Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 12/15 kur. 562-568
  • Wewe Utafanyaje Ushambuliwapo na Shetani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wewe Utafanyaje Ushambuliwapo na Shetani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NJIA ZA KUSHAMBULIA
  • KUJITAYARISHA NI KWA MAANA SANA
  • Simama Imara Dhidi ya Hila za Shetani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Uwe Macho​—Shetani Anataka Kukumeza!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Adui wa Uzima wa Milele
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Jihadhari na Adui Yako, Ibilisi!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 12/15 kur. 562-568

Wewe Utafanyaje Ushambuliwapo na Shetani?

“Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani.”​—⁠Efe. 6:11.

1. Lazima sote tujihadhari na nani, na kwa sababu gani?

UWE unajua hivyo au usiwe unajua, wewe na wengine wote wa taifa la kibinadamu mna adui mkali wa kupambana naye. Pengine hukujua kwamba mchukiaji huyo wa wanadamu wote yuko kweli, lakini usikosee. Unanyemelewa na mwuaji-mwongo, aliyepanga mauaji mapema. Watakiwa uwe macho sana sana kwa sababu haonekani. Huwezi kumwona akisimama pale pale karibu yako. Hata hivyo yeye anazo “nguvu za kufisha,” kwa kutumia njia za jeuri. Yeye ni nani? Ndiye Shetani Ibilisi,​—⁠Ebr. 2:14, NW.

2. Shetani ni nani, na mradi wake mkuu ni nini?

2 Lakini yeye ataka nini? Kwa sababu gani wewe mwenyewe umo hatarini? Lazima tukumbuke kwamba wakati mmoja yeye alikuwa mwabudu wa Mungu wa kweli, Yehova, lakini “hakusimama katika kweli.” Akawa mwasi imani, akatanguliza tamaa yake kuu ya kuabudiwa mbele ya faida za Muumba wake. Ili atetee matendo yake na kujitwalia ibada alijiwekea mradi wa kuvunja ukamilifu wa viumbe vyote vya mbinguni na duniani. Ataka kuharibu uhusiano wako na Mungu. Kwa hiyo unashambuliwa.​—⁠Yohana 8:44; Mt. 4:9.a

3. Ni kwa kadiri gani Ibilisi anavyoongoza dunia?

3 Huenda ukawa huwazi hata kidogo juu ya kuabudu Ibilisi, hata hivyo uhakika ni kwamba wengi wa wale wanaodhani wanaabudu Mungu wa kweli wako hasa upande wa Shetani na malaika zake wa kishetani ambao wamefuata kuwaza kwa Ibilisi. Huenda watu wengine wakatilia hilo shaka; lakini Ufunuo 12:9 wamtaja “aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote.” Tena, 1 Yohana 5:19 yasema: “Dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.” Kwingine katika Maandiko anaitwa “mungu wa dunia hii.” (2 Kor. 4:4) Mitajo hii yapaswa kutufahamisha wazi kwamba kulingana na maoni ya Muumba wanadamu wengi sana wanaongozwa na kutawalwa na Ibilisi.

4. Shetani amewezaje ‘kufanikiwa’ kiasi cha tutosha?

4 Huenda ukauliza, ‘Imewezekanaje walio wengi wa wanadamu wakaja chini ya maongozi ya Shetani, bila ya wao hata kujua?’ Ni kwa sababu ya njia atumiazo, njia zenye nguvu sana hata ziliweza kuwaharibu Adamu na Hawa. Kwa kuwa wakati mmoja alikuwa “katika kweli” ajua sana jinsi ya kujigeuza “awe mfano wa malaika wa nuru.” (Yohana 8:44; 2 Kor. 11:14) Kama vile chakula chenye sumu kilichopikwa kikiwa na ladha za kufurahisha kinavyoweza kuvuta sana mtu asiyejua neno, ndivyo Shetani hufanya mara nyingi mambo yanayovuta tamaa za asili na kuyapotoa kwa njia inayoweza kufisha. Anataka kututia mahali ambapo hatutambui lililotukia, mpaka imekuwa kuchelewa mno. Kukaa katika mwendo huo wenye hatari kwa kipindi fulani karibuni kunaunguza dhamiri yetu hata mwishowe twaona mwendo wetu mpotovu kama ‘jambo la kawaida tu,’ na twaanza kudhani kila mtu mwingineyo anakosea. Je! inawezekana kwamba hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa “ulimwengu wote,” “dunia yote”? Ndivyo! kulingana na Neno la Mungu mwenyewe lililoandikwa.

5. Kwa sababu gani yaweza kusemwa Shetani hana ‘silaha ya siri’?

5 Kwa kuwa ndivyo ilivyo kulingana na Maandiko, huenda mtu akashangaa kwa kuuliza hivi, ‘Mtu ye yote aweza kufanikiwa kupinga shambulio la Shetani lenye madhara na lisiloonekana? Je! iko njia yo yote ya kujulia mapema njia zake ni nini hasa?’ Kwa furaha, jibu ni, Ndiyo! Kwa kujifunza Neno la Mungu na historia ya kisasa ya kundi la Kikristo twaweza kujua hila zake zote. Kwa kweli yeye hana ‘silaha ya siri.’ Yuko kama vile Mhubiri 1:9 isemavyo: “Yaliyokuwako ndiyo yatakayokuwako; na yaliyotendeka ndiyo yatakayotendeka; wala jambo jipya hakuna chini ya jua.” Shetani si muumba hata aweze kutunga kitu kipya kabisa na kutuzukia bila ya sisi kujua lo lote. Yeye ana ukomo wa uwezo wake. Kwa hiyo, na tufikirie nyingine za “hila” ambazo Shetani ametumia katika shambulio lake lililo kali zaidi juu ya wanadamu kisha tuone tunaloweza kufanya tuwe tayari kujikinga.​—⁠Efe. 6:11.

NJIA ZA KUSHAMBULIA

6. Shambulio la Shetani la uso kwa uso ni nini, na Wakristo wanawezaje kupambana nalo?

6 Katika vita yake Shetani hushambulia uso kwa uso mara nyingi. Njia hiyo inahusu vitisho, kufungwa gerezani, kupigwa marufuku, na matendo ya jeuri, ambayo yanachochewa na utukuzo wa taifa mara nyingi. Wengine wamepoteza kazi, nyumba, washiriki wa jamaa na hata maisha zao kwa sababu ya kuchukua msimamo wa kutoridhiana (kutokubaliana) na adui wanaposhambuliwa hivyo. Kwa maarifa hayo ya kuogofya, adui yetu atumaini kutulemea na kututisha ili tushindwe. Yeye ajua ni jambo la kawaida kwa wanadamu kuchukua hatua ya kujitafutia faraja wanapokuwa katika taabu au hangaiko. Ukiwa na maumivu ya kichwa, unajaribu kuyaondoa. Shetani anawaza kwamba, akiweza kukutaabisha sana, utaridhiana naye upate kitulizo, hivyo uvunje uhusiano wako na Yehova Mungu. Katika nyakati za kisasa, katika bara zote za dunia, mashahidi wa Kikristo wa Yehova wamevumilia mambo haya. Tisho linapofanywa la mambo hayo watu walio wengi hufuata waambiwavyo, lakini Wakristo wa kweli, wasioogopa kustahimili, wameendelea kuwa waaminifu.

7. Shetani hutumiaje woga?

7 “Hila” nyingine ya Shetani inayohusu wale hasa walioanza kushirikiana na kundi la Kikristo karibuni ni kuwafanya waogope vile majirani, rafiki na watu wa ukoo watakavyofikiri. Huenda washiriki wa karibu wa jamaa wakageukia kwingine, na hata mwenzi wetu wa ndoa huenda akatupinga. Je! hilo litupate kama shambulio la ghafula? Sivyo! Kwani Yesu hakuonya hivi: “Msidhani ya kuwa nimekuja kuleta amani duniani; la! sikuja kuleta amani, bali upanga. Kwa maana nalikuja kumfitini mtu na babaye, na binti na mamaye, na mkwe na mkwe mtu; na adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake?” (Mt. 10:34-36) Unapojaribu kufuata kanuni za Biblia huenda watu hao wakakuletea mikazo. Kwa njia hiyo Shetani anatumaini kwamba tamaa yako ya kutaka kukubaliwa na watu hao itakufanya ukubali kufuata yao. Je! wewe umeshambuliwa hivyo?

8. Tamaa yetu ya kutaka usalama yawezaje kutumiwa kama shambulio?

8 Upande mwingine ambao Shetani hujaribu kutudhoofisha unahusu tamaa yetu ya kibinadamu ya kutaka usalama. Kristo Yesu alishauri wasikiaji wake hivi: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini?” Baadaye mtume Paulo alisema: “Msijisumbue kwa neno lo lote.” (Mt. 6:25, 31; Flp. 4:6) Ndiyo kusema, tukitimiza wajibu wetu, Yehova Mungu atahakikisha tunapata riziki. Walakini, Shetani hataki tumtegemee Muumba. Bali, ataka tudhani yatupasa kutumia akili nyingi sana isivyo kawaida ili tujikinge na kupanda kwa bei za vitu na vilevile upungufu wa mafuta, chakula na vifaa vingine, akitaka tusifikirie kabisa faida za kiroho. Hata watu wasio na shida za mahitaji yao ya karibuni wanasumbukia yatakayotukia miezi na miaka mingi ijayo. Wengine wanaona yawapasa kulundika vitu vya kupita kiasi wajikinge na upungufu wa vitu unaopangwa au unaotabiriwa. Ni watu wachache sana wanaofuata shauri la wazi lililomo katika Neno la Mungu: “Tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.” Watu wengi wameruhusu shambulio hili lenye hila la Shetani liwafanye wasitafute utatuzi wa kiroho wa matatizo ya maisha. Kwa hiyo katika mambo haya, wewe waendeleaje?​—1 Tim. 6:8; Ufu. 6:5, 6.

9. Toa mfano wa vile Shetani aweza kutumia tamaa safi kutushambulia.

9 Tamaa nyingine ya asili ambayo sote tunayo ni uhitaji wa kujifurahisha na kujiburudisha. Lakini Shetani mjanja aweza kubadili tamaa safi ya kutaka kuburudika ikawa shambulio kali lenye kuharibu sana hali yetu ya kiroho kama vile kusumbukia vitu, kuogopa wanadamu, na kutukuza taifa kunavyoiharibu. Kupendezwa kwetu na michezo, muziki na namna nyingine za kujifurahisha (tafrija) kwaweza kutuvuta sana hata matumizi ya wakati na pesa kwa njia hii yakatuzuia kutimiza wajibu wetu wa kiroho. Wewe ukilinganisha wakati, mapendezi na pesa unazotumia kwa starehe na zile unazotumia kuangalia mambo ya kiroho, ni zipi zitakazokuwa nyingi zaidi? Kwa kadiri fulani jibu lako laonyesha vile Shetani amefaulu kukushambulia.

10. Mojawapo ya njia mbovu zaidi za kushambulia kwa Shetani ni nini? Eleza.

10 Pengine njia mbovu zaidi ya kushambulia kwa Ibilisi inahusu ile tamaa iliyo ya kawaida kabisa ya kutaka kuoa au kuolewa na ya kutaka mambo ya ndani ndani ya ndoa. Kwa mfano, mvulana na msichana waliochumbiana huenda wakaanza kuwaza hivi, ‘Siku zijazo tutaoana, tena twapendana. Ingawaje, ndoa yenyewe ni kipande tu cha karatasi na maneno machache. Jambo la maana hasa ni vile tunavyodhaniana. Kwa hiyo kuna ubaya gani kuanza kufurahia sasa mengine ya mapendeleo ya ndani ndani ya watu waliooana?’ Katika Bustani ya Edeni tunda lililokatazwa lenyewe halikuwa baya, lakini Yehova Mungu alisema lisiliwe, hiyo ikafanya kulila kuwe kosa. Ndivyo ilivyo kwa habari ya uhusiano kati ya mwanamume na mwanamke. Linaloweza kufaa kesho laweza kuwa baya leo. Njia ya ujanja anayotumia Shetani ni kutufanya tudhani Yehova anatunyima pasipo haki kitu chenye faida na cha kutufurahisha. Yeye amekuza wazo la kwamba mwanadamu hana “haki” ya kujiamulia yaliyo mema na yaliyo mabaya. Ngono zinazofanywa ovyo ovyo bila kujali mtu azifanya na nani zimesababishwa na mawazo hayo na huo ni mtego tunaopaswa kujilinda nao. Lazima Wakristo waonyeshe wanashikamana kabisa na sheria za Mungu ikiwa wataendelea kuwa imara washambuliwapo na Shetani.

KUJITAYARISHA NI KWA MAANA SANA

11. Twaweza kufanya nini tujitayarishe kwa shambulio la Shetani?

11 Jambo la kwanza katika kujitayarisha kwa shambulio la Shetani ni kutambua kwamba kinga yetu si ya kimwili bali ya kiroho hasa. Twafahamishwa wazi hivyo katika Waefeso 6:11-13: “Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.” Kwa hiyo katika kujikinga haifanyizi tofauti yo yote kama tu vijana au wazee, kama tuna maungo yenye nguvu au kama tu dhaifu, kama tuna afya njema au kama tuna kasoro za kimwili. Kama vile Daudi alivyomfanya Goliathi, tunaweza kupambana na adui anayeonekana sana kuwa mwenye nguvu kuliko sisi, na bado sisi tuwe ndio washindi. Tutashinda kwa kujitayarisha kiroho, si kwa sababu ya ufundi wetu wenyewe. Kwa kweli, hii ndiyo njia yetu ya pekee ya kujikinga.

12. Lazima tufahamu suala gani ili tuendelee kuwa imara?

12 Ni jambo moja kusoma na kusikia wengine wanaendelea kuwa waaminifu wanapokuwa katika majaribu makali sana ya ushikamanifu kwa Mungu. Lakini sisi mmoja mmoja tutafanya nini tujaribiwapo hivyo kinaganaga, wakati maisha yetu wenyewe na ukamilifu wetu ndio utakaokuwa hatarini? Ili kuweza kupambana na upinzani huo sisi wenyewe na kuendelea kuwa imara, ni jambo la maana sana tujijulie sababu gani Yehova aruhusu tushambuliwe hivyo. Yatupasa tukumbuke kwamba tunapatwa na jaribu la ushikamanifu (loyalty), na kwamba wasiotumikia Mungu kwa sababu wanampenda watachujwa na kuondolewa. Tena, kuendeleza ukamilifu wetu kwamhakikisha Ibilisi kuwa mwongo na kuunga mkono uhalali wa enzi kuu ya Yehova. Tukisahau sababu hiyo ya kuteswa kwetu, huenda tukajiacha vyepesi tuanze kujihurumia, na hiyo yaweza kutufanya turidhiane (tukubaliane) na adui na kutia mwanya katika kinga zetu. Ni jambo la faida watu wote wa Mungu warudie-rudie kuchunguza waone wao wenyewe wanatimiza wajibu gani katika suala la ulimwengu wote linalohusu enzi kuu ya Mungu.​—⁠Luka 22:31.

13. Ni uchunguzi gani wa historia utakaotusaidia?

13 Njia moja ya kujikinga kwa matokeo mazuri ni kujua mapema tutakavyopambana na kila jaribu linaloweza kutokea. Kama vile Wakorintho wa Pili 2:11 isemavyo juu ya jitihada za Shetani: “Hatukosi kuzijua fikira zake.” Katika Biblia tuna historia kamili ya maarifa yake, hivi kwamba hakuna anayepaswa kuwa bila habari. Askari hodari huchunguza habari za mapigano ya zamani na kutumia anayojifunza kwa faida. Huamua mapema akilini mwake jinsi atakavyofanya adui wakitumia maarifa fulani. Huenda hata akapambana na adui wa kuwazia tu akamilishe njia zake za kupigana. Sasa basi, je! kila mmoja wetu “kama askari mwema wa Kristo Yesu” hawezi kufaidi kutokana na maandishi ya zamani yanayohusu mashambulio ya Shetani juu ya watu wa Mungu yaliyoandikwa katika Biblia, na vilevile hivi karibuni katika Yearbook of Jehovah’s Witnesses? Kwa sababu gani usiwe unajifunza peke yako njia mbalimbali za werevu anazotumia Shetani, ukifikiria jinsi utakavyoendelea kuwa thabiti katika kila hali? Kwa kufanya hivyo hutanaswa bila ya kutazamia ukiwa dhaifu. Haitakupasa kufanya uamuzi wa ghafula, wa haraka haraka, maana utakuwa umekwisha ufanya. Utaelekea kutenda kwa njia unayojua yafaa.​—2 Tim. 2:3.

14. Ni nini linalohakikisha inawezekana kupinga shambulio la Shetani?

14 Usaidizi zaidi wa kuendeleza ukamilifu waweza kupatikana kwa kukumbuka yanayosemwa katika Petro wa Kwanza 5:9: “Mpingeni huyo [Shetani], mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani.” Wengine wana wenzi wasioamini na wana matatizo mazito ya jamaa. Na wengine wamevumilia kufanyiwa hila, kupoteza kazi zao na kuteswa kikatili, hata hivyo wakaendelea kuwa waaminifu. Watu wa kawaida wenye udhaifu mbalimbali ulio kawaida yetu sote ‘wamesimama’ wakawa washindi. Ikiwa wao wamefanya hivyo, hata wewe waweza kusukumia kando shambulio la Shetani. Kumbuka hivi, ‘mpinge Shetani, naye atakukimbia.’​—⁠Yak. 4:7.

15. Twaweza kupata msaada wapi, na yatupasa tujitieje nguvu?

15 Kupitia kwa makundi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, watu wanaweza kusaidiwa waimarishe kinga zao. Yehova atazamia watu wake wote wajitwalie kadiri wawezavyo mipango mbalimbali iliyofanywa ili wajijenge kiroho. Kama vile tupatavyo njia ya kwenda dukani tukanunue chakula, tukaone daktari na kuangalia mambo mengine ya lazima maishani, vivyo hivyo lazima tutumie kwa faida mpango uliofanywa na kundi wa kupata chakula cha kiroho kilicho cha lazima, kushirikiana nalo na kufanya kazi nalo ili tutiwe nguvu kwa ajili ya siku tutakayoshambuliwa.

16. Sala yaweza kusaidiaje tunapopambana na Shetani?

16 Kwa kuwa Shetani hupenda kushambulia tunapokuwa hatutazamii sana, Baba yetu atupendaye ametupa njia ya kujikinga pale pale wakati wo wote. Inaitwa sala. Wale ambao wamevumilia shambulio la Shetani mara nyingi husema sikuzote kwamba sala ni chanzo kikuu cha kupatia nguvu. Utaona kwamba njia mbalimbali tulizo nazo za kujikinga na Shetani zinaposimuliwa, kama zilivyopangwa katika sura ya sita ya Waefeso, jambo lifuatalo linatajwa: “Mkisali kila wakati katika” roho. Ingawa huenda ukajisikia u dhaifu ndani yako mwenyewe, sala yaweza kukufanya uwe ngome yenye nguvu.​—⁠Efe. 6:18; Flp. 4:13.

17. Faida kuu ya kuendelea kusali ni kutuliza akili tu?

17 Lakini sala inasaidia kwa njia gani? Je! faida kuu ya sala ni kututuliza akilini tu? Hata! Kulingana na Yakobo 5:16, “Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana [kuna nguvu nyingi, NW].” Kwa hiyo sala husaidia sana. Ni kweli, huenda matukio ya ulimwengu kwa ujumla yakakosa kuondolewa, lakini sala yaweza kufanyiza tofauti juu ya vile mambo yatakavyofanywa. Kwa mfano, Paulo alikuwa na maoni gani alipokuwa gerezani? Je! wadhani alisema, ‘Akina ndugu, nimo gerezani. Bila shaka haya ni mapenzi ya Mungu kwangu na hakuna ye yote kati yetu aliye na la kufanya’? Hata kidogo! Bali, alitia ndugu zake moyo wasali kwa ajili yake. Kwa sababu gani? Angalia: “Nami nawasihi zaidi sana kufanya hayo ili nirudishwe kwenu upesi.” Kudumu kwao katika sala kungeweza kubadili wakati wa kufunguliwa kwake. Sala huwa na matokeo.​—⁠Ebr. 13:19; linganisha Filemoni 22.

18. Ni kwa njia gani mbalimbali Mungu anavyojibu sala?

18 Lakini namna gani shambulio la Shetani likiendelea ingawa unadumu katika sala? Je! hii yamaanisha Mungu amekupa kisogo? Sivyo! Uwe na hakika kwamba Yehova anajibu sala zako ingawa huenda asilete ushindi mahakmani, asiondoe marufuku iliyopigwa na serikali, au asiondoe kipingamizi au kishawishi fulani. Huenda akawa ana njia nyingine ya kuleta faraja, au huenda kuruhusu upinzani uendelee kukatimiza kusudi lake lenye haki. Katika habari hii tunakumbushwa aliyosema Paulo juu ya kifungo chake mwenyewe Rumi. Bila shaka angalitaka kufunguliwa, lakini alifahamu sababu gani Yehova angeweza kumwacha akae gerezani. Alisema: “Lakini, ndugu zangu, nataka mjue ya kuwa mambo yote yaliyonipata yametokea zaidi kwa kuieneza Injili; hata vifungo vyangu vimekuwa dhahiri katika Kristo, miongoni mwa askari, na kwa wengine wote pia. Na wengi wa hao ndugu walio katika Bwana, hali wakipata kuthibitika kwa ajili ya kufungwa kwangu, wamezidi sana kuthubutu kulinena neno la Mungu pasipo hofu.”​—⁠Flp. 1:12-14; linganisha 2 Wakorintho 12:7-10.

19. Ukiendelea kuwa imara utasaidiaje wengine?

19 Mungu ameruhusu wengine wa Mashahidi wa Yehova wa mahali kama Ujeremani ya Nazi, Korea na Malawi wateswe kikatili kwa muda mrefu. Lakini je! uaminifu wao haukututia moyo sana? Je! hawakufanyiza kumbukumbu linaloweza kusomwa na watu wote, kuonyesha kwamba wao kama tengenezo hawataacha kamwe kushikamana na Mungu? Upatwapo na majaribu katika jamaa yako, upatwapo na matatizo ya afya au upingwapo na ulimwengu, kumbuka matokeo mema ya kujenga ndugu zako wa Kikristo yanayoweza kuletwa na mfano wako wa uaminifu. Lo! ni pendeleo namna gani kutumiwa na Mungu katika njia hii! Sala yaweza kukupa nguvu za kuvumilia mateso na za kuvumilia uachwapo na waliokuwa “rafiki” zako. Itakusaidia uzuie mikazo ya kutaka kufuatia vitu vya kimwili na vishawishi vya kufanya ufisadi. Lo! tu wenye furaha namna gani kuwa na kinga yenye nguvu ya kiroho tushambuliwapo na Shetani!

[Maelezo ya Chini]

a Tazama Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, kur. 55-74.

[Picha katika ukurasa wa 566]

USHERATI

ANASA ZA KUPITA KIASI

MASUMBUFU YA MAISHA

KUOGOPA WANADAMU

MAOGOFYO, MATESO

IMANI

Funzo la Biblia litakusaidia ‘kutwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo utaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu.’​—⁠Efe. 6:16.

[Picha katika ukurasa wa 567]

Wakati wa kifungo chake mtume Paulo alitia ndugu zake moyo wasali kwa ajili yake, na bado angeweza kuona sababu gani Mungu angeweza kumwacha akae gerezani​—⁠“kwa kuieneza Injili.”​—⁠Flp. 1:12-14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki