Upendo Hushinda Wivu Usiofaa
“Upendo hauna wivu.”—1 WAKORINTHO 13:4, NW.
1, 2. (a) Yesu aliwaeleza wanafunzi wake nini kuhusu upendo? (b) Je, yawezekana kuwa na upendo na pia kuona wivu, na kwa nini unajibu hivyo?
UPENDO ni ishara ya kutambulisha Ukristo wa kweli. “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi,” akasema Yesu Kristo. (Yohana 13:35) Mtume Paulo alipuliziwa kueleza jinsi upendo unavyopasa kuathiri mahusiano ya Kikristo. Miongoni mwa mambo mengine, aliandika: “Upendo hauna wivu.”—1 Wakorintho 13:4, NW.
2 Paulo alipoandika maneno hayo, alikuwa akirejezea wivu usiofaa. Ama sivyo hangeliambia kutaniko hilohilo hivi: “Nawaonea wivu, wivu wa Mungu.” (2 Wakorintho 11:2) ‘Wivu wake wa Mungu’ ulichochewa kwa sababu ya watu waliokuwa na uvutano wenye kufisidi kutanikoni. Wivu huu ulimsukuma Paulo aandikie Wakristo Wakorintho barua ya pili iliyopuliziwa yenye shauri lenye upendo sana.—2 Wakorintho 11:3-5.
Wivu Miongoni mwa Wakristo
3. Tatizo lililohusu wivu lilitokeaje miongoni mwa Wakristo Wakorintho?
3 Katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, Paulo alilazimika kushughulikia tatizo lililokuwa likizuia Wakristo hawa wapya wasipatane. Wao walikuwa wakitukuza watu fulani, ‘wakijivuna kwa ajili ya huyu, kinyume cha mwenziwe.’ Hilo lilitokeza migawanyiko katika kutaniko, watu tofauti-tofauti wakisema: “Mimi ni wa Paulo,” “Mimi ni wa Apolo,” “Mimi ni wa Kefa.” (1 Wakorintho 1:12; 4:6) Akiongozwa na roho takatifu, mtume Paulo aliweza kugundua chanzo cha tatizo hilo. Wakorintho walikuwa wakitenda kama watu wenye fikira za kimwili, si kama “watu wa kiroho.” Hivyo, Paulo akawaandikia: “Bado nyinyi ni wa kimwili. Kwa maana kwa kuwa kuna wivu na zogo miongoni mwenu, je, nyinyi si wa kimwili na je, hamjiendeshi kama watu?”—1 Wakorintho 3:1-3, NW.
4. Paulo alitumia kielezi gani ili kusaidia ndugu zake kufikia maoni mazuri juu ya mmoja na mwenzake, nasi twaweza kujifunza somo gani kutokana nacho?
4 Paulo alisaidia Wakorintho kuwa na maoni mazuri juu ya vipawa na uwezo mbalimbali wa watu tofauti-tofauti katika kutaniko. Aliuliza: “Ni nani anayekupambanua na mwingine? nawe una nini usichokipokea? Lakini iwapo ulipokea, wajisifia nini kana kwamba hukupokea?” (1 Wakorintho 4:7) Katika 1 Wakorintho sura ya 12, Paulo alieleza kwamba wale waliokuwa washiriki wa kutaniko walikuwa kama viungo mbalimbali vya mwili wa binadamu, kama vile mkono, jicho, na sikio. Alitaja kwamba Mungu alifanyiza viungo vya mwili kwa njia ya kwamba vinatunzana. Paulo pia aliandika: “Kiungo kimoja kikitukuzwa, viungo vyote hufurahi pamoja nacho.” (1 Wakorintho 12:26) Watumishi wote wa Mungu leo wapaswa kutumia kanuni hii katika uhusiano wao na wengine. Badala ya kuonea wivu mtu mwingine kwa sababu ya mgawo wake au matimizo yake katika utumishi wa Mungu, tushangilie pamoja naye.
5. Ni nini kinachofunuliwa kwenye Yakobo 4:5, na Maandiko yakaziaje ukweli wa maneno haya?
5 Ni kweli, ni rahisi kusema kuliko kutenda. Mwandikaji wa Biblia Yakobo atukumbusha kwamba “mwelekeo wa kuhusudu” umo katika kila binadamu mwenye dhambi. (Yakobo 4:5, NW) Kifo cha binadamu wa kwanza kilitokea kwa sababu Kaini alishindwa na wivu usiofaa. Wafilisti walimnyanyasa Isaka kwa sababu walihusudu ufanisi wake wenye kukua. Raheli aliuonea wivu uwezo wa dada yake wa kuzaa watoto. Wana wa Yakobo waliuonea wivu upendeleo alioonyeshwa ndugu yao mdogo Yusufu. Yaonekana Miriamu alimwonea wivu wifi yake asiye Mwisraeli. Kwa husuda Kora, Dathani, na Abiramu walitunga hila dhidi ya Musa na Haruni. Mfalme Sauli alikuwa mwenye wivu kwa mafanikio ya kivita ya Daudi. Hakuna shaka kwamba wivu pia ulihusika katika kufanya wanafunzi wa Yesu kubishana kila mara juu ya ni nani aliyekuwa mkubwa zaidi kati yao. Hakika ni kwamba hakuna binadamu asiyekamilika ambaye hana kabisa ‘mwelekeo wenye dhambi wa kuhusudu.’—Mwanzo 4:4-8; 26:14; 30:1; 37:11; Hesabu 12:1, 2; 16:1-3; Zaburi 106:16; 1 Samweli 18:7-9; Mathayo 20:21, 24; Marko 9:33, 34; Luka 22:24.
Katika Kutaniko
6. Wazee wanaweza kudhibitije mwelekeo wa kuhusudu?
6 Wakristo wote wanahitaji kulinda dhidi ya husuda na wivu usiofaa. Hii yatia ndani mabaraza ya wazee waliowekwa rasmi kutunza makutaniko ya watu wa Mungu. Mzee akiwa na akili ya kujishusha, hatajaribu kwa udi na uvumba kushinda wengine. Kwa upande mwingine, mzee fulani akiwa na uwezo mbalimbali wenye kutokeza sana kama vile kuwa mratibu-mambo mzuri au msemaji bora wa peupe, wengine watashangilia juu ya hilo, wakiliona kuwa baraka kwa kutaniko. (Warumi 12:15, 16) Huenda ikawa ndugu anafanya maendeleo mazuri, akitoa uthibitisho wa kutokeza matunda ya roho ya Mungu maishani mwake. Wakati wa kufikiria ustahili wake, wazee wapaswa kuwa waangalifu wasikazie upungufu fulani kidogo ili kutetea hali yao ya kutompendekeza kuwa mtumishi wa huduma au mzee. Hilo laonyesha ukosefu wa upendo na pia hali ya kukubali sababu.
7. Ni tatizo gani linaloweza kutokea Mkristo apatapo migawo fulani ya kitheokrasi?
7 Mtu akipokea mgawo wa kitheokrasi au baraka ya kiroho, wengine kutanikoni wanahitaji kulinda dhidi ya husuda. Kwa mfano, dada mwenye uwezo anaweza kuwa anatumiwa kutoa maonyesho mara nyingi kuliko mwingine katika mikutano ya Kikristo. Hilo laweza kutokeza wivu kwa upande wa dada fulani. Huenda tatizo kama hilo lilikuwapo kati ya Euodia na Sintike wa kutaniko la Filipi. Wanawake kama hawa wa siku hizi huenda wakahitaji kitia-moyo chenye fadhili kutoka kwa wazee kuwa wanyenyekevu na kuwa wa “nia moja katika Bwana.”—Wafilipi 2:2, 3; 4:2, 3.
8. Wivu waweza kutokeza matendo gani yenye dhambi?
8 Mkristo anaweza kujua upungufu wa wakati uliopita wa yule ambaye sasa amebarikiwa na mapendeleo katika kutaniko. (Yakobo 3:2) Kwa sababu ya wivu, kunaweza kuwa na ushawishi wa kusema na wengine juu ya jambo hili na kutilia shaka mgawo wa huyo kutanikoni. Hili lingepinga upendo, ambao “husitiri wingi wa dhambi.” (1 Petro 4:8) Mazungumzo yenye wivu yaweza kuvuruga amani ya kutaniko. “Mkiwa na wivu wenye uchungu na ugomvi mioyoni mwenu,” akaonya mwanafunzi Yakobo, “msijisifu, wala msiseme uongo juu ya kweli. Hekima hiyo siyo ile ishukayo kutoka juu, bali ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani.”—Yakobo 3:14, 15.
Katika Familia Yako
9. Waume na wake wanaweza kudhibitije hisia za wivu?
9 Ndoa nyingi hazifaulu kwa sababu ya wivu usiofaa. Kukosa kutumainiana na mume au mke ni kukosa upendo. (1 Wakorintho 13:7) Kwa upande mwingine, mume au mke anaweza kukosa kutambua hisia za wivu wa yule mwingine. Kwa mfano, mke anaweza kuona wivu kwa sababu ya uangalifu ambao mume wake anampa mtu mwingine wa jinsia tofauti. Au mume anaweza kuona wivu kwa sababu ya wingi wa wakati ambao mke wake anatumia kutunza mtu wa ukoo mwenye uhitaji. Wakiona haya juu ya hisia hizo, waume na wake wanaweza kunyamaza na kuonyesha mifadhaiko yao katika njia zinazofanya tatizo hilo liwe gumu hata zaidi. Badala ya hivyo, mume au mke anayeona wivu anahitaji kuwasiliana na kuwa mnyoofu juu ya hisia zake. Naye yule mwingine anahitaji kuonyesha ufahamu na kumhakikishia upendo wake. (Waefeso 5:28, 29) Wote wawili wanaweza kuhitaji kuondoa hisia za wivu kwa kuepuka hali zinazoleta hisia hizo. Nyakati nyingine mwangalizi Mkristo anaweza kuhitaji kusaidia mke wake kufahamu kwamba anatoa uangalifu kidogo na ufaao kwa watu wa jinsia tofauti ili kutimiza daraka lake akiwa mchungaji wa kundi la Mungu. (Isaya 32:2) Bila shaka, mzee anapaswa kuwa mwangalifu asitokeze sababu yoyote halali ya kutokeza wivu. Hilo lahitaji usawaziko, akihakikisha kwamba anatumia wakati kuimarisha uhusiano wake mwenyewe wa ndoa.—1 Timotheo 3:5; 5:1, 2.
10. Wazazi wanaweza kusaidiaje watoto wao kukabili hisia zao wa wivu?
10 Ni lazima wazazi pia wasaidie watoto wao wafahamu wazo la wivu usiofaa. Mara nyingi watoto huhusika katika mabishano yatokezayo mapigano. Mara nyingi chanzo huwa ni wivu. Kwa sababu mahitaji ya kila mtoto ni ya kipekee, watoto hawawezi kutendewa kwa njia iliyo sawa. Isitoshe, watoto wanahitaji kufahamu kwamba kila mmoja wao ana sifa na udhaifu tofauti-tofauti. Mtoto mmoja sikuzote akitiwa moyo kufanya kama yule mwingine, hiyo yaweza kusitawisha husuda kwa mmoja na kiburi kwa mwingine. Hivyo, wazazi wanapaswa kuzoeza watoto wao kupima maendeleo yao kwa kufikiria vielelezo vilivyomo katika Neno la Mungu, si kwa kushindana. Biblia yasema: “Tusijisifu bure, tukichokozana na kuhusudiana.” Badala ya hivyo, “kila mtu na aipime kazi yake mwenyewe, ndipo atakapokuwa na sababu ya kujisifu ndani ya nafsi yake tu, wala si kwa mwenzake.” (Wagalatia 5:26; 6:4) Jambo la maana zaidi, wazazi Wakristo wanahitaji kusaidia watoto wao kupitia funzo la Biblia la kawaida, wakikazia vielelezo vizuri na vibaya vilivyomo katika Neno la Mungu.—2 Timotheo 3:15.
Vielelezo vya Kushinda Wivu
11. Musa alikuwaje kielelezo kizuri cha kushughulikia wivu?
11 Tofauti na viongozi wa ulimwengu huu wenye kutamani mamlaka, ‘Musa alikuwa mnyenyekevu sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.’ (Hesabu 12:3) Uongozi juu ya Waisraeli ulipokuwa mzigo kwa Musa kuubeba peke yake, Yehova alifanya roho Yake itende juu ya Waisraeli wengine 70, ikiwapa uwezo wa kumsaidia Musa. Wawili kati ya wanaume hawa walipoanza kutenda kama manabii, Yoshua alihisi kwamba jambo hilo lilikengeusha isivyofaa kutoka kwa uongozi wa Musa. Yoshua alitaka kuzuia wanaume hawa, lakini Musa alisababu hivi kwa unyenyekevu: “Je! umekuwa na wivu kwa ajili yangu; ingekuwa heri kama watu wote wa BWANA wangekuwa manabii, na kama BWANA angewatia roho yake.” (Hesabu 11:29) Ndiyo, Musa alifurahi wengine walipopokea mapendeleo ya utumishi. Yeye hakujitakia utukufu mwenyewe kwa wivu.
12. Ni nini kilichomwezesha Yonathani kuepuka hisia za wivu?
12 Kielelezo kizuri cha jinsi upendo hushinda hisia zisizofaa za wivu kiliandaliwa na Yonathani, mwana wa Mfalme wa Israeli Sauli. Yonathani alikuwa awe mrithi wa baba yake katika utawala, lakini Yehova alikuwa amemchagua Daudi, mwana wa Yese, kuwa mfalme ambaye angefuata. Wengi katika hali ya Yonathani wangalimwonea wivu Daudi, wakimwona kuwa mpinzani wao. Lakini upendo wa Yonathani kwa Daudi ulizuia hisia hiyo isipate kumshinda. Aliposikia juu ya kifo cha Yonathani, Daudi alisema: “Nimesikitika kwa ajili yako, Yonathani, ndugu yangu, ulikuwa ukinipendeza sana; upendo wako kwangu ulikuwa wa ajabu, kupita upendo wa wanawake.”—2 Samweli 1:26.
Vielelezo Vyenye Kutokeza Zaidi
13. Ni nani aliye kielelezo bora zaidi kwa habari ya wivu, na kwa nini?
13 Yehova Mungu ndiye kielelezo chenye kutokeza zaidi cha kushinda hata wivu ufaao. Yeye amedhibiti hisia hizo kikamilifu. Wonyesho wowote wenye nguvu wa wivu wa kimungu sikuzote hupatana na upendo, haki, na hekima ya Mungu.—Isaya 42:13, 14.
14. Ni kielelezo gani alichoweka Yesu akiwa tofauti na Shetani?
14 Kielelezo cha pili chenye kutokeza cha kushinda hisia za wivu ni Mwana-mpendwa wa Mungu, Yesu Kristo. “Alikuwa yuna namna ya Mungu,” Yesu “hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho.” (Wafilipi 2:6) Ni mwendo tofauti kama nini na ule uliochukuliwa na malaika mwenye kutaka makuu aliyekuja kuwa Shetani Ibilisi! Kama “mfalme wa Babeli,” kwa wivu Shetani alitamani ‘kufanana na yeye Aliye juu’ akijiweka kuwa mungu mpinzani dhidi ya Yehova. (Isaya 14:4, 14; 2 Wakorintho 4:4) Shetani hata alijaribu kumfanya Yesu ‘aanguke chini na kumfanyia tendo la ibada.’ (Mathayo 4:9, NW) Lakini hakuna kitu ambacho kingemkengeusha Yesu atoke kwenye mwendo wake mnyenyekevu wa kunyenyekea enzi kuu ya Yehova. Tofauti na Shetani, Yesu ‘alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam mauti ya mti wa mateso.’ Yesu alitegemeza haki ya Baba yake ya kutawala, akipinga kabisa mwendo wa Ibilisi wa kiburi na wivu. Kwa sababu ya uaminifu wa Yesu, ‘Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba.’—Wafilipi 2:7-11.
Kuushinda Wivu Wako
15. Kwa nini ni lazima tuwe waangalifu kudhibiti hisia za wivu?
15 Tofauti na Mungu na Kristo, Wakristo si wakamilifu. Wakiwa wenye dhambi, nyakati nyingine wanaweza kutenda kwa wivu wenye dhambi. Basi, badala ya kuruhusu wivu utusukume kuchambua mwamini mwenzetu juu ya upungufu fulani kidogo au juu ya jambo tunalowazia kuwa ni kosa, ni muhimu kutafakari maneno haya yaliyopuliziwa: “Usiwe na haki kupita kiasi; wala usijiongezee hekima mno; kwani kujiangamiza mwenyewe?”—Mhubiri 7:16.
16. Ni shauri gani zuri juu ya wivu lililotolewa katika toleo la zamani la gazeti hili?
16 Kwa habari ya wivu, The Watch Tower la Machi 15, 1911, lilitahadharisha hivi: “Ingawa twapaswa kuwa wenye bidii sana, wenye wivu sana kwa ajili ya makusudi ya Bwana, lakini ni lazima tuhakikishe kabisa kwamba [upungufu] wa mwingine ni jambo la kibinafsi; nasi twapaswa kufikiria ikiwa sisi ni ‘watu wa kushughulikia mambo ya watu wengine’ au hapana. Kisha, pia twapaswa kufikiria iwapo linafaa kwa wazee kulishughulikia jambo hilo na iwapo ni jukumu letu kwenda kwa wazee au hapana. Sote twapaswa kuona wivu sana kwa ajili ya makusudi ya Bwana na kazi ya Bwana, lakini tuwe waangalifu kwamba hatuoni wivu ule wenye uchungu . . . yaani, twapaswa kuhakikisha kabisa kwamba si kuonea wivu yule mwingine, bali wivu kwa ajili ya mwingine, kwa ajili ya mapendezi na hali-njema yake.”—1 Petro 4:15.
17. Tunaweza kuepukaje matendo ya dhambi ya wivu?
17 Sisi tukiwa Wakristo, twaweza kuepukaje kiburi, wivu, na husuda? Suluhisho ni kuruhusu mtiririko usiozuiliwa wa roho takatifu ya Mungu maishani mwetu. Kwa kielelezo, twahitaji kusali kwa ajili ya roho ya Mungu na msaada katika kuonyesha matunda yayo mazuri. (Luka 11:13) Twahitaji kuhudhuria mikutano ya Kikristo, ambayo hufunguliwa kwa sala ili iwe na roho ya Mungu na baraka yake. Isitoshe, twahitaji kujifunza Biblia, iliyopuliziwa na Mungu. (2 Timotheo 3:16) Twahitaji pia kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme ambayo hufanywa kwa uwezo wa roho takatifu ya Yehova. (Matendo 1:8) Kusaidia Wakristo wenzao ambao wamepondeka kutokana na maono fulani mabaya ni njia nyingine ya kunyenyekea uvutano mzuri wa roho ya Mungu. (Isaya 57:15; 1 Yohana 3:15-17) Kutimiza wajibu huo mbalimbali wa Kikristo kutasaidia kutulinda dhidi ya matendo ya dhambi ya wivu, kwa sababu Neno la Mungu lasema hivi: “Enendeni kwa Roho, wala hamtatimiza kamwe tamaa za mwili.”—Wagalatia 5:16.
18. Kwa nini hatutalazimika sikuzote kujitahidi dhidi ya hisia zisizofaa za wivu?
18 Upendo unaorodheshwa kwanza miongoni mwa matunda ya roho takatifu ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23) Kudhihirisha upendo kutatusaidia kudhibiti mielekeo yenye dhambi sasa. Lakini vipi juu ya wakati ujao? Mamilioni ya watumishi wa Yehova wana tumaini la kupata uhai katika Paradiso ya kidunia inayokuja, ambako wao wanaweza kutazamia kuinuliwa hadi ukamilifu wa kibinadamu. Katika ulimwengu huo mpya, upendo utaenea na hakuna mtu atakayeshindwa na hisia zisizofaa za wivu, kwa kuwa “viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.”—Warumi 8:21.
Mambo ya Kutafakari
◻ Paulo alitumia kielezi gani ili kusaidia kukinza wivu?
◻ Wivu unaweza kuvurugaje amani ya kutaniko?
◻ Wazazi wanaweza kuzoezaje watoto wao kukabili wivu?
◻ Tunaweza kuepukaje matendo ya dhambi ya wivu?
[Picha katika ukurasa wa16]
Usiache wivu uvuruge amani ya kutaniko
[Picha katika ukurasa wa17
Wazazi wanaweza kuzoeza watoto wao kukabili hisia za wivu