Uwe Mwenye Hekima—Usiwe Mwenye Pupa
“ANGALIENI, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.”—Luka 12:15.
Ni jambo gani lililosababisha Yesu aseme hivyo? Mkutano mkubwa ulikuwa ukimsikiliza wakati mtu mmoja alipopaza sauti akasema: “Mwambie ndugu yangu anigawie urithi wetu.” (Luka 12:13) Kwa kweli hakukupaswa kuwe na sababu ya ombi kama hilo, kwa sababu sheria ya Musa ilikuwa imeweka sharti kwamba mzaliwa wa kwanza apate sehemu mbili za mali zote zilizokuwa za baba yake. Kwa hivyo, bila shaka, mtu huyu aliyetaka Yesu afanye hukumu kwa faida yake alikuwa anatamani kisichokuwa chake.
Maneno ya Yesu kuhusu kutamani, yanayotajwa hapo juu, yalikuwa yameelekezwa kwa mkutano uliokuwa umesikia ombi la mtu huyo. Maneno haya yanafunua kwamba ni lazima mtu aone thamani ya vitu kwa njia inayofaa ili ajiepushe na tamaa au pupa. Hapaswi kusahau uhakika wa kwamba, cho chote anachokitamani vibaya, hakiwezi kamwe kusaidia katika kuhifadhiwa kwa uhai wake. Kwa kweli, pupa inaweza kuongoza kwenye msiba.
Hii inaonyeshwa vizuri na yale yaliyompata Gehazi, mtumishi wa nabii Mwebrania Elisha. Mkuu wa jeshi la Shamu Naamani, alikuwa ameponywa ugonjwa mbaya sana wa ukoma na Elisha. Naamani alitaka kumtolea Elisha zawadi ili aonyesha kuthamini kwake kuponywa huku kwa mwujiza. Lakini nabii huyo alikataa kuichukua, kwa kuwa hakutaka kujifaidi na cheo na uwezo aliokuwa amepewa na Yehova. Lakini, Gehazi, alitamani sana zawadi hiyo, akiwaza kwamba ilikuwa sawa kuikubali. Alimfuata Naamani, na kwa jina la Elisha, akaomba talanta ya fedha na mavazi mawili, akisingizia kwamba nabii huyo alikuwa amebadili mawazo yake kwa sababu vijana wawili kutoka kwa wana wa manabii walikuwa wamefika. Naamani alifurahia kusaidia, akamtolea Gehazi, si talanta moja tu ya fedha, bali talanta mbili za fedha na mavazi mawili.—2 Fal. 5:15, 16, 20-23.
Inaonekana kama kwamba pupa ya Gehazi ilimfaidi. Lakini sivyo. Alipoteza pendeleo la kuwa mtumishi wa Elisha. Kwa pupa yake, na kwa kutumia vibaya jina la bwana yake ili ajipatie faida ya kichoyo na kwa kusema uongo kuhusu nabii huyo, Gehazi alijiletea msiba yeye mwenyewe na uzao wake. Akiitaja hukumu ya Mungu, Elisha alimwambia Gehazi hivi: “Ukoma wa Naamani utakushika wewe, na uzao wako hata milele.” Kutekelezwa kwa hukumu hiyo hakukukawia. Habari hiyo inaendelea kusema: “Naye akatoka usoni pake [Elisha] mwenye ukoma mweupe kama theluji.”—2 Fal. 5:27.
Bila shaka Yehova Mungu anawaona kwa uzito sana wale wanaotafuta faida za kichoyo kutokana na zawadi zake. Hii ingetia ndani kutumia daraka alilo nalo mtu katika kundi la Kikristo kujifaidi kichoyo. Kwa kweli, takwa moja la wale wanaowekwa katika mgawo fulani wa utumishi katika kundi ni kwamba ‘wasiwe wenye pupa ya mapato ya udanganyifu.’ (1 Tim. 3:8, NW) Wazee wanaonywa hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo katika uungalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa moyo wa kupenda; wala si kwa upendo wa mapato ya udanganyifu, bali kwa bidii.”—1 Pet. 5:2, NW.
Kuna sababu nzuri ya yale Biblia inayoamuru. Kwa mfano, watumishi waliowekwa katika kundi huenda wakashughulika na fedha. Hiyo inawahitaji wawe na mfano mzuri wa kutokuwa na pupa. Ikiwa sivyo, wakiwekwa katika mgawo hata ingawa wana udhaifu katika jambo hili, huenda wakajaribiwa watumie vibaya waliyoaminiwa, wakitumia kwa faida yao vitu ambavyo si vyao. Pia wazee nao, ni lazima wawe waangalifu wasitumie cheo chao kwa faida au mapato yo yote. Haingekuwa makosa kujipatia mapato ya mambo ya kimwili kwa sababu ya cheo, mamlaka, heshima au sifa tu, bali pia faida nyingine yo yote ya kibinafsi.
Mzee au mtumishi aliyewekwa kundini akianza kuwa mwenye pupa, yeye kama Gehazi, atapoteza cheo chake. Lililo zito hata zaidi, huenda hata akapoteza uhusiano wake na Yehova.
Jambo hili la kujiepusha na pupa linapaswa kuangaliwa sana, si na wale tu walio na mgawo katika kundi la Kikristo, bali pia na Wakristo wote wa kweli. Biblia inawatia watu “watamanio,” au wenye “pupa” kati ya wale ambao “hawataurithi ufalme wa Mungu.” (1 Kor. 6:9, 10) Pupa kama hiyo huenda ikajionyesha katika njia mbalimbali. Huenda ikawa ni kupenda fedha, tamaa ya kuwa na uwezo au sifa, kujitoa katika kula au kunywa kupita kiasi, ngono isiyo halali na kadhalika.
Ili ujiepushe na kuwa mwenye pupa, ni lazima mtu aangalie mambo yale anayoyafikiria na kuyazungumza. (Flp. 4:8; Efe. 5:3) Pupa haipaswi kuwamo kati ya Wakristo wa kweli.
Kwa hiyo ukitaka kudumisha uhusiano mwema na Mungu, jiepushe na pupa. Badala ya kuachilia tamaa mbaya ikue moyoni mwako, jitahidi kufikiria mambo mema na yenye kujenga. Hiyo inaweza kuongeza furaha yako katika maisha sasa na ikuhakikishie wakati ujao salama. Ndiyo, uzima unapatikana, si kutokana na kitu kinachotamaniwa na mtu, bali kwa kuyapinga maelekeo yo yote ya kuwa na pupa na kudumisha uhusiano unaokubaliwa na Yehova Mungu.