Wakristo wa Kweli Watajilindaje na Watu Wanaowavunjia Heshima?
MAFUNDISHO yote ya Kikristo, yaliyopata kuwa sehemu ya Neno la Mungu lililoandikwa, ndiyo “kweli ya habari njema” au “kweli,” kwa ufupi. (Gal. 2:5; Rum. 2:8, NW) Katika karne zote zilizopita ni watu wachache wameukubali uhakika huo. Wengi wamepofushwa na “mungu wa dunia hii,” Shetani Ibilisi, wakaipinga sana “kweli ya habari njema” kwa kusingizia Wakristo wa kweli pamoja na mafundisho yao na makusudi yao.—2 Kor. 4:3, 4.
Wakristo wanayaona masingizio hayo kama ushuhuda mmoja wa kuonyesha kwamba kweli wanatembea kupatana na kweli ya Mungu. Kwa hiyo wanaweza kufurahi, wakijua kwamba watapata baraka za milele kwa sababu ya kushikamana na ile kweli. Ni kama vile Yesu Kristo alivyosema katika Mahubiri juu ya Mlima: “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu.”—Mt. 5:11, 12.
Bila shaka, mtu hafurahii kushutumiwa. Huenda akataka sana watu watakaokubaliana na masingizio hayo wapatwe na mabaya. Hasa akivunjiwa heshima na watu ambao wakati mmoja walielekea kuwa wanatembea kupatana na kweli ya Neno la Mungu, huenda akataka kushindana nao. Lakini je! ni hekima kufanya hivyo?
Tusisahau kwamba watu wengi hawataki kuijua kweli kwa vyo vyote. Watu wengine wanaamini kwamba haiwezekani kuzifuata kanuni bora za Neno la Mungu, kwa hiyo wanatafuta kisababu cha kutousikiliza ujumbe wa Biblia unaohubiriwa na mashahidi Wakristo wa Yehova. Wakati Mashahidi wa Yehova wanaposingiziwa, watu hao wanataka kuamini uongo unaosemwa juu yao ili kutetea msimamo wao wenyewe. Ni kama vile 2 Wathesalonike 2:11, 12 inavyotuambia: “Mungu awaletea nguvu ya upotevu, wauamini uongo; ili wahukumiwe wote ambao hawakuiamini kweli, bali walikuwa wakijifurahisha katika udhalimu.” Ni wazi kwamba watumishi wa Yehova hawawezi kusaidia watu wa namna hiyo kwa kubishana nao juu ya kila shtaka la uongo wanalowafanyia. Hata kama wangefanya hivyo watu hao wangependelea kuamini uongo tu.
Mashahidi wa Yehova wakijishughulisha kupinga mashtaka yote ya uongo wanayofanyiwa, wao pia wanaweza kuingia katika mtego wa mshtaki mkuu, Shetani Ibilisi. Kwa njia gani? Shetani angependezwa sana kuona upungufu wa kazi ya kusaidia watu wenye mioyo myeupe wajifunze kweli. Lakini jambo hilo linaweza sana kutokea. Watumishi wa Yehova wanaweza kupoteza wakati mwingi wa maana kwa kuacha fikira zao zielekezwe upande usiofaa, wakati ambao ungaliweza kutumiwa kwa mafaa ya kusaidia watu wenye mioyo myeupe wajifunze mapenzi na makusudi ya Mungu kwa wanadamu.
Vivyo hivyo, mtu akitumia wakati mwingi kusoma vitabu vinavyoshambulia Mashahidi wa Yehova na kujitahidi kutafuta njia za kupinga madai yanayotolewa, anaweza kuchafuka moyoni kwa wepesi. Anaweza kuvurugika moyo, hasa kwa sababu mwanadamu hana njia ya kunyamazisha watu wote wanaomfanyia mashtaka ya uongo. Jitihada za kujitetea sana hadharani zingesaidia kueneza zaidi mashtaka hayo ya uongo. Huenda watu wengine wakadhani jitihada za kupinga mashtaka hayo zinahakikisha kwamba mashtaka yenyewe ni ya kweli.
Walakini, kuna njia ya kupinga mashtaka ya uongo bila ya kushindana sana na wenye kuyatoa. Njia gani hiyo? Mtume Petro anaionyesha anapowaambia Wakristo wenzake hivi: “Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa. . . . Kwa sababu ndiyo mapenzi ya Mungu, kwamba kwa kutenda mema mzibe vinywa vya ujinga vya watu wapumbavu.” (1 Pet. 2:12-15) Naam, wakati watazamaji wenye mioyo myeupe wanapoona kwamba Mashahidi wa Yehova wanaishi kwa kupatana sana na kanuni zenye haki za Neno la Mungu na kufanya utumishi wao kwa sababu wanapenda wengine kikweli, watazamaji hao wanaweza kuona vyepesi kwamba mashtaka ambayo Wakristo hao wanafanyiwa hayana msingi.
Kwa hiyo hakuna haja ya kuhangaika sana juu ya mashtaka ya uongo ya watu wasiotosheka, wanaotaka tu kushambulia na kubomoa umoja na utumishi wa Mashahidi wa Yehova. Watu wanaotaka kujua mambo yanayofanywa na kufundishwa na Mashahidi wa Yehova watapashwa habari hizo na mashahidi wenyewe bila ugumu wo wote. Kila mwezi Mashahidi wa Yehova wanagawia watu mamilioni ya vitabu vinavyoonyesha msingi wa Biblia wa imani zao. Watu wote wanakaribishwa kuhudhuria mikutano yao katika Majumba ya Ufalme, na vilevile makusanyiko yao ya taifa zima na ya mataifa yote. Tena, kila mmoja wa Mashahidi wa Yehova anakuwa tayari nyakati zote kueleza waulizaji wenye mioyo myeupe sababu za kuwa na imani walizo nazo.
Lakini watu wakichagua kuamini mashtaka ya uongo, watapatwa na mabaya kwa sababu ya kutofanya uchunguzi kwa unyofu. Hilo linapatana na maneno ya Yesu Kristo: “Kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili.”—Mt. 15:14.
Kwa hiyo, badala ya kubishana wakati wanapofanyiwa mashtaka ya uongo, Mashahidi wa Yehova wanaona ni afadhali wawaachie wenye kuwashtaki mzigo wa kuhakikisha mambo wanayosema. Mfano mwema wa jambo hilo ni mtume Paulo. Wakati adui za kidini walipomfanyia mashtaka ya uongo mbele ya Feliki liwali Mrumi, Paulo hakujaribu kuyapinga mashtaka hayo ya uongo bali alionyesha kwa ufupi tu kwamba washtaki wake hawakuweza kuyahakikisha ‘mambo waliyokuwa wakimshtaki.’ (Matendo 24:13) Vivyo hivyo, wakati mmoja Yesu Kristo aliwauliza wapinzani wake hivi: “Ni nani miongoni mwenu anishuhudiaye ya kuwa nina dhambi?”—Yohana 8:46.
Hata hivyo, ziko nyakati inapokuwa lazima kujitetea katika hali zisizofaa. Wakuu wa serikali, kama mahakimu, wanaweza kudai tuwajibu. Ingawa huenda shahidi wa Yehova akaulizwa maulizo kwa njia ya kumdharau yeye na ujumbe wake, asikasirike wala kuonyesha ameudhika. Anaweza kuendelea kutulia na kuonyesha upole anapojibu. Kwa kuwa anajua kwamba ‘macho ya Yehova huwaelekea wenye haki,’ inafaa aonyeshe heshima nyingi sana, kama kwamba yu mbele za Mungu. (1 Pet. 3:12) Kufanya hivyo ni kupatana na onyo la upole linalopatikana katika 1 Petro 3:14, 15: “Mtakaseni Kristo Bwana mioyoni mwenu. Mwe tayari sikuzote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu.”
Ijapokuwa mambo yanaweza kuharibika zaidi kukiwa na mabishano, ushuhuda unaotolewa na mwenendo mwema haupingiki. Hakuna mtu mwenye akili nzuri anayeweza kusema kwamba sifa kama ukarimu, fadhili, kusaidia watu na kuwahurumia wanapokuwa na shida zinaonyeshwa na watu wenye chuki. Kwa hiyo njia bora ya Wakristo wa kweli ya kujilinda na watu wanaowavunjia heshima ni kuwa na mwenendo wenye kusifika na kutulia nyakati zote watoleapo watu mafundisho ya Biblia kwa kuwatakia mema. Mwenendo mwema unaweza kufunga vinywa vya wapuzi na kusaidia watu wawe wakimtukuza Yehova Mungu.