Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 5/1 kur. 6-8
  • Furaha Inayotokana na “Roho ya Kupenda”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Furaha Inayotokana na “Roho ya Kupenda”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Habari Zinazolingana
  • Ile Roho Ambayo Yehova Hubariki
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Jinsi Yehova Anafanikisha Kazi Yake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Jinsi Kazi za Ufalme Zinavyogharimiwa
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Yote Hayo Hugharimiwaje?
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 5/1 kur. 6-8

Furaha Inayotokana na “Roho ya Kupenda”

“NAWEZA KUSAIDIA?” Maneno hayo mawili tu yenye fadhili yanaonyesha sana jinsi mtu alivyo. Yanaonyesha nini? Yanaonyesha “roho ya kupenda.”Kusaidia mtu fulani au kushiriki kufanya kazi fulani ya maana kunampa mwenye kusaidia furaha nyingi sana. Watu wengi leo wanapokea furaha nyingi sana kwa kushiriki katika kazi ambayo Yesu aliamuru ifanywe ulimwenguni pote. Kazi gani hiyo? “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14, NW) Naam, 1978 Yearbook of Jehovah’s Witnesses kinaonyesha kwamba watu 2,223,538 walionyesha roho hiyo ya kupenda mwaka 1977 kwa kutii amri hiyo, nao walitumia saa 321,424,305 wakieleza watu “habari njema” katika nchi na visiwa mbalimbali vya bahari 216. Hakika huo ni utimizo wa ajabu wa maneno ya unabii yaliyosemwa na Daudi: “Watu wako wanajitoa kwa hiari; siku ya uwezo wako.”​—Zab. 110:3.

Nyakati zote roho hiyo ya kupenda imepatikana kati ya wamwabuduo Yehova, tangu Habili kuja kwenye wapendao haki leo. Yehova amewabariki sana watu wake kwa sababu ya kuwa na roho hiyo ya kupenda. Jinsi tunavyoshukuru kwamba ametupa nafasi ya kuionyesha, kisha tukajipatia furaha kwa kufanya hivyo! Wale walio na roho hiyo leo wanaweza kuyathamini maneno ya Yesu mwenyewe aliposema kwamba “ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) Wewe umeipata furaha hiyo? Naam, furaha ya kweli inatokana na kugawana vitu na wengine, kushiriki nao katika mambo, kupenda kuwasaidia. Tunaweza kujipatia furaha nyingi sana tukiziona nafasi tulizo nazo za kutoa na kujua jinsi ya kufanya hivyo.

Fikiria jinsi Yehova alivyoshughulika na taifa la Israeli nyakati zilizopita. Wao walipewa nafasi nyingi waonyeshe roho ya kupenda, nao walipofanya hivyo walibarikiwa sana. Masimulizi yaliyo katika Kutoka 19:7, 8 yanatueleza kuhusu wakati ambao ‘Musa alikwenda akawaita wazee wa watu, akawafunulia maneno hayo yote, Yehova aliyokuwa amemwagiza.’ Waisraeli waliitikiaje? “Watu wote wakaitika pamoja wakasema, Hayo yote aliyoyasema [Yehova] tutayatenda [“tuna nia ya kuyatenda,” NW].” (Angalia pia Kutoka 24:3 na 24:7.) Maandishi yanaonyesha kwamba maadamu waliendelea kuonyesha roho hiyo ya kupenda walifanikiwa.

Tena kulikuwa na nyakati ambazo nafasi zilitokea kwa njia nyingine. Wakati Waisraeli walipokuwa jangwani, ikawa lazima vifaa vikusanywe kujenga hema. Ni kama vile Musa alivyosema: “Katwaeni kati yenu matoleo kwa [Yehova]; mtu awaye yote aliye na MOYO WA KUPENDA, ayalete matoleo; dhahabu na fedha na shaba; na nyuzi za rangi ya samawi,” na vitu vingine. (Kut. 35:4-9, 20-29) Roho ya kupenda ya Waisraeli haikuonekana kwa kutoa vifaa vya kuutosha ujenzi tu, bali ilionekana pia kwa njia tunayoelezwa katika Kutoka 36:6, 7, kwamba “Musa akatoa amri, nao wakatangaza mbiu katika marago yote, wakisema, Wasifanye kazi tena, mtu mume wala mwanamke, kwa ajili ya matoleo kwa mahali patakatifu. Basi watu wakazuiwa wasilete tena. Kwani vile vitu walivyokuwa navyo vilikuwa vyatosha kwa kuifanya kazi hiyo yote kisha vilizidi.” Loo! watu walishangilia kama nini!

Tofauti kabisa na jambo hilo, makanisa mengi na matengenezo mengi ya kidini leo yana matatizo makubwa ya kupata pesa, na vilevile yana matatizo mengineyo yanayotokea kwa sababu washiriki wao hawana roho ya kupenda. Wanatumia mazoea ya namna zote wapate pesa. Katika United States makanisa yanaendesha michezo ya bahati-nasibu, yanapitishia watu sahani za sadaka, bahasha za kutia pesa na sasa wameanza kuiga kamari inayochezwa nyakati za usiku mjini Las Vegas. Gazeti fulani la majuzi la mjini New York lilisema wachungaji 407 walio katika Wilaya Kuu ya Askofu wa New York walieleza kwamba kuna ukosefu mwingi wa pesa katika makanisa yao. Walisema kwamba leo pesa zao zinakaribia sana kumalizika na kwamba ‘wana wasiwasi juu ya kesho.’ Ripoti hiyo iliendelea kusema hivi: “Kwa sababu ya wasiwasi huo, wachungaji wengi wanapanga kuanzisha chumba cha kamari ili mchezo huo uhudhuriwe na watu wote baada ya sheria kukubali uchezwe nyakati za usiku kama inavyokuwa mjini Las Vegas, kuanzia Februari 1, 1977. Labda wachungaji hao hawapendi mchezo wa kamari, lakini wanazihitaji sana pesa zinazopatikana kwa njia hiyo.” Je! unaweza kuwaza Kristo Yesu akianzisha mazoea hayo hekaluni katika siku zake? Maandishi yanaonyesha waziwazi jinsi alivyowaona wafanya biashara waliojaribu kufanya mambo kama hayo.​—Mt. 21:12, 13.

Wala Wakristo wa kwanza hawakuwa na mazoea kama hayo. Wao walikuwa na roho ya kupenda. Kulingana na yanayosemwa na wanahistoria wa kwanza, hakuna jambo lo lote linaloonyesha walipitishia watu sahani za sadaka, wakacheza kamari au wakatoza zaka. Tertullian, aliyeongoka akawa Mkristo karibu na mwaka 190 W.K., aliandika hivi: “Hata kukiwa na sanduku fulani la hazina, haliwi limetengenezwa kwa pesa ambazo watu wanatozwa kama kiingilio, kama kwamba dini ni mkataba. Kila mwezi kila mtu analeta kisarafu kidogo​—au wakati wo wote atakapo, tena anafanya hivyo ikiwa anaweza; kwa maana hakuna mtu anayelazimishwa; ni toleo la hiari ya mtu.” (Apology XXXIX 5) Wakristo wa kwanza walitoa vitu kwa moyo, na kwa kufanya hivyo wakawa na furaha. Walikuwa na roho ya kupenda.

Wakati mtu anapojisikia ni lazima atoe kitu, kwa sababu ya kukazwa au kwa sababu ya kutazamwa na wengine kwa njia isiyofaa, anapoteza furaha. Halafu, tena, wako matajiri fulani wanaopenda kutoa kwa sababu wana wingi, lakini labda kusudi lao linakuwa kujipatia fahari. Lakini, ingawa watu wa namna hiyo wanaweza kupata thawabu yao kamili sasa, yaani ‘kutukuzwa na watu,’ wao pia wanaikosa baraka na furaha aliyoitaja Yesu. (Mt. 6:1-4) Basi tunaweza kuyathamini sana maneno ya mtume Paulo yanayotutia moyo yasemapo: “Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu. Mkitajirishwa katika vitu vyote mpate kuwa na ukarimu wote, umpatiao Mungu shukrani.”​—2 Kor. 9:7, 11.

Ingawa sisi sote bi nafsi tuna daraka la kushiriki katika kazi ya Ufalme na kutoa michango kwa njia nyingi, wengi wameona inafaa na inafurahisha moyo kupeleka michango ya hiari moja kwa moja kwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, 124 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201. Kwa sababu gani? Kwa sababu ya kuisaidia kazi kubwa sana inayoendeshwa na Sosaiti hiyo kuwapa watu elimu ya Biblia ulimwenguni pote, nayo michango hiyo inatumiwa kusaidia maeneo ambayo sisi hatuwezi kuyasaidia. Katika nchi nyingine Mashahidi wanapeleka upaji wao kwenye maafisi ya matawi katika nchi za kwao. Matawi hayo yamepangwa upande wa nyuma wa vitabu na vijitabu vingi vya Sosaiti. Kwa kutumia njia hiyo watu wengi walifurahi kujua kwamba wameshiriki kuifanya kazi ya Yehova, kwa maana upaji hautumiwi kwa makusudi mengine ila kusaidia kazi ya kuutangaza ufalme wa Mungu. Tunaweza kupata furaha nyingi tukiitumia nafasi hiyo ya kutoa michango. Jambo la maana ni ile roho ya kupenda, kama inavyoonyeshwa na mifano ifuatayo.

Hivi majuzi Watch Tower Society ilipokea barua yenye kusema hivi, kwa ufupi: “Ndugu Wapendwa, Humu ndani nimetia mchango kutoka kwa mama yangu mwenye umri wa miaka themanini na sita. Aliniomba niwape shukrani zake mwenyewe kwa ajili ya magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! anayopokea kwa ukawaida kwa njia ya posta. . . Mama anakua kiroho kwa sababu ya kusoma Biblia kwa ukawaida pamoja na Mnara wa Mlinzi, naye anamhimidi Yehova daima kwa ajili ya fadhili zake za upendo.” Barua nyingine ilisema hivi: “Ndugu Wapendwa wa Betheli, Jina langu Marisa. Nina miaka minane. Naishi Iowa. Babu yangu alinipelekea dola 2.00, kwa hiyo nimewapelekea dola moja, kwa sababu ile dola nyingine nataka niiweke nikaitumie katika lile kusanyiko kubwa. Nimewapelekea dola hii ili mweze kutengeneza Minara zaidi . . . Nazipenda picha nzuri sana zinazokuwa katika Minara . . . Paradiso itakuja wakati gani?” Bila shaka Yehova anawabariki sana watoto hao kwa sababu wana roho ya kupenda. Roho ya namna hiyo inaonyesha pia kwamba wazazi wao wamewafundisha vizuri, wakasitawisha moyo wa kupenda wa kuuliza “Naweza Kusaidia?”

Naam, roho hiyo ya kupenda kusaidia imeiwezesha Sosaiti hiyo itumiwe na Mashahidi wa Yehova kama chombo cha kuendeshea kazi za namna nyingi, na zote zimewafaidi watu Wake. Angalia kazi chache kati ya hizo: Sosaiti hiyo inatumiwa kupanga makusanyiko katika nchi inayohusika na katika majimbo, mengine yakiwa ya taifa zima na ya mataifa yote, ili kuwatia moyo na kuwajenga kiroho wote wapendao haki. Inasaidia kutuma wanaume waliokomaa wakawe waangalizi wenye kusafiri ili wasaidie makundi yafanye kazi kulingana na mapenzi ya Mungu. Inatumiwa kuiendesha Watchtower Bible School of Gilead ili kuzoeza wamisionari na kuwatunza wakiisha zoezwa na kupelekwa katika sehemu zote za ulimwengu, hata katika maeneo ambako “habari njema” hazijapata kuhubiriwa. Sosaiti hiyo inawapa “mapainia wa pekee” msaada wa pesa kuwawezesha wakae katika maeneo yaliyo peke yake ili kufundisha watu Biblia na kuanza makundi mapya. Halafu, tena, Sosaiti hiyo inasaidia na kutunza wafanya kazi katika matawi yake 97, na wote wanakuwa na roho hiyo ya kupenda. Kila mwaka mamilioni ya shilingi yanatumiwa kusaidia wafanya kazi hao wa wakati wote ambao sasa ni zaidi ya 22,700.

Tena, kumbuka kwamba si wajumbe hao peke yao wanaopata msaada wa pesa, bali Watch Tower Society imetumiwa pia kuwapa msaada wa pesa watu waliopatwa na maafa ya matukio yasiyotazamiwa, matetemeko ya ardhi na dhoruba. Zaidi ya hilo, mavazi na chakula yanapelekwa kwenye eneo la maafa kusaidia wenye taabu.

Sisi sote tuna mapendeleo mazuri ajabu ya kupata furaha kwa kuonyesha roho ya kupenda katika nchi za kwetu. Namna gani katika kundi letu? Je! pesa zinahitajiwa kuhusu Jumba la Ufalme​—kodi yake, ujenzi, vifaa vya kulitunza, umeme, maji na kadhalika? Kwa kuwa tunajua kwamba mambo hayo hayajitimizi yenyewe, je! tunakuwa macho tusaidie? Roho ya kupenda inaondoa matatizo yote yanayohusu mambo hayo.

Kwa hiyo kazi ya kuuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi iendeleapo kupanuka na kusonga mbele kwa nguvu nyingi, tunatangaza kwa uthabiti kwamba Yehova Mungu ndiye Msaidiaji wa kazi yake na watu wake. Mpanuko huo uendeleapo kutokea ulimwenguni pote, acheni tutafute daima nafasi za kuonyesha roho yetu ya kupenda, kisha tuipate furaha ya kweli inayoletwa na roho hiyo. Tukifanya hivyo, maoni yetu ya moyoni yatakuwa kama ya Daudi wakati aliposema hivi: “Unirudishie shangwe ya wokovu utokao kwako wewe, tena unisaidie mimi hata kwa roho ya kupenda.”​—Zab. 51:12, NW.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki