Watendaji wa Mapenzi ya Mungu Watimiziwa Ahadi
1, 2. (a) Ingawa ulimwengu unatatiza watendaji wa mapenzi ya Mungu, tumekaza nia tufanye nini? (b) Ni wapi tunapopata ahadi ya Mungu kwamba atatupa uwezo tunaohitaji ili tuvumilie?
ULIMWENGU huu unajaribu kutatiza mtu asifanye mapenzi ya Mungu. Lakini, maadamu ulimwengu huu upo muda mfupi uliobaki, tumekaza nia kufanya mapenzi Yake. Hivyo itatupasa tuvumilie upinzani na mateso zaidi ya ulimwengu. Lakini Mungu atupa ahadi yake tukufu kwamba atatutia nguvu tuendelee kuvumilia mpaka ahadi yake itakapotimizwa. Kwa hiyo ni juu yetu sasa kuamini ahadi Yake, kama Ibrahimu wa kale. Mungu Mwenye Nguvu Zote aweza kutupa imani na uwezo tunaohitaji tuvumilie. Ametuahidi hivyo katika Warumi 15:4, 5:
2 “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini. Na Mungu mwenye saburi na faraja awajalie kunia mamoja ninyi kwa ninyi, kwa mfano wa Kristo Yesu [ambaye hakujipendeza mwenyewe, bali alimpendeza Mungu].”
3. (a) Kristo aliniaje, akapata thawabu gani? (b) Ni kwa kufanya nini Mungu atatutimizia ahadi yake?
3 Sikuzote Kristo Yesu alinia kufanya mapenzi ya Mungu Baba yake wa mbinguni. Nia yake ilimwelekeza kuvumilia lo lote lililompata kwa kufanya mapenzi ya Mungu. Kwa hiyo yeye hakuyumba-yumba. Hakurudi nyuma kamwe. Hakuepuka kufanya mapenzi ya Baba yake aliyetaka auawe kama dhabihu, kama yalivyotabiri Maandiko “yaliyotangulia kuandikwa.” Alipewa thawabu ya ufufuo wa maisha ya mbinguni kwa kuvumilia afie imani. Hivyo alivumilia mpaka alipotimiziwa alilokuwa ameahidiwa na Mungu, ingawa alijua kwamba kutimizwa kwa ahadi hiyo kulimhitaji Mungu afanye tendo lake hodari zaidi kupita yote. (Efe. 1:19-21) Kupatana na habari ya Kristo mwenyewe, mtume Paulo aliomba Mungu Mwenye Nguvu Zote atupe uvumilivu. (Rum. 15:5) Sala hiyo haitakosa kutufaidi maadamu tunastahimili kufanya mapenzi ya Mungu. Tukivumilia, mpaka mwisho Mungu atatutimizia ahadi yake.
4. Sasa watendaji wa mapenzi ya Mungu walio na nia ya Kristo wanatakiwa wafanye nini, na kwa muda gani zaidi?
4 Nia ya Kristo na itusaidie tustahimili mambo yo yote ambayo Mungu anaruhusu yatupate kutokana na ulimwengu mkatili ambamo sisi ni “wapitaji na wasafiri.” Na tukumbuke sikuzote yanayotakiwa kwa watendaji wa mapenzi ya Mungu sasa katika huu “wakati wa mwisho” uliobaki. (Dan. 12:4) “Mnahitaji uvumilivu, kusudi, mkiisha kufanya mapenzi ya Mungu, mpokee utimizo wa ile ahadi. Kwa maana bado kitambo kidogo sana,’ na ‘yeye anayekuja atafika wala hatakawia.’” (Ebr. 10:36, 37, NW) Je! twaweza kuvumilia “kitambo kidogo” zaidi? Tukifanya hivyo, Mungu, “yeye anayekuja,” atafika wakati wake na kututimizia alilotuahidi.
“YEYE ANAYEKUJA ATAFIKA”
5. Kulingana na vile Habakuki 2:2, 3 inavyosema katika Kiebrania, mwenye kuona njozi alipaswa kuendelea kutazamia nini?
5 Katika Waebrania 10:37 mtume Paulo atumia maneno ya Maandiko yaliyoongozwa na Mungu kabla ya Ukristo. Lakini hayatumii kutokana na maandishi ya asili ya Kiebrania, bali kutokana na tafsiri ya Kigiriki ya maandishi hayo inayoitwa Septuagint Version ya Kigiriki (LXX), iliyotafsiriwa muda wa karne tatu zilizotangulia Wakati wetu wa Kawaida. Kulingana na maandiko ya Kiebrania, Habakuki 2:2, 3 yasema: “Na Yehova akaendelea kunijibu na kusema: ‘Iandike njozi, uionyeshe wazi juu ya mbao, ili kwamba mwenye kuisoma kwa sauti kuu afanye hivyo kwa ufasaha. Kwa maana njozi haitakuja mpaka wakati uliowekwa, nayo inaendelea kufanya haraka mpaka mwisho, nayo haitasema uongo. Hata ikikawia, endelea kuitazamia; kwa maana itatimia bila kushindwa. Haitachelewa.’”
6. Kulingana na Septuagint Version ya Kigiriki, ambayo Paulo. alitumia maneno yake, ni nini kinachopaswa Kungojewa—kitu au mtu?
6 Walakini, kulingana na The Septuagint Bible ya Charles Thomson na Septuagint Version iliyochapwa na S. Bagster and Sons, Ltd., Habakuki 2:2, 3 yasema: “Naye Bwana akajibu [mimi] na kusema: Andika njozi; iandike waziwazi katika kitabu ili msomaji apate kuyafahamu mambo haya [apate kupiga mbio]; kwa maana njozi ni ya wakati utakaokuja. Lakini itafyatuka mwishowe nayo haitakuwa ubatili. Ajapokawia, mngojee; kwa maana kwa hakika atakuja bila kushindwa [naye hatakaakaa].”
7. Huenda Paulo akawa alivutwaje na Septuagint ya Kigiriki aseme habari ya ‘kuvumilia’ ili kutimiziwa ahadi?
7 Hivyo Septuagint Version inaondoa fikira zetu katika njozi na kuzielekeza kwa mtu anayekuja. Pia, inaposema, “mngojee,” maandishi ya Kigiriki yatumia kitendo (au verb) kinachomaanisha “kuvumilia,” hivyo maana ni kusubiri mpaka anayekuja atakapofika. Vivyo hivyo matumizi haya ya kitendo cha Kigiriki kinachomaanisha “kuvumilia” yaliongoza mtume Paulo kutumia jina (au noun) la Kigiriki linalohusiana na kitendo hicho katika mstari uliotangulia (Waebrania 10:36, NW): “Kwa maana mnahitaji uvumilivu, kusudi, mkiisha kufanya mapenzi ya Mungu, mpokee utimizo wa ile ahadi.”
“KITAMBO KIDOGO SANA”
8. Kulingana na maneno ambayo Paulo alitumia katika Hagai 2:6, ni wakati gani anayekuja atakapofika kama Mfishaji tupate faraja?
8 Yule anayekuja, atakayefika wakati wake, ni Yehova Mungu, ambaye wakati huo atakuja kufikiliza hukumu, kisasi, juu ya wenye kuonea watu Wake. Kuja kwake kutatimiza pia yaliyoandikwa juu ya “njozi.” Yeye atakuja akiwa Mfishaji wakati gani au karibuni kadiri gani? Mtume Paulo aandika: “Bado ‘kitambo kidogo sana.’” Hapa anataja maneno ya Hagai 2:6, ambayo inasema: “[Yehova] wa majeshi asema hivi, Mara moja tena, ni kitambo kidogo tu, nami nitazitikisa hizo mbingu, na hii nchi, na bahari, na nchi kavu.” Hivyo Yehova aonyesha kwamba muda uliowekwa, “kitambo kidogo sana,” wamhusu yeye mwenyewe. Na kwa kuwa mtume Paulo aongozwa na Mungu na kuhusianisha kipindi hicho na kuja kwa Yehova bila kukawia, twaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakuja karibuni sana kufikiliza hukumu juu ya wapinzani na watesi.
9, 10. (a) Kwa sababu gani twaweza kuwa na hakika kwamba muda ambao Mungu anauita “kitambo kidogo sana” hautakuwa mrefu sana kwetu? (b) Shetani na jeshi lake la mashetani wanajua nini juu ya wakati wao wa kuwa huru duniani?
9 Muda ambao ni “kitambo kidogo sana” kwa Mungu wa Milele waweza kuwa muda mrefu sana kwetu. Hata hivyo, na tukumbuke tuko wapi katika “wakati wa mwisho.” (Zab. 90:4; 2 Pet. 3:8; Dan. 12:4) Adui wetu mkuu zaidi, Shetani Ibilisi, anajua kwamba tuko katika sehemu ya kumalizia ya mwisho wa taratibu ya mambo ambayo amekuwa akiiongoza muda mrefu, kwa sababu yeye ndiye “mkuu wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31) Anajua kwamba sasa ni karibu miaka elfu sita tangu alipoingia katika mwendo wake wa kuasi akashawishi wazazi wetu wa kwanza wajiunge naye kuasi enzi kuu ya ulimwengu wote ya Mungu Aliye Juu Zaidi. Wakati uliobaki akiwa huru kudanganya dunia yote inayokaliwa na watu unakaribia sana kwisha. Baada ya ufalme wa Mungu wa Kimasihi kuzaliwa mbinguni mwishoni mwa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914. Shetani Ibilisi na jeshi lake la mashetani walishindwa mbinguni wakatupwa chini katika ujirani wa dunia hii. Ndipo waliposikia sauti kubwa ya ushindi ikipazwa:
10 “Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku. Nao wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo, na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hawakupenda maisha yao hata kufa. Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”—Ufu. 12:10-12.
11. “Ole” unaotajwa katika Ufunuo 12:12 unahusu nani, na jinsi gani?
11 Kwa hiyo Ibilisi na jeshi lake la mashetani wanajua kwamba wana kipindi kifupi tangu kutupwa kwao kutoka mbingu takatifu. Wakati wa kipindi hiki kifupi wameweza kuleta madhara mengi sana hapa duniani. Huo “ole wa nchi na bahari” hauhusu ndugu Wakristo ambao Ibilisi na mashetani wake wamewashtaki mbele za Mungu wetu. “Ole” huo wahusu walimwengu hapa katika nchi kavu na bahari. Wao wako katika uwezo wa yule mwovu. (1 Yohana 5:19) “Ole” huo unatia ndani magumu yote ya kisiasa, ya kijamii, ya kiuchumi na ya kidini ambayo Shetani na mashetani wake wanaleta wakiwa na “ghadhabu nyingi.” Kwa hiyo wanadamu wanaopatwa na ole huo wanaelekea kuharibiwa na Mfikilizaji anayekuja katika ‘dhiki kubwa’ ambayo sasa yaukaribia sana ulimwengu. (Ufu. 7:14) Shetani na mashetani wake wamejikaza wafanye madhara makubwa sana kama wawezavyo, katika “wakati mchache” sana uliobaki.—Ufu. 12:12.
VITA JUU YA MABAKI YA UZAO WA MWANAMKE
12. Shetani atendaje kama joka kuelekea wanadamu kwa ujumla, naye anajaribu kufanyaje wahubiri wa Ufalme?
12 Kwa kuleta “ole” juu ya walimwengu wanaofanya biashara kwa uchoyo katika nchi kavu na bahari, Shetani Ibilisi kama joka anameza wanadamu kwa ujumla wawe sehemu ya tengenezo lake la kidunia linaloonekana. Anawashughulisha mno watafute mali za kimwili kwa uchoyo kwa sababu ya “ole” walio nao, hata wanakosa wakati, fikira au shauku juu ya ufalme wa Mungu wa Kimasihi uliozaliwa karibuni. Ni wachache sana kati yao wanaochukua kwa uzito au kuchukua hatua juu ya “habari njema ya ufalme” inayohubiriwa ulimwenguni pote na mashahidi Wakristo wa Yehova. Lakini, Shetani Ibilisi hatosheki na hilo. Akiwa na tamaa mbovu ya kushinda kusudi la Yehova Mungu, anajitahidi sana kusukumiza wahubiri wa Ufalme katika kambi yake, ambamo watu bado wanapendelea ulimwengu utawalwe na serikali za kisiasa za kibinadamu. Katika “wakati mchache” alioruhusiwa, “joka” amejitahidije kufanya hivyo?
13. Kwa hiyo Shetani ameendelea kufanya nini, na hiyo yapatanaje na yaliyosemwa na Mungu katika Mwanzo 3:15?
13 Anafanya hivyo kwa kupiga vita juu ya wanafunzi wa Kristo wanaoelekea kutawala naye katika ufalme wake wa mbinguni kwa miaka elfu. Vita hiyo si ya kuwazia tu, bali ni halisi kabisa kama Yehova alivyomwambia nyoka wa mfano katika Bustani ya Edeni baada ya uasi wa Adamu na Hawa. Huko Yehova alisema: “Nami nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwa. 3:14, 15) “Uadui” huo umeendelea mpaka leo hii. Huyo “nyoka wa zamani,” “joka” wa mfano, Shetani Ibilisi, ajua kwamba ufalme wa Mungu wa Kimasihi ulizaliwa katika mbingu mwaka wa 1914, ijapokuwa alijitahidi kuuzuia usizaliwe. (Ufu. 12:1-5, 9) Hawezi kuondoa uhakika wa kwamba Ufalme ulizaliwa.
14. Sasa Shetani ana lengo la kushambulia nani?
14 Lakini, karne zote hizo kumi na tisa zilizopita, Shetani amejua kwamba Yehova amekuwa akiita na kuchagua warithi wenzi wa Yesu Kristo wakatawale naye kwa muda wa mileani moja. Sasa duniani yamebaki mabaki machache tu ya hao wanaotazamiwa kuwa warithi wenzi wa Yesu. Lengo la Shetani ni kuwashambulia wao hasa.
15. (a) Mungu anazuiaje “ole” unaopata wanadamu usipate mabaki ya Ufalme? (b) Shetani bado anajitahidi kufanya nini ili ashinde kusudi la Mungu?
15 Mabaki ‘yanafurahi’ pamoja na “mwanamke” wa Mungu, tengenezo la mbinguni la Yehova, juu ya kuzaliwa kwa “uzao” wa Ufalme wa mwanamke huyo. Mabaki hayo ya wanaotazamiwa kuwa warithi wenzi wa Kristo ndiyo mabaki ya “uzao” wa “mwanamke” wa mbinguni wa Mungu. (Ufu. 12:12, 17) Kwa kuagiza “joka” na mashetani wake watupwe duniani kutoka mbinguni, Yehova hakuleta ole juu ya mabaki ya Ufalme ambao wangali duniani. Bali, ameufanya huu “wakati wa mwisho” uwe na baraka zaidi kwa mabaki ya Ufalme. Baraka hizo za kiroho zinashinda “ole” unaowapata walio chini ya utawala wa Ibilisi. Lakini Shetani Ibilisi anajaribu kuvunja hali ya kubarikiwa ya mabaki ya “uzao” wa Ufalme. Yeye angali anataka kushinda kusudi la Mungu la kuwa na warithi wenzi wa Kristo 144,000. Anajitahidi sana kuzuia mabaki wasistahili kuwa watawala katika Ufalme huo. Jinsi gani?
16. Kulingana na Ufunuo 12:17, Shetani anajaribuje kuzuia mabaki wasistahili kupata Ufalme, na amekuwa akifanya hivyo tangu wakati gani?
16 Ufunuo 12:17 waeleza. Unaeleza anaofanya “joka,” Shetani Ibilisi, na mashetani wake baada ya kuondolewa mbinguni kwa nguvu, yaani: “Joka akamkasirikia yule mwanamke, akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.” “Joka” wa mfano na malaika zake wa kishetani walipiga vita wakashindwa kudumu katika cheo chao katika mbingu takatifu baada ya kuzaliwa kwa ufalme wa Mungu wa Kimasihi mwaka wa 1914 W.K. Kwa hiyo sasa, wanapokuwa wamezuiwa katika ujirani wa dunia yetu, wanafanya vita kwa chuki juu ya wale walio duniani wanaoitwa kwenye ufalme wa Kimasihi waliopigana nao mbinguni.—Ufu. 12:7-13.
17. Ni kwa njia gani “vita” hiyo ni halisi juu ya watendaji wa mapenzi ya Mungu, naye Yesu ataikomeshaje?
17 Hiyo si vita ya maneno tu, bali ni vita halisi. Imekwisha ua sana mamia mengi ya mashahidi Wakristo wa Yehova, kati ya “waliosalia” wanaotazamiwa kuwa warithi wenzi wa Kristo na kati ya “mkutano mkubwa” wa wale wanaojitayarisha sasa kuwa raia za kidunia za ufalme wa Kristo wa miaka elfu. (Ufu. 7:9-17; 20:4-6) Kwa umoja mabaki wa Ufalme na “mkutano mkubwa” wanafanya “mapenzi ya Mungu” kwa kushika amri Zake na kutimiza kazi ya “kuwa na ushuhuda wa Yesu.” Wanatoa ushuhuda juu ya Yesu kwamba sasa ametawazwa mbinguni na anajitayarisha kuharibu mawakili wote wa kidunia wa joka ili akomeshe vita anayofanya juu ya wanafunzi wake waaminifu, na baada ya hapo amfunge na kumtia gerezani pamoja na mashetani wake kwa miaka elfu ya utawala Wake utakaoleta amani.
18. Mabaki watatimiziwa ahadi gani ya Mungu, na hiyo itakuwa na matokeo gani juu ya ushirika wa Ufalme?
18 Mungu atatimiza ahadi Yake kwa wale watakaotenda mapenzi Yake duniani mpaka mwisho. Jitihada ambazo “joka” anafanya kwa nguvu zake zote azuie mabaki wasiingie katika ufalme wa mbinguni zitashindwa tu. Ufunuo 20:4-6 watuhakikishia kwamba watendaji hawa wa mapenzi ya Mungu ambao wanahitajiwa bado kukamilisha ushirika kamili wa warithi wenzi wa Ufalme 144,000 watavumilia kwa uaminifu mpaka kufa, ili waweze kupata furaha ya kushiriki katika “ufufuo wa kwanza.” Ufalme wa Mungu wa Kimasihi hautakosa hata mmoja wa warithi wenzi wa Kristo waliowekwa tangu zamani.
19. “Mkutano mkubwa” watatimiziwa ahadi gani ya Mungu, na kwa sababu ya kufanya nini?
19 “Mkutano mkubwa” wanaotazamiwa kuwa raia za kidunia za ufalme wa Kristo wanaunga mkono mabaki wa Ufalme kwa kushikamana nao katika jitihada za kufanya “mapenzi ya Mungu” mpaka mwisho. Wanajiunga kishujaa na mabaki kufanya mapenzi ya Mungu, mpaka enzi kuu ya ulimwengu wote ya Yehova Mungu itakapoondolewa lawama. “Mkutano mkubwa” huu wenye uaminifu na utii utatimiziwa ahadi ya Mungu ya kuwa na makao ya Paradiso duniani. Watafurahi ajabu wakati Mwana wa Mungu anayetawala atakapowaalika kwa upendo akisema: “Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu.”—Mt. 25:34.