Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 11/15 kur. 509-511
  • Uwezo Wenye Kuharibu wa Wivu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uwezo Wenye Kuharibu wa Wivu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Habari Zinazolingana
  • Unalopaswa Kujua Juu ya Wivu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Upendo Hushinda Wivu Usiofaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Daudi na Sauli
    Masomo Unayoweza Kujifunza Katika Biblia
  • Sababu Yampasa Daudi Akimbie
    Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 11/15 kur. 509-511

Uwezo Wenye Kuharibu wa Wivu

WIVU unaweza kumaanisha juhudi inayofaa kwa yaliyo haki. Kwa mfano, Yehova Mungu ni mwenye wivu kwa jina lake jema, ndivyo na watumishi wake waliojitoa. (Kut. 34:14; 1 Fal. 19:10,14; Eze. 39:25) Walakini, mara nyingi mno wivu huwa na kusudi baya au huelekea upande mbaya. Huenda mwenye wivu akatilia wengine mashaka bila sababu au kuchukia wengine wanapofanyiwa mema, akijiona kwamba yeye peke yake ndiye anayestahili kutendewa hivyo.

Wivu usiofaa una uwezo wenye kuharibu. Unaweza kumfanya mtu asitosheke na kukuza hasira na chuki. Madaktari wameona kwamba wivu waweza kudhuru sana. Mtu mwenye wivu hata aweza kufikia hatua ya kukosa usingizi nyakati za usiku, aweza kutapika, kupatwa na masumbufu ya tumbo au mmojawapo wa magonjwa mengine mengi. Ni kama vile mithali ya Biblia isemavyo: “Husuda [wivu] ni ubovu wa mifupa.”​—⁠Mit. 14:30.

Wivu huo unaweza kuharibu pia uhusiano bora. Hiyo yaonyeshwa vizuri katika habari ya Mfalme Sauli wa Israeli na raia wake thabiti Daudi.

Ushujaa wa Daudi wa kumwendea Mfilisti jitu Goliathi na kumshinda kwa kombeo la mchungaji ulimshangaza Sauli. Kwa hiyo alimweka Daudi asimamie mashujaa. Akiwa katika cheo hicho, Daudi aliunga mkono kwa uthabiti ufalme wa Sauli akapata ushindi mwingi sana juu ya Wafilisti. Mwishowe Daudi alipata kusifiwa kwa nyimbo hata zaidi kuliko Mfalme Sauli. Walipokuwa wakiwalaki mashujaa washindi wenye kurudi, wanawake Waisraeli walikuwa wakidansi na kuimba hivi: “Sauli amewaua elfu zake, na Daudi makumi elfu yake.” Sauli alichukizwa sana na jambo hilo, akiona kwamba heshima ambayo angalipaswa kupewa yeye kama mfalme ilienda kwa Daudi. Hiyo ilimfanya Sauli amtilie Daudi mashaka​—⁠akimwona kuwa mshindani mwenye kutaka kiti cha ufalme.​—1 Sam. 17:57, 58; 18:5-9.

Uhusiano mwema uliokuwamo wakati mmoja kati ya Sauli na Daudi ulikoma. Ingawa hakukuwa na sababu yo yote ya kumtilia mashaka, Sauli hakumtumaini Daudi tena. Alishikilia wazo la kwamba Daudi alikuwa hatari kwa ufalme wake. Sauli alikaza nia amwue. Kwa hiyo, Daudi alilazimika kuwa mtoro, akamkimbia Sauli aokoe maisha yake.​—1 Sam. 18:10-25; 19:9-12.

Namna ya wivu ambao Mfalme Sauli alimwonyesha Daudi yaweza kuepukwa. Kwa njia gani? Yampasa mtu awe mwangalifu asihangaikie mno cheo chake, uwezo wake mbalimbali wa kufanya mambo au sifa yake. Watu wasifupo wengine mtu akiwapo, asiamue kwamba wanajaribu kwa makusudi kushusha mambo yake mwenyewe aliyotimiza. Hata ikiwa maelezo yanaelekea kuwapa wengine sifa ya kutimiza mambo makubwa zaidi kuliko yeye, kama vile wanawake walivyosema juu ya Daudi, mtu asisahau kwamba mambo mengi husemwa kwa uaminifu bila wazo la kulinganisha watu. Hasa maneno yale yanayosemwa kwa sababu ya shauku ya wakati huo yapaswa kueleweka kwa kufikiria hali za wakati huo na hayawezi kuchukuliwa kama yenye kulinganisha watu kwa ubaya. Kwa hiyo, ni jambo la kusikitisha mtu akichukia mwingine kwa sababu ya maneno hayo.

Biblia yaonyesha kwamba upendo ni wa lazima ili kushinda wivu. Katika Maandiko, twasoma hivi: “Upendo hauhusudu [hauoni wivu].” (1 Kor. 13:4) Ikiwa mtu ana maelekeo ya kutilia wengine mashaka au kuwachukia kwa sababu ya heshima wanayopewa, ingemfaa apate kuwajua wale anaowaonea wivu. Imempasa ajaribu kuona sifa zao njema na kujitahidi kuthamini wanayofanya. Badala ya kuwa na maoni ya kwamba wengine wanafanya mambo anayotimiza yasionekane, yampasa awe na nia ya kuona sifa ikitolewa inapofaa. Kwa wazi hakuna mtu mmoja ye yote anayeweza kufanya kila jambo. Unyenyekevu na kuwaza kwa utimamu kwapaswa kutuonyesha kwamba ni baraka wakati kunapokuwa na watu wengi wenye kustahili kuchukua madaraka.

Bila shaka mwanamume Musa alikuwa na nia ifaayo katika habari hii. Wakati Eldadi na Medadi walipopokea roho ya Mungu bila ya Musa kuwapo wakaanza kutoa unabii katika kambi ya Israeli, Yoshua, mtumikiaji wa Musa, aliona wivu kwa ajili ya “bwana” wake. Yoshua aliona kwamba kutabiri kwao kulifanya watu wasione mamlaka ya Musa na kwamba walipaswa kuzuiwa. Lakini Musa hakuona wivu kwamba si yeye peke yake tena aliyekuwa na roho ya Mungu ndani yake ikitenda kwa njia ya pekee. Alimsahihisha Yoshua kwa maneno haya: “Ingekuwa heri kama watu wote wa [Yehova] wangekuwa manabii, na kama [Yehova] angewatia roho yake.”​—⁠Hes. 11:10-29.

Lakini namna gani ikiwa mtu anayesifiwa sana hata hastahili kusifiwa? Namna gani ikiwa amesifiwa kupita kiasi? Bila shaka, hilo laweza kutukia. Mwandikaji wa Mhubiri mwenye ufahamu alisema hivi: “Liko baa nililoliona chini ya jua, nalo ni kama kosa litokalo kwake yeye atawalaye; ya kuwa upumbavu huwekwa mahali pa juu sana, nao wakwasi [matajiri] hukaa mahali pa chini. Mimi nimeona watumwa wamepanda farasi, na wakuu wakienda kwa miguu juu ya nchi kama watumwa.”​—⁠Mhu. 10:5-7.

Kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu, maafisa, matajiri wa kazi na wengine wenye mamlaka hufanya makosa makubwa katika uamuzi. Huenda wakawapa heshima ndogo wale ambao wametia bidii na walio “wakuu” au bora katika nia na njia zao, wakiwatendea kama watumishi tu. Wakati uo huo, huenda wakapendelea watu wasiostahili sana. Hiyo yaweza kuudhi sana.

Hata hivyo, kusingekuwa na faida ya kuudhika sana juu ya mambo hayo. Hiyo ingeondolea mtu tu amani ya akili na moyo. Yaweza pia kuharibu afya ya mtu. Ni afadhali zaidi kungojea kwa saburi. Mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu alionya hivi kwa upole: “Umngojee [Yehova] kwa saburi; usimkasirikie yeye afanikiwaye katika njia yake.” (Zab. 37:7) Katika wakati ufaao hata wenye kufanya kosa hilo huenda wakalazimika kuuona upumbavu wao.

Yatupasa tujitahidi pia kuepuka kuchochea wivu ndani ya wengine. Wanawake Waisraeli waliomshangilia Daudi kwa nyimbo kwa sababu ya matendo yake hodari kwa wazi hawakujua hiyo ingechochea wivu mwingi sana ndani ya Mfalme Sauli. Hata hivyo kama wangalifikiria sana jambo hilo, wangalikuwa waangalifu zaidi wasionekane kama kwamba walikuwa wakiheshimu zaidi raia wa mfalme kuliko mfalme mwenyewe. Tukijua watu hawajakamilika, yatupasa tujiangalie tunaposifu mtu au mambo aliyotimiza mbele ya mwingine. Yatupasa tuhakikishe kwamba tunayosema hayataelekea kuchukuliwa na msikilizaji kuwa na maana ya kwamba yeye analinganishwa isivyofaa na yule anayesifiwa sana.

Tukifikiria vile wivu usiofaa unavyoweza kudhuru, yatupasa kujizuia wenyewe tusiwe nao na kuepuka kuuchochea ndani ya wengine. Kwa kusudi hilo, yatupasa tujitahidi kusitawisha upendo mwingi zaidi kwa namna zote za watu, tukithamini sifa zao njema na mambo wanayotimiza. Yatupasa pia tufikirie maneno na matendo yetu yanaweza kuwa na matokeo gani juu ya wengine. Hiyo itatufurahisha sana na itasaidia kuendeleza uhusiano mwema na wanadamu wenzetu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki