Je! Sanamu Inaweza Kuleta Amani na Usalama?
WEWE walifikiriaje ulizo, ‘Je! sanamu inaweza kuleta amani na usalama’? Je! unaona ni ajabu kwamba ulizo hilo limeulizwa? Ni nani anayeweza hata kufungua kinywa aseme sanamu inaweza kumaliza vita?
Lakini, kuna sanamu ambayo imetegemewa zaidi ya miaka 30 kuwa ndiyo tumaini bora la kuletea wanadamu amani. Hiyo si sanamu ya mwanadamu wala mnyama, bali ni tengenezo la mataifa yote. Tengenezo gani? Umoja wa Mataifa. Gazeti Inquirer la Philadelphia lilitaja afisa wa United States akisema hivi: “Umoja wa Mataifa unaonyesha jinsi ulimwengu ulivyo hasa—si jinsi ambavyo sisi tungependa uwe.” Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dag Hammarskjold, alikuwa akisema ivyo hivyo.
Linaloshangaza ni kwamba, Biblia ilitabiri kwamba sanamu hiyo ya taratibu ya kisiasa ingetokea ulimwenguni pote. Tukichunguza yanayosemwa na Biblia, tunaweza kujua mapema jambo litakalotendwa ulimwenguni na Umoja wa Mataifa. Kuna faida nyingi sana za kujijulia hivyo, kwa maana tunaweza kufuata njia inayofaa katika kipindi hiki chenye hatari katika historia ya wanadamu.
NI SANAMU YA NINI?
Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinatumia usemi wa mfano kuonyesha matukio ya ulimwengu. Tunaweza kufahamu maana kwa kusaidiwa na sehemu nyingine za Biblia na matukio halisi ya historia.
Maelezo ya mfano yanayoufaa Umoja wa Mataifa yanapatikana katika Ufunuo 13:14, 15, tunaposoma juu ya ‘kufanywa kwa sanamu ya yule mnyama.’ Hapo nyuma kidogo, mnyama huyo anatajwa kuwa “mfano wa chui” akiwa na “vichwa saba” na “pembe kumi” (kila kimoja kikiwa na kilemba), ‘miguu kama ya dubu,’ na kinywa kama cha simba.—Ufu. 13:1, 2.
Katika unabii wa Danieli, wanyama wanne wanatajwa, yaani, simba, dubu, chui na mnyama wa kutisha mwenye pembe kumi, na kila mmojawapo anafananisha ‘mfalme’ au ‘ufalme.’ (Dan. 7:4-7, 17, 23) Basi, hali za “mnyama” wa Ufunuo zinafanana na hali za wanyama wa unabii wa Danieli. Kwa hiyo, The Interpreter’s Dictionary of the Bible inakata maneno hivi: “Wa kwanza kati ya wanyama hao [wanaotajwa katika Ufunuo sura ya 13] ana hali zote za wanyama wanne walioonekana na Danieli katika njozi . . . Kwa hiyo, mnyama huyo wa kwanza anafananisha mamlaka ya utawala wote wa kisiasa ulimwenguni, unaompinga Mungu.”—Vol. 1, uku. 369.
Kwa kuwa una wajumbe wa mataifa mengi, Umoja wa Mataifa ni sanamu ya tawala hizo za kisiasa zinazosimamia wanadamu.
“MNYAMA MWEKUNDU SANA”
Baadaye sanamu ya mnyama inatajwa katika Ufunuo 17:3 kuwa “mnyama mwekundu sana.” Huyo “mnyama mwekundu sana” ana “vichwa saba na pembe kumi,” kama “mnyama” anayetajwa katika Ufunuo 13:1, 2. Kwa hiyo yeye anaonyesha sifa zile kubwa za “mnyama” huyo wa kwanza. Lakini, pembe za “mnyama mwekundu sana” hazina vilemba. Hilo linafaa, kwa sababu huyo “mnyama mwekundu sana” hafananishi taratibu nzima ya utawala wa kisiasa, kwa maana utawala huo umetumiwa na mamlaka saba mbalimbali za ulimwengu, moja baada ya nyingine. Bali, kulingana na Ufunuo 17:11, mnyama huyo mwekundu sana ni ‘mnyama wa nane, naye ni mmoja wa wale saba.’ Hilo linapatana na uhakika wa kwamba, mamlaka zile kubwa au mabaki yazo yaliyotawala maeneo makubwa wakati mmoja, zina wajumbe katika Umoja wa Mataifa. Umoja wa Mataifa unatenda kama “mfalme” mmoja, ukiwa na mamlaka kama ile inayotumiwa na mtawala mmoja.
NI MAMBO GANI YALIYOKO MBELE?
Lakini, Biblia haisemi kwamba ‘mfalme wa nane’ ataleta amani na usalama wa kweli. Inaonyesha kwamba huyo “mnyama mwekundu sana” ‘ataenenda kwenye uharibifu.’ (Ufu. 17:11) Lakini, ingawa Umoja wa Mataifa hauwezi kuleta amani ya kudumu, huenda ukasaidia kufanya hali zifikie hatua ambayo watu watakuwa wakisema: “Kuna amani na salama”!
Wenye hekima ni wale ambao hawatadanganywa na tangazo hilo. Kwa sababu gani? Biblia inajibu hivi: “Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa.”—1 The. 5:3.
Njia ya pekee ya kuokokea msiba huo ni kuendelea kujitenga na mipango ya kibinadamu ya kuleta “amani na salama” kwa njia inayompuza Mungu na Neno lake. Hilo linaonekana wazi kutokana na maneno ambayo Biblia inaendelea kuambia Wakristo wa kweli: “Ninyi, ndugu, hammo gizani, hata siku ile iwapate kama mwivi.”—1 The. 5:4.
Huenda watu wengine wakadhani hawana jambo la kuwatia wasiwasi. Kwa sababu wanafuata dini fulani, huenda wakadhani hawatapatwa na msiba. Lakini mawazo hayo yaweza kuwa hatari sana. Biblia inaonyesha si dini zote zinazokubaliwa na Mungu. Mwanafunzi Yakobo aliandikia waamini wenzake barua, akawaambia: “Dini iliyo safi isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.” (Yak. 1:27) “Enyi wazinzi, hamjui ya kwamba kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu?” (Yak. 4:4) Kwa hiyo matengenezo ya kidini yanayoitwa ya Kikristo kwa jina tu, yanayofuata njia na nia za ulimwengu, yanaonekana na Mungu kuwa malaya. Yanakosa kuonyesha uaminifu kwa Mungu yanayesema ndiye Bwana wao.
Kwa hiyo, inapendeza kuona kwamba Maandiko Matakatifu yanataja malaya pamoja na yule “mnyama mwekundu sana.” Tunasoma hivi: “Nikaona mwanamke, ameketi juu ya mnyama mwekundu sana, mwenye kujaa majina ya makufuru, mwenye vichwa saba na pembe kumi. Na mwanamke yule alikuwa amevikwa nguo ya rangi ya zambarau, na nyekundu, amepambwa kwa dhahabu, na kito cha thamani, na lulu, naye alikuwa na kikombe cha dhahabu mkononi mwake, kilichojawa na machukizo, na machafu ya uasherati wake. Na katika kipaji cha uso wake alikuwa na jina limeandikwa, la siri, BABELI MKUU, MAMA WA MAKAHABA NA MACHUKIZO YA NCHI.”—Ufu. 17:3-5.
Namna gani dini za ulimwengu kwa ujumla? Je! zinatenda kama “BABELI MKUU” malaya? Je! zimetegemea Umoja wa Mataifa kama tumaini la pekee la kuletea wanadamu amani na usalama, na kuonyesha kwamba zinauhitaji ili ziendelee kuwapo? Basi, je! dini hizo haziutegemei Umoja wa Mataifa sawasawa na mpanda farasi? Mambo yako wazi.
Kanisa Katoliki na Baraza ya Ulimwengu ya Makanisa, yenye makanisa zaidi ya 250, limetangaza mara nyingi kwamba Umoja wa Mataifa ni “tumaini la pekee la amani ya ulimwengu.” New Catholic Encyclopedia kinasema hivi: “Maaskofu wa karibuni wamekaza kwamba kunahitajiwa tengenezo la mataifa yote na kanuni za kuliongoza, tena wameusifu Umoja wa Mataifa kwa sababu ya makusudi yake, mipango yake mbalimbali na mambo uliyoyatimiza. Makao ya Papa yana mtu wa kuangalia daima mambo ya Umoja wa Mataifa, tena yanauchangia pesa na kuusaidia katika shughuli zake za kiuchumi, za kijamii, za kisayansi, za utamaduni, na za ubinadamu. Yanahusika kabisa katika Idara fulani kuu au yanazichunguza, na kushiriki pia katika makusanyiko ya kupatanisha mataifa na katika mikutano mingineyo, inayopangwa na Umoja wa Mataifa. Matengenezo kumi na sita ya mataifa ya Kikatoliki yana mipango rasmi ya kusaidia kazi ya ECOSOC na Idara mbalimbali kuu kwa kupashana habari nazo, tena Wakatoliki katika nchi mbalimbali wanasaidia kutunga kanuni za mataifa na kupanga mambo yanayohusiana na Umoja wa Mataifa.”—Vol. 14, uku. 423.
Je! dini yo yote ya ulimwengu itapata faida yo yote kwa kuwa rafiki ya ulimwengu? Sivyo, Biblia inasema kwamba “BABELI MKUU,” yaani milki ya kidini iliyo kama malaya, itashtuliwa sana. Ufunuo 17:16 unasema: “Zile pembe kumi ulizoziona, na huyo mnyama, hao watamchukia yule kahaba, nao watamfanya kuwa mkiwa na uchi, watamla nyama yake, watamteketeza kabisa kwa moto.”
Kwa hiyo kuna hatari kubwa ya kuwa na uhusiano na yule “mnyama mwekundu sana.” Hataweza kamwe kuleta amani na usalama wa kweli. Lakini kwa hasira nyingi ataangamiza dini ambazo zimetegemea hilo “tumaini la pekee la amani ya ulimwengu” kwa wanadamu. Hiyo si ajabu. Hata sasa wanachama wengi wa Umoja wa Mataifa wanataja wazi kwamba hawataki mambo ya Mungu. Kwa hiyo, yule “mnyama mwekundu sana” na “pembe kumi” zake hatashambulia dini kwa sababu ya kumpenda Aliye Juu Zaidi. Atafanya hivyo kwa sababu ya kutotaka mambo ya Mungu. Kwa hiyo hata akileta amani na usalama wa kiasi fulani, atastahili kuharibiwa kwa sababu ya kujiinua ampinge kabisa Yehova Mungu. Basi watu watakaojiunga na Umoja wa Mataifa kutangaza “Kuna amani na salama”! watapatwa na msiba, hata ikiwa hawakubaliani na “BABELI MKUU.”
Je! kujua hivyo mapema kunakuongoza uchukue hatua zinazofaa? Je! umejitenga na njia za ulimwengu, nia zake na matendo yake? Je! unahakikisha kwamba unautegemea ufalme wa Mungu unaosimamiwa na Kristo kama njia ya pekee ya kuleta amani na usalama wenye kudumu? Njia ya pekee ya kuepuka vizuizi vinavyoweza kutupotezea kibali ya Mungu na uzima ni kuendelea kufanya mambo hayo.