Wakati wa Kutojali Yanayosemwa na Wengine
JINA au sifa nzuri ni mali yenye thamani nyingi. “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi,” yasema mithali ya kale. (Mit. 22:1) Nyakati za kisasa jina jema linathaminiwa sana hata kustahili kulindwa na sheria juu ya kuchongewa na kukashifiwa. Kwa kufaa watu hutaka jina lao liondolewe masingizio mabaya, hasa ikiwa masingizio hayo yanaweza kuwaharibia riziki yao.
Lakini mara nyingi yanayosemwa na wengine si ya uchongezi hata yakiwa ya kulaumu na yasiyo ya fadhili. Utendeje ukilaumiwa? Je! uudhiwe na jambo hilo?
Biblia inasaidia mtu kukadiri yanayoweza kusemwa na watu. Inasihi hivi: “Usitie moyoni mwako maneno yote yaliyosemwa; usije ukamsikia mtumwa wako mwenyewe ali anakutukana. Kwa kuwa mara nyingi moyo wako pia unajua ya kwamba wewe mwenyewe umewatukana watu wengine.”—Mhu. 7:21, 22.
Onyo hilo la upole la Maandiko lapatana kabisa na vile maisha yalivyo hasa. Hata watu walio bora wana makosa yao. “Hakuna mwanadamu mwenye haki hapa duniani,” twasoma katika Biblia, “ambaye afanya mema, asifanye dhambi.” (Mhu. 7:20) Wanadamu wote ni wazao wenye dhambi wa Adamu asiye mkamilifu. Ndiyo sababu haimpasi mtu kushangaa hata rafiki mkubwa akimnena kwa wengine kwa kumlaumu, pengine akiwa na hasira au uchungu. Hata wajaribu sana, watu wasiokamilika hushindwa mara nyingi kutumia ulimi wao kwa mema. Mwanafunzi wa Kikristo Yakobo alikubali hivi: “Twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.”—Yak. 3:2.
Ni kweli kabisa kwamba wanadamu hawakukamilika. Sisi mmoja mmoja hukosa sana kuwa aina ya watu tunaotaka kuwa. Kwa wazi, basi, hatuwezi kuchukua kwa uzito kila neno linalosemwa na watu. Mtu akilichukua kwa uzito, ataumia sana moyoni. Kwa mfano, huenda akasikia kwamba rafiki mkubwa alimnena kwa njia isiyofaa. Huenda akawaza hivi, ‘Haya, ikiwa ndivyo anionavyo, nitamkatilia mbali. Sitaki urafiki naye.’ Kwa njia hiyo uhusiano mwema unaweza kuharibiwa.
Jinsi ilivyo afadhali zaidi kufuata shauri la Biblia ‘kutotia moyoni maneno yote yaliyosemwa’! Hiyo inawezesha mtu kuwa na maoni yanayofaa juu ya mambo yanayosemwa na watu. Mtu mnyofu ajua kwamba yeye amesema mara nyingi mambo yasiyofaa juu ya wengine, bila ya kuwa na ubaya. Hiyo imepaswa kumsaidia aone kwamba hakuna haja ya kudhani ametukanwa na wengine wanapomnena.
Halafu tena, imetupasa tukumbuke kwamba habari za kusikia kwa mtu mwingine (si kwa mwenye kuzianza) mara nyingi hazitegemeki. Kwa hiyo, kanuni nzuri ya kufuata ni hii: “Usikubali mashitaka juu ya mzee, ila kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu.” (1 Tim. 5:19) Kutenda kupatana na kanuni hiyo kutatuzuia tusiwe wenye haraka haraka kukubali mambo tukipashwa habari za vile wengine walivyotunena.
Pia, kutaka sana kusikia yanayosemwa na watu kwa njia ya kufaa kunaweza kuleta matata. Sifa yao huenda ikawa mtego, ikimfanya mwenye kusifiwa aanze kujifikiria ni bora sana. Kiburi cha mtu kikikuzwa hivyo, huenda sifa zake njema zikasukumiwa nyuma. Kwa sababu hiyo, huenda akapoteza sifa njema aliyokuwa nayo. Mithali ya Biblia husema hivi: “Kiburi hutangulia uangamivu; na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko.”—Mit. 16:18.
Kwa upande mwingine, huenda mtu akajua kwamba maneno au matendo yake yamefanya kuwe na msingi mzuri wa kulaumiwa. Ikiwa hivyo itamfaa afikirie anaweza kufanya nini kuepuka kufanya wengine wanung’unike wakati ujao. Hiyo itakuwa kupatana na shauri la Maandiko: “Hakikisheni mambo yaliyo ya maana zaidi, ili msiwe na kosa na msiwe mkikwaza wengine.”—Flp. 1:10, NW.
Hata mtu anaposingiziwa, inaweza kuwa hekima kutolichukua hilo kama jambo kubwa. Mtu akijaribu kujitetea kuonyesha analosingiziwa si kweli, badala ya kuliachilia tu singizio, huenda hiyo ikalikuza jambo lenyewe na kufanya watu zaidi waamini analoshtakiwa ni kweli.
Yesu Kristo aliweka mfano mwema wa kutenda mtu anaposingiziwa. Aliposhtakiwa kwa uongo kuwa mlevi na mlafi, yeye hakutoa ubishi. Alisema tu: “Hekima huhakikishwa kuwa haki na matendo yake.” (Mt. 11:19, NW) Kwa kusema hayo, alikaribisha wengine wauone ushuhuda. Ushuhuda huo, yaani, matendo yenyewe, ulionyesha wazi kwamba mashtaka hayo yalikuwa ya uongo.
Mtu anayeendelea kuwa na mwenendo mwema, akitendea wengine kwa huruma, mwishowe hunyamazisha waliomsingizia. Haichukui muda kwa watazamaji wanyofu kuona kwamba mambo waliyoambiwa juu ya mtu huyo ni ya uongo.
Hasa wale wanaotaka kujipatanisha na mapenzi ya Mungu wamepaswa kushughulikia kuendelea kuwa na mwenendo mwema. Biblia huwatia moyo hivi: “Ndiyo mapenzi ya Mungu, kwamba kwa kutenda mema mzibe vinywa vya ujinga vya watu wapumbavu.”—1 Pet. 2:15.
Unapoambiwa uko hivi na vile kwa njia ya matusi au kwa kusingiziwa kwa njia nyingine inayokusudiwa kukukasirisha, kwa kawaida ni afadhali zaidi kujifanya husikii. Mtumishi mwaminifu wa Mungu Daudi alifanya hivyo akawa na matokeo mema. Katika mojawapo ya zaburi zake, alisema hivi: “Kwa habari yangu mimi, kama kiziwi, sikusikiliza; na kama bubu, mimi sikufungua kinywa changu. Nikawa kama mtu asiyesikia, wala katika kinywa changu hamkuwa ubishi.”—Zab. 38:13, 14, NW.
Ni nini kilichomwezesha Daudi kutenda hivyo alipochokozwa? Yeye alijua kwamba asingeweza mwenyewe kuyanyosha mambo yawe barabara. Lakini alikuwa na hakika kwamba Mungu wake, Yehova, angeweza kufanya hivyo. Ndiyo sababu alisema hivi: “Kwa maana nilikungoja wewe, Ee Yehova; wewe mwenyewe ulinijibu, Ee Yehova Mungu wangu.” (Zab. 38:15, NW) Je! isingefaa kufuata mfano wa Daudi? Bila shaka ingefaa. Mtu asiyejaribu kutumia nguvu juu ya kila jambo alinyoshe, kwa kuwa hana mamlaka ya kufanya hivyo, lakini anayemngoja Mungu wake, hapatwi na fadhaa wala udhia kwa sababu ya kujaribu bure tu kuondoa makosa ya adili.
Kwa kweli, katika mambo ya kila siku ya maisha, limeonekana kuwa jambo la hekima kutohangaika sana juu ya yanayosemwa na wengine. ‘Kutotia moyoni maneno yote yanayosemwa na watu’ kunatuzuia tusiudhike bure au tusiwe wenye kiburi. Vilevile tunaweza kufaidika kwa kulaumiwa kwa haki, tukijaribu kufanya maendeleo. Kisha, kwa kuendelea kuwa na mwenendo mwema, tunaweza kuziba “vinywa vya ujinga vya watu wapumbavu.”