Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 8/1 kur. 17-20
  • “Kuwa Kama Mianga Katika Ulimwengu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kuwa Kama Mianga Katika Ulimwengu”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “NYOTA” KATIKA MKONO WA KUUME WA KRISTO
  • MIPANGO YA UTARATIBU NA KUFUNDISHA
  • Kundi la Kikristo na Utendaji Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • “Ninayajua Matendo Yako”
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2019
  • Kristo Analiongoza Kutaniko Lake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Uangalizi Wenye Upendo Hujenga
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 8/1 kur. 17-20

“Kuwa Kama Mianga Katika Ulimwengu”

ULIMWENGU wa wanadamu unahitaji sana mwangaza kutoka kwa Mungu. Udanganyifu, uvunjaji wa sheria, jeuri, uonevu na matendo yasiyo ya haki yameongezeka. Watu wengi wanavunjika moyo na kukata tamaa. Wanaona maisha hayana kusudi. Wengine wanajaribu kutafuta njia ya kuepuka kwa kutumia vileo, dawa za kulevya, tafrija, ngono za namna yote, ndiyo, kwa kutumia cho chote kinachowasaidia wasahau magumu ya sasa. Bado wengine wanaweza kusahau namna mambo yalivyo kwa kujitia sana katika kazi yao, Jamaa na watu. Lakini maisha yao yanapokuwa yenye taabu, wanalazimishwa kuona kwa uzito namna ulimwengu huu ulivyo.

Bila shaka, watu wanahitaji uongozi na mwangaza ili wapate faida zote za maisha wakati huu na kuwa na tumaini imara wakati ujao. Lakini ni nani wanaoweza kutoa mwangaza huo leo? Bila shaka hawawezi kuwa watu wenyewe wale wanaoongozwa na roho ya ulimwengu huu​—⁠choyo chake, pupa, kutofikiria wengine, tamaa isiyo na kizuizi ya anasa ya mwili au uvunjaji wa sheria. Watu peke yao wanaoweza kuangazia akili za wengine ni Wakristo wa kweli, ambao wametiwa mwangaza na Neno la Mungu na utendaji wa roho yake. Kwa sababu hiyo, imewapasa watumishi wote wa Aliye Juu Zaidi “kuwa kama mianga katika ulimwengu.”​—⁠Flp. 2:15.

Kwa kuwa Wakristo wote wa kweli wanapaswa kuwa mianga, makundi ya watu wa Mungu yanafananishwa katika kitabu cha Ufunuo kama “vinara.” Zaidi ya hayo, baraza za wazee wanaopaswa kuwa mifano kwa kundi lote zinafananishwa na “nyota.” (Ufu. 1:20) Akisimulia mambo aliyoona, mtume Yohana, mwandikaji wa kitabu cha Ufunuo, anatuambia hivi: “Niliona vinara vya taa saba vya dhahabu; na katikati ya vile vinara nikaona mtu mfano wa Mwanadamu. . . . Naye alikuwa na nyota saba katika mkono wake wa kuume.”​—⁠Ufu. 1:12-16.

“NYOTA” KATIKA MKONO WA KUUME WA KRISTO

Ili washiriki wa kundi watumike kama kinara cha taa katika ulimwengu wenye giza, inawapasa wapatane na mambo yanayofunuliwa katika maneno hayo. Kichwa cha kundi zima la Kikristo ni Yesu Kristo, maana Yeye ndiye aliye “katikati ya vile vinara.” Kwa hiyo, washiriki wa kundi wanatumika kama mianga kwa kufuata sana Kichwa chao na kufuata mfano wake kwa maneno na kwa matendo. Kwa kunyenyekea sana ukichwa wa Kristo, wazee wanaendelea kuwa kama “nyota” katika “mkono wake wa kuume,” yaani, katika kibali yake. Zikiwa katika mkono wake, baraza za wazee ziko chini ya uongozi wake. Jambo hilo latokeza ulizo hili, Yesu Kristo anataka wazee wafanye nini katika kusaidia makundi yatumike kama vinara vya taa?

Hizi ni amri za msingi ambazo Mwana wa Mungu aliwapa wanafunzi wake:(1) “Kesheni basi, kwa maana hamjui ajapo bwana wa nyumba, kwamba ni jioni, au kwamba ni usiku wa manane, au awikapo jimbi, au asubuhi; asije akawasili ghafula akawakuta mmelala. Na hilo niwaambialo ninyi, nawaambia wote, Kesheni.” (Marko 13:35-37) (2) “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo.” (Yohana 13:34) (3) “Enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na [roho takatifu]; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.”​—⁠Mt. 28:19, 20.

Basi, je! si jambo linalofaa kwetu kutazamia wazee kuwekea kundi zima mfano kwa kufuata amri hizo kwa ushikamanifu? Ni lazima wawe macho kiroho, wafuate sana matakwa bora ya Neno la Mungu katika mambo yanayopasa mwenendo wa bi nafsi. Katika ushirika wao na washiriki wa kundi, imewapasa wawe wakionyesha upendo wa kujinyima, wakitanguliza mapendezi ya wengine kuliko yao wenyewe. Maneno na matendo yao yamepaswa kuonyesha kwamba wanafahamu ubora wa kufanya wanafunzi. Ndiyo, imewapasa wazee wawe ndugu wanaoweza kustahili kutajwa kama “nyota.” Hilo lawataka wawe mfano wenye kutia moyo, si washiriki walio dhaifu tu wa kundi, bali wote. Jambo hilo linapatana na shauri la upole lililoongozwa na Mungu ambalo mtume Paulo alimpa Timotheo, kama mzee mwenzake: “Uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.”​—⁠1 Tim. 4:12.

Nehemia anaonyesha namna mfano mwema ulivyo wa maana sana. Upinzani wa kujenga upya kuta za Yerusalemu ulikuwa mkubwa. Hata hivyo, Nehemia aliongoza kazi hiyo kwa uhodari akimtumaini Yehova na kumwomba kila siku abariki kazi hiyo. Yeye vilevile alifanya kazi hiyo ya kujenga. Matokeo yalikuwa nini? Kazi hiyo ya kujenga ilimalizika vizuri baada ya siku 52 tu.​—⁠Neh. sura 4, 6.

Vilevile, Liwali Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua waliongoza kazi ya kujenga upya hekalu la Yehova kwa bidii walipochochewa na neno la Yehova kupitia kwa manabii Hagai na Zekaria. Aliye Juu Zaidi aliwapa roho yake kupitia kwa manabii wake. Ndipo taifa zima la Israeli lililorudishwa lilipopewa roho ya Yehova kupitia kwa liwali na kuhani mkuu huyo. Namna gani? Ni kwa vile Yoshua na Zerubabeli waliendelea kufanya kazi mpaka ikamalizika, wakatia moyo wajenzi wa hekalu kwa neno na kwa mfano.​—⁠Zek. 4:2-14,

MIPANGO YA UTARATIBU NA KUFUNDISHA

Mipango mizuri ya tengenezo ilihitajiwa ili kazi ya kujenga upya hekalu ipate kufanywa. Kwa mfano, Nehemia aliona lazima ya kuchukua hatua ya kugeuza mipango hiyo ili ipatane na hali hizo. Wakati kazi ya kujenga upya ilipoanza kuendelea vizuri, Sanbalati, Tobia na watu waliokuwa jirani walizidi sana upinzani wao, wakafanya shauri pamoja ili wafanye vita juu ya Yerusalemu. Nehemia alimwomba Yehova kwa sababu hiyo, akawatia watu moyo wamtumainie Yehova, akawapa watu silaha, akapanga wengine kuwa walinzi na kuweka mpango wa kutoa onyo. Ndipo kazi hiyo ilipoendelea na mipango ya adui ikazuiwa kabisa.​—⁠Neh. 4:7-20.

Vilevile, wazee leo wanaweza kufanya mipango itakayosaidia vizuri mahali pao kutenda kazi ya maana ya kufanya wanafunzi. Nafasi bora ya kufanya hivyo inajitokeza katika funzo la kitabu la kundi au funzo la Biblia linalofanywa kila juma. Nyakati zinazofaa zaweza kuwekwa ili kikundi kidogo kikutane washiriki katika kueneza kweli ya Biblia. Kwa vile ni kikundi kidogo, mzee anayeongoza funzo anaweza kutoa msaada kwa mtu mmoja mmoja. Labda atapenda afanye kazi kwanza na wachache mpaka wazoee kujulisha watu ujumbe wa Biblia nyumba kwa nyumba. Anaweza vilevile kuwapanga watangazaji wenye ujuzi wa “habari njema” wafanye kazi pamoja na vijana au pamoja na wengine ambao wangepata faida ya ujuzi wao.

Jambo la kwanza ili kazi ifanywe ni kumtayarisha kila mmoja kwa maarifa ya Maandiko ambayo anaweza kushiriki pamoja na wengine. Wakati wa funzo, labda kiongozi anaweza kuomba wasikilizaji mara kwa mara waeleze namna jambo fulani wanalojifunza lingeweza kutumiwa wakati wa kushiriki kweli ya Biblia pamoja na wasioamini. Angeweza kuuliza wakati habari hiyo ingetumiwa katika kumsaidia mtu kiroho na namna gani hilo lingeweza kufanywa katika kazi za mtu za kila siku. Anaporudia kuzungumza tena pamoja na kikundi mambo ambayo wamejifunza, angeweza kuuliza ikiwa mtu mmoja angependa kuonyesha namna wazo la Maandiko lililozungumzwa siku hiyo lingeweza kutumiwa wakati wa kutembelea watu nyumbani kwao.

Vilevile kuna faida ya kukitayarisha kikundi hicho mapema juu ya watu watakaotembelea. Kwa habari yake mwenyewe, mtume Paulo alisema hivi: “Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi . . . Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu.” (1 Kor. 9:20-22) Jambo linalopendeza mtu mmoja au sehemu ya watu halipendezi mwingine au watu wengine. Basi, tukijua hali ya watu tunaojaribu kufikia kwa ujumbe wa Biblia, tunaweza kufikiria mapema tunalotaka kuwaambia. Labda itafaa kuomba maoni kutoka kwa watu mbalimbali katika funzo la kitabu waeleze njia ambayo wameona kuwa yenye matokeo na sababu gani iko hivyo.

Jambo jingine linaloweza kuzungumzwa kwa faida nzuri nyakati nyingine ni namna tunavyoona watu wengine. Watu wote wamenunuliwa kwa damu yenye bei kuu ya Mwana wa Mungu, kwa hiyo wanapaswa waambiwe namna wangepata faida zaidi mmoja mmoja. Hata wawe na maoni gani juu ya watangazaji wa “habari njema,” Yehova Mungu anataka sana watubu. (2 Pet. 3:9) ingekuwa vema kama nini kuchunguza mara kwa mara tuone kama kazi yetu ya kuhubiri hadharani inaonyesha kama tunafahamu jambo hilo! Kwa mfano, je! tungekuwa tayari kutoa maisha zetu ikiwa kufanya hivyo kungeleta matokeo ya kusaidia watu walio katika mtaa wetu wapate ujuzi usio na makosa wa kweli ya Mungu? Mtume Paulo alikuwa tayari kufanya hivyo. Katika barua yake aliyowaandikia Warumi, alisema hivi: “Nasema kweli katika Kristo, sisemi uongo, dhamiri yangu ikinishuhudia katika [roho takatifu], ya kwamba nina huzuni nyingi na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu. Kwa maana ningeweza kuomba mimi mwenyewe niharimishwe na kutengwa na Kristo kwa ajili ya ndugu zangu, jamaa zangu kwa jinsi ya mwili.”​—⁠Rum. 9:l-3.

Tukizungumza maonyesho hayo tunaweza kusaidiwa tuchunguze namna sisi wenyewe tunavyoona wengine na kama kweli tunafikiria mambo ya Maandiko. Tunapopenda watu wengine, hilo linajifunua katika njia yenye ‘kuvutia ambayo katika hiyo tunawafikia. Kwa sababu hiyo, watu wenye mioyo minyofu wataona wepesi wa kuitikia “habari njema.”

Zaidi ya kuweka mfano mwema na kuzitumia nzuri nafasi zake afundishe wale walio katika kikundi chake, mzee anaweza vilevile kutia moyo waamini wenzake. Wakati wa manabii Hagai na Zakaria, Wayahudi hawangemaliza kazi ya kujenga upya hekalu kwa nguvu zao wenyewe. Kulikuwako vizuizi vikubwa. Kwa hiyo, walijengwa sana bila shaka waliposikia maneno haya: “Iweni hodari, enyi watu wote wa nchi hii.” “Mimi [Yehova] ni pamoja nanyi.” “Msiogope.” (Hag. 2:4, 5) Vivyo hivyo, mzee anapoonyesha imani yake katika msaada ambao Yehova anawapa watu wake ambao yeye mwenyewe ameshuhudia na anatenda kupatana na imani hiyo, jambo hilo linawatia wengine nguvu sana. Vilevile, furaha yake ya kumtumikia Yehova inaweza kuwa yenye kuhimiza na kutia moyo sana.

Walakini, haitegemei uhodari wa watu wala uwezo wa tengenezo wa kuleta matokeo mazuri, bali inategemea roho ya Mungu ambayo ndiyo nguvu inayowezesha Wakristo wa kweli waangaze kama mianga katika ulimwengu wa uadui. Ndiyo nguvu iliyomwezesha Liwali Zerubabeli na Wayahudi wafanya kazi wapate kumaliza kazi ya kujenga upya hekalu ijapokuwa upinzani kutokana na watu waliowazunguka. Yehova alimtumia nabii wake Zekaria atangaze kwamba “si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho [yake].”​—⁠ Zek. 4:6.

Bila shaka wazee wanahitaji kufundisha vizuri, kutia moyo na kuweka mfano mwema ili roho ya Mungu iwatie bidii washiriki wa kundi. Namna gani? Kwa sababu leo roho ya Mungu haiwapi Wakristo mmoja mmoja maarifa ya mwujiza. Inatenda kama kumbukumbu na kama mwalimu. Ikiwa kumbukumbu, roho hiyo inamkumbusha Mkristo mambo ambayo amejifunza kutokana na Maandiko na, ikiwa mwalimu, inamwezesha afahamu namna habari hiyo ambayo amekumbushwa inavyopaswa kutumiwa. (Yohana 14:26) Kwa hiyo, Mkristo anaweza kujulisha wengine kweli na kuwasaidia waifuate kwa msaada wa roho hiyo ya Mungu, kwa kadiri anavyojua yaliyomo katika Biblia. Ikiwa hakuna wazee wengi, wanaweza kuomba watumishi wa huduma na Wakristo wengine waliokomaa wawasaidie kulijenga kundi kwa kutumia maarifa ya Maandiko.

Yapaswa mikutano yote ya kundi itumiwe kutoa maagizo yanayokusudiwa kusaidia wote wawe “kama mianga,” katika neno na katika tendo vilevile. Kwa hiyo, ni lazima kujitayarisha kwa uangalifu ili mikutano iwe yenye kutoa elimu na kuvuta fikira za wahudhuriaji. Vilevile wazee wanaweza kufundisha wanapotembelea washiriki wa kundi katika nyumba zao, wanapozungumza nao kabla na baada ya mikutano na wanapotangaza pamoja “habari njema” hadharani.

Basi ili kundi litumike kama “kinara” cha taa katika mtaa fulani, washiriki walo wanapaswa kujua na kufahamu Maandiko kusudi roho ya Mungu iweze kuwa msaada mkubwa zaidi wa kuwa kumbukumbu na mwalimu. Kwa kuwa roho ya Mungu ni takatifu, itatenda juu ya wale tu wanaoendeleza hali yao safi mbele za Aliye Juu Zaidi, juu ya wale tu wanaoendelea kukesha kiroho na kuwapenda kweli kweli wanadamu, sana sana waamini wenzao. Je! wewe unashiriki kukifanya “kinara” cha taa kiangaze sana katika mtaa wako, kwa sifa ya Yehova Mungu na kwa kumtii sana Yesu Kristo, kichwa cha kundi la Kikristo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki