafsiriwa “mtu” au “mtu wa dunia,” mtu mmoja au watu walio duniani kwa ujumla. (Mwa. 1:26; 6:7; 7:21; 9:6; 1 Sam. 15:29, NW) Neno adam lahusiana na neno jingine la Kiebrania, adamah, linalomaanisha “dunia” au “nchi.” Wanafunzi Waebrania wanaona kwamba maneno yote hayo mawili yametokana na neno adom la Kiebrania, linalomaanisha “-ekundu.” Kinapotoa sababu inayoelekea kuwa ya kweli ya kutoa neno “nchi” katika neno “-ekundu,” Theological Dictionary of the Old Testament (1974) chaonyesha labda nchi ilikuwa na chuma na hivyo ikaonekana kuwa nyekundu. Vivyo hivyo, wakuu wengine wanaoshikilia kwamba neno adam (Adamu, mtu) limetokana na neno adom (-ekundu) wamekisia kwamba Adamu labda alikuwa na ngozi nyekundu.

Lakini, angalia uhusiano unaoonyeshwa katika Mwanzo 2:7: “Mungu akamfanya mtu [adama] kwa mavumbi ya ardhi [adamah], akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu [adam] akawa nafsi hai.” Je! hapa Biblia yazungumza habari ya rangi ya udongo au inajaribu kuonyesha rangi ya ngozi ya mwanadamu wa kwanza? Sivyo. Maneno makubwa yanayohusianishwa ni “mtu” na “ardhi.” Neno la Mungu lilikuwa likielekeza fikira za watu juu ya uhakika wa kwamba mtu alitoka katika ardhi; alikuwa mtu wa ardhi au wa dunia. Kila kitu cha Adamu kilitoka mahali pamoja​—ngozi yake, nywele zake, macho yake, meno yake, na kadhalika. Sehemu zote za mwili wa Adamu zilitoka katika ardhi ile ile, hata ziwe zilikuwa na mwundo au rangi gani. Zote hazikuwa nyekundu ati kwa sababu labda udongo ulikuwa mwekundu. Baada ya Adamu kutenda dhambi, Mungu alimwambia mambo ambayo yangetukia nje ya Bustani ya Edeni: “Hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.”​—Mwa. 3:19.

Kwa hiyo, pengine ngozi ya Adamu ilikuwa nyekundu, au pengine haikuwa. Kwa kuwa uhusiano mkubwa wa maneno adam (Adamu, mtu) na adamah (ardhi) katika Mwanzo 2:7 ulikazia kwamba Adamu alikuwa wa dunia, kwamba alitoka katika ardhi, pengine rangi ya ngozi yake ilikuwa yo yote kati ya rangi mbalimbali tunazoona leo kati ya mataifa duniani pote.

Jambo kubwa tusilopaswa kusahau ni kwamba wanadamu wote wametoka kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. Watu wote​—wawe wana ngozi nyekundu, ya mizeituni, ya rangi ya kahawa, nyeusi, nyeupe au ya manjano​—ni wazao wa Adamu. Sote tu watoto wake. Biblia yasema: “[Mungu] alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja [Adamu], wakae juu ya uso wa nchi yote.” (Matendo 17:26) Mungu alimpa Adamu nguvu za uzazi ambazo zingeweza kufanya wazao wake wawe na rangi mbalimbali za nywele na maumbo mbalimbali, rangi mbalimbali za ngozi, ukubwa unaotofautiana wa mwili, nyuso za namna mbalimbali, na kadhalika. Inaelekea kwamba, kwa sababu ya kukaa sehemu mbalimbali na mambo mengine, hali hizo zilidumu kati ya watu wenye kuhusiana sana ambao nyakati za kisasa wameitwa mataifa ya wanadamu. (Ili upate maelezo zaidi, angalia Awake! la Februari 8, 1973, kurasa 5-7.) Bado, sote tu wazao wa Adamu.

Maulizo yanayohusu rangi ya ngozi ya Adamu au hali zenyewe za uso wa mwili wake hayawezi kujibiwa sasa. Hivyo, wakati wachoraji wanapochora Adamu na Hawa wakiwa katika Bustani ya Edeni katika vitabu vya Watch Tower Society, wanajaribu tu kuwaonyesha wanadamu wawili wa kwanza wakiwa katika paradiso. Vivyo hivyo, “Adamu wa mwisho,” Yesu, huenda akaonyeshwa akiwa kama Myahudi, lakini leo hakuna mwanadamu anayejua barabara sura yake ilikuwaje. (1 Kor. 15:45) Lakini, jambo la maana zaidi kuliko maulizo yasiyojibika kwa sasa juu ya jinsi hali za mwili wa Adamu zilivyokuwa, ni sababu gani na jinsi gani Adamu alipoteza upendeleo wa Mungu, na somo tunalopata hapo.​—Rum. 5:12.

Tukijishughulisha na fundisho hilo la maana la Biblia, twaweza sasa kuungana na Mashahidi Wakristo wa Yehova wa mataifa yote, wanaojitahidi kufanya mapenzi ya Muumba. Taifa alimozaliwa mtu wala rangi ya ngozi yake siyo inayoamua kama atapata kibali ya Mungu. Ni kama vile mtume Petro alivyosema: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa naye.”​—Matendo 10:34, 35.

Watu wanaotimiza matakwa Yake leo wanaweza kutazamia kuishi katika dunia ya paradiso atakayoanza Mungu karibuni. Humo wataweza kuzungumza na Habili, mwana wa Adamu atakayefufuliwa, na kupata habari halisi juu ya jinsi jamaa ya kibinadamu ilivyoanza. Wataweza pia kushiriki kutimiza kusudi la Mungu kujaza dunia na wanadamu wenye kupendeza wa namna mbalimbali, watakaoishi kwa amani na umoja na kuweza kumtumikia milele.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki