‘Ni Nani Mtumwa Mwaminifu Mwenye Akili’?
◆ Siku tatu tu kabla ya kufa kwake, Yesu Kristo aliwapa mitume wake unabii wa mambo ambayo yangetukia baada ya kufa kwake na kufufuka, mpaka wakati wa mwisho wa taratibu hii ya ulimwengu ya mambo. Maneno ya Yesu yalifunua kwamba wakati wa kipindi hiki kirefu cha wakati kungekuwako “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ambaye angekuwa akiwapa watu wa Mungu “chakula kwa wakati wake.”—Mt. 24:45.
Je! twaweza kujua “mtumwa” huyu? Ni lazima turudie maneno ya Mungu aliyosema kwa taifa lake la kale la Israeli, ambao Mungu aliambia hivi: “Ninyi ni mashahidi wangu, . . . na mtumishi niliyemchagua.” (Isa. 43:10) Hivyo Israeli kama taifa lilitajwa hapa kuwa “mtumishi” au ‘mtumwa’ wa Mungu.
Walakini, mtume Paulo alieleza kwamba, wakati huo, Israeli wa asili hawakuwa tena “mtumishi” wa Mungu. Kwa sababu gani? Kwa sababu taifa hilo lilikuwa limemkataa Kristo, isipokuwa mabaki ya Wayahudi wachache ndio waliomwamini. Paulo aliandika hivi: “Maana yeye si Myahudi aliye Myahudi kwa nje tu, wala tohara siyo ile ya nje tu katika mwili; bali yeye ni Myahudi aliye Myahudi kwa ndani; na tohara ni ya moyo, katika roho, si katika andiko.”—Rum. 2:28, 29.
Basi yule ‘mtumishi’ au “mtumwa” ambaye Yesu alitabiri bila shaka ni washiriki wa Israeli wa kiroho duniani—si mtu mmoja, bali jamii. Kwa hiyo wangekuwa warithi washirika na Yesu Kristo waliozaliwa kwa roho, watakaoshiriki kama wafalme pamoja na Kristo katika ufalme wake wa kimbinguni wakati wa utawala wa miaka elfu juu ya dunia. (Ufu. 5:9, 10; 20:4-6) Wakati wapo duniani kazi yao imekuwa ya kugawa chakula cha kiroho miongoni mwa washiriki wa nyumba ya Mungu, hasa kuhakikisha kwamba wanapatiwa vifaa vya kiroho kukabili matatizo yanayowapata mara kwa mara.