Ile Roho Ambayo Yehova Hubariki
“BWANA awe na roho unayoionyesha. Fadhili zisizostahilika zake ziwe na ninyi watu.” Kwa maneno haya, Paulo alimalizia barua yake ya pili kwa Timotheo. (2 Timotheo 4:22, NW) Lo! ni lazima maneno hayo ya sifa yawe yalimpa Timotheo na wale waliokuwa pamoja naye furaha iliyoje—kujua kwamba wao walionyesha ile roho ambayo Yehova hubariki!
Lakini hasa ni roho ipi ambayo Yehova hubariki? Ni tabia ipi hasa huwatambulisha wale walio na roho hii? Na sisi pia tunawezaje kuonyesha roho hii na kupokea baraka ya Yehova?
Kutusaidia kujibu maswali hayo, acheni turudi nyuma kwenye wakati wa Musa. Waisraeli wako jangwani. Hivi karibuni Yehova alifanya agano la Sheria pamoja nao, na sasa yeye anawaagiza katika njia ambayo inawapasa kumwabudu yeye. Hiyo inatia ndani kujengwa kwa hema ya kukutania inayoweza kubebwa ambayo itahitaji kiasi kikubwa cha dhahabu, vitu vyenye thamani, na ustadi wa kazi kuijenga. Nafasi ya kutoa matoleo kwa hiari kutimiza mahitaji ya vifaa na kazi inatolewa kwa taifa katika maneno haya: “Katwaeni kati yenu matoleo kwa [Yehova, NW]; mtu awaye yote aliye na moyo wa kupenda, ayalete matoleo; dhahabu na fedha na shaba; na nyuzi za rangi ya samawi, na za rangi ya zambarau, na za rangi nyekundu . . . Na kila mtu kati yenu aliye na moyo wa hekima [na aje], na kuyafanya hayo yote ambayo [Yehova, NW] ameyaagiza; yaani, hiyo maskani na hema yake, na kifuniko chake.”—Kutoka 35:5-19.
Taifa hilo liliitikiaje nafasi hii? Sehemu inayobaki ya sura ya 35 husimulia jinsi wale ambao ‘moyo wao uliwahimiza’ na ‘roho yao iliwafanya kuwa wapenda’ walitoa michango na kufanya kazi kwa bidii iliyoonyesha kwamba walithamini sana nafasi hii iliyokuwa imewekwa mbele yao. (Mistari 21, 22,26) Itikio lao lilikuwa la aina ya kwamba sura ya 36, mstari 6, hutuambia kwamba “Musa akatoa amri, nao wakatangaza mbiu katika marago yote, wakisema, Wasifanye kazi tena, mtu mume wala mwanamke, kwa ajili ya matoleo kwa mahali patakatifu. Basi watu wakazuiwa wasilete tena.” Ndiyo, ilikuwa lazima wazuiwe! Yehova hakuwa ametumia njia za werevu za kuwakaza wakati alipofanya itangazwe hivi: “Mtu awaye yote aliye na moyo wa kupenda . . . “Matokeo yalikuwa ya kwamba taifa lilionyesha roho ya kupenda, na hilo lilileta baraka kwa namna ya furaha kuu, pamoja na ulinzi wa Yehova na mwelekezo katika yote waliyofanya.
Miaka mingi baadaye, roho iyo hiyo ilidhihirishwa kwa mara nyingine tena. Hili lilitukia wakati Mfalme Hezekia alikuwa akifanya kazi kurudisha ibada safi katika Israeli. Simulizi linatuambia kwamba lilipopewa nafasi, “kusanyiko wakaleta dhabihu na matoleo ya shukrani; na wote wenye moyo wa ukarimu, wakaleta sadaka za kuteketezwa.” Matokeo yakawaje? “Akafurahi Hezekia, na watu wote, kwa sababu ya hayo Mungu aliyowatengenezea watu; maana jambo hilo likawa kwa ghafula.”—2 Nyakati 29:31-36.
Wakristo Waonyesha Ile Roho Inayofaa
Je! sisi tunaona roho iyo hiyo ya kujidhabihu kwa moyo wa kupenda katika nyakati za Kikristo? Angalia yale Paulo aliandika juu ya Wakristo Wafilipi kwenye Wafilipi 1:3-5: “Namshukuru Mungu wangu kila niwakumbukapo, sikuzote kila niwaombeapo ninyi nyote nikisema sala zangu kwa furaha, kwa sababu ya ushirika wenu katika kuieneza Injili, tangu siku ile ya kwanza hata leo hivi.” Ni katika njia zipi Wakristo wa Filipi walikuwa wenye kutokeza katika “ushirika [wao] katika kuieneza Injili”? Mistari inayofuata inafanya iwe wazi kwamba si kwamba tu kwa moyo wa kupenda wao walipatanisha njia yao ya maisha na kanuni za Biblia ili kuendeleza habari njema bali pia wao walikuwa wenye bidii katika kuhubiri na kufundisha kwao habari njema kwa wengine.
Kwamba Wakristo wote wanapaswa kushiriki kwa moyo wa kupenda katika kazi ya kuhubiri katika njia hizi inakaziwa kwenye Waebrania 13:15, NW: “Kupitia kwake yeye na tumtolee Mungu sikuzote dhabihu ya kusifu, yaani, lile tunda la midomo linalofanya tangazo la hadharani kwa jina lake.” Kwa hiyo kuhubiriwa kwa habari njema na kila Mkristo ni njia moja kubwa ambayo katika hiyo sisi tunaweza kuonyesha roho ya moyo wa kupenda ambayo ni tabia inayowatambulisha waabudu wa Yehova leo. Zaidi ya hilo, Wakristo wanakumbushwa kwamba haiwapasi kamwe ‘kusahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu anapendezwa sana na dhabihu kama hizo.’—Waebrania 13:16, NW.
Ndugu Wafilipi walionyesha roho hii ya moyo wa kupenda katika njia nyingine bado. Katika sura ya 4 Paulo anataja pindi kadha walipomsaidia kwa njia ya kifedha, hivi kwamba kuhubiriwa kwa habari njema kuliendelezwa. (Wafilipi 4:14-17) Wao waliiga hivyo ule mfano mwema wa wale waabudu wa Yehova wa nyakati za mapema. Wao kwa wazi walimheshimu “Yehova kwa vitu vyenye thamani [vyao].” (Mithali 3:9, NW) Je! sisi tunaonyesha roho iyo hiyo wakati nafasi zinazofanana na hizo zinapowekwa mbele yetu?
Ile Roho Inayokubaliwa Yaonekana Leo
Zaburi 110 huonyesha kwamba kungekuwako wengi wakionyesha roho ii hii nzuri ya kujidhabihu kwa moyo wa kupenda katika siku za mwisho wa huu mfumo uliopo wakati ambapo watu walio wengi wanapendezwa tu na “mimi.” Tunaambiwa katika mstari wa 3, NW kwamba, baada ya Masihi kuchukua utawala katika Ufalme katika 1914, watu wa Mungu ‘wangejitoa wenyewe kwa moyo wa kupenda’ na kwamba wale wanaofanya hivyo wangekuwa wengi kama “umande.” Je! hilo limethibitika kuwa kweli?
Katika Aprili 1881 Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) ulichapisha mwito kwa kutaka wahubiri 1,000 wachukue kazi ya kuhubiri kwa wakati wote. Toleo la Mei 1881 lilikazia kwamba wale wanaoshiriki katika kazi hii lazima wawe wale ambao wangekuwa “wakifanyia kazi mishahara ya kimbingu.” Katika muda wa miaka minne, zaidi ya 300 walikuwa wameitikia—jambo lenye kutokeza kwa sababu ya hesabu ndogo ya Wakristo walio wakfu walioshirikiana na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi wakati huo.
Roho iyo hiyo inaendelea kuonekana leo. Kwa mfano, katika 1986 kulikuwako mapainia (wahudumu wa wakati wote) 391,294 wakiripoti, kwa wastani, kila mwezi. Hilo lilikuwa ongezeko la asilimia 21.2, au 68,473 zaidi ya mwaka uliotangulia! Hata hivyo, roho hii ya moyo wa kupenda si ya wale tu ambao wanaweza kutumia wakati wao wote katika kazi ya kuhubiri.a
Wengi walio na madaraka mengine ya Kimaandiko—kama vile kuangalia jamaa, kuangalia wazazi wasio na nguvu au waliozeeka—na wale ambao afya yao haiwaruhusu washiriki katika huduma ya Kikristo ya wakati wote pia wanaonyesha roho ii hii ya kujidhabihu kwa moyo wa kupenda ambayo inampendeza sana Yehova. Hiyo inakuwa wazi wakati mtu anapotambua kwamba sehemu iliyo kubwa ya kazi ya kuhubiri Ufalme katika nchi zilizo nyingi inafanywa hasa na wahudumu ambao wanalazimika kutumia sehemu iliyo kubwa zaidi ya wakati wao wakifanya kazi ya kimwili au katika kuangalia wajibu wa jamaa au madaraka mengine ya Kimaandiko. Wonyesho wenye kusifika kweli kweli wa ile roho ambayo Yehova hubariki.
Kuonyesha Ile Roho Inayofaa Katika Maeneo Mengine ya Maisha
Kama vile katika siku za Musa na Hezekia, nafasi za kuonyesha roho ya moyo wa kupenda hujitokeza zenyewe leo wakati makundi ya mahali yanapojenga Jumba la Ufalme au vifaa vingine vya aina hiyo. Je! roho ile ile inaonekana katika visa kama hivyo? Ndiyo, hakika kabisa inaonekana!
Hilo limedhihirishwa hasa katika njia za sasa za ujenzi wa Jumba la Ufalme zinazoitwa mara nyingi miradi ya kujenga kwa haraka Jumba la Ufalme. Mamia mengi ya Mashahidi wanakusanyika na kujenga kuanzia mapema Jumamosi asubuhi na kuendelea mpaka jioni ya Jumapili—baadhi yao wakifanya kazi usiku wote—kutimiza kile ambacho magazeti ya habari yamekiita “muujiza wa mwisho-juma.” Mahali ambapo hakukuwa na kitu isipokuwa ubapa wa saruji kwenye uwanja Ijumaa, Jumba la Ufalme lililomalizika linatumiwa kwa mkutano jioni ya Jumapili!b
Hata nafasi kubwa zaidi za kuonyesha roho ya moyo wa kupenda zinajitokeza zenyewe kuhusiana na ujenzi wa vifaa vya tawi katika nchi mbalimbali. Kiasi cha kazi ya kujitolea kabisa kinachochangwa kwenye kazi inayofanywa katika hii miradi mbalimbali inaduwaza mawazo. Kuongezea michango ya kazi, kuna, bila shaka, ile michango ya kifedha inayowezesha kununua vifaa vya ujenzi vinavyohitajiwa. Mara nyingi, Mashahidi wanatoa kwa hiari yao wenyewe misaada ya vitu vinavyohitajiwa ambayo inapunguza sana gharama ya ujenzi.
Kwa mfano hilo lilitukia wakati wa ujenzi wa tawi jipya katika Sydney, Australia. Huko, ndugu wanaoishi katika sehemu ya mbali ya kaskazini mwa Queensland walitayarisha na kutuma kwenye mahali pa ujenzi malori marefu manne yenye shehena za mbao zilizokadiriwa kuwa na thamani ya kutoka dola 60,000 kufika 70,000! Wakati wa ujenzi wa tawi hilo, Mashahidi walisafiri kwa basi kutoka sehemu za mashambani za mbali kama vile Australia Magharibi, umbali wa kilometa 4,000, wakafanye kazi ya kujitolea kwa majuma manne kwa wakati mmoja. Idadi fulani ya ndugu wenye ustadi wa kazi fulani-fulani walifanya kazi kwa kujitolea penye mahali pa ujenzi kwa miezi na baadhi yao hata kwa mwaka mmoja au zaidi. Huu ulikuwa kweli kweli udhihirisho wa roho ile ile ambayo Yehova amebariki kwa wingi sana katika muda wote wa karne zilizopita na ambayo leo inarudiwa mara nyingi katika nchi nyinginezo.
Nafasi zaidi za kuonyesha roho ya moyo wa kupenda hujitokeza wakati wa kukusanyika kwenye makusanyiko na mikusanyiko. Kila kusanyiko kama hilo linahitaji wenye kujitolea wengi, mara nyingi miezi mingi kabla ya tukio hilo, kuhakikisha kwamba kila jambo litaendelea barabara na litakuwa limepangwa vizuri. Na mara lianzapo, nyakati nyingine kufikia mmoja kati ya Mashahidi wanne wanaohudhuria watajitolea kusaidia kufanya zile kazi nyingi zinazohitajiwa zinazofanyiza mkusanyiko wenye kupendeza na wenye kufaulu. Kazi hiyo huenda ikahusu kupakua chakula au kusafisha. Huenda ikawa kazi ngumu ambayo haionwi na walio wengi wa wale wanaohudhuria. Lakini haipiti bila kuonwa na Yehova! Yeye anathawabisha wale ambao wanajitoa wenyewe kwa moyo wa kupenda kufanya yanayohitajiwa. Je! wewe pia unavuna thawabu inayotokea wakati Wakristo ‘wanatumikiana kwa upendo’ kwa kutoa utumishi wako mbalimbali kwa kujitolea kwenye nyakati za kusanyiko? Je! ninyi mmefikiria kufanya hivyo mkiwa jamaa?—Wagalatia 5:13.
Ingawa miradi hii ya pekee inatupa nafasi nzuri za kujitolea wenyewe kwa hii roho ya moyo wa kupenda, kuna nafasi nyingine nyingi za kuonyesha roho ii hii siku kwa siku na juma kwa juma. Kwa mfano, mara Jumba la Ufalme likiisha jengwa, je! wewe unashiriki kikamili katika kulisafisha na kuliweka katika hali nzuri? Je! wewe unategemeza utendaji walo kwa kutoa michango ya kifedha kadiri Yehova anavyokubariki kwa mambo ya kimwili? Je! wewe unategemeza kazi ya kuhubiri katika nchi yako kwa kutoa michango kwa afisi ya tawi ya kwenu. Na la maana hata zaidi, je! wewe unashiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi wa watu katika eneo lenu? Hakuna kitu kinachoweza kweli kweli kuchukua mahali pa ushiriki wetu wa kibinafsi katika kazi hii ambayo Yesu aliionyesha kuwa kazi iliyo ya maana zaidi sana ambayo ingefanywa wakati huu wa sasa, kabla ya mwisho wa mfumo huu.—Mathayo 24:14; 28:19, 20; Matendo 1:8.
Wote wanaositawisha roho hii ambayo Yehova hubariki kwa wingi sana wamepata kuliona kuwa jambo la kweli kwamba Yehova “si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake.” Wewe unaweza pia, kwa kuonyesha roho hii ya kujidhabihu kwa moyo wa kupenda, kuthibitisha kwamba “baraka ya [Yehova, NW] hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.”—Waebrania 6:10; Mithali 10:22.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa baadhi ya mifano yenye kuchangamsha moyo na kutia-moyo ya wale walio jitumikisha wenyewe kwa moyo wa kupenda katika kazi ya kuhubiri wakati wote, ona makala za Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) za 5/15/55, kurasa 317-8; 6/15/62, kurasa 375-9; 7/15/63, kurasa 437-42; 11/1/70, kurasa 666-70; 3/15/71, kurasa 186-90; 8/15/76, kurasa 485-90; 6/15/80, kurasa 24-7. Ona Watch Tower Publications Index 1930-1985 chini ya kichwa “Masimulizi Juu ya Maisha ya Mashahidi wa Yehova” kwa mifano zaidi.
b Ona Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa 8/1/82, kurasa 8-11 na Amkeni! ya 3/8/84, kurasa 12-17.