Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Je! Mashahidi wa Yehova wanamwamini Yesu Kristo?
Bila shaka tunamwamini. Tunakubali kwa moyo wote na kuhubiri kila jambo ambalo Neno la Mungu linasema juu ya Kristo. Hilo ni kutia na tangazo la mtume Petro: “Hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”—Matendo 4:12.
Hata watu wasio Mashahidi wa Yehova ambao wamechunguza mafundisho yetu yenye msingi wa Biblia wanafahamu kwamba tunamwamini Yesu. Kwa mfano, New Catholic Encyclopedia (1967) chasema katika makala yake “Jehovah’s Witnesses” hivi:
“Wao wanamwona Yesu kama mkubwa zaidi kuliko Mashahidi wa Yehova wote, ‘mungu’ (ndivyo wanavyotafsiri Yohana 1:1), asiye mdogo kwa ye yote ila Yehova. Kabla ya kuwako kama mwanadamu, yeye alikuwa kiumbe cha kiroho aliyeitwa Logos, au Neno, au Mikaeli Malaika Mkuu. Alikufa kama mwanadamu akafufuliwa kama Mwana wa kiroho asiyeweza kufa. Mateso yake na mauti yake ilikuwa ndiyo bei iliyolipwa ili awapatie tena wanadamu haki ya kuishi milele duniani.”—Vol. VII, uku. 864.
Basi yale maoni ya kwamba Mashahidi wa Yehova hawamwamini Yesu si ya kweli kabisa! Mara nyingi uongo huu mkubwa mno umeenezwa na wapinzani wa kidini kwa sababu Mashahidi wa Yehova hawafundishi Utatu. Wapinzani hawa wanashikilia sana imani yao ya fundisho la Utatu, kwamba Yesu alikuwa sehemu ya Mungu mwenye nafsi tatu, na kwamba alipokuwapo duniani alikuwa Mungu katika mwili.
Ukweli ni wa kwamba Mashahidi wa Yehova wanafahamu na kukubali kwamba Biblia inatumia mtajo huu “mungu” (god) kwa habari ya Yesu. (Yohana 1:1, 18, NW) Lakini Yesu mwenyewe alitumia maneno ya Zaburi 82:6, akikubali kwamba hata mahakimu wa kibinadamu wenye nguvu wanaweza kutajwa “miungu.” (Yohana 10:33-36) Hata Biblia inatumia neno hili “mungu,” ikimaanisha mwenye nguvu au yeye anayeabudiwa, kumaanisha Shetani. (2 Kor. 4:4) Kwa wazi ingekuwa makosa kukata shauri kwamba kwa vile neno hili “mungu” linatumiwa, kiumbe cho chote kilichopewa uzima na Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote kinalingana na Muumba mwenyewe.—Rum. 1:25.
Kwa wazi Yesu alikubali kwamba yeye hakulingana wala kuwa mtu yule yule kama Baba yake ambaye aliomba. Kristo alisema hivi: “Naenda kwa Baba; kwa maana Baba ni mkuu kuliko mimi.” Katika sala kwa Mwenye Nguvu Zote, Yesu alisema maneno haya yenye maana: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 14:28; 17:3.
Mashahidi wa Yehova wanakubali kabisa maneno haya yenye kueleweka ya kweli. Nasi tuna bidii katika kazi ya maana ya Kikristo ya kusaidia wengine wajue na kuyakubali yale ambayo Biblia inasema juu ya ‘Mungu Yehova wa pekee wa kweli na juu ya Yesu Kristo, ambaye alituma.’
● Pesa ambazo yule mjane-mke alitoa zilikuwa kiasi gani?
Yesu Kristo aliona wakati mmoja mjane-mke mwenye shida akitumbukiza sarafu mbili ndogo katika sanduku la hazina ya hekalu. (Marko 12:42) Kulingana na andiko la asili la Kigiriki, kila mojawapo ya sarafu hizo ilikuwa lepton, na hiyo ndiyo iliyokuwa sarafu ndogo zaidi ya shaba nyekundu ya Kiyahudi wakati huo. Mchango wa mwanamke huyo wa lepta mbili ulikuwa kiasi cha moja juu ya 64 cha mshahara wa siku. Mtu angeweza kununua nusu shomoro (namna ya ndege) akiwa na kiasi hicho kidogo, nacho kipande hicho cha ndege huyo kilikuwa kidogo sana kisiweze kumshibisha hata chakula kimoja. (Mt. 10:29; sarafu inayotajwa katika andiko hili ni assarion, inayolingana na lepta nane.) Mwanamke huyo alichanga kuonyesha alimpenda Mungu wa kweli aliyeabudiwa katika hekalu hilo. Akilinganishwa na uwezo wake, mwanamke huyo alitoa zawadi kubwa zaidi kuliko wale waliotoa michango mingi lakini kwa sababu walikuwa wamezidiwa na pesa zao.—Marko 12:43, 44.