Wivu kwa Ajili ya Ibada Safi ya Yehova
“BWANA, ambaye jina lake ni mwenye wivu, ni Mungu mwenye wivu.”—KUTOKA 34:14.
1. Sifa kuu ya Mungu ni nini, nayo inahusikaje na wivu wake?
YEHOVA ajifafanua kuwa “Mungu mwenye wivu.” Huenda ukashangaa ni kwa nini yuko hivyo, kwa kuwa neno “wivu” linaleta wazo hasi. Bila shaka sifa kuu ya Mungu ni upendo. (1 Yohana 4:8) Kwa hiyo hisia zozote za kuona wivu kwa upande wake ni lazima ziwe za hali njema ya wanadamu. Hata tutaona kwamba wivu wa Mungu ni muhimu kwa amani na upatano wa ulimwengu wote mzima.
2. Ni zipi baadhi ya njia za kutafsiri maneno ya Kiebrania yanayomaanisha “wivu”?
2 Maneno ya Kiebrania yanayohusiana na “wivu” hutukia zaidi ya mara 80 katika Maandiko ya Kiebrania. Karibu nusu ya marejezo hayo humrejezea Yehova Mungu. “Unapotumiwa kumhusu Mungu,” aeleza G. H. Livingston, “wazo la wivu halina maana ya hisia-moyo iliyo mbaya, bali, lenye kusisitiza ibada ya Yehova peke yake.” (The Pentateuch in Its Cultural Environment) Hivyo, nyakati nyingine New World Translation hutafsiri nomino ya Kiebrania kuwa “-enye kusisitiza ujitoaji usiohusisha mwingine.” (Ezekieli 5:13) Tafsiri nyingine zifaazo ni “juhudi” au “bidii.”—Zaburi 79:5; Isaya 9:7.
3. Ni katika njia zipi ambazo wivu nyakati nyingine waweza kutumika kwa kusudi zuri?
3 Mwanadamu aliumbwa na uwezo wa kuona wivu, lakini kuanguka kwa mwanadamu katika dhambi kumetokeza kupotoshwa kwa wivu. Hata hivyo, wivu wa kibinadamu waweza kutumika kwa kusudi zuri. Unaweza kumsukuma mtu alinde mpendwa wake kutokana na uvutano mbaya. Isitoshe, wanadamu wanaweza kwa kufaa kuonyesha wivu kwa Yehova na ibada yake. (1 Wafalme 19:10) Ili kutoa uelewevu sahihi wa wivu huo kwa Yehova, nomino ya Kiebrania yaweza kutafsiriwa “kutovumilia ushindani wowote” kumwelekea.—2 Wafalme 10:16, NW.
Yule Ndama wa Dhahabu
4. Ni amri ipi inayohusu wivu wenye uadilifu iliyotokeza sana katika Sheria ya Mungu kwa Israeli?
4 Kielelezo kimoja cha wivu wenye uadilifu ni kile kilichotendeka baada ya Waisraeli kupokea Sheria kwenye Mlima Sinai. Kwa kurudia-rudia, walikuwa wameonywa wasiabudu miungu iliyofanyizwa na wanadamu. Yehova aliwaambia: “Mimi Yehova Mungu wako ni Mungu anayedai ujitoaji usiohusisha mwingine [au, “Mungu mwenye wivu (bidii); Mungu asiyevumilia upinzani”].” (Kutoka 20:5 NW, kielezi-chini; linganisha Kutoka 20:22, 23; 22:20; 23:13, 24, 32, 33.) Yehova alifanya agano pamoja na Waisraeli, akiahidi kuwabariki na kuwaingiza katika Bara Lililoahidiwa. (Kutoka 23:22, 31) Nao watu walisema: “Hayo yote aliyoyanena BWANA tutayatenda, nasi tutatii.”—Kutoka 24:7.
5, 6. (a) Waisraeli walitendaje dhambi iliyo nzito sana walipokuwa wamepiga kambi kwenye Mlima Sinai? (b) Yehova na waabudu wake waaminifu-washikamanifu walionyeshaje wivu wenye uadilifu katika Sinai?
5 Hata hivyo, upesi Waisraeli walitenda dhambi dhidi ya Mungu. Walikuwa wangali wamepiga kambi chini ya Mlima Sinai. Musa alikuwa amekuwa mlimani kwa siku nyingi, akipokea maagizo zaidi kutoka kwa Mungu, nao watu wakamsonga ndugu ya Musa, Haruni, awafanyizie mungu. Haruni alikubali akafanyiza ndama kutokana na dhahabu ambayo watu walitoa. Ilidaiwa kwamba sanamu hiyo ilimwakilisha Yehova. (Zaburi 106:20) Siku iliyofuata walitoa dhabihu nao wakaendelea “kuisujudia,” (NW). Kisha ‘wakacheza.’—Kutoka 32:1, 4, 6, 8, 17-19.
6 Musa akashuka kutoka mlimani Waisraeli walipokuwa wakisherehekea. Alipoona mwenendo wao mbaya sana, alipaaza sauti hivi: “Ni nani aliye upande wa Yehova?” (Kutoka 32:25, 26, NW) Wana wa Lawi wakamkusanyikia Musa, naye akawaagiza watwae panga na kufisha hawa wenye kufurahia karamu ya ibada ya sanamu. Wakionyesha wivu wao kwa ajili ya ibada safi ya Mungu, Walawi waliwaua ndugu zao wenye hatia wapatao 3,000. Yehova akategemeza tendo hilo kwa kupeleka tauni miongoni mwa waokokaji. (Kutoka 32:28, 35) Kisha Mungu akarudia amri hii: “Hutamwabudu mungu mwingine, kwa kuwa BWANA, ambaye jina lake ni mwenye wivu, ni Mungu mwenye wivu.”—Kutoka 34:14.
Baal-Peori
7, 8. (a) Waisraeli wengi walitumbukiaje kwenye ibada ya sanamu iliyo mbaya sana kwa kuhusiana na Baal-Peori? (b) Pigo la Yehova lilikwishaje?
7 Miaka 40 baadaye, taifa la Israeli lilipokuwa karibu kuingia katika Bara Lililoahidiwa, wanawake Wamoabu na Wamidiani wenye kuvutia walishawishi Waisraeli wengi kuja kufurahia ukaribishaji wao. Wanaume hao walipaswa kukataa uhusiano wa kindani pamoja na waabudu wa miungu bandia. (Kutoka 34:12, 15) Badala ya hivyo, wao waliwakimbilia kama kondoo waendao machinjoni, wakifanya uasherati pamoja na wanawake hao na kusujudia Baal-Peori pamoja nao.—Hesabu 25:1-3; Mithali 7:21, 22.
8 Yehova alipeleka pigo la kuwaua wale waliojihusisha na ibada hiyo ya ngono yenye kuaibisha. Mungu pia aliwaamuru Waisraeli wasio na hatia kuwaua ndugu zao wenye hatia. Katika hali ya kukaidi waziwazi, mkuu mmoja wa Israeli aitwaye Zimri alimleta binti-mfalme fulani Mmidiani katika hema lake ili afanye ngono naye. Akiona hilo, kuhani mwenye kumhofu Mungu Finehasi aliwafisha watu hawa wawili waliokosa adili. Kisha pigo likakoma, Mungu akatangaza: “Finehasi . . . amezigeuza hasira zangu zisiwe juu ya wana wa Israeli, kwa kuwa alikuwa na wivu kati yao kwa wivu wangu mimi, hata nisiwaangamize wana wa Israeli katika wivu wangu.” (Hesabu 25:11) Ingawa taifa hilo liliokolewa lisiangamizwe, angalau Waisraeli 23,000 walikufa. (1 Wakorintho 10:8) Walipoteza tumaini lao la muda mrefu la kuingia katika Bara Lililoahidiwa.
Somo Lenye Kuonya
9. Ni nini kilichowapata watu wa Israeli na Yuda kwa sababu hawakuona wivu kwa ajili ya ibada safi ya Yehova?
9 Kwa kusikitisha, upesi Waisraeli walisahau masomo haya. Wao hawakuwa wenye wivu kwa ajili ya ibada safi ya Yehova. “Wakamtia [Mungu] wivu kwa sanamu zao.” (Zaburi 78:58) Matokeo yakawa kwamba Yehova aliruhusu makabila kumi ya Israeli kuchukuliwa mateka na Waashuru katika 740 K.W.K. Ufalme wa Yuda uliobaki wa makabila mawili ulipata adhabu kama hiyo wakati jiji lao kuu la Yerusalemu lilipoharibiwa katika 607 K.W.K. Wengi waliuawa, na waokokaji walichukuliwa mateka kwenda Babiloni. Hicho ni kielelezo chenye kutoa onyo kama nini kwa Wakristo leo!—1 Wakorintho 10:6, 11.
10. Ni nini kitakachowapata waabudu-sanamu wasiotubu?
10 Thuluthi moja ya watu wote ulimwenguni—wapatao milioni 1,900—hudai sasa kuwa Wakristo. (1994 Britannica Book of the Year) Wengi wao ni wa makanisa ambayo hutumia visanamu, sanamu, na misalaba katika ibada zao. Yehova hakuacha kuadhibu watu wake mwenyewe waliomtia wivu kwa kuabudu sanamu. Wala hatawaacha wale wanaodai kuwa Wakristo wanaoabudu kwa msaada wa vitu vinavyoonekana. “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli,” akasema Yesu Kristo. (Yohana 4:24) Isitoshe, Biblia huonya Wakristo wajilinde na ibada ya sanamu. (1 Yohana 5:21) Waabudu-sanamu wasiotubu ni miongoni mwa wale ambao hawataurithi Ufalme wa Mungu.—Wagalatia 5:20, 21.
11. Mkristo anawezaje kuwa na hatia ya ibada ya sanamu bila kusujudia sanamu fulani, na ni nini kitakachosaidia mtu kuepuka ibada ya sanamu ya aina hiyo? (Waefeso 5:5)
11 Ingawa Mkristo wa kweli hawezi kusujudia sanamu, ni lazima aepuke kitu chochote ambacho Mungu anaona kuwa cha ibada ya sanamu, kisicho safi, na chenye dhambi. Kwa mfano, Biblia yaonya hivi: “Fisheni viungo vya mwili wenu vilivyo juu ya dunia kwa habari ya uasherati, ukosefu wa usafi, hamu ya ngono, tamaa yenye kuumiza, na choyo, ambako ni ibada ya sanamu. Kwa sababu ya mambo hayo hasira ya kisasi ya Mungu inakuja.” (Wakolosai 3:5, 6, NW) Kutii maneno haya huhitaji kukataa tabia isiyo ya adili. Hilo lamaanisha kuepuka vitumbuizo vinavyokusudiwa kuamsha tamaa ya ngono isiyo safi. Badala ya kutosheleza tamaa hiyo, Wakristo wa kweli wanaona wivu kwa ajili ya ibada safi ya Mungu.
Vielelezo vya Baadaye vya Wivu wa Kimungu
12, 13. Yesu aliwekaje kielelezo chenye kutokeza sana katika kuonyesha wivu kwa ajili ya ibada safi ya Mungu?
12 Kielelezo chenye kutokeza zaidi cha mtu aliyekuwa na wivu kwa ajili ya ibada safi ya Mungu alikuwa Yesu Kristo. Katika mwaka wa kwanza wa huduma yake, aliona wafanya biashara wenye pupa wakiendesha biashara katika ua wa hekalu. Huenda Wayahudi waliokuwa wakizuru walihitaji msaada wa wabadili pesa ili wavunje fedha zao za kigeni kwa pesa ambazo zingekubalika kuwa kodi ya hekalu. Pia walihitaji kununua wanyama na ndege wa kutolewa dhabihu zilizohitajiwa na Sheria ya Mungu. Biashara hizo zilipaswa kufanywa nje ya ua wa hekalu. Isitoshe, kwa wazi wafanya biashara walikuwa wakitumia vibaya mahitaji ya kidini ya ndugu zao kwa kuwatoza bei za juu sana. Akiliwa na wivu kwa ajili ya ibada safi ya Mungu, Yesu alitumia mjeledi kuondosha nje kondoo na ng’ombe. Pia alipindua meza za wabadili pesa, akisema: “Msiifanye nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara.” (Yohana 2:14-16) Hivyo Yesu alitimiza maneno ya Zaburi 69:9, (NW): “Bidii pekee [au, “wivu,” Byington] kwa ajili ya nyumba yako imenila.”
13 Miaka mitatu baadaye, Yesu aliwaona tena wafanya biashara wenye pupa wakifanya biashara katika hekalu la Yehova. Je, angelisafisha mara ya pili? Wivu wake kwa ajili ya ibada safi ya Mungu ulikuwa wenye nguvu sana wakati huo kama tu ulivyokuwa alipoanza huduma yake. Aliwafukuza wote wauzaji na wanunuaji. Akatoa sababu yenye nguvu hata zaidi kwa hatua alizochukua, akisema: “Je! haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote? Bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang’anyi.” (Marko 11:17) Hicho ni kielelezo kizuri kilichoje cha kudumu katika kuonyesha wivu wa kimungu!
14. Wivu wa Yesu kwa ajili ya ibada safi wapasa utuvutieje?
14 Utu wa Bwana Yesu Kristo ambaye ametukuzwa sasa haujabadilika. (Waebrania 13:8) Katika karne hii ya 20, yeye anaona wivu kwa ajili ya ibada safi ya Baba yake kama tu alipokuwa duniani. Hilo laweza kuonwa katika ujumbe mbalimbali wa Yesu kwa makutaniko saba uliorekodiwa katika kitabu cha Ufunuo. Ujumbe huo unatumika kwa sehemu kubwa sasa, katika “siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10; 2:1–3:22) Katika njozi mtume Yohana alimwona Yesu Kristo aliyetukuzwa akiwa na ‘macho kama mwali wa moto.’ (Ufunuo 1:14) Hilo laonyesha kwamba Kristo hawezi kukosa kuona jambo lolote anapokagua makutaniko ili kuhakikisha kwamba yanabaki yakiwa safi na kukubalika kwa utumishi wa Yehova. Wakristo wa siku hizi wanahitaji kukumbuka onyo la Yesu dhidi ya kujaribu kutumikia mabwana-wakubwa wawili—Mungu na mali. (Mathayo 6:24) Yesu aliwaeleza hivi washiriki wa kutaniko la Laodikia wenye kufuatia vitu vya kimwili: “Kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu. . . . Uwe na bidii, ukatubu.” (Ufunuo 3:14-19) Kupitia maneno na kielelezo, wazee wa kutaniko waliowekwa rasmi wapaswa kusaidia waamini wenzao kuepuka mtego wa kufuatia vitu vya kimwili. Ni lazima wazee pia walinde kundi kutokana na ufisadi wa kiadili wa ulimwengu huu unaotilia mkazo ngono. Na zaidi, watu wa Mungu hawathubutu kuvumilia uvutano wowote wa Kiyezebeli kutanikoni.—Waebrania 12:14, 15; Ufunuo 2:20.
15. Mtume Paulo alimwigaje Yesu katika kuonyesha wivu kwa ajili ya ibada ya Yehova?
15 Mtume Paulo alikuwa mwigizaji wa Kristo. Ili kulinda Wakristo wapya waliobatizwa kutokana na uvutano mbalimbali usiofaa wa kiroho, yeye alisema: “Nawaonea wivu, wivu wa Mungu.” (2 Wakorintho 11:2) Kabla ya wakati huo, wivu wa Paulo kwa ajili ya ibada safi ulikuwa umemsukuma kufundisha kutaniko hilihili kutenga na ushirika mfanya uasherati asiyetubu aliyekuwa na uvutano wenye kuchafua. Maagizo yaliyopuliziwa yaliyotolewa katika pindi hiyo yamekuwa msaada mkubwa kwa wazee leo wanapojaribu kudumisha usafi wa zaidi ya makutaniko 75,500 ya Mashahidi wa Yehova.—1 Wakorintho 5:1, 9-13.
Wivu wa Mungu Hunufaisha Watu Wake
16, 17. (a) Mungu alipoadhibu Yuda la kale, mataifa yalionyesha mtazamo gani? (b) Baada ya utekwa wa miaka 70 wa Yuda, Yehova alionyeshaje wivu wake kwa ajili ya Yerusalemu?
16 Mungu alipoadhibu watu wa Yuda kwa kuwaruhusu kuchukuliwa mateka Babiloni, walidhihakiwa. (Zaburi 137:3) Kwa wivu wenye chuki, Waedomu hata walisaidia Wababiloni kuletea watu wa Mungu uangamivu, na Yehova aliona jambo hilo. (Ezekieli 35:11; 36:15) Wakiwa utekwani waokokaji walitubu, na baada ya miaka 70 Yehova aliwarudisha kwenye bara lao.
17 Kwanza, watu wa Yuda walikuwa katika hali mbaya sana. Jiji la Yerusalemu pamoja na hekalu lalo lilikuwa magofu. Lakini mataifa yaliyolizingira yalikinza jitihada zote za kujenga upya hekalu. (Ezra 4:4, 23, 24) Yehova alihisije juu ya jambo hilo? Rekodi iliyopuliziwa yasema: “BWANA wa majeshi asema hivi, Naona wivu kwa ajili ya Yerusalemu, na kwa ajili ya Sayuni; naona wivu mkuu sana. Nami ninawakasirikia sana mataifa wanaokaa hali ya raha; kwa maana mimi sikukasirika ila kidogo tu, na wao waliyahimiza mateso. Kwa sababu hiyo BWANA asema hivi, Ninaurudia Yerusalemu kwa rehema nyingi; nyumba yangu itajengwa ndani yake, asema BWANA wa majeshi.” (Zekaria 1:14-16) Na kwa kupatana na ahadi hii, hekalu na jiji la Yerusalemu lilijengwa upya kwa mafanikio.
18. Wakristo wa kweli walipata ono gani katika kipindi cha vita ya ulimwengu ya kwanza?
18 Kutaniko la Kikristo la kweli lilipata ono kama hilo katika karne ya 20. Katika kipindi cha vita ya ulimwengu ya kwanza, Yehova aliadhibu watu wake kwa sababu hawakuwa wameshikamana kabisa na kutokuwamo kwao katika pigano hilo la kilimwengu. (Yohana 17:16) Mungu aliruhusu mamlaka za kisiasa kuwanyanyasa, na makasisi wa Jumuiya ya Wakristo walishangilia msiba huo. Makasisi hata walikuwa katika mstari wa mbele katika kuchochea wanasiasa kupiga marufuku kazi ya Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo.—Ufunuo 11:7, 10.
19. Yehova ameonyeshaje wivu wake kwa ajili ya ibada yake tangu 1919?
19 Hata hivyo, Yehova aliona wivu kwa ajili ya ibada yake akarudishia watu wake waliotubu upendeleo wake katika mwaka wa baada ya vita wa 1919. (Ufunuo 11:11, 12) Tokeo likawa kwamba idadi ya wasifaji wa Yehova imeongezeka tokea 4,000 katika 1918 hadi zaidi ya milioni 5 leo. (Isaya 60:22) Upesi, wivu wa Yehova kwa ajili ya ibada yake safi utaonyeshwa kwa njia za kutazamisha hata zaidi.
Matendo ya Wakati Ujao ya Wivu wa Kimungu
20. Mungu atafanya nini karibuni ili kuonyesha wivu wake kwa ajili ya ibada safi?
20 Kwa karne nyingi makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamefuata mwendo wa Wayahudi waasi-imani waliomchochea Yehova aone wivu. (Ezekieli 8:3, 17, 18) Upesi Yehova Mungu atatenda kwa kuweka wazo la kuchukua hatua akilini na mioyoni mwa washiriki wa Umoja wa Mataifa. Hilo litasukuma mamlaka za kisiasa kuharibu na kuacha ukiwa Jumuiya ya Wakristo na sehemu inayosalia ya dini bandia. (Ufunuo 7:16, 17) Waabudu wa kweli wataokoka kule kutekelezwa kwa hukumu ya kimungu kunakohofisha. Wataitikia maneno ya viumbe vya kimbingu vinavyosema: “Sifuni Yah, nyinyi watu! . . . Kwa maana ametekeleza hukumu juu ya kahaba mkubwa [dini bandia] aliyeharibu dunia kwa uasherati wake [mafundisho yake bandia na utegemezo wake wa siasa yenye ufisadi], na amelipizia kisasi damu ya watumwa wake mkononi mwa huyo kahaba.”—Ufunuo 19:1, 2, NW.
21. (a) Shetani na mfumo wake atafanya nini baada ya dini bandia kuharibiwa? (b) Mungu ataitikiaje?
21 Ni nini kitakachotendeka baada ya uharibifu wa milki ya ulimwengu wa dini bandia? Shetani atazichochea mamlaka za kisiasa kupanga shambulizi la duniani pote dhidi ya watu wa Yehova. Mungu wa kweli ataitikiaje jaribio hilo la Shetani la kuondosha kabisa ibada ya kweli duniani pote? Ezekieli 38:19-23 chatueleza: “Katika wivu wangu, na katika moto wa ghadhabu yangu, [mimi Yehova] nimenena. . . . Nami nitamhukumu [Shetani] kwa tauni, na kwa damu; nami nitanyesha mvua ifurikayo, na mvua ya mawe makubwa sana, na moto na kiberiti juu yake, na vikosi vyake, na watu wa kabila nyingi walio pamoja naye. Nami nitajitukuza, na kujitakasa, na kujidhihirisha, mbele ya macho ya mataifa mengi; nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA.”—Ona pia Sefania 1:18; 3:8.
22. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuna wivu kwa ajili ya ibada safi ya Yehova?
22 Linafariji kama nini kujua kwamba Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima hujali kwa wivu waabudu wake wa kweli! Kwa sababu ya uthamini wenye kina kwa fadhili zake zisizostahiliwa, na tuone wivu kwa ajili ya ibada safi ya Yehova Mungu. Na tuendelee kuhubiri habari njema kwa bidii na kungoja kwa uhakika siku kuu ambapo Yehova atatukuza na kutakasa jina lake kuu.—Mathayo 24:14.
Mambo ya Kutafakari
◻ Inamaanisha nini kuona wivu kwa ajili ya Yehova?
◻ Tunaweza kujifunza nini kutokana na kielelezo kilichowekwa na Waisraeli wa kale?
◻ Tunaweza kuepukaje kumchochea Yehova kwa wivu?
◻ Mungu na Kristo wameonyeshaje wivu kwa ajili ya ibada safi?
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
Upendo Hauna Wivu
KUHUSU husuda, msomi wa Biblia wa karne ya 19 Albert Barnes aliandika: “Ni mojawapo maonyesho yaliyo ya kawaida zaidi ya uovu, na inaonyesha wazi upotovu wenye kina wa mwanadamu.” Yeye aliongezea hivi: “Mtu yeyote awezaye kuchunguza vita vyote na magomvi yote na mipango yote ya kilimwengu hadi vyanzo vyayo—mipango yote ya hila na makusudi yote ya hata wale wanaojiita Wakristo, ambayo hudhuru sana dini zao na kuzifanya kuwa za kilimwengu, kwa vyanzo vyayo kabisa—atashangaa kugundua kiasi kinachotokezwa na husuda. Sisi huumia kwa sababu wengine wamestawi kutushinda; sisi hutamani vitu vya wengine, ingawa hatuna haki ya kuwa navyo; na hilo hutokeza njia nyingi zenye hatia ambazo hufuatwa ili kupunguza kadiri wanavyovifurahia, au kuvipata viwe vyetu wenyewe, au kuonyesha kwamba hawana vitu kama inavyodhaniwa kwa kawaida. . . . kwa hiyo roho ya husuda iliyo vifuani mwetu itatoshelezwa.”—Warumi 1:29; Yakobo 4:5.
Kwa kutofautisha, Barnes alitoa taarifa yenye kupendeza kuhusu upendo, ambao “hauhusudu.” (1 Wakorintho 13:4) Aliandika hivi: “Upendo hauhusudu wengine kwa furaha wanayopata; hufurahia hali-njema yao; na furaha yao iongezekapo . . . , wale wenye uvutano wa upendo . . . hawawezi kuipunguza [furaha yao]; hawawezi kuwaaibisha kwa sababu ya mali zao; hawawezi kuacha kuwa na furaha; hawawezi kunung’unika au kutamauka kwamba wao hawajapendelewa hivyo. . . . Ikiwa tunawapenda wengine—tukishangilia furaha yao, hatupaswi kuwahusudu.”
[Picha katika ukurasa wa10]
Finehasi aliona wivu kwa ajili ya ibada safi ya Yehova