Wahudumu Wenye Bidii Wanahitaji Kusali na Kutafakari
1. Ni nini kilichomsaidia Yesu kuepuka kukengeushwa kutoka katika kazi yake kuu?
1 Yesu alikuwa ametumia kipindi cha jioni kuwaponya watu na kufukuza roho waovu. Wanafunzi wake walipompata siku iliyofuata, walimwambia: “Watu wote wanakutafuta,” wakimsihi aendelee na kazi zake zenye nguvu. Hata hivyo, Yesu hakukengeushwa kutoka katika kazi yake kuu ya kuhubiri habari njema. Aliwaambia: “Twendeni mahali pengine, katika miji ya vijiji iliyo karibu, ili nipate kuhubiri huko pia, kwa maana nilitoka kwa kusudi hilo.” Ni nini kilichomsaidia Yesu kuendelea kukazia fikira huduma yake? Alikuwa ameamka mapema ili kusali na kutafakari. (Marko 1:32-39) Kusali na kutafakari kunaweza kutusaidiaje sisi pia kuwa wahubiri wenye bidii?
2. Tunaweza kutafakari kuhusu nini ili kudumisha bidii yetu katika huduma?
2 Tutafakari Kuhusu Nini? Yesu aliona kwamba watu walikuwa “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:36) Vivyo hivyo, tunaweza kutafakari kuhusu jinsi watu wanavyohitaji habari njema. Tunaweza kutafakari kuhusu uharaka wa nyakati zetu. (1 Kor. 7:29) Tunaweza pia kutafakari kuhusu kazi za Yehova na sifa zake, pendeleo letu la kuwa Mashahidi wa Yehova, na hazina za kiroho zenye thamani ambazo tumejifunza katika Neno la Mungu, na ambazo bado watu wengi katika eneo letu hawazijui.—Zab. 77:11-13; Isa. 43:10-12; Mt. 13:52.
3. Tunaweza kutafakari wakati gani?
3 Tutafakari Wakati Gani? Kama Yesu alivyofanya, wengine huamka mapema wakati hakuna kelele. Wengine hupendelea kutafakari wakati wa jioni kabla ya kuenda kulala. (Mwa. 24:63) Hata tukiwa na ratiba yenye shughuli nyingi, tunaweza kupata wakati wa kutafakari. Wengine hufanya hivyo wanaposafiri. Wengine hutumia wakati wao wa chakula cha mchana ili kutafakari bila kukengeushwa. Wengine huona kwamba kutafakari, hata kwa dakika chache, kabla ya kushiriki katika huduma huwasaidia kuhubiri kwa bidii zaidi na kwa ujasiri.
4. Kwa nini tutafakari?
4 Kusali na kutafakari kutatuchochea tutake kumtumikia Yehova zaidi, kutatusaidia kuona ibada yetu kwa Yehova kuwa ya maana zaidi, na kutaimarisha azimio letu la kuendelea kuhubiri. Yesu, yule Mhudumu Mkuu wa Mungu, alifaidika kwa kutafakari, nasi pia tutafaidika.