Kutohesabu Maisha Zetu Kuwa Zenye Thamani Mno
1. Yesu alisema wafuasi wake wangepatwa na nini “siku za mwisho”?,
KATIKA unabii wa Yesu wenye kuchukua kipindi cha miaka 1,900, alitabiri mateso makali sana ambayo yangepata wafuasi wake waaminifu katika siku za mwisho: “Watawakamata na kuwaudhi; watawapeleka mbele ya masinagogi, na kuwatia magerezani, mkipelekwa mbele ya wafalme na maliwali kwa ajili ya jina langu. Na hayo yatakuwa ushuhuda kwenu. . . . Mimi nitawapa kinywa na hekima ambayo watesi wenu wote hawataweza kushindana nayo wala kuipinga. Nanyi mtasalitiwa na wazazi wenu, na ndugu zenu, na jamaa zenu, na rafiki zenu, nao watawafisha baadhi yenu. Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu.”—Luka 21:12-17.
2. (a) Wakristo hawateswi kwa sababu gani hasa? (b) Lakini mateso yaweza kutazamiwa kutoka chanzo gani?
2 Yesu hakuyasema hayo avunje wafuasi wake moyo, bali awaonye mapema. Aliwaambia ‘wasiogope’ kwa maana “mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataiona.” (Mt. 10:31, 39) Kwa hiyo Wakristo wa wakati huo mpaka sasa hawakushangazwa wala kufadhaishwa na upinzani ambao umewapata kwa sababu ya kutetea kweli au kueleza wengine habari njema. Walakini, wao hawajateswa kamwe kwa sababu ya kutenda mabaya. Petro aliwasihi akisema, “Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa. . . . Maana wakati wa maisha yetu uliopita watosha kwa kutenda mapenzi ya Mataifa; kuenenda katika ufisadi.” (1 Pet. 2:12; 4:3) “Ni afadhali kuteswa kwa kutenda mema, ikiwa ndiyo mapenzi ya Mungu, kuliko kwa kutenda mabaya.” (1 Pet. 3:17) Ilikuwa lazima watumishi wa Yehova wapingwe na adui mpinzani mkuu, Shetani, pamoja na wenye kumwunga mkono. Paulo angeweza kuhakikisha hilo kutokana na yaliyompata mwenyewe, maana alimwandikia Timotheo hivi: “Wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa [“watateswa,” NW].”—2 Tim. 3:12; 1:7, 8.
KUPIGA VITA YA KIROHO
3. (a) Shetani amefanya shtaka gani juu ya watumishi wa Mungu? (b) Yampasa kila mtu afanye uamuzi gani, na kwa sababu gani uamuzi huu ni mgumu?
3 Kitabu cha mwisho cha Biblia kilitabiri pia kwamba mateso yangeendelea kuwako katika wakati wa mwisho. Masimulizi katika Ufunuo sura ya 12 yafunua kwamba Shetani alitupwa duniani kutoka mbinguni, “akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufu. 12:9, 12) Sikuzote amedai kwamba wanadamu wanaongozwa na choyo, si kumpenda Mungu, na kwamba watamwacha Mungu maisha zao zikiwa hatarini. Sasa wakati wa Shetani na waliojipanga upande wake unakwisha, kwa hiyo anazidisha upinzani wake juu ya watumishi wa Mungu, akifanya vita nao. Lazima kila mmoja wetu aamue anataka kuwa upande gani wa mpambano huo, tena aamue kama atamtumikia Mungu kwa uaminifu na upendo hata kutukie nini.
4. Ni vyombo gani vilivyotabiriwa kwamba vingeshiriki kushambulia waabudu wa kweli?
4 Shetani hutumia vyombo fulani anapofanya mashambulio juu ya Wakristo wa kweli. Kimoja, kinachosimuliwa katika Ufunuo 13:1, 6-8 kama “mnyama” au wanasiasa, kilisababisha kifo cha Kristo na wafuasi wake wengi katika karne ya kwanza, na vilevile kilionekana mapema kwamba kingefanya vita juu ya “watakatifu” na ‘kumtukana Mungu’ kikijaribu kuungwa mkono na kuabudiwa na mataifa yote katika siku za mwisho. Lenye kuunga mkono “mnyama” huyu wa kisiasa katika matendo yake ni tengenezo la dini za uongo linalosimuliwa kwa kufaa katika Ufunuo 17:5, 6 kuwa ‘Babeli Mkuu,’ linaloonyeshwa kama ‘limelewa kwa damu ya watakatifu, na kwa damu ya mashahidi wa Yesu.’ Vyombo hivyo vyote viwili, cha kisiasa na cha kidini, vilishirikiana kumfisha Yesu, na vilevile kumtia mtume Paulo gerezani, na Yesu akatiwa mikononi mwa serikali ya Kirumi na wafuasi wenye bidii wa dini ya Kiyahudi.
5. (a) Ni silaha gani kuu ambayo Shetani ametumia kuvunja ukamilifu? (b) Twawezaje kuepuka woga?
5 Katika karne zote Shetani ametumia woga wa kifo cha jeuri kama tisho kuu zaidi, kama silaha kuu ya kujaribia kuvunja ukamilifu wa watumishi wa Yehova. Watu walio wengi hawaoni wasiwasi juu ya kuzeeka wakiwa na tumaini la kufa mwishowe, lakini huenda wakaogopa sana wakikabiliwa na kifo cha ghafula, hata wawe na maelekeo ya kukubali kufanya lo lote waambiwalo ndio wakiepuke. Shetani ajua sana hivyo. Lakini yatupasa tuukumbuke mwendo wa uaminifu wa Yesu, kwamba alijifunza utii kutokana na mateso yake na kwamba alionyesha uthabiti hata kufa. Kama Waebrania 2:14, 15 isemavyo, “alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi, awaache huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa.” Hatutaki kuwa utumwani kwa kuogopa kifo. Bali, yatupasa tumtumaini Yehova na kuwa tayari kupambana na majaribu yo yote yawezayo kuja, kama Paulo na watu wengine wenye imani walivyofanya nyakati zilizopita.
6. Twaona mfano gani mwema wa uaminifu katika Danieli sura ya tatu, naye Yehova aliwakomboaje?
6 Ndivyo walivyokuwa Waebrania watatu wale waliokuwa utumwani Babeli, wasiochukua maisha zao kuwa zenye thamani mno, na wasiokuwa na nia ya kuacha yaliyo haki ingawa wangeweza kuuawa. Walipoonywa kwamba wangetupwa katika tanuru ya moto wasipoiinamia sanamu ya dhahabu iliyosimamishwa na Mfalme Nebukadreza, walijibu kwa ujasiri hivi: “Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme. Bali kama si hivyo, ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako.” Masimulizi yaonyesha kwamba wanaume hao walikombolewa na tanuru, hata unywele mmoja wa vichwa vyao haukuunguzwa wala hawakupatwa na harufu ya moto.—Dan. 3:17, 18, 27.
7. (a) Yesu alionyesha nia gani alipochekwa na kutishwa na kifo? (b) Kwa sababu gani Yehova alimwacha auawe?
7 Yesu pia alikabiliwa na kifo akimtumikia Baba yake wa kimbinguni. Wakati mmoja wenye kumsikiliza katika sinagogi Nazareti walikasirika sana hata wakampeleka ukingoni pa mlima, wakitaka kumtupa chini, wakashindwa. (Luka 4:28-30) Lakini wakati ulifika afe ili atimize kusudi la Yehova. Wakati huo wakuu wa makuhani walimcheka, wakisema: “Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu.” (Mt. 27:43) Lakini Mungu hakuzuia Yesu asiuawe. Kwa sababu hiyo, Yehova “ameweka juu yake maovu yetu sisi sote.” Lakini “kwa kupigwa kwake sisi tumepona.” (Isa. 53:6, 5) Hivyo akiwa mkombozi wa jamaa ya kibinadamu, alitimiza mambo mengi zaidi kwa kifo chake cha uaminifu kuliko yale aliyotimiza kwa huduma yake nyingine yote ya duniani. (Marko 10:45) Mwendo wa uaminifu alioufuata haukuwa mwepesi, lakini yeye hakuhesabu maisha yake kuwa yenye thamani mno, bali alikuwa na nia ya kuyatoa kama dhabihu kwa ajili ya wanadamu. (1 Tim. 2:5, 6) Hata alipokuwa akiteswa, hakurudisha matisho wala matukano. Kama Petro alivyoeleza: “Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.”—1 Pet. 2:21-24.
UTHABITI MPAKA KUFA
8, 9. (a) Sasa Yesu ana uwezo gani? (b) Kwa sababu gani tusiogope kukabiliwa na majaribu?
8 Baada ya kuwa thabiti mpaka kufa, Yesu alifufuliwa na Yehova kwenye uzima wa kiroho katika mbingu aliko na cheo cha ‘kumharibu Shetani’ ambaye amejitahidi kutawala wanadamu na kuvunja imani ya wenye haki kwa kutumia vitisho na kuwaua kwa jeuri. (Ebr. 2:14) Yesu alishauri wanafunzi wake Andrea na Filipo hivi: “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele.” (Yohana 12:25) Kwa hiyo kupenda maisha yetu na kutaka sana kuyahifadhi kwa vyo vyote kwaweza kutupotezea matumaini yetu ya uzima wa milele. Lakini tusipohangaishwa mno na vitisho vya kutulazimisha tuache imani yetu tunaweza kulinda matumaini yetu ya kupata baraka za milele katika taratibu mpya ya Yehova.
9 Yafaa tukumbuke kwamba kwa kuwa Kristo “mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wao wanaojaribiwa.” (Ebr. 2:18) Yehova ameahidi pia kututia nguvu tuvumilie majaribu. (Zab. 55:16, 22; Isa. 35:4) Kwa hiyo Wakristo wanatiwa moyo ingawa wanatazamia mateso. Kutaabika kwa sababu wanashikamana na kweli hakuwaaibishi, bali kunawaletea furaha kwamba wanaweza kusimama imara wakisutwa kwa njia inayoheshimu jina la Yehova.—1 Pet. 4:12-14.
10. (a) Paulo alionyesha ni nini kilichokuwa cha thamani zaidi kwake? (b) Ni kwa njia gani wafuasi wa Kristo wanaweza kuwa washindi?
10 Kama Paulo alivyosema: “Siyahesabu maisha yangu kuwa kitu cha thamani kwangu kama kuumaliza mwendo wangu na huduma ile niliyopokea kwa Bwana Yesu.” (Matendo 20:24) Vivyo hivyo katika unabii ulio katika Ufunuo 12:11 twaambiwa kwamba ndugu za Kristo wangemshinda Shetani ijapokuwa awafanyia mashtaka ya uongo mbele za Mungu. “Nao wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo, na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hawakupenda maisha yao hata kufa.” Hivyo ushindi juu ya Shetani utatia na ushindi wa adili wa watumishi wote waaminifu wa Mungu watakaojionyesha waaminifu hata wakikabiliwa na kifo, si kushindwa kwake tu na “Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme.” (Ufu. 17:14; 20:1-4) Wafuasi wa Kristo ni washindi kwa sababu ya “damu ya Mwana-Kondoo,” kwa kuwa wanautumaini ubora wa ukombozi wa dhabihu yake. Wanajionyesha pia kuwa washindi kwa “neno la ushuhuda wao,” wasiogofywe na upinzani unaokusudiwa kukomesha utangazaji wa ujumbe wa Ufalme.
11. Mateso yawezaje kuongeza imani na furaha yetu?
11 Je! tunayo roho iyo hiyo? Je! twampenda Yehova sana sana hata tusiweze kurudi nyuma kwa kuogopa hata ikiwa lazima tufe tuhakikishe uthabiti wetu? Je! kweli twaamini kwamba Yehova ndiye mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii, kwamba hata tukifa twajua hatujashindwa bali tuna tumaini la kufufuliwa? Kwa kuwa kuchukiwa na kuteswa kwa wafuasi wa Yesu katika mataifa yote ni mojawapo ya ishara alizotoa kuhusu wakati wa mwisho, uhakika wa kwamba mambo hayo yanatukia sasa wapaswa kutia imani yetu nguvu. (Luka 21:12) Yatufaa tuyakumbuke maneno ya Yesu: “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu.” (Mt. 5:11, 12) Naam, kupewa pendeleo la kuonyesha ubora uliojaribiwa wa imani yetu kwaweza kuleta furaha huku tukiendelea kuwa na dhamiri njema mbele za Mungu,—Yak. 1:2, 3.
WACHUKIWA BILA SABABU
12. (a) Petro alisema nini juu ya mateso ya Wakristo? (b) Mashahidi wa Yehova wanapatwa na matatizo gani katika nchi nyingine?
12 Wakristo wanajua kwamba wanateswa kwa sababu ya haki. Si kwa sababu ya kujiunga na siasa, wala kuhusika katika uchochezi wa fitina juu ya serikali, wala uvunjaji wa sheria. Kama alivyoandika Petro: “Mtu wa kwenu asiteswe kama mwuaji, au mwivi, au mtenda mabaya . . . Lakini ikiwa kwa sababu ni Mkristo asione haya, bali amtukuze Mungu katika jina hilo.” (1 Pet. 4:15, 16) Kwa hiyo Wakristo hawateswi kwa sababu ya ubaya wo wote kama huo katika kizazi hiki, bali kwa sababu ya kuzishika kwa bidii amri za Mungu na kushiriki katika kazi ya kumtolea Yesu ushuhuda. (Ufu. 12:17) Si ajabu basi kwamba, katika zaidi ya nchi 40 kati ya zile 210 ambako Mashahidi wa Yehova walishughulika sana mwaka jana wakiuhubiri ufalme wa Mungu, kumekuwa na vizuizi au upinzani kwa kazi hiyo, kama vile kuzuiwa wasiwe na makusanyiko ya watu wote, au kukatazwa wasiende nyumba kwa nyumba, au kukataliwa kisheria kwa kazi au kunyimwa ruhusa ya kuingiza vitabu fulani nchini, au kukatazwa kuandikisha ndoa kisheria, hata kupigwa marufuku kabisa na kutiwa gerezani kwa wenye kueleza wengine “habari njema.”
13. Kwa sababu gani Wakristo wa kweli wanachukiwa na Ulimwengu?
13 Kama Yesu alivyosema, wafuasi wake ‘wangechukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu.’ (Mt. 24:9) Bila shaka Wakristo wa jina tu hawachukiwi, wale ambao ni ‘rafiki za ulimwengu,’ wenye kuunga mkono taratibu ya kale na mipango yake, hata wanapokwenda kinyume sana cha kanuni za Maandiko. (Yak. 4:4) Lakini wanaofuata maagizo ya Yesu, wanaojifanya “si wa ulimwengu,” wanachukiwa. Kabla tu ya kufa kwake Yesu alitayarisha wafuasi wake kwa mambo ambayo yangekuja na upinzani ambao wangepatwa nao, si katika karne hiyo tu, bali pia katika siku za mwisho, aliposema hivi: “Haya nawaamuru ninyi, mpate kupendana. Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi . . . Lakini litimie lile neno lililoandikwa katika torati yao, Walinichukia bure.”—Yohana 15:17-25.
14. Ni kwa njia gani Mashahidi katika nchi moja wamewekwa chini ya mkazo?
14 Kwamba chuki hiyo ipo nyakati za kisasa yaweza kuonekana kutokana na ripoti zifuatazo kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu. Mashahidi katika nchi moja ya wasema-Kispania waripoti hivi: “Tunashambuliwa kutoka pande zote, katika radio, katika televisheni, katika magazeti, katika sehemu za wafanya kazi, mahospitalini, barabarani, katika shule, hata jumba baada ya jumba. Rafiki wengi hawana kazi. Sisi ni kama Waisraeli walipokuwa Misri. Twaendelea kutia rafiki moyo waendelee kuzihubiri habari njema kwa sababu hakuna shetani wala mwanadamu anayeweza kuzikomesha.” Walakini, akina ndugu wanapatwa na magumu makali. Wazazi wametiwa gerezani kuanzia miezi mitatu mpaka mwaka mmoja kwa sababu watoto wao wamekataa kushiriki katika sherehe za bendera. Wamefuata kwa imara mwendo wa Waebrania waaminifu wanaotajwa katika sura ya tatu ya Danieli. Suala hilo limehusu visa visivyopungua elfu moja. Kulingana na sheria, watoto wanaweza kutolewa kwa wazazi wao mahakimu wakiona inafaa. Mama waja wazito wamefungwa na kufanyiwa mambo mabaya ya namna zote kinyume cha sheria, tena wamelazimishwa kuacha watoto wao nyumbani huku wenye kuwafanyia hivyo wakijitahidi kukomesha mama hao wasifundishe watoto wao Neno la Mungu.—Kut. 20:4, 5.
15. Akina ndugu wamelazimika kuvumilia majaribu na magumu gani, nao wametiwaje nguvu?
15 Ndugu mmoja mwenye umri wa miaka 57 alishtakiwa juu ya kuongoa watu akatozwa faini ya dola 100 (shilingi 800 au 50Z). Dada wa miaka kumi na tisa alihukumiwa kifungo cha mwezi mmoja kwa sababu iyo hiyo. Wengi wameshtakiwa juu ya kujaribu kuchochea chuki juu ya idara ya Amerika ya uchunguzi wa uvunjaji wa sheria iitwayo Central Intelligence Agency. Mara nyingi ndugu wanakamatwa kwa sababu ya kuwa na “mikutano haramu,” nyakati nyingine hata wakikamatwa kwa shtaka hilo usiku sana wakati watu wote nyumbani wamelala. Wengine wamefungwa kwa sababu wamekataa utumishi wa jeshi kulingana na dhamiri zao. Wengi wamepigwa au wakalazimishwa kufanya kazi saa nyingi mashambani. Ndugu watatu walihukumiwa kifungo cha miaka miwili kwa kukataa kupalilia tumbako kwa sababu ya dhamiri zao. Serikali hairuhusu watoto wa Mashahidi wa Yehova wahudhurie mikutano wakapate mafundisho ya kidini. Majumba ya Ufalme yamefungwa na vizuizi vya namna zote vikawekwa juu ya mikutano ya Kikristo ili watu walioanza kupendezwa karibuni na wachanga wasiweze kupokea mafundisho ya Neno la Mungu. Hata hivyo akina ndugu wanaandika hivi: “Yehova Mungu wetu ndiye tunayetumaini. Yehova hupenda sana watu wake naye huonyesha uwezo wake kwa njia ya ajabu.”
16. Kwa sababu gani akina ndugu wamekuwa na nia ya kufungwa, nao wametumiaje hali hiyo kumletea Yehova sifa?
16 Katika nchi nyingine ambako kazi imepigwa marufuku ndugu wengine walipanga kusafiri kwenye nchi ya karibu wakafurahie programu ya kusanyiko. Walakini, waliporudi, kumi na mmoja kati yao walipigwa wakatiwa gerezani kwa siku mbili. Ndugu mmoja aliyewatembelea huko alikamatwa akanyang’anywa vitabu vya mafunzo ya Biblia. Baada ya kukaa gerezani kwa muda mwishowe alifukuzwa nchini. Usiku uliotangulia kuondoka kwake kituo cha huko cha televisheni kikatangaza kwamba dini zote zi huru katika nchi hiyo, lakini Mashahidi wa Yehova hawakutajwa. Ndugu saba walitiwa gerezani miezi kadha katika nchi hiyo, lakini mwangalizi wa mzunguko alisema hivi: “Wana shughuli nyingi za kuhubiri habari njema kwa wafungwa wenzao.” Mipango ilifanywa ndugu hao wasaidiwe kwa chakula wasitaabike mno wakati wa kifungo chao.
17. Dini ya uongo imechocheaje fitina ndugu wengine wafungwe?
17 Mapainia wawili wa pekee walitiwa gerezani kwa sababu ya kazi yao ya kuhubiri katika nchi ambamo dini imekuwa na mamlaka sana juu ya serikali mpaka hivi karibuni. Wanasema kwamba makusanyiko hayawezi kufanywa nchini, na barabarani vituo vya uchunguzi vimepewa amri kali sana kutowezesha mtu ye yote kuondoka nchini akafurahie kusanyiko la kwingineko. Barua ya kutoka huko yasema: “Ijapokuwa inasemekana kila raia ana uhuru wa kipekee, Wakristo kadha walitiwa gerezani kwa sababu ya kuhubiri mambo ya Biblia tu, kwa maana huo waonwa kuwa utendaji mkatili kwa kanisa. Tulipokea habari kwa makundi yasiyopungua matatu ambako vikundi vya akina ndugu vilikamatwa wakati wa utumishi wao wa nyumba kwa nyumba, wakati wa mikutano, na hata wakiwa nyumbani kwao. Wengine waliambiwa wangeachiliwa wakitoa faini kwa sababu wamehubiri mambo yasiyopatana na mafundisho ya kanisa. Walipendelea kukaa gerezani badala yake, wakaihesabu kuwa heshima kuteswa kwa ajili ya Kristo.”
18. Ni kwa sababu ya masuala gani Mashahidi wengine wamevumilia mapigo na kutiwa jelani kwa ushujaa?
18 Katika nchi nyingine ambako serikali imekataa kutambua kazi kisheria, akina ndugu wanaendelea na kazi yao ya kufundisha Biblia ingawa wanapingwa sana. Kwa sababu ya kutohusika katika siasa, kutonunua kadi za chama cha kisiasa au kuimba nyimbo za kisiasa, ndugu na dada wengi wamepigwa vibaya sana na zaidi ya 500 wakatiwa jelani. Mwangalizi wa mzunguko alipotembelea eneo moja lenye upinzani mkali, alipigwa vibaya hata akazimia, lakini hakuacha kutia akina ndugu moyo na kuwajenga. Alipoambiwa lazima alipe faini, alieleza hivi: “Wale ambao mmetia kizuizini pamoja nami ndio wanaonipa nyumba, chakula na ndio ndugu zangu, sasa nitoe wapi pesa za kulipa faini?” Hata walipoogofywa sana, mmoja wa ndugu hawa alisema hivi: “Lo! ni pendeleo namna gani kujaribu imani yangu na kuona unabii mbalimbali ukitimia!”
19. Mashahidi walifanyiwa vitisho gani walipofunguliwa, lakini wameitikiaje?
19 Kati ya wale 502 waliotiwa kizuizini 124 walikuwa wanawake na 21 kati yao walikuwa waja wazito. Mtoto wa dada mmoja aliyezaliwa gerezani kwa sababu ya mateso alipewa jina la kumfaa “Mateso.” Wakati wa kifungo chao akina ndugu hawakulishwa sawasawa isipokuwa na watoto wao wenyewe waliowaletea chakula. Walipoachiliwa mwishowe, walionywa wasilime mashamba yao. Waliambiwa hivi pia: “Msionekane mkiwa wawili wala watatu mahali pamoja. Msionekane mkiwa na trakti, vijitabu, vitabu wala mkiimba nyimbo za dini yenu. Msionekane mkisali. Jina la Yehova lisisikiwe kwenu. Msionekane mkifanya mikutano. Msiwe mkiitana ‘ndugu.’ “(Linganisha Danieli 6:7, 10.) Ijapokuwa hayo yote yametokea, akina ndugu hawakuacha. Walikaza nia wakutane pamoja vikundi vikundi katika nyakati mbalimbali na siku mbalimbali. Ijapokuwa mateso hayo yametokea katika eneo hilo, ushuhuda mkubwa sana umetolewa maana watu wanaona Mashahidi wa Yehova hawalipi kisasi juu ya wenye kuwatesa.—Rum. 12:17-21; 1 Kor. 10:13.
20. (a) Kwa sababu gani tusihesabu maisha zetu kuwa zenye thamani mno? (b) Watakaotokea wakiwa washindi wana matumaini ya ajabu ya kupata nini?
20 Kwa hiyo katika ulimwengu mzima Yehova ana watu waaminifu, vijana na wazee pia, ambao wameonyesha uthabiti na kujitoa kwao wakiwa chini ya majaribu, bila kuhesabu maisha zao kuwa zenye thamani mno wanapokabiliwa na kifo. Tuwe tunapingwa na jamaa au rafiki au hata kuteswa sana na vyanzo vingine, jambo la maana ni kumtumaini Yehova. Ingawa watu mmoja mmoja wanaweza kufa kama Stefano na Paulo, Shetani na mawakili wake hawatafutilia mbali kamwe watu wa Mungu. Bali, Ufunuo watabiri waziwazi kwamba “mkutano mkubwa” wa watumishi waaminifu wa Yehova watasalimishwa wapite “dhiki kubwa,” wakihakikisha wamejitoa kwa Mungu kwa kumtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku. Badala ya kuogopa sasa ghadhabu ya Shetani au ya mwanadamu ye yote, yatupasa tuhangaikie kuendelea kuwa na upendeleo wa Yehova na kutokuwa kati ya wale watakaopigwa na miale mikali ya “jua” au “hari” ya hasira ya Mungu. Ni afadhali zaidi kuendelea kufurahia uongozi wenye mafaa wa Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye ameahidi kuchunga wanadamu waaminifu, akiwaongoza kwenye chemchemi za maji ya uzima. Huko “Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao” wakati mateso na chuki za taratibu ya sasa zitakapoondolewa zisiwapate tena.—Ufu. 7:14-17.
—Kutoka The Watchtower, May 1, 1976.