Uwezo wa Neno la Mungu Katika Maisha Yangu
MIMI nakumbuka miaka mitatu iliyopita, wakati maisha yangu yalipokuwa yamejawa na msukosuko. Wakati huo sikumjua Yehova Mungu, na maisha yangu yalionyesha sikumjua.
Nilikuwa katika mwaka wa pili wa ndoa yenye mashaka mengi sana. Ndoa yangu ya kwanza, iliyoanza nikiwa na umri wa miaka kumi na sita, ilivunjika baada ya miaka minane, mume wangu wa kwanza alipopelekwa gerezani. Miezi michache baadaye nilikutana na mtu ambaye akawa mume wangu wa pili. Baada ya kuishi pamoja miezi sita, tuliamua kuoana kisheria.
Mume wangu nami tulifanya kazi ya wakati wote. Yeye alikuwa msimamizi wa duka, nami nilitunza hesabu za kampuni ya bima. Tulitumia wakati wetu wote na nguvu zetu zote tukifanya kazi hizo. Muda mwingi tuliacha watoto wetu wawili (niliokuwa nimezaa wakati wa ndoa ya kwanza) wakiwa pamoja na baba na nyanya yao.
Tulitumia wakati wetu wa anasa kwa kujirusha akili tukivuta bangi au kasumba kali. Tulipoivuta mwishoni mwa juma, ilikuwa vigumu kwenda kazini asubuhi ya Jumatatu. Lakini tulitumia dawa fulani za kichwa ili kuweza kufanya kazi. Maisha hayo yalituongoza kufanya uasherati, ikaonekana kwamba ndoa yetu iliyokuwa ya pili kwetu wote ingemalizika kwa kutalikiana.
KUJIFUNZA KWELI ZA BIBLIA
Wakati huo ndipo mwanamke mmoja aliye rafiki yangu mkubwa, aliyekuwa na matatizo yake ya ndoa, alipoamua kwenda Colorado akatulize akili. Alipokuwa akikaa na rafiki zake wa zamani, aliona kwamba walikuwa wakijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Kwanza hakupendezwa, lakini akaanza kuona ubora wa habari za Biblia walizokuwa wakizungumza naye.
Aliporudi nyumbani alipeleka habari kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova katika mtaa huo, akawaomba wampelekee mtu wa kujifunza naye Biblia. Alipelekewa. Baada ya hapo mwanamke huyo aliye rafiki yangu alinitembelea, ukawa ndio mwanzo wa mazungumzo mengi marefu juu ya Biblia.
Mwishowe rafiki yangu huyo alinikaribisha nyumbani kwake nikaonane na mume na mke waliokuwa wakijifunza naye. Baada ya kukaa nao saa moja, nilistaajabu. Hawakuwa watu wajinga kama nilivyodhani. Walikuwa wamezoezwa sana kutumia Biblia. Nilifanya haraka mume wangu apate kuwaona. Lakini yeye hakupendezwa. Aliniambia ikiwa nilitaka mambo hayo, ni SAWA tu, lakini hakutaka nimwingize ndani yake.
Baadaye alisikiliza kwa siri habari za Biblia nilizokuwa nikizungumza na rafiki yangu, halafu akawa na hamu. Alikubali kuonana na yule mume na mkewe. Alipendezwa kama mimi, tukaanza kufunzwa Biblia. Baada ya miezi michache tulijua kwamba tulikuwa tukifunzwa kweli inayotajwa na Biblia katika Yohana 8:32: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” Ilituweka huru. Ilituweka huru tukaacha kutumia dawa za kulevya, kufanya uasherati, na kufanya shughuli za kutafuta mali bila kutosheka.
TENDO LA WIVI
Wakati ulipokaribia wa kujiweka wakf tumtumikie Yehova Mungu kwa kubatizwa majini, dhamiri yangu ilianza kunisumbua. Kuna dhambi moja niliyotenda ambayo nilijua lazima imalizwe. Nilikuwa nimeiba.
Cheo changu cha kazi kiliniwezesha kutunza pesa za kampuni pamoja na taarifa za kila mwezi za hesabu ya pesa. Nilianza kuzichukua wakati wa ndoa yangu ya kwanza. Mume wangu wa kwanza alikuwa akifanya matendo haramu nyakati zote, naye alihitaji pesa nyingi ili kujiondoa matatani. Mwishowe, alitiwa gerezani.
Alipokwenda gerezani, niliachwa na watoto wawili wa kutunza. Mapato yangu hayakutosha kulipa deni zetu zote na kutunza jamaa. Basi, niliiba.
Sasa, nilikuwa tayari kuweka maisha yangu wakf kwa Yehova, na ingawa nilikuwa nimeacha kuiba, nilikuwa nikisema uongo nilipokuwa nikitoa taarifa ya pesa kila mwezi. Nilijua nisingeweza kumtumikia Yehova mpaka niweze kuishi kupatana na kweli.—Mit. 14:5.
KULITATUA TATIZO
Mume wangu nami tulisali Yehova atusaidie. Ndipo tulipomweleza mzee Mkristo aliyekuwa akitufunza habari zote. Nilidhani watu hao wazuri wangeona sistahili msamaha kwa sababu ya matendo yangu. Kumbe sikuwajua watu wa Yehova! Upendo, huruma na msaada walionipa ni sifa ambazo huwezi kuona katika ulimwengu wa leo.
Nilifanyiwa mpango nipelekee wakili tatizo langu. Nilipokuwa garini kwenda afisini kwa wakili, na kupanda kipandishio cha umeme nikaone watu wake, nilisali Yehova anipe nguvu za kufanya mapenzi Yake. (Flp. 4:13) Mawakili hawakushangaa kwa sababu nilikuwa nikiziiba pesa. Walishangaa kwa sababu nilitaka kukubali wivi wangu waziwazi.
Walisema, “Hakuna aliyejua. Mbona usizirudishe polepole?”
Niliwaeleza kwamba nilitaka kumtumikia Yehova Mungu, na kwamba ilinipasa kuanza kumtumikia nikiwa na dhamiri safi. Waliamua kufanya mpango wa kuonana na tajiri wangu wamweleze habari za wivi wangu. Ikanipasa kungoja juma moja kabla hawajaonana naye. Sitasahau kamwe juma hiyo! Siku hizo nililala karibu sana na watoto wangu, nikidhani kwamba labda ningepelekwa gerezani, nikashindwa kujua hali yao itakuwaje nikifungwa.
Mume wangu anawapenda. Anajisikia kama kwamba wao ni watoto wake mwenyewe, lakini wazazi wangu walipinga vikali imani yetu mpya, nami nikaogopa kwamba watamnyang’anya watoto. Ndoa yetu sasa ilikuwa imebadilika ikawa nzuri kwa sababu ya kufuata kanuni za Biblia, nami nilihuzunika sana nilipodhani kwamba ningetenganishwa na mume wangu.
Tulisali daima Yehova atusaidie. Nilimwomba anipe nguvu za kufanya mapenzi yake ikiwa aliona ningemtumikia vizuri zaidi nikiwa gerezani. Ingawa tajiri wangu alishtuka kwa sababu ya udanganyifu wangu, alipendezwa sana na uaminifu niliopata kwa sababu ya imani yangu mpya. Alikubali kunifanyia mipango ya kulipa pesa kwa kuipasha habari kampuni yenye kuweka dhamana. Alitaka pia niendelee kufanya kazi huko, lakini kampuni hiyo ikakataa. Tulikaa miezi minane tukingoja uamuzi.
Mimi sikuandika habari hizi nikiwa gerezani, bali nyumbani kwangu mwenyewe. Walikubali kuniruhusu nilipe deni hiyo. Basi, sisi tumefurahi kuona watoto wetu wakijifunza habari za Yehova, na katika kusanyiko letu la mzunguko lililokwisha, tulimwona binti yetu mwenye miaka kumi na sita akionyesha wakf wake amtumikie Yehova Mungu. Alihitimu shule kiangazi kilichopita, na sasa ni painia msaidizi. Julai 1, 1976, mimi pia nilianza kazi ya kuwapa watu ushuhuda wakati wote.
Sasa mume wangu anafurahi kuwa na madaraka ya kundi, naye alipata pendeleo la kufanya kazi katika makusanyiko mawili ya wilaya wakati wa likizo lake, kiangazi kilichopita.
Tunamshukuru Yehova kwa sababu ya fadhili zake za upendo, msamaha wake na ruhusa aliyotupa tumtumikie. Sisi tumeona kwamba Zaburi 144:15 inasema kweli itajapo kwamba: “Heri watu wenye [Yehova] kuwa Mungu wao.”