Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 12/1 kur. 535-540
  • Habari Njema kwa Wanadamu Wote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Habari Njema kwa Wanadamu Wote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO NDANI YAZO
  • TANGAZO LILILOENEZWA
  • MFALME ATAWAZWA
  • KUWA ULIZO KUU
  • ‘Habari Njema Zenye Utukufu Kutoka kwa Mungu Aliye na Furaha’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • “Habari Njema”!
    ‘Mwimbieni Yehova kwa Shangwe’
  • Kutangaza Habari Njema Katika Dunia Yote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Habari Njema ya Ufalme Yahusu Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 12/1 kur. 535-540

Habari Njema kwa Wanadamu Wote

1-3. Kuna habari njema kwa nani, na ni mahali gani pa pekee tuwezapo kuzipata?

HABARI NJEMA! Katika ulimwengu huu yaliyo habari njema kwa mtu mmoja mara nyingi ni habari mbaya kwa mwingine. Na inasikitisha kwamba habari njema zinafuatana sana na habari mbaya maishani.

2 Hata hivyo, ziko habari njema kwa wanadamu wote zisizofuatana na habari mbaya kwa wapendao haki. Ni habari njema kwa watu kama hao bila ya kujali taifa lao, rangi wala hali ya maisha.

3 Yehova Mungu, Muumba wa wanadamu, ndiye Chanzo cha habari njema hizi. Biblia ndilo Neno lake la kupashana habari nasi. Tazama po pote pale, huwezi kuzipata hizi habari njema penginepo. (Gal. 1:6, 7, 11, 12) Mtume Paulo, mhudumu aliyeagizwa na mtume, alichaguliwa waziwazi na Kristo mwenyewe kama mhubiri wa habari njema kwa mataifa yasiyo ya Kiyahudi. Zamani wakati wa Paulo, walikuwako Wakristo wachoyo wenye kupotoa habari njema. (2 Kor. 11:4) Paulo aliandika hivi kwa mkazo: “Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe.”​—Gal. 1:8, 15, 16.

YALIYOMO NDANI YAZO

4. Kwa ufupi, habari njema zikoje?

4 Habari njema za kweli ni zipi, kama zilivyotangazwa na mitume wa Yesu Kristo? Kwa ufupi, ndizo hizi: Mungu amepanga na kutayarisha iwepo serikali ya pekee ya kutatua magumu ya dunia hii. Itatawala ikiwa peke yake na bila ya kuvurugwa kwa miaka elfu. Wakati huo itaondoa kila kitu kilichopata kutokeza habari mbaya. Wakaaji wote wa dunia wanaotaka kuishi kupatana na Mungu na wanadamu wenzao watakuwa hai, nazo habari mbaya za zamani hazitalemea mioyo yao kwa njia yo yote, zikiwakosesha furaha. Kwa unabii mtumishi wa Mungu Isaya alisema hivi: “Mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.”​—Isa. 65:17.

5, 6. (a) Kwa sababu gani yaweza kusemwa kwamba sasa twaishi katika wakati wenye furaha? (b) Kwa sababu gani Mungu hajayaleta mambo yote mema yaliyomo katika habari njema?

5 Anayoyasema Mungu hayawezi kukosa kutimia, naye anayo orodha ya wakati ya matendo yake yote. (Ebr. 6:18; Isa. 46:11; linganisha Wagalatia 4:4.) Tukitumia wakati kulichunguza Neno lake, twaona kwamba sasa twaishi katika wakati wenye furaha sana kuhusiana na habari njema. Kwa sababu gani? Kwa sababu unabii mbalimbali wa Biblia unaotimia na mambo yanayotokea yanaonyesha kwamba Mungu amekwisha mweka mfalme wake wa Kimasihi juu ya kiti cha enzi mbinguni na kwamba utawala wake wa miaka elfu umetukaribia sana.

6 Walakini, huenda mtu akasema, ‘Sababu gani kuendelea kuzungumza juu ya “habari njema”? Kwa sababu gani Mungu hajayaleta mambo haya yote yaliyo mema duniani?’ Kwa maana yeye anaiheshimu akili na uhuru wa hiari aliotupa​—haki ya kuchagua njia tunayotaka kufuata​—kama tutainyenyekea enzi kuu ya Mungu au tutachagua utawala wa wanadamu. Mungu ameruhusu wanadamu wajaribu kila namna ya serikali iliyowazika, na kufikia sasa watu wote wenye akili wameona kwamba “njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake.” (Yer. 10:23) Zaidi ya hayo, kama ilivyotangulia kutajwa, Mungu anayo orodha ya wakati ambayo katika hiyo anafanyiza mambo kabisa kwa faida ya wote. Sasa anaruhusu wanadamu wakati wa kutosha pia waweke msingi imara wa imani katika serikali yake ya Kimasihi.

7-9. (a) Habari njema alizoambiwa Ibrahimu zilikuwa nini? (b) Twajuaje uliokuwa uzao ambao kupitia kwao baraka zilizoahidiwa zingewajia wanadamu? (c) Kwa sababu gani agano la Torati halikuitangua ahadi aliyopewa Ibrahimu? (d) Kwa hiyo ni kwa sababu gani Torati ilitolewa?

7 Hii imefanywaje? Ebu na tuendelee kuona aliyoyasema mtume Paulo juu ya habari njema alizokabidhiwa: “Na andiko, kwa vile lilivyoona tangu zamani kwamba Mungu atawahesabia haki Mataifa kwa imani, lilimhubiri Ibrahimu habari njema zamani, kusema, Katika wewe Mataifa yote watabarikiwa. Basi hao walio wa imani hubarikiwa pamoja na Ibrahimu aliyekuwa mwenye imani.”​—Gal. 3:8, 9; Mwa. 12:3; 22:18.

8 “Mataifa yote” watabarikiwa kupitia kwa Ibrahimu. Mungu alimwambia hivi Ibrahimu Mwebrania kabla ya kutokea kwa taifa la Kiyahudi. Kwa hiyo, ijapokuwa baadaye Mungu alishughulika na Wayahudi peke yao kwa kitambo, baraka kamili ni ya watu wa mataifa yote.

9 Mtume Paulo anasema baraka hii itakujaje? Anaeleza hivi: “Basi ahadi zilinenwa kwa Ibrahimu na kwa mzao wake. Hasemi, Kwa wazao, kana kwamba ni wengi, bali kana kwamba ni mmoja, Kwa mzao wako, yaani, Kristo.” (Gal. 3:16) Kwa hiyo, baraka ilipaswa ije kupitia kwa “mzao” mmoja wa Ibrahimu, yaani, “Kristo.” Paulo anaendelea kusema kwamba agano la Torati, lililofanywa karne nyingi baada ya ahadi hii kwa Ibrahimu, bila shaka halikuitangua ahadi iliyofanywa kwa Ibrahimu. “Torati ni nini basi?” anauliza. Anaeleza kwamba iliwaonyesha wanadamu kuwa wenye dhambi, wakihitaji msaada wa Mungu. Ilielekeza kwenye Uzao mkuu wa ahadi ambao kupitia kwao baraka zingewajia wanadamu: “Hivyo torati imekuwa kiongozi kutuleta kwa Kristo.”​—Gal. 3:19-29, 7-9.

10. Yohana Mbatizaji alikuwaje wa kwanza kuzifahamu habari njema za kwamba Masihi alikuwa amekuja?

10 Kwa hiyo, kufika kwa Masihi kulikuwa habari njema bila shaka. Wakati Yesu alipomfikia Yohana Mbatizaji akabatizwa, nayo roho takatifu ikajionyesha juu yake kwa umbo lenye kuonekana la hua, Yohana alipata uhakikisho kwamba Masihi aliyekuwa amengojewa kwa muda mrefu alikuwa amefika kweli.​—Mt. 3:16, 17; Yohana 1:32-34.

TANGAZO LILILOENEZWA

11. Nyingine za njia ambazo kwazo Kristo Yesu alifunua mambo fulani ya habari njema alipodhihirishwa ni nini?

11 Mambo haya yalipotukia habari njema zilienezwa sana na kutiwa nguvu nyingi. Paulo anasema kwamba Kristo Yesu ‘aliufunua uzima na kutokuharibika, kwa ile Injili’ alipodhihirishwa. (2 Tim. 1:10) Tangu wakati huo na kuendelea, mambo ya habari njema yalieleweka zaidi. Yesu Kristo alikuwa ndiye Masihi aliyeahidiwa, yeye ambaye dhabihu yake ililipia dhambi za wanadamu. Huyu Ndiye ambaye angekuwa Mfalme. Ufalme wake ungetawala kutoka kiti cha enzi cha kimbinguni, si cha kidunia. Pia, ilionyeshwa wazi kwamba muda mrefu ungepita kabla baraka kamili za ufalme hazijawajia wanadamu wote. Yesu mwenyewe alisema kwamba mataifa yangetawala dunia “hata majira ya Mataifa yatakapotimia.” (Luka 21:24) Huu ulikuwa mtajo juu ya unabii wa Danieli wa “nyakati saba,” zilizoanza tangu kuharibiwa kwa Yerusalemu na Babeli mwaka wa 607 B.C.E., kupita wakati Yesu alipozungumza, na kuendelea mpaka Oktoba wa mwaka wa 1914 C.E.a​—Dan. 4:16, 23, 25, 32.

12. Ni nini kilichotukia tangu wakati wa ufufuo wa Kristo mpaka mwisho wa “majira ya Mataifa”?

12 Ni nini kilichopaswa kitukie wakati huo wote? Twaambiwa, katika Waebrania 10:12, 13, kwamba Kristo “alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu.” Baada ya kufufuliwa kwake na kupaa mbinguni “Kristo hakuingia katika patakatifu palipofanyika kwa mikono [kama vile hekaluni Yerusalemu], ndio mfano wa patakatifu halisi; bali aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu.” (Ebr. 9:24) Sasa msingi ulikuwa umewekwa wa msamaha wa dhambi, nazo habari njema hizi zilipaswa zitangazwe pote, si kwa Wayahudi peke yao, bali kwa ulimwengu mzima. (Matendo 17:30) Hilo limefanywa chini ya usimamizi wa kimbinguni wa Kristo mpaka siku zetu.​—1 Tim. 2:5, 6.

MFALME ATAWAZWA

13. Kwa sababu gani habari njema ni bora hata zaidi sasa?

13 Sasa, tangu mwaka wa 1914 C.E., wakati “majira ya Mataifa” yalipokoma, habari njema ni bora zisivyopata kuwa wakati mwingine wo wote. Sasa Mfalme ametawazwa, nao Ufalme umeanza kufanya kazi! Njozi aliyopewa mtume Yohana iliyoandikwa katika kitabu cha Ufunuo inatupa maono madogo juu ya ‘kuzaliwa’ kwa Ufalme unaowekwa mikononi mwa Kristo: “Naye [‘mwanamke’ wa kimbinguni wa Mungu] akazaa mtoto mwanamume, yeye atakayewachunga mataifa yote kwa fimbo ya chuma. Na mtoto wake akanyakuliwa hata kwa Mungu, na kwa kiti chake cha enzi.” Kwa hiyo Kristo alikuwa huko juu kati ya jamaa ya kimbinguni ya Mungu, akiwa tayari kupokea mamlaka ya kifalme. Huko alitokezwa, akaonyeshwa kwa majeshi ya kimbinguni na kutawazwa kama Mfalme wa Kimasihi.​—Ufu. 12:5; Ebr. 1:6.

14, 15. Ni nini kilichotukia mara tu baada ya kutawazwa kwa Kristo kulikokuwa habari za kupendeza mbinguni?

14 Wakati huu zaburi aliyoitaja mtume katika Waebrania 10:12, 13 ilitimizwa sehemu nyingine zaidi: “Neno la [Yehova] kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako. [Yehova] atainyosha toka Sayuni [wa kimbinguni] fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako.” (Zab. 110:1, 2) Njozi ya Ufunuo inalitaja tendo lililofuata kwa njia hii: “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli [Yesu Kristo, anayeitwa pia “malaika mkuu.” (Linganisha Yuda 9; 1 Wathesalonike 4:16; Danieli 12:1.)] na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.”​—Ufu. 12:7-9.

15 Lo! zilikuwa habari njema kama nini! Sauti kubwa mbinguni ilitangaza, ikishangilia: “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku. . . . Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo.” Hii ingewaletea wanadamu majaribu zaidi, kwa maana sauti ya kimbinguni iliendelea kusema hivi: “Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache.”​—Ufu. 12:10-12.

16. Kwa sababu gani kutangazwa kwa habari njema sasa ni kwa muhimu?

16 Habari njema hizi za kwamba Ufalme unafanya kazi na kwamba Shetani Ibilisi, adui mkuu wa Mungu, anao wakati mfupi sasa duniani, zinastahili zitangazwe kwa kila mwanamume na mwanamke duniani. Na inachukua muda kuyafikia mataifa. Huenda kila mtu asifikiwe mwenyewe na kuelezwa kabla Ufalme haujauanza utawala wake usiopingwa juu ya dunia. Lakini Yesu alisema hivi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.”​—Mt. 24:14.

17. Unabii katika Zaburi 110:3 umetimizwaje wakati wetu?

17 Sasa, kwa kuwa Kristo ameshinda mbinguni na kumzuia Shetani na malaika zake wa kishetani katika ujirani wa dunia, habari njema zinatangazwa pote zisivyopata kutangazwa hapo kwanza, katika nchi 208 duniani, hata katika nchi zinazotawaliwa na Wakomunisti. Utumishi huu unaotolewa na wafanya kazi wengi wa kujitolea ulitabiriwa na mtunga zaburi, alipoendelea kusema hivi: “Watu wako [watajitoa] kwa hiari, siku ya uwezo wako; . . . unao umande wa [vijana] wako.” (Zab. 110:3) Kama mashujaa vijana, wenye jitihada, wengi kama vile matone ya umande, mashahidi wa Yehova, vijana na wazee, wanaume na wanawake, wanawaeleza watu habari njema hizi za utendaji wa kifalme wa Kristo kwa hiari na bidii. Je! wewe umetiwa moyo utende pamoja nao?

18, 19. Kitabu cha Ufunuo chaonyeshaje anavyofanya Kristo sasa?

18 Tamasha ya Ufunuo inaonyesha Kristo anavyofanya na atakavyofanya karibuni, naye Yohana anatuandikia mfano huu kwa maneno haya: “Nikaona, na tazama, farasi mweupe, na yeye aliyempanda ana uta, akapewa taji, naye akatoka, ali akishinda tena apate kushinda.”​—Ufu. 6:2.

19 Akiwa ‘ameshinda’ mbinguni, sasa Kristo anawaelekeza adui zake mahali ambapo ‘atapata kushinda kabisa,’ akiisafisha dunia na dini zote za uongo zilizo mbovu, vyombo vyote vya kisiasa na kibiashara, na wote wanaojitahidi wadhulumu wanadamu wenzao. Mwishowe, atawafanya Shetani na mashetani zake hoi kabisa ili maongozi yao yenye kufisha yatoweke.​—Ufu. 20:1-3.

KUWA ULIZO KUU

20. Je! ubaridi mwingi wa watu kwa habari njema utaendelea kwa wakati usiojulikana?

20 Kwa sasa, habari njema za Ufalme zinaenezwa na kutangazwa zaidi sana, na kila mwaka maelfu mengi ya watu wanazisikia kwa kuziamini. Ni kweli kwamba kungali na ubaridi mwingi kwa upande wa watu wengi. Lakini kwa kuwa habari njema zinahusu kweli juu ya enzi kuu ya Yehova Mungu, zingali zitakuwa ulizo kuu zaidi.

21, 22. Ni hali gani katika Misri ya kale inayolingana na hali fulani leo?

21 Kwa mfano, chukua yaliyotukia katika Misri ya kale, wakati Musa na Haruni, kwa amri ya Mungu, walipomwomba Farao awafungue watu wa Mungu waliotumikishwa, wazao wa Ibrahimu. Hii iliongoza kwenye utimizo wa ahadi iliyokuwa imefanywa karne nyingi mapema.​—Mwa. 15:13-16.

22 Twaweza kuona ulinganifu leo: Kama vile katika Misri, watu wenye mioyo minyofu leo wanadhulumiwa kwa njia ya kidini, kisiasa, na kibiashara, haya yote yakiongozwa na Ibilisi, anayetaka kuhakikisha kwamba taabu inaongezeka. Ni nini kilichotukia huko nyuma katika Misri wakati wa Mungu wa kukomboa watu wake ulipofika?

23. Farao na Wamisri waliitikiaje wakati Musa alipolileta ombi la Mungu kwa mara ya kwanza kwamba Waisraeli wafunguliwe, na je! waliendelea kuwa na nia hii?

23 Musa aliwajia Waisraeli na habari njema mno kwamba wakati wa Mungu wa kuwakomboa ulikuwa umefika. Angalia kwamba sasa enzi kuu ya Mungu ilikaidiwa na Farao, aliyemwambia Musa hivi: “[Yehova] ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao?” (Kut. 5:2) Kwa hiyo aliyoyasema Musa katika jina la Yehova kwanza yalielekea kuwa ya bure kwa Farao na kwa watu wake. Lakini yakawa ya maana sana kwao. Kwa kweli, mwishowe Wamisri walilazimishwa kuwa na nia ya kukata maneno, ya waziwazi, si ya ubaridi. Kwa njia gani?

24. Mungu alimtumiaje Musa kwa habari ya mapigo kumi?

24 Basi, wakati wa yale mapigo kumi Mungu alimjulisha Musa mapema atakalolifanya. Naye Musa alimwambia Farao na Wamisri. Kisha ikatukia sawasawa na alivyokuwa amesema Musa. Kila pigo lilitabiriwa na Musa, kisha kila pigo likatukia sawasawa na lilivyotabiriwa, na katika wakati wake. Mwishowe, wazaliwa wa kwanza wa Misri walipokufa, Farao aliwaacha Israeli waende. Lakini yeye alikuwa kama Shetani, asiache jitihada zake, akaharibiwa pamoja na jeshi lake huku Yehova akikomboa Israeli kupita Bahari ya Shamu.​—Kut. 14:26-28; Zab. 136:15.

25. Kwa sababu gani tangazo la Musa la mapigo kabla ya wakati wake lilikuwa la lazima kwa kusudi la Mungu, nalo lilitimiza nini?

25 Habari alizozitangaza Musa kwa watu wa Mungu waliotumikishwa zilikuwa habari njema, na habari njema pia kwa wale Wamisri waliosikia na kuamini. Hawa, “kundi kubwa la watu waliochangamana,” walitoka Misri pamoja na Israeli. (Kut. 12:38) Ilisaidia sana pia kuwajulisha Wamisri kwamba “hapana mwingine mfano wa [Yehova], Mungu wetu.” (Kut. 8:10) Iliwahakikishia wote kwamba Yehova alikuwa ‘akifanya hukumu juu ya miungu yote ya Misri.’ (Kut. 12:12) Tangazo la Musa lilikuwa la lazima sana. Kama Mungu angalileta mapigo bila ya kufanya tangazo kwanza, Wamisri wangalisema kwamba walikuwa wameiudhi miungu yao wenyewe, ambayo kati yake ilikuwako miungu iliyosimamia mazao ya mashamba, mifugo, miungu ya jua, mvua na ya wazaliwa wa kwanza, na kadhalika. Lakini mapigo yalipokuja, walielewa vizuri, kwa maana mapigo yalitokea wakati ule ambao Musa alikuwa ametangulia kutangaza na kwa njia aliyoitangaza. Miungu yao ilikuwa hoi isiweze kuwalinda.

26. Kuna ulinganifu gani katika kutangazwa kwa habari njema leo, na katika itikio la mataifa juu yazo?

26 Vivyo hivyo, habari njema juu ya ufalme wa Mungu uliosimamishwa na ukombozi wake juu ya wanadamu katika kizazi hiki ni za lazima sana nazo zinasikiwa, hasa katika nchi zinazoitwa Kristendomu. Machoni pa watu, halijawa ulizo KUBWA bado. Lakini Mungu atayalazimisha mataifa wawe na nia ya waziwazi. Kwa maana mataifa yote yanataka enzi yao wenyewe ya kitaifa. Lakini watangazaji wa habari njema wanatetea enzi kuu ya Mungu. Mataifa haya “ndipo watakapojua ya kuwa nabii amekuwapo kati yao.”​—Eze. 33:33.

27. Unabii wa Danieli unaonyesha kwamba “mfalme wa kaskazini” atawatendaje watangazaji wa habari njema?

27 Kama mfano wa uzito ambao kwao mataifa yataliitikia tangazo la habari njema, angalia hatua ambayo unabii unasema itachukuliwa kwa haraka juu ya mataifa yenye mamlaka ya mtu mmoja tu na yenye watawala wa kutumia nguvu, yanayotajwa katika Maandiko kama “mfalme wa kaskazini.” Unabii wa Danieli unamtaja “mfalme” huyu: “Habari zitokazo mashariki na kaskazini zitamfadhaisha; naye atatoka kwa ghadhabu nyingi, ili kuharibu, na kuwaondolea mbali watu wengi. . . . lakini ataifikilia ajali yake, wala hakuna atakayemsaidia.” (Dan. 11:44, 45) Kikitoa maelezo juu ya maneno haya, kitabu cha Watch Tower Society “Your Will Be Done on Earth” kinasema hivi:

“Kufikia sasa . . . [mashahidi wa Yehova] wamekuwa wakitoa habari juu ya enzi kuu ya ulimwengu wote ya Yehova, juu ya kusimamishwa kwa ufalme wake mikononi mwa Kristo mwishoni mwa ‘nyakati zilizowekwa za mataifa’ katika mwaka wa 1914, na juu ya ‘vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi’ inayokuja . . .

“Kwa kuwa habari hizi zinatoka hasa kwa Yehova kupitia kwa Mfalme wake anayetawala Yesu Kristo, inasemekana kulingana na Maandiko kwamba habari hizo zinatoka kaskazini na mashariki. . . . (Zab. 75:6, 7; 48:2; . . . Isa. 46:10, 11) Kwa hiyo, si habari zenyewe tu, bali pia majeshi ya uharibifu yatatoka pande hizo yamjilie mfalme wa kaskazini. Kwa kuwa habari hizo lazima zimfikie mfalme huyu kwa njia ya Yehova ionekanayo na ya kidunia ya kupashia habari, ili kumghadhibisha mfalme kumwelekeza kwenye mwendo wake wa uharibifu, unabii huu unaonyesha wazi jambo moja: jamii ya patakatifu pa Yehova na kundi kubwa la waabudu wenzao itazidi kutii Mathayo 24:14 kwa kuzihubiri ‘habari njema hizi za Ufalme’ katika dunia yote inayokaliwa na watu.”

28. Matendo ya Yesu na Paulo yalitokezaje itikio linalolingana na lile ambalo habari njema zitatokeza juu ya mataifa?

28 Habari hizi zimekuwa matangazo ya habari njema, na pia zimefuatana na vipeo vya kukimbia kwa hesabu kubwa ya watu kuingia katika ngome ya ulinzi ya jina la Yehova, na kuabudu penye hekalu lake kuu la kiroho. (Mit. 18:10; Isa. 2:2-4) Habari hizi zinatia hofu, si “mfalme wa kaskazini” peke yake, bali pia ile jamii ya upinzani ya mataifa, “mfalme wa kusini.” Habari hizi zitakuwa ulizo kubwa, zikiwafanya wachukue hatua. Nia ile ile ndiyo Wayahudi waliyoifuata juu ya Yesu, wakisema: “Tukimwacha hivi, watu wote watamwamini; na Warumi watakuja, watatuondolea mahali petu na taifa letu.” (Yohana 11:48) Tena, walisema hivi kwa hofu: “Tazameni, ulimwengu umekwenda nyuma yake.” (Yohana 12:19) Pia walisema hivi kwa habari ya Paulo na wahubiri wenzake wa habari njema katika Thesalonike: “Watu hawa walioupindua ulimwengu wamefika huku nako.” (Matendo 17:6) Kwa hiyo ili kuwakomesha watangazaji wa habari njema mataifa yatachukua hatua, kuelekea kwenye uharibifu wao wa mwisho.

29, 30. Watangazaji wa habari njema wanajisikiaje juu ya shambulio lijalo la mataifa?

29 Kwa hiyo, ni jambo linalotazamiwa kwamba mataifa ya dunia yatawashambulia wale wanaozitangaza habari njema, kwa maana mataifa haya yanaichukia enzi kuu ya Mungu. Lakini wahubiri wa habari njema wanajua kwamba wao wanatetea upande ufaao wa ulizo, upande wenye kufaulu na wenye kutegemezwa na Mungu, nao wanaendelea kuzitangaza habari njema zilizo za maana kupita zote kwa ukamili uwezekanao.

30 Je! wewe unasimama wapi katika shauri hili? Je! u mtu anayeziamini habari njema? Je! unayo roho ya kuzitangaza kwa wengine? Namna gani na wapi? Hii ndiyo itakayokuwa habari ya mazungumzo yafuatayo.

[Maelezo ya Chini]

a Tazama kitabu True Peace and Security​—From What Source?, kilichochapwa na Watch Tower Bible and Tract Society (1973).

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki