Maoni ya Kimungu Juu ya Deni
MUNGU mwenye haki, Yehova, hapendelei watu wasiolipa deni zao. Naye alimwongoza mtunga zaburi aseme hivi: “Asiye haki hukopa wala halipi.” (Zab. 37:21) Naye mtume Paulo alieleza jinsi inavyowapasa Wakristo kuwa, akawasihi hivi: “Msiwiwe na mtu cho chote, isipokuwa kupendana.”—Rum. 13:8.
Basi, inapasa mtu anayetaka kuwa na kibali ya Mungu awe na uaminifu wa kulipa pesa alizokopa au kulipia vitu au utumishi anaopokea bila kukawia. Inampasa ajiangalie asikope vitu vinavyopita uwezo wake wa pesa. Ama sivyo huenda akajikuta hawezi kulipa. Tena, haipasi mtu akawie kulipa deni. Ungekuwa upumbavu na ukosefu wa shukrani mtu akichelewesha malipo na kumbe anatumia pesa nyingi akijifurahisha mambo ya anasa au kwenda katika malikizo yenye gharama nyingi.
Huenda watu wengine wakadhani kwamba si vibaya sana kukawia kulipa deni ya mtu wa ukoo au rafiki. Lakini je! kutolipa si kukosa uaminifu, kumwumiza mtu ati kwa sababu ni wa ukoo wako au ni rafiki?
Mtu anayekosa kulipa wengine deni kwa sababu ya kutojali haonyeshi upendo. Anawanyima nafasi ya kutumia pesa wanazostahili. Huenda akawaumiza kwa sababu ya kutowalipa. Kwa mfano, ifikirie hali ya watu wenye kazi zao wenyewe—waganga, mawakili, mafundi wa umeme, maseremala na wengineo. Wanapata gharama fulani wanapofanya kazi zao. Lazima wapate malipo ili kuweza kulipia gharama zao, na vilevile kuwa na kiasi cha kutosha kujipatia riziki. Sasa, watu wengi wakikosa kuwalipa, huenda watu hao wakashindwa kulipia vitu walivyotumia, na huenda hata wakalazimika kufunga kazi zao. Ni wazi kwamba watu wanaonyima wenzao riziki hawaonyeshi upendo.
Hili si jambo la mchezo. Mtume Yohana alionyesha hivyo alipowaandikia Wakristo akawaambia: “Kila amchukiaye ndugu yake ni mwuaji: nanyi mnajua ya kuwa kila mwuaji hana uzima wa milele ukikaa ndani yake. Katika hili tumelifahamu pendo, kwa kuwa yeye aliutoa uhai wake kwa ajili yetu; imetupasa na sisi kuutoa uhai wetu kwa ajili ya hao ndugu. Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo?”—1 Yohana 3:15-17.
Ikiwa ndugu huyo mwenye shida hawezi kupata msaada mahali pengine, atakufa akinyimwa riziki yake muda mrefu kupita kiasi. Kwa hiyo, mtu anayejiita Mkristo na huku anakataa kumsaidia atakuwa na hatia ya kutojali. Vivyo hivyo, Wakristo wakijifaidi wenyewe kwa kuchelewesha kumlipa mwamini mwenzao deni, wanaweza kuwa na hatia ya kumfanya afunge kazi yake. Hapo wanaweza kumletea matatizo makubwa ya pesa na kumfanya awe na shida. Ikitukia hivyo, je! hatuwezi kusema kwamba waliokataa kulipa deni zao walimwonyesha ndugu yao chuki nyingi?
Wakristo waaminifu hawajaribu kujifaidi wenyewe huku wakiumiza mtu ati kwa sababu ni ndugu yao wa kiroho. Wanajua kwamba kufanya hivyo kungekuwa ‘kutamani fedha ya aibu.’ (1 Tim. 3:8) Tunajifunza katika Maandiko kwamba pupa hiyo inaweza kuharibu uhusiano wa mtu na Yehova Mungu. Kisa cha Gehazi mtumishi wa Elisha kinaonyesha jambo hilo vizuri. Elisha alitumiwa kuponya Naamani, jemadari wa jeshi la Shamu, ukoma mbaya sana. Naamani alitaka kumpa nabii zawadi ili kushukuru kwa sababu ya kuponywa. Lakini Elisha aliikataa, maana hakutaka kujifaidi na cheo cha unabii alichopewa na Mungu, wala kutokana na miujiza iliyohusika. Lakini, Gehazi alikuwa mwenye pupa, basi akatamani zawadi iliyokataliwa na Elisha, akaichukua kwa kumwambia Naamani uongo. Kwa sababu hiyo, Gehazi alipatwa na ukoma kuonyesha kwamba Yehova ndiye aliyemhukumu.—2 Fal. 5:15, 20-23, 27.
Basi, ikiwa mtu anakataa kulipa deni zake kwa sababu ya pupa, anaweza kujiletea hukumu kali. Biblia inatuonya kwa kutuambia kwamba ‘wenye pupa hawataurithi ufalme wa Mungu.’ (1 Kor. 6:10, tafsiri ya Kiingereza ya New World) Naam, pupa yake inaweza kumkosesha zawadi ya uzima wa milele. Loooo!
Basi, inatupasa sisi Wakristo tuwe waaminifu tunaposhughulika na watu wote. Inatupasa tuongozwe na kanuni zifuatazo: “Yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mt. 7:12) “Kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Gal. 6:10) Kwa hiyo, ikiwa sisi tunataka wenzetu wawe waaminifu kwa kulipa deni zao, je! haitupasi kuwawekea mfano unaofaa? Inatupasa tufikirie sana kutendea ndugu zetu Wakristo mema, bila kutumia vibaya fadhili zao kwa kukawia kuwalipa vitu vyao.
Ingekuwa vibaya Wakristo wakidhani kwamba waamini wenzao wanapaswa kuwahurumia kidogo na kuwapunguzia bei wanapowauzia vitu. Lakini waamini wenzetu wakituhurumia, inatupasa tuwashukuru. Inapasa Wakristo watake kuona ndugu zao wakipata wanachostahili kupata. Shauri ambalo mtume Paulo aliandikia watumwa Wakristo linatuwekea uongozi mzuri: “Wale walio na mabwana wenye kuamini wasiwadharau, kwa sababu ni ndugu. Bali, na wawatumikie kwa hiari zaidi, kwa sababu wale wanaopokea faida ya utumishi wao mzuri ni waamini na wapendwa.” (1 Tim. 6:2, tafsiri ya Kiingereza ya New World) Mkristo akiwa mwaminifu katika kulipa waamini wenzake deni alizo nazo, atakuwa amefuata onyo hilo la upole.
Na tuonyeshe kwa vile tunavyolipa deni kwamba tunaendesha mambo yetu kupatana na kanuni za Biblia. Tusisahau kamwe kwamba ni Uovu kukataa makusudi kulipa wengine vitu vyao. Aliye Juu Zaidi hawezi kukubali kamwe watu wasiolipa deni zao kwa sababu ya pupa au uchoyo. Tunaweza kutazamia baraka ya Yehova tukihakikisha kwamba ‘hatuwiwi na mtu cho chote, isipokuwa kumpenda.’