Kutangaza Habari Njema Katika Dunia Yote
“Sauti yao imeenea duniani mwote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu.”—Rum. 10:18.
1. (a) Sasa tumefikia siku gani kubwa? (b) Twawezaje ‘kujihakikisha kuwa tayari’? (Marko 13:32-37)
WAKATI unakwisha haraka! Kizazi hiki sasa kimeona sehemu kubwa ya “ishara” kuu ya unabii wa Yesu ikitimia tangu 1914, inayoeleza habari za “mwisho wa taratibu ya mambo.” “Dhiki kubwa ambayo haijapata kutokea tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatokea tena,” inakaribia kutokea ikiwa na mshindo mkuu katika dunia yote. Lazima tuendelee kukesha na kuwa macho, kuwa tayari sikuzote. Ni kama vile Yesu alivyosema: “Kwa sababu hiyo ninyi pia jihakikisheni wenyewe kuwa tayari, kwa sababu katika sasa msiyodhani kuwa ndiyo hiyo, Mwanadamu [Kristo Yesu] anakuja.” Saa ya Yehova ya kufanya hesabu na ulimwengu wa Shetani inakaribia sana!—Mt. 24:3, 21, 22, 34, 42, 44, NW.
2. Twawezaje kuepuka kuzishiriki dhambi za Babeli Mkuu? (Yer. 51:6)
2 Kujitayarisha kwatia ndani na kujitenga kabisa na dini yote ya kilimwengu ya uongo na kuendelea kuwa hivyo. (Yak. 1:27) Wale wanaompenda Mungu na kweli wanaambiwa waziwazi hivi: “Tokeni kwake [Babeli Mkuu], enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake. Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake.”—Ufu. 18:4, 5.
3. Ni matendo gani yameonyesha dini ya uongo yastahili kuharibiwa tu?
3 Katika Jumuiya ya Wakristo na nchi zisizo za Kikristo, milki hiyo ya ulimwengu ya dini ya uongo imekuwa na matendo ya kutisha. Imemkataa Mungu wa kweli aliye hai, Yehova, isitake hata kutaja jina lake. Imefundisha mafundisho ya uongo ya kishetani, kama vile kutokufa kwa nafsi na mateso ya wafu katika moto wa milele. Baraza zake za kukomesha uzushi, vita vyake na maonezi yake yametesa mamilioni ya watu yakawaletea msiba. Kumbuka kwamba vile vita viwili vya ulimwengu vya karne hii, vilivyoua watu milioni 69, vilianza katika Jumuiya ya Wakristo kati ya nchi zinazojidai kuwa za Kikristo. Looo! jinsi Jumuiya ya Wakristo ilivyo na hatia nyingi! Ushirikina wa dini ya uongo, ubashiri wake, uchawi na matumizi ya dawa za uchawi pia yanamchukiza Yehova.—Kum. 18:9-13; Isa. 65:11, 12.
4. Waabudu wa kweli wanatakiwa wachukue hatua gani njema?
4 Walakini, haitoshi kutoka tu katika dini ya uongo. Ni lazima kuingia katika safina ya ulinzi wa kiroho ambao Yehova afanya upatikane leo. Huo si mjengo halisi, si hekalu fulani wala si mahali halisi palipo duniani. Ni kama vile Mwana wa Mungu, Kristo Yesu, alivyosema: “Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” (Yohana 4:24) Kwa hiyo waabudu wa kweli wa Mungu hawajitengi tu na ibada yote ya sanamu na mazoea ya ushirikina; bali wanajifunza na kutumia pia Neno la Mungu katika maisha zao, kusitawisha nyutu za Kikristo nao wanatumikia ‘kwa roho,’ wakimpenda Mungu na jirani kwa moyo na nafsi.—Marko 12:28-31.
KUUAWA KWA ADUI ZA MUNGU
5. Dini ya uongo itahukumiwaje? (Yer. 25:34, 36)
5 Yehova atahukumu milki ya ulimwengu ya dini ya uongo kwa ghafula sana! Ufunuo 18:21 waeleza hivi: “Malaika mmoja mwenye nguvu akainua jiwe, kama jiwe kubwa la kusagia, akalitupa katika bahari, akisema, Kama hivi, kwa nguvu nyingi, utatupwa Babeli, mji ule mkuu, wala hautaonekana tena kabisa.” Hukumu yake itafanywa haraka nayo haitarudiwa tena.
6. Kwa sababu gani zile “pembe kumi” zitashindwa kushambulia wafuasi wa “Mwana-Kondoo”? (Mt. 10:28)
6 Lakini si hayo tu yatakayotukia! Zile “pembe kumi” za mnyama zitageukia dini ya kweli baada ya hapo, na hivyo ‘zifanye vita na Mwana-Kondoo,’ Kristo Yesu. (Ufu. 17:12-14) Haziwezi kumfikia Kristo katika kiti chake cha kifalme mbinguni, lakini zinadhani zinaweza kuwafikia wanafunzi wake hapa duniani wanaoelekea kutokuwa na ulinzi. Je! “pembe” hizo za kisiasa zitafaulu katika shambulio lao? Sivyo? Kwa maana watumishi wenye kushikamana na Yehova watasimama imara wapinge shambulio hilo la mwisho la kishetani, kama wanavyofanya sasa katika nchi nyingi za Afrika, za Mashariki na za Ukomunisti.
7. Kwa sababu gani matukio yatakayokuwa katika Har–Magedoni na baada ya hapo yaweza kusimuliwa kuwa “habari njema”? (Ufu. 14:6, 7)
7 Ndipo “wafalme wa ulimwengu wote” wa kisiasa watakapojikuta katika hali ya ulimwengu iitwayo Har–Magedoni, na hapo ndipo “Mwana-Kondoo atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme.” (Ufu. 16:14, 16; 17:14) Mwishowe Kristo mwenye ushindi atamtupa Shetani na mashetani wake katika shimo refu wasimoweza kufanya lo lote, kisha utawala Wake mtukufu wa miaka elfu uanze kubariki wanadamu wote. Lo! hizo ni “habari njema” zenye kupendeza namna gani!
PARADISO YENYE FURAHA!
8. Ni paradiso gani ya furaha ambayo tayari yapatikana kwa wale wanaompenda Yehova? (Isa. 35:10)
8 Hizo ndizo baraka wanazopata wampendao Yehova—si baada ya lile pigano kuu katika Har–Magedoni tu, bali sasa pia! Kwa maana katika huu wakati wa mwisho ‘mlima wa nyumba ya Yehova [yaani, mahali pa ibada yake ya kweli], umekwisha ‘wekwa imara juu ya milima,’ naye Babeli Mkuu aendesha madhehebu zake juu ya “milima” hiyo. Lo! furaha wee! Maelfu ya watu wa mataifa wanamiminika kwenye Majumba ya Ufalme na mahali penginepo, wajiunge na watu wa Yehova katika ibada ya kweli. Ni kama vile unabii usemavyo: “Mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova]. . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.”—Isa. 2:2, 3.
9. Ni kwa kadiri gani paradiso ya kiroho imerudishwa sasa?
9 “Mkutano mkubwa” umejiunga na mabaki waaminifu wa mashahidi wa Yehova waliotiwa mafuta walioendelea na kazi na wakavumilia mateso siku za mwanzo-mwanzo wa huu “wakati wa mwisho.” Ni umati mkubwa sana uliojiunga nao! Hiyo yaonyeshwa na uhakika wa kwamba, mwaka wa 1976 zaidi ya watu 4,870,000 walikusanyika katika makundi zaidi ya 39,600 ya Mashahidi wa Yehova duniani pote, katika mwadhimisho wa kila mwaka wa Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Kweli paradiso ya kiroho imeenea katika dunia yote!—Dan. 12:4; Ufu. 7:9.
10. (a) Paradiso ya kiroho itakuwaje kama safina? (Isa. 26:20, 21) (b) Dunia yote itakuwaje mfano wa paradiso ya kiroho? (Zab. 72:18, 19)
10 Paradiso hii ya kiroho itakuwa kama Safina ya ulinzi, yenye abiria wenye thamani kuu, itakapokuwa ikipita “dhiki kubwa” kuingia katika dunia isiyo na uchafu! Wakati huo watawala wakatili hawataonea watu wala kuwatesa tena. Haitakuwa lazima tena waabudu wa Yehova wapigane na Shetani na ulimwengu wake wenye ufisadi. “Mkutano mkubwa” watakuwa na kazi inayofaa, inayothawabisha na kusisimua, ya kugeuza dunia yote iwe paradiso halisi yenye uzuri mwingi, ikiwa mfano wa paradiso ya kiroho ambayo Isaya aliandika habari zake akasema: “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi. Litachanua maua mengi, na kufurahi, naam, kwa shangwe na kuimba; . . . watauona utukufu wa [Yehova], ukuu wa Mungu wetu.”—Isa. 35:1, 2.
11. Biblia inatoa uhakikisho gani kwamba wafu hawatasahauliwa?
11 Wala wafu hawatasahauliwa! Ni wangapi wanaoishi duniani leo wawezao kukumbuka au hata kutaja majina ya babu zao walioishi miaka mia moja iliyopita? Ni wachache sana! Lakini Mungu awakumbuka. Akumbuka babu zetu wote, ambao wamefanya kazi ngumu na kutaabika miaka elfu sita iliyopita ya historia ya kibinadamu. (Yohana 5:28, 29; Marko 12:26, 27) Kwa sababu ya dhabihu ambayo Yesu aliitoa kwa upendo, Yehova, ambaye ndiye Mungu mkuu mwenye fadhili za upendo, atawafufua wadogo kwa wakubwa, Watasimama mbele za kiti chake cha ufalme, wakiwa na nafasi ya kutimiza matakwa yake zaidi ya kuingia katika maisha mengi yenye furaha yanayoendelea milele, (Ufu. 20:12) Hizo zote ni habari njema kweli kweli! Lo! jinsi imetupasa tumshukuru sana Mungu wetu mtukufu, Mtoaji wa habari njema!
HABARI NJEMA KWA JAMAA ZETU
12. Katika Wakolosai, sura ya 3, kuna mashauri gani ya upendo kwa jamaa?
12 Yatupasa tutake kutii “habari njema” katika jamaa zetu. Kwa maana habari njema zinaweza kutusaidia tuishi maisha yenye furaha pamoja, sasa na mpaka wakati ujao. Kitabu cha Habari Njema, Biblia, kinatupa kanuni njema kweli kweli zinazohusu jambo hilo! Kwa mfano, ukisoma tu sura yote ya tatu ya Wakolosai, utakuta mashauri yenye upendo ya kusaidia jamaa zote zivumilie mikazo mikubwa sana juu ya huu “wakati wa mwisho.” Si vigumu mno kufaulu pamoja kama jamaa katika nyakati hizi zenye hatari, hasa ‘mnapojivika upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.’—Kol. 3:14.
13. Ni mifano gani ya Maandiko inayoonyesha ubora wa kuongoza watoto tangu wanapokuwa vitoto vichanga?
13 Namna gani watoto wetu? Twawapenda na twataka watupende. Kwa hiyo wazazi wanaweza kufuata vielelezo bora vya kulea watoto vinavyoonyeshwa katika Neno la Mungu, navyo vilisaidia kutokeza wateteaji thabiti wa kweli kama Samweli, Daudi, Yohana Mbatizaji, Timotheo, na pia Bwana wetu mwenyewe, Yesu! Lakini yatupasa tuangalie watoto wetu na kuwaongoza tangu wanapokuwa vitoto vichanga wakuze nyutu za Kikristo. Hatuwezi kutazamia kuwe na ukamilifu katika ulimwengu huu usiokamilika, lakini tunaweza kutazamia kwamba Yehova atatubariki kwa jitihada zetu, kwa maana Zaburi 127 (mstari wa 3, NW) yasema watoto wetu ni “urithi kutoka kwa Yehova,” nao watafurahisha wazazi waliowalea katika njia Yake.
KUSIMAMA IMARA KWA AJILI YA UFALME
14. Ni njia gani ya maisha itakayoongoza kwenye furaha ya milele?
14 Je! hatuna furaha kwa vile tumepata kumjua Yehova na Mwanawe? Kumjua kumetuingiza katika njia ya uzima inayoongoza kwenye furaha ya milele. Ni maisha yenye utendaji na yenye maana. Yanategemea kuonyesha kwetu upendo mwingi sana kwa Yehova na upendo wa kujitoa tutumikie jirani zetu, na hasa jamaa zetu wenyewe na ndugu zetu. Si lazima tufuate orodha ndefu yenye makatazo ndipo tuishi. kupatana na kweli. Yako mambo machache “yaliyo lazima” tunayopaswa kujiepusha nayo, mambo ambayo yangetudhuru kiroho, kwa mfano yale yanayotajwa katika Matendo 15:28, 29: Ibada ya sanamu, damu, uasherati. Lakini maisha yetu ya Kikristo yapaswa kupatana kabisa na kweli, tuwe wenye furaha kama watumwa wa Mungu walio wakf na waliobatizwa. Ni maisha yenye kusudi. Tutakuwa wenye furaha sana, kutoka sasa na kuendelea mpaka dunia ya paradiso, tukitii sana maneno ya Paulo: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa Bwana, wala si kwa wanadamu, mkijua ya kuwa mtapokea kwa Bwana ujira wa urithi.” (Kol. 3:23, 24) Nayo kazi kubwa ambayo lazima ifanywe leo ni kuzihubiri “habari njema hizi za ufalme” katika dunia yote kama ushuhuda kabla ya mwisho kuja!—Mt. 24:14, NW.
15. Ni mambo gani ya “habari njema” ambayo hayajatimizwa bado yanayopaswa kujaza mioyo yetu na sifa?
15 Tunatazamia wakati ambao Yehova ataumba “mbingu mpya na dunia mpya” ambamo “haki itakaa.” Lo! itakuwa siku tukufu namna gani wakati washiriki wote 144,000 wa “Bibi-arusi” wa Kristo watakapoungana naye mbinguni kwa kufufuliwa kama viumbe vya kiroho, na wakati jamii mpya iliyo safi ya wanadamu itakapokuwa ikitenda kazi kabisa duniani! Uhalisi wa “habari njema” hizi unajaza mioyo yetu kumsifu Mungu mkuu anayefanya “yote kuwa mapya” na anayeahidi ‘kufuta kila chozi’ na kuondoa mambo yote yanayoleta kilio au maumivu. Naam, hata kifo ambacho ni adui kitakwisha katika utawala mtukufu wa ufalme wa Kristo. Wakati sisi leo tunaposimama imara kwa ajili ya ufalme huo, na kwa kuunga mkono enzi kuu ya Yehova, na tufanye yote tuwezavyo ili mwishowe tupatikane “bila doa na bila waa na katika amani.”—2 Pet. 3:13, 14, NW; Ufu. 21:1-5; 1 Kor. 15:25, 26.
KUNA KAZI YA KUFANYA!
16. Ni kazi gani kubwa ambayo lazima imalizwe? (Yohana 14:12)
16 Wakati Yesu alipokuwa duniani, alianza jambo ambalo lapaswa likue mpaka liijaze dunia. Hata katika kizazi hicho ilisemwa hivi: “Habari njema hizo . . . zilihubiriwa katika kuumba kote kuliko chini ya mbingu.” (Kol. 1:23, NW) Lakini, Yesu mwenyewe alitabiri kwamba ushuhuda mkubwa zaidi ungetolewa wakati wa “mwisho wa taratibu ya mambo,” akasema kwamba “sharti Injili ihubiriwe kwanza katika mataifa yote.” Halafu? “Hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Marko 13:10; Mt. 24:3, 14, NW) Je! sasa kazi hiyo ya kuhubiri imemalizwa? Sivyo! Kwa maana mwisho haujaja bado.
17. Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova watajishughulisha mpaka wakati wa “dhiki kubwa”? (Isa. 6:8, 11)
17 Mwisho hautakuja kwa sababu tu sisi twadhani wakati wake umefika. wala kwa sababu twadhani tumefanya kazi vya kutosha katika eneo letu. Utakuja wakati Yehova atakapokuwa ameimaliza kazi ile kuu ya kuuhubiri Ufalme kwa kadiri anavyotaka, na ndipo atakapoleta “dhiki kubwa.” Kabla wakati huo haujafika iko kazi ya kufanya! Nasi Mashahidi wa Yehova ndisi tumepewa mgawo wa kuifanya! “Dhiki kubwa” ifikapo yapaswa kazi ya kuhubiri iwe imesonga mbele kwa haraka sana katika dunia yote. Bwana Yesu atafika kufikiliza hukumu kwa ghafula kabisa—hata watu wa Yehova hawatakuwa wakimtazamia wakati huo, kwa maana bila shaka atawakuta wakiwa na shughuli nyingi zaidi kuliko wakati mwingine wo Wote!
18. Kwa sababu gani ni lazima “kukesha”? (Luka 21:34-36)
18 Yesu atuambia hivi: “Angalieni, kesheni, kwa kuwa hamjui wakati ule utakapokuwapo. . . . Kesheni.” (Marko 13:32-37) Namna gani kama mwaka wa 1914, mwaka wa 1925, mwaka wa 1975 au wakati mwingineo Mashahidi wa Yehova wangalilegea na kuacha kukesha na kufanya mipango ya wakati ujao, wakiitazamia “dhiki kubwa”—je! kungalikuwa na paradiso ya kiroho yenye kupanuka kama tunavyoiona ikipanuka leo? Jinsi tulivyo na furaha kwa vile Yehova ametia watu wake bidii waendelee kuzitangaza habari njema katika dunia yote!
19. Katika siku zetu, maana yake nini kumwabudu Mungu kwa roho na kweli? (Ufu. 7:15)
19 Jamii ya Yehova ya kitheokrasi itakuwa tengenezo lenye kusonga mbele, itasonga mbele mpaka ikaipite “dhiki kubwa.” Kwa maana kuabudu Mungu kwa roho na kweli kunaelekea upande ufaao, ni kwenye shauku, uchangamfu na maendeleo. Sasa sehemu zaidi na zaidi za dunia, katika nchi za Magharibi, katika nchi za Mashariki na kwingineko, zinapokea ushuhuda kamili, na hakuna mtu anayejua “habari njema zenye utukufu” zitaendelea kutangazwa kadiri gani kabla ya mwisho! Kama Paulo alivyosema, “ole” ni wetu tusipozitangaza habari njema, kwa maana kufanya kazi hiyo ni mapenzi ya Mungu leo!—1 Kor. 9:16.
20. Ni kwa njia gani “imani chanzo chake ni kusikia”? (Rum. 10:10)
20 Yesu mwenyewe aliweka kielelezo cha kuzitangaza habari njema, nao wafuasi wake waliotiwa mafuta wamefuata nyayo zake mpaka leo hii. Alipokuwa akitaja hilo, mtume Paulo alitaja Isaya 52:7, akasema: “Ni mizuri kama nini miguu yao wahubirio habari ya mema!” Sasa katika dunia yote “mkutano mkubwa” unajiunga na mabaki waliotiwa mafuta kuzitangaza habari njema. Lakini si watu wote wanaoutii ujumbe huo. Paulo atuambia hivi: “Lakini si wote walioitii ile habari njema. Kwa maana Isaya asema, Bwana, ni nani aliyeziamini habari zetu? Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo. Lakini nasema, Je! wao hawakusikia? Naam, wamesikia, Sauti yao imeenea duniani mwote, na maneno yao hata miisho ya ulimwengu.”—Rum. 10:15-18; Isa. 53:1; Zab. 19:4.
21. Ni nini kinachoonyesha “habari njema” hazishindiki? (Ufu. 10:7)
21 Leo hali inafanana na ile iliyokuwako siku za Paulo. “Habari njema zenye utukufu za Mungu aliye na furaha,” zinazohusu Kristo wake, zinatangazwa katika sehemu za mbali zaidi za dunia. Katika nchi nyingine, watawala wakatili au dini za Kibabeli zilizoimarika sana katika nchi hizo, wamejaribu kuzuia nuru ya kweli ising’ae. Lakini habari njema zinaendelea kutangazwa, na mahali pengi zaidi na zaidi watu wanaamini wasikiapo.
22. Tunapotazamia ushindi wa “habari njema,” yatupasa sasa tuwe tunafanya nini?
22 Miguu yetu na iendelee ‘kufungiwa utayari tupatao kwa Injili ya amani,’ nasi tuendelee “kuishuhudia Habari Njema ya neema ya Mungu,” kama Paulo. (Matendo 20:24; Efe. 6:15) Naam, ‘mwenendo wetu na uwe kama inavyoipasa Injili ya Kristo, tusimame imara katika roho moja, kwa moyo mmoja tukiishindania imani ya Injili; bila kuogopa adui zetu.’ (Flp. 1:27, 28) Lazima “habari njema” (au Injili) zishinde! Kila mmoja wetu na ajishughulishe sana ‘kuzitangaza habari njema katika dunia yote.’ Kwa njia hiyo tutaendelea kuwa wenye furaha, nasi tutafurahisha wengi kweli kweli!
—Kutoka The Watchtower, Nov. 15, 1976.