Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 3/1 kur. 99-103
  • Siri ya Kupata Maisha Yenye Furaha ya Jamaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Siri ya Kupata Maisha Yenye Furaha ya Jamaa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAHALI AMBAKO KANUNI ZIFAAZO ZINATOKA
  • MAONI YANAYOFAA JUU YA UKICHWA WA JAMAA YAENDELEZA FURAHA
  • DARAKA LA MKE NI LA LAZIMA ILI KUWE NA FURAHA KATIKA JAMAA
  • WATOTO HULETA FURAHA
  • MUHTASARI
  • Kutimiza Fungu Letu la Kuendeleza Maisha Yenye Furaha ya Jamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Kufanikisha Maisha ya Jamaa
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Mume Anayejipatia Heshima Nyingi
    Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha
  • Jinsi Familia Yako Inavyoweza Kuwa na Furaha
    Biblia Inatufundisha Nini?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 3/1 kur. 99-103

Siri ya Kupata Maisha Yenye Furaha ya Jamaa

“Nampigia Baba magoti, ambaye kwa jina lake kila jamaa mbinguni na juu ya dunia inaitwa.”​—Efe. 3:14, 15, NW.

1-3. Watu wengine wanaonaje kanuni za maisha yenye furaha ya jamaa, na hiyo inatokeza maulizo gani?

NI MTU gani mwenye akili nzuri asiyetaka maisha ya jamaa yake yawe yenye furaha? Ikiwa si yenye furaha sasa, watu wengi wangekuwa na nia ya kutumia njia yo yote wanayodhani itawawezesha kupata umoja na furaha halisi ya jamaa.

2 Wengine wanapotafuta siri ya kupata maisha yenye furaha ya jamaa, wanaona kwamba ulimwengu huu wenye elimu ya ufundi unatokeza matatizo yasiyopata kuwako katika kizazi kingine cho chote. Kwa hiyo wanaona kunahitajiwa kanuni tofauti ya adili. Wanaamini pia kwamba ulimwengu umeelimishwa zaidi katika njia zote kuliko katika vizazi vilivyopita.​—Mit. 30:13.

3 Je! hiyo ni kweli? Ndiyo, elimu ya ufundi imeondoa mengine ya matatizo ya kale. Lakini hali ya kibinadamu imebadilika? Je! watu wameacha kutaka watendewe kwa fadhili na upendo? Je! njia ambayo tumetumia maendeleo yetu ya kisayansi na ya viwandani imetuondolea matatizo yetu, au badala yake imetufanya tutendeane mambo bila huruma?

4. Kwa sababu gani si hekima kudhani kwamba tunaweza kuharibu kanuni zote za zamani zinazohusu maisha ya jamaa?

4 Tukiamua mambo kwa uaminifu, lazima tukubali kwamba kizazi cha leo hakina akili wala si bora kuliko vizazi vya zamani. Kwa kweli, sisi tulirithi akili tuliyo nayo kutoka kwao. Kwa hiyo hatuwezi kuwa salama wala hatuwezi kuwa na akili tukitupa kanuni zote za msingi ambazo zimefuatwa karibu na kila taifa duniani kwa maelfu ya miaka​—kwa mfano, kuoa mke mmoja tu, kuwa na ukichwa na ubora wa jamaa​—​hasa kwa sababu mambo hayo yamekuwa na manufaa. Kwa kweli, kuacha kanuni hizo ndiko kumeleta huzuni nyingi ya jamaa.

MAHALI AMBAKO KANUNI ZIFAAZO ZINATOKA

5, 6. (a) Warumi 2:14, 15 yaonyeshaje asili ya kanuni za ndoa na nyinginezo ambazo mataifa mengi yamefuata? (b) Maandiko kama Kumbukumbu la Torati 6:7 na 31:12 yanaonyeshaje kwamba jamaa zapaswa kuungana kadiri iwezekanavyo? (c) Kichwa cha jamaa apaswa kuyaonaje maoni ya washiriki wengine wa jamaa?

5 Lakini hasa, kanuni hizi za maisha ya jamaa zilitoka wapi? Je! zilitungwa kwa akili ya mwanadamu, au zilitokezwa baada ya makosa mengi kufanywa? Sivyo. Zilitokana na Muumba wa wanaume na wanawake, Mwanzilishi wa jamaa. Biblia yasema yafuatayo hata juu ya mataifa yasiyomtambua Mungu wa kweli: “Watu wa Mataifa wasio na sheria [ya Musa] wafanyapo kwa tabia zao yaliyo ndani ya torati, hao wasio na sheria wamekuwa sheria kwa nafsi zao wenyewe. Hao waionyesha kazi ya torati iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia, na mawazo yao, yenyewe kwa yenyewe yakiwashitaki au kuwatetea.”​—Rum. 2:14, 15.

6 Kwa hiyo sheria za mataifa mengi, yaani sheria zao zinazoelekea kuunganisha jamaa, zimetokana na kanuni za adili na mawazo ya kijamaa yaliyotiwa ndani ya mwanadamu alipoumbwa. Kwa hiyo, katika mataifa yote twaona jamaa fulani zenye furaha ya kadiri fulani. Washiriki wa jamaa hizo wanao upendano wa asili. Kwa kawaida kupashana habari kwema na kufanya mambo pamoja ndiko huunganisha jamaa. Wanafanya kazi pamoja,”‏ wanacheza pamoja, na wanaheshimiana. Ingawa kichwa cha jamaa ndiye hufanya maamuzi ya mwisho juu ya mambo ya maana, kila mtu anaheshimiwa kwa kusikilizwa anapotoa maoni yake. Anajisikia yuko huru kutoa maoni, kusema na kutenda, lakini anazuiwa wakati tu anapoelekea kuharibu faida bora za jamaa na zake mwenyewe.

7. Zaburi 127:1 yaonyeshaje jambo la kwanza linaloleta furaha katika maisha ya jamaa?

7 Lakini ili tuwe na uhakikisho mkubwa zaidi kwamba furaha itakuwa ya kudumu isimalizwe na matatizo ya uchumi, vishawishi vya iitwayo “adili mpya” na mambo yenye kukatisha tamaa ya ulimwengu huu, lazima kwanza tuwe na uhusiano mwema na Mungu. Tukiupata uhusiano huo na kuuendeleza, mambo mengine yote ya maisha ya jamaa yatakuwa sawa, na hata yasipokwenda tunavyotaka nyakati nyingine, tunaweza kuyashughulikia kwa matokeo mazuri zaidi iwezekanavyo.​—Zab. 127:1.

8, 9. Kwa kutumia Warumi 7:19, 20, onyesha sababu gani ni lazima kujitahidi kutumia kanuni za Biblia.

8 Ni nini baadhi ya mambo yanayohusika katika kuendeleza uhusiano mwema na Mungu, kisha uhusiano huo na Mungu ulete uhusiano mwema kati ya washiriki wa jamaa?

9 Kwanza, lazima wapendane na kuoneana shauku, na kuonyesha kikweli sifa hizo. Wanadamu, ambao hapo mwanzo walifanywa ‘kwa sura ya Mungu,’ wanazo bado sifa hizo njema kwa kadiri fulani, ingawa dhambi imefanya sana zififie. (Mwanzo 1:26, 27) Kwa hiyo, ni lazima kujitahidi daima kutumia kanuni za Biblia zinazoongoza jamaa. Acheni tuangalie baadhi ya sifa hizo.

10. Ni ulinzi gani wa ndoa tunaopata katika Mwanzo 2:24, Mathayo 19:6 na Waebrania 13:4?

10 Hapo mwanzo Mungu alisema: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwa. 2:24) Yesu Kristo aliongeza hivi: “Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.” (Mt. 19:6) Kujua hivyo ni ulinzi, unaozuia mwanamume au mwanamke aliyeolewa asitazame wengine kwa macho ya tamaa, na unamzuia pia asitende mambo yanayoweza kuchafua ndoa, Mwana; mume au mwanamke anajua kwamba kukosa uaminifu katika ndoa kunaweza kuharibu furaha ya jamaa na kuvunja uhusiano wake na Mungu. Hata iweje, kufanya hivyo kunatia katika moyo na maisha ya kila mshiriki wa jamaa makovu ya daima.

MAONI YANAYOFAA JUU YA UKICHWA WA JAMAA YAENDELEZA FURAHA

11. Ni kwa njia gani mume ndiye kichwa cha jamaa?

11 Baada ya kukubali maoni haya ya umoja wa mume na mke, sasa twaona katika Biblia kwamba, lazima kuwe na utaratibu, ingawa ndoa ni mpango wa ushirikiano. Mungu ameleta utaratibu kwa kumfanya mume awe ndiye kichwa cha jamaa. Mume ndiye mwenye cheo cha kwanza, naye aweza kupewa maoni na kufanya maamuzi ya mwisho juu ya mambo yanayohusu hali njema ya jamaa. Paulo, mtume Mkristo, aliandika hivi: “Mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; . . . Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza.”​—Efe. 5:23-29

12. Kwa sababu gani kulingana na Waefeso 5:29 mume mwema hatumii mamlaka kwa ukatili, kwa hiyo atashughulikaje na washiriki wa jamaa yake?

12 Mume mwema atatambua daraka aliloamriwa na Mungu alitimize na kujaribu kuonyesha heshima, si kwa sababu yeye ni kichwa tu, wala si kwa kujidhania kuwa “bwana-mkubwa,” bali kwa sababu mkewe ni mwili mmoja naye na hataki kumwumiza wala kujiletea yeye mwenyewe (na Muumba wake) heshima mbaya kwa kutumia mamlaka kwa uonezi. Badala yake, atamtia mkewe moyo na washiriki wengine wa jamaa wawe huru kuelezana maoni na mawazo yao. Ataacha njia za kupashana habari zikiwa wazi na kuwa mwepesi na mpole wa kuambilika juu ya habari au tatizo lo lote. Ataheshimu maoni yao pia na kuyafikiria kwa kutumia haki, na kuwapa mamlaka fulani katika utendaji wao wa jamaa.

13, 14. Kwa kueleza masimulizi ya “mke mwema” yaliyomo katika Mithali 31, onyesha mamlaka na wajibu ambao aweza kupewa.

13 Kwa mfano, mara nyingi mke ndiye husimamia mambo ya nyumba. Biblia yasema hivi juu ya “mke mwema”: “Humtendea [mumewe] mema wala si mabaya.” “Hutafuta sufu na kitani; hufanya kazi yake ya mikono kwa moyo.” “Mume wake hujulikana malangoni; aketipo pamoja na wazee [wenzake] wa nchi.” “Wanawe huondoka na kumwita heri; mumewe naye humsifu.”​—Mit. 31:10,12,13, 23, 28.

14 Kutokana na hayo inaonekana kwamba mke apaswa kupewa hiari ya kusimamia mambo ya jamaa. Akijihakikisha kuwa mfanya kazi mwema, hodari na mwelekevu wa kufanya mambo hayo, kwa kawaida ndiye atakayetayarisha mapambo ya nyumba, ndiye atakayenunua chakula, na pengine atanunua pia vifaa kama meza, viti, na vitu vinginevyo vyenye kuendeleza furaha ya jamaa. Mume ataingilia mipango au matumizi ya mke wakati inapokuwa ya upumbavu tu au inapoelekea kumalizia jamaa pesa, au kuharibu hali yao njema.

15. Yampasa mume atoe shukrani za nini kwa mke mwema, na matokeo atakayopata ni nini akifanya hivyo, kama yaonyeshwavyo katika Mithali 31:23, 28 na 1 Wakorintho 11:7?

15 Mume mwenye shukrani hasahau kamwe kumtia mkewe moyo na kumshukuru kwa moyo wa kupenda kwa ajili ya kazi ngumu na mambo anayofanyia jamaa. Wenzi wa mume humheshimu kwa sababu sifa njema za mkewe zaonyesha yeye ana ukichwa mzuri na anamtunza kwa upendo. (1 Kor. 11:7) Mumewe na watoto pia husema mema juu yake kila wakati. Mume mwema wala mke mwema hadharau kamwe mwenzi wake kwa kumnenea yasiyofaa mbele ya wengine. Wanajizuia wasiletee jamaa aibu hivyo mbele ya wengine.

DARAKA LA MKE NI LA LAZIMA ILI KUWE NA FURAHA KATIKA JAMAA

16, 17. (a) Je! mke akiwa mtii kulingana na Maandiko, huo ni utumwa? (b) Mke mwema atatendaje katika hali ambamo mumewe amekataa jambo fulani linalohusu jamaa lisifanywe?

16 Mke aweza kusaidia sana kuleta furaha katika jamaa. Kwanza, yeye ajua shauri hili la Biblia ni la kweli “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu.” “Kama vile Kanisa limtiivyo Kristo, vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo.” “Mke asikose kumstahi mumewe.” (Efe. 5:22, 24, 33) Badala ya utii huo kuwa utumwa, unampa mwanamke uhuru wa kutochukua madaraka yale mazito ambayo lazima mume, ambaye ndiye kichwa, atimize mbele za Mungu na wanadamu.

17 Mke mwema hufahamu kwamba, hata ikiwa anadhani ana maoni mazuri juu ya jambo fulani, yampasa atii uamuzi wa mume ikiwa ana maoni tofauti. Asijifanye, kwa unafiki kwamba amekubali, na kumbe anatumia vipengee akijaribu kufanya alilokatazwa. Hata hivyo, ikiwa jambo hilo laweza kuchafua dhamiri ya Kikristo, Mkristo atamtii Mungu kwanza.​—Matendo 5:29.

18, 19. (a) Toa maelezo juu ya matokeo ya mke mgomvi, kama yanavyoelezwa katika Mithali 27:16. (b) Wakati mmoja wa wenzi wa ndoa anapoudhika kwa kuona kwamba mwenzake ni mwenye shingo ngumu au mwenye matata, yampasa akumbuke nini?

18 Mke mwema hufahamu pia kwamba, ingawa mumewe ameagizwa na Maandiko ‘asiwe na uchungu naye,’ lazima ajiangalie asimpe mumewe sababu ya kumwonea uchungu. (Kol. 3:19) Mume mwenye nia njema hatataka kugombana na mkewe, wala hatatumia nguvu aonyeshapo ukichwa wake. Matokeo ya mke asiyetii, mwenye hasira-hasira au mgomvi-mgomvi, yanaelezwa katika Mithali 27:16: “Atakaye kumzuia huyo huuzuia upepo; na mkono wake wa kuume hukuta mafuta.” Mume anatatizwa akilini, anashindwa kumzuia mkewe, na watu wote wanajua mke si mtiifu, kisha jamaa inaaibika.

19 Bila shaka, hali zenye kuudhi haziepukiki, kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu. Lakini kwa kawaida watu wanataka kuwa wenye furaha na si kawaida yao kujaribu kufanya matata. Kwa hiyo, badala ya wenzi wote wawili kujilipiza, watajiweza na kusema maneno yenye kuendeleza upendo na furaha.

WATOTO HULETA FURAHA

20-22. (a) Mtoto apaswa kuanzwa kuzoezwa kabisa wakati gani, na kwa sababu gani? (b) Kwa sababu gani hata kitoto kidogo kinaweza kuona kwamba hakipendwi au kinadhulumiwa, na kwa hiyo lazima wazazi waangalie mambo gani tangu kitoto kizaliwapo?

20 Watoto husaidia sana kuleta umoja na furaha nyumbani wakipendwa, wakishukuriwa na kuzoezwa vizuri. Mazoezi hayo yataanza wakati gani?

21 Kwanza, wazazi wasidharau akili ya kitoto kilichozaliwa karibuni. Kitoto si mtu hafifu tu. Kumbuka, kitoto kinazaliwa kikiwa na sifa za kimungu, upendo na haki ya hukumu. Yeye ni kiumbe mwenye akili sana. Kama mtoto angalikuwa na maarifa na ujuzi, angalikuwa na akili ya mtu mzima. Mtoto wa kibinadamu si kama wa wanyama ambaye hujikuta amejua mambo azaliwapo, bali lazima ajifunze karibu mambo yote. Kwa hiyo yeye huingiza akilini mambo yote aonayo na kusikia, kwa bidii nyingi. Hivyo mazoezi huanza kitoto kizaliwapo, kwa maana kila jambo linalosemwa au kufanywa kikiwapo yapaswa kuwa yenye kujenga. Lazima kipendwe sana. Tena, kikifanya kosa lo lote chapaswa kusahihishwa kwa fadhili na huruma.​—2 Tim. 3:15; 1:5.

22 Kumbuka kwamba mtoto ni chapa yako wewe. Mtoto hapendi watu wakiongea naye kwa usemi wa kipuzi, sawa na vile wewe usivyopenda. Maisha si jambo la mchezo naye mtoto hutaka kufanya mambo kama watu wazima. Kwa kuwa mtoto si mjanja, yeye huona upesi akitendewa udhalimu, kwa unafiki au bila upendo. Ndiyo sababu sifa za haki ya hukumu, upendo, rehema na matunda mengine ya roho hayapaswi kuepukwa wakati wa kushughulika na mtoto. Lazima yasitawishwe pia katika mtoto tangu mwanzo.​—Mit. 22:6.

23, 24. (a) Kwa sababu gani kumfukuza mtoto anapouliza maulizo, au kutopendezwa na mambo anayofanya kunamshusha moyo? (b) Ikiwa mzazi hawezi kusikiliza wakati anapoulizwa maulizo, anapaswa kufanya nini?

23 Baadaye huenda mtoto akakujia amekukodolea macho, akitaka kukuuliza ulizo, au kukuonyesha kwa uchangamfu kitu ambacho amegundua. Ukimfukuza kwa kumwambia, “Usinisumbue sasa,” utamshusha moyo. Wewe, ambaye alikutegemea sana, utakuwa umemkatisha tamaa. Huenda akakosa kusema neno, lakini anakuwa na kovu la daima, kisha kunaanza kuwa na mtengano kati yenu.

24 Lakini namna gani ikiwa kweli una kazi nyingi wakati huo? Mweleze kwa upole, sawa na vile ambavyo ungeeleza mtu mzima, sababu gani huwezi kuwa na wakati saa hiyo, na kwamba mtalizungumza jambo lenyewe baadaye. Halafu hakikisha utafanya hivyo upesi iwezekanavyo. Mtoto aweza kuzoezwa kwa upendo afahamu kwamba ziko nyakati zinazofaa mambo fulani.

25, 26. Je! kuna faida ya kuzungumza na mtoto na kumpa sababu za mambo hata akionyesha tamaa au nia mbaya?

25 Tangu wanapokuwa wachanga, watoto hutaka kupewa sababu. Wakati fulani uliopita onyesho moja lipendwalo sana la televisheni lilionyesha vijana wa masomo ya juu pamoja na wazazi wakihojiwa. Mwandikaji wa kitabu kinachohusu uhusiano wa wazazi na watoto alikuwako. Wakati hali inayotokea katika maisha ya kweli ilipoonyesha mzazi akieleza kijana sababu ya kumkatalia ombi lake, mwandikaji alimwambia mzazi huyo hivi: “Mimi nakupinga. Kama ingalikuwa mimi ningalimwambia, ‘Hapana, huwezi kupata utakacho.’ “Ndipo vijana wale wote waliposimama pamoja wakakataa. Walisema: “Twataka sababu, si amri za vivi hivi tu.” Kuzungumza na vijana kwa kuwaeleza sababu za mambo husaidia kuweka wazi njia za kupashana habari.

26 Mzazi akiona ni vigumu kuzungumza na watoto wake na kuwapa sababu, aweza kufuata maelezo mazuri sana ya kitabu cha Mithali, hasa sura saba za kwanza, zinazosimulia baba mcha Mungu akimpa mwanawe mashauri.

MUHTASARI

27. (a) Mume anaweza kuiga nani anapotumia ukichwa wake? (b) Kwa sababu gani kuitwa ‘binti wa Sara’ ni sifa njema kwa mwanamke, kama Petro asemavyo katika 1 Petro 3:6?

27 Kwa hiyo, kwa maana Mungu ndiye Mpangaji wa mpango wa jamaa, na kwa maana mwanadamu aliumbwa kwa mfano wa Mungu, mume mwema hutambua sifa za kimungu, tamaa na mawazo ya washiriki wa jamaa yake. Yeye hutumia ukichwa akimwiga Mungu na Kristo. Huonyesha kwamba anatambua Ukichwa wa Mungu juu yake na kuongoza jamaa yake iheshimu Ukichwa huo, zaidi ya mambo mengine yote. (1 Kor. 11:3) Wake wanaotambua kanuni hii wanafuata kielelezo cha Sara, Rebeka na wanawake wengine waaminifu waliomtumikia Mungu. Mke hawezi kupata sifa inayopita kuitwa ‘binti wa kweli wa Sara.​—1 Pet. 3:5, 6.

28, 29. Kwa sababu gani adabu zinahitajiwa na ni zenye manufaa? (Ebr. 12:9-11)

28 Kutakuwa na upendo na fadhili katika jamaa yenye furaha, lakini adabu hazitasahauliwa, kwa sababu wote wanahitaji mazoezi, hasa kwa sababu sisi ni watenda dhambi wasiokamilika. (Ebr. 12:9-11) “Adabu na rekebisho la moyoni la Yehova” ndio msingi wa kuzoezea watoto. (Efe. 6:4, NW) Hiyo inatia ndani kuzungumza nao na kuwapa sababu, si kutumia ukatili. Vile-vile, inatia ndani kuwawekea mfano kwa maana mzazi hufanya jamaa impende Mungu akiionyesha kwamba yeye anampenda kwa moyo wote.

29 Kila mmoja katika jamaa akitendea wengine kama vile Mungu amtendeavyo, bila shaka maisha ya jamaa yatakuwa yenye furaha.

[Picha katika ukurasa wa 102]

Wazazi wanapaswa kutumia kila nafasi kuhakikisha kwamba watoto wao wanajua jinsi vitu vilivyoumbwa na Mungu vilivyo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki