Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 8/15 kur. 17-19
  • Kwa Sababu Gani Utafakari?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Sababu Gani Utafakari?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Habari Zinazolingana
  • Kutafakari Ambako Hunufaisha
    Amkeni!—2000
  • Tafakari Mambo ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Kutafakari
    Amkeni!—2014
  • Wahudumu Wenye Bidii Wanahitaji Kusali na Kutafakari
    Huduma Yetu ya Ufalme—2010
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 8/15 kur. 17-19

Kwa Sababu Gani Utafakari?

INAKUBIDI utumie wakati ili kutafakari, yaani kujikumbusha, kuwaza au kufikiri kwa uzito juu ya jambo. Lakini ni wakati uliotumiwa vizuri. Kutafakari juu ya mambo yanayofaa kunathawabisha (kunaleta faida) sana.

Biblia inatoa uongozi juu ya mambo ambayo tunapaswa kufikiria kwa kufaa. Tunasoma hivi: “Mambo yo yote yaliyo ya kweli, yo yote yaliyo ya staha, yo yote yaliyo ya haki, yo yote yaliyo safi, yo yote yenye kupendeza, yo yote yenye sifa njema; ukiwapo wema wo wote, ikiwapo sifa nzuri yo yote, yatafakarini hayo.”​—⁠Flp. 4:8.

Mtu aendeleapo kutafakari juu ya mambo kama hayo yenye kujenga, yanakuwa na matokeo mazuri katika moyo wake. Kuthamini kwake juu ya kufaa kwa mambo hayo bora kunazidi kukua, na anazidi kufahamu kwamba kutenda kulingana na kutafakari kwake kunaleta matokeo mema kwake yeye mwenyewe na kwa wanadamu wenzake. Na kama matokeo, yale anayosema na kufanya yanakaribia sana kanuni za Mungu za usafi. Hiyo inaonyeshwa na maneno ya Yesu: “Mtu mwema katika hazina njema ya moyo wake hutoa yaliyo mema, na mtu mwovu katika hazina mbovu ya moyo wake hutoa yaliyo maovu; kwa kuwa mtu, kinywa chake hunena yale yaujazayo moyo wake.”​—⁠Luka 6:45.

Kulingana na hayo, kadiri mtu azidivyo kufikiria mambo yanayofaa, ndivyo yanavyozidi kuonekana katika usemi na matendo yake. Ni kama vile Mithali inavyosema: “Moyo wa mwenye haki hufikiri [hutafakari, NW] jinsi atakavyojibu; bali kinywa cha wasio haki humwaga mabaya.” (Mit. 15:28) Kutafakari kunakoleta faida kunazuia mtu asitoe majibu yasiyosawazika, ya upuzi. Hatakuwa akisema tu yale yaliyomo akilini mwake. Pahali pake, yeye atafikiria mambo yote, pamoja na kufikiria hali na maono ya watu wengine kabla ya kutoa jibu katika mambo mazito. Yeye hatasikitikia jibu lake la unyofu baadaye.

Pamoja na kuendeleza ushirika mzuri na wanadamu wengine, kutafakari kunasaidia sana kuendeleza msimamo mzuri mbele za Muumba. Kama alivyofanya mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu, vilevile, sisi tutafanya vizuri tukitumia nyakati za faragha zenye utulivu. tukitafakari juu ya sifa na matendo ya Yehova Mungu. Daudi mtunga zaburi alisema hivi: “Ninapokukumbuka kitandani mwangu, nakutafakari Wewe makesha yote ya usiku. Maana Wewe umekuwa msaada wangu, na uvulini mwa mbawa zako nitashangilia.” (Zab. 63:6, 7) Mtunga zaburi mwingine alisema: “Pia nitaitafakari kazi yako yote; nitaziwaza habari za matendo yako.”​—⁠Zab. 77:12.

Wote wanaotamani kuwa watumishi wanaokubalika wa Mungu wanaweza kujiuliza hivi: Je! mimi ninapata wakati wa kutafakari juu ya Muumba kama alivyofanya mtunga zaburi? Je! mimi ninajikumbusha kwa kuthamini mambo ambayo amenifanyia​—⁠kutoa Mwanawe awe ukombozi, kufungua moyo wangu niikubali kweli yake, kunisaidia niyashinde magumu ya maisha ya kila siku, kunipa tumaini imara la wakati ujao, na mengine mengi? Je! mimi ninayafikiria matendo yake ya wakati uliopita kwa wanadamu jinsi alivyoonyesha upendo, rehema, haki ya hukumu, hekima na sifa nyingine nyingi nzuri sana.

Kutafakari mambo yanayofaa kama huko kunaweza kukuza upendo wetu kwa Yehova Mungu. Na kama matokeo, uhusiano (urafiki) wetu utakuwa kama ule wa mtoto anayemtumaini na kumpenda babaye na kutaka kumpendeza. Uhusiano wetu na Baba yetu wa mbinguni utakuwa wa kipekee, yaani, tutamjua na kujua Mwanawe kweli kweli aliyemtoa kwa ajili yetu. Inapokuwa hivyo, hatutakuwa wenye kuzoea dhambi kwa makusudi. Mtume Yohana alionyesha hili alipoandika juu ya matokeo ya kumjua Yesu Kristo: “Kila akaaye ndani yake hatendi dhambi; kila atendaye dhambi hakumwona yeye, wala hakumtambua.”​—⁠1 Yohana 3:6.

Watoto wanaowapenda sana wazazi wao hawawaasi. Vivyo hivyo, wale wanaomjua Mungu na Mwanawe Yesu Kristo hawapi kisogo, wakifuata mwenendo uliyo kinyume cha mapenzi ya kimungu kwa makusudi.

Kwa upande mwingine, uhusiano dhaifu na Muumba unaweza kuongoza kwenye hatari kubwa. Ndiyo, kukosa kutafakari juu ya mambo ya kiroho kunaweza kuongoza kwenye kupoteza kibali ya Mungu. Yesu Kristo alionyesha jambo hili katika mfano wake juu ya mpanzi. Akieleza maana ya mfano huo, alisema kwa wanafunzi wake hivi: “Wale wa karibu na njia ndio wasikiao, kisha huja Ibilisi akaliondoa hilo neno mioyoni mwao, wasije wakaamini na kuokoka. Na wale penye mwamba ndio wale ambao wasikiapo hulipokea lile neno kwa furaha; nao hawana mizizi, huamini kitambo kidogo, na wakati wa kujaribiwa hujitenga. Na zilizoanguka penye miiba ni wale waliosikia, na katika kuenenda kwao husongwa na shughuli na mali, na anasa za maisha haya, wasiivishe lo lote.”​—⁠Luka 8:12-14.

Katika kila moja ya hali hizo tatu zilizoelezwa na Yesu Kristo kulikuwako na kutothamini sana kwa moyo “neno la Mungu” au “neno la ufalme.” (Mt. 13:19; Luka 8:11) Udongo uliokuwa karibu na njia ulikuwa mgumu sana kwa sababu ya kukanyagwa na watu. Vivyo hivyo, mtu akiruhusu wengine waongoze maisha yake sana watumie wakati wake mwingi na nguvu zake, atakuwa na shughuli (kazi) nyingi mno hata akose nafasi ya kulifikiria “neno la Mungu” kwa moyo. Hata ingawa huenda akalisikia, kukosa kulitafakari kutaufanya moyo usiitikie. Hali zile nyingine mbili vilevile zinatokea kwa sababu ya kukosa kutafakari juu ya mambo yanayofaa vya kutosha. Kwa hiyo, kiasi cha kuthamini “neno la ufalme” kinachositawishwa si chenye nguvu kutosha kuvumilia majaribu makali au kushinda masumbufu ya maisha ya kila siku au tamaa ya mali au anasa.

Bila shaka tunayo sababu nzuri ya kuwa na wakati wa kutafakari juu ya mambo yanayofaa. Kutafakari kama huko kunaweza kutia nguvu uhusiano wetu na Muumba, na kutuwezesha tuendelee kuwa safi machoni pake. Vilevile kunaweza kutusaidia sana tuwe chanzo cha kutia wengine moyo na baraka kwa neno na tendo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki