Mtoto Mpotevu Arudi
MARA ya kwanza nilionana na Mashahidi wa Yehova mwaka 1956, nilipokuwa mwenye umri wa miaka kumi na mitatu. Wakati huo baba yangu wa kambo alianza kujifunza na Shahidi mmoja, mfanya kazi mwenzake. Nilipokuwa na miaka yapata kumi na mitano nilibatizwa. Halafu nilipotimu miaka kumi na sita, nilianza kufanya mambo kijinga, kama vijana wengi wanavyofanya, nikafanya uasherati na msichana shuleni. Muda mfupi baada ya hapo nilitengwa na ushirika wa kundi la Kikristo, halafu nikaingia jeshini. Baada ya kuwa huko juma mbili, niliamua kutetea kanuni za Biblia. Wawili kati yetu tulichukua msimamo huo katika Fort Ord, tukasumbuliwa sana akilini na mwilini. Tulisumbuliwa kwa kupigwa-pigwa, kufungiwa tukiwa peke yetu kabisa, kupewa chakula kidogo tu, na mambo kama hayo. Baada ya miezi mitatu nilifunguliwa kwa njia ya heshima. Miaka mingi baadaye niligundua kwamba baba yangu halisi, aliye mlimwengu hodari sana, ndiye aliyefanya mipango nifunguliwe.
Baba yangu halisi alikuwa mjanja sana, na baada ya muda mfupi aliweza kuongoza maisha yangu. Niliingia siasani, nikawa mcheza kamari, nikapata pesa nyingi sana kwa kutumia ujanja. Lakini wakati wo wote nilipoona Mashahidi au vitabu vyao nilitamani sana kubarikiwa na Yehova na kushirikiana na watu wake. Nilijisikia nikitaka kuwaambia, “Angalieni hali yenu ya kiroho, msiache kitu cho chote kiwazuie kumtumikia Yehova.”
Agosti mwaka 1974, karibu miaka kumi na mitano tangu nilipotengwa na ushirika, baba yangu wa kambo, ambaye sasa alikuwa mwangalizi wa mzunguko wa Mashahidi wa Yehova, alimwita mwangalizi-msimamizi wa kundi liitwalo Palm Springs West Congregation akaagiza kwamba mmoja wa wazee anitembelee na kuniachia toleo la Agosti 1, 1974 la The Watchtower (Kiswahili ni Februari 1, 1975), lililokuwa na makala yenye kusema “Rehema ya Kimungu Yaonyesha Njia ya Kurudi kwa Wenye Kutenda Makosa.” Wakati huo nilikuwa nimekwisha tulia nikifanya kazi ya televisheni, nikawa naibu-msimamizi wa kituo cha televisheni katika California. Wakati mzee wa kundi aliponijia akaongea nami, akaniletea toleo hilo la pekee la The Watchtower, nilijisikia nikitaka sana kurudi, nikaona ndugu huyo alikuwa mnyofu sana. Nilikuwa ningali na mazoea maovu sana katika ulimwengu, nikadhani nisingeweza kutoka humo kamwe.
Baadaye nilipata habari kwamba mzee huyo aliona kwamba nilitaka sana kurudi. Nilihudhuria mikutano kadha, na miezi saba iliyofuata alinitembelea kwa ukawaida katika kituo cha televisheni.
Desemba 1975 mzee huyo alinitembelea tena afisini mwangu. Wazo la kwanza kuingia akilini mwangu lilikuwa ulizo, “Umekuwa wapi?” Nilifurahi sana kumwona, nikajisikia nikirudiwe na tamaa ya mambo ya kiroho. Nilifurahi sana kusaidia Mashahidi wapate habari za televisheni juu ya mambo yaliyokuwa yakitendeka Malawi. Wakati huo nilikuwa nimekaza nia nifuate kweli, naye mzee huyo alinisaidia nikaona ubora wa sala na kutegemea rehema ya Yehova na fadhili zake za upendo.
Miezi michache iliyofuata nilianza kusafisha maisha yangu. Kwanza, nilifanya mabadiliko katika shughuli za kazi ili kuwa mwaminifu. Baada ya muda mfupi nililazimika kutafuta kazi nyingine. Mapato yangu yalipungua zaidi ya 60 kwa mia. Nilijitenga kabisa na udanganyifu nikaacha bidhaa zenye pesa nyingi nilizopata kwa kucheza kamari. Mke wangu alikubali kwanza, halafu akaniacha. Mambo yote hayo yaliwapa wanasiasa, wakuu wa shirika na wengineo nafasi nzuri sana ya kusikia kweli. Jambo lililokuwa gumu zaidi ni kuwaeleza habari za paradiso ya Yehova itakayokuwa duniani, kisha niwaambie kwamba mimi sikuwa bado katika hali ya kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Halafu, Aprili 1976, baada ya kutengwa karibu miaka kumi na saba, nilirudishwa nikawa mmoja wa Mashahidi Wakristo wa Yehova. Kuweza kuchukua jina hilo, na kueleza watu habari za makusudi mazuri sana ya Yehova, ndilo pendeleo kubwa zaidi ulimwenguni. Nimefurahi sana kuwa safi na huru, na kuwa tena na baraka ya Yehova.
Nimekuwa na pendeleo la kugawia watu vitabu vingi vinavyohusu habari za Biblia, na kufanya watu wapendezwe. Maono yanayopendeza zaidi yanahusu aliyekuwa katibu wangu katika kituo cha televisheni. Kwa kuwa mwanamke huyo alikuwa katibu wangu miaka kadha, alistaajabu kuona nikibadilika upesi sana. Mabadiliko niliyofanya yalimpendeza, halafu Februari 1976 yeye na watoto wengine wawili wakaanza kujifunza Biblia. Alibatizwa Septemba 12, 1976 katika kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova, akawa Shahidi aliye wakf.