Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w99 11/1 kur. 30-31
  • Toleo la Hiari ili Kuendeleza Ibada Safi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Toleo la Hiari ili Kuendeleza Ibada Safi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuchanga Vifaa na Ustadi
  • Somo Kwetu
  • Jifanyieni Rafiki kwa Mali ya Udhalimu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kuzijua Njia za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kitabu Cha Biblia Namba 2—Kutoka
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Wakati Mioyo Yetu Inapotusukuma Tufanye Yote Tuwezayo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
w99 11/1 kur. 30-31

Walifanya Mapenzi ya Yehova

Toleo la Hiari ili Kuendeleza Ibada Safi

WAISRAELI walijionea nguvu za kuokoa za Yehova. Waliona maji ya Bahari Nyekundu yakigawanyika kimwujiza, yakiwawezesha kuvuka pakavu na kuponyoka jeshi la Wamisri. Wakiwa upande ule mwingine, walitazama kutoka mahali salama wakati maji hayohayo yaliporudi kwa nguvu na kuangamiza watu waliowafuata. Yehova alikuwa ameokoa uhai wao!—Kutoka 14:21-31.

Lakini inasikitisha kwamba Waisraeli wengine hawakutilia maanani yale ambayo Mungu wao alikuwa amefanya. Musa alipokuwa kwenye Mlima Sinai, walitoa vito vyao vya dhahabu na kumpa Aroni na kutaka awatengenezee sanamu ili waiabudu. Musa aliporudi, aliukuta umati huo wenye kuasi ukila, ukinywa, ukicheza dansi, na kuinamia ndama ya dhahabu! Kwa mwelekezo wa Yehova watu wapatao 3,000—yaelekea wachochezi wakuu wa uasi huo—waliuawa. Siku hiyo watu wa Mungu walijifunza somo muhimu juu ya uhitaji wa kumpa Yehova ujitoaji usiohusisha wengine.—Kutoka 32:1-6, 19-29.

Mara baada ya tukio hilo, Musa alijiandaa kutekeleza amri ya Mungu ya kujenga tabenakulo, hema la kuabudia ambalo lingeweza kubebwa. Kazi hiyo ya ujenzi ingehitaji vifaa ghali sana na wafanyakazi wenye ustadi. Vifaa na wafanyakazi wenye ustadi wangetoka wapi? Nasi twaweza kujifunza nini kutokana na masimulizi hayo ya Biblia?

Kuchanga Vifaa na Ustadi

Kupitia Musa, Yehova aliwaamuru Waisraeli hivi: ‘Toeni katika mali zenu mchango wa kumpa Mwenyezi-Mungu. Kila mtu mwenye moyo mwema atamletea Mwenyezi-Mungu mchango.’ Mchango wa aina gani? Baadhi ya vitu ambavyo Musa aliorodhesha vilikuwa dhahabu, fedha, shaba, kitani, vitambaa, ngozi, mbao, na madini yenye thamani.—Kutoka 35:5-9, BHN.

Waisraeli walikuwa na vitu vya kutosha kuweza kutoa mchango kama huo wa ukarimu. Kumbuka kwamba walipotoka Misri walichukua vito vya dhahabu na fedha pamoja na nguo nyingi. Kwa kweli, “wakawateka Wamisri nyara.”a (Kutoka 12:35, 36) Hapo awali, Waisraeli walikuwa wametoa vito vyao kwa hiari ili kutengeneza sanamu kwa ajili ya ibada isiyo ya kweli. Je, sasa wangeonyesha hamu hiyohiyo katika kutoa michango ya kuendeleza ibada ya kweli?

Ona kwamba Musa hakuagiza kila mtu atoe kiasi fulani hususa, wala hakuwafanya watu wajihisi wenye hatia, au wenye kuaibika ili kuwachochea wachange. Badala yake, aliwasihi tu ‘wowote walio na moyo wa kupenda.’ Ni wazi kwamba Musa hakuona haja ya kuwalazimisha watu wa Mungu. Alikuwa na uhakika kwamba kila mmoja wao angetoa kwa kadiri ya uwezo wake.—Linganisha 2 Wakorintho 8:10-12.

Hata hivyo, kazi hiyo ya ujenzi haingehitaji michango na vifaa tu. Yehova pia aliwaambia Waisraeli hivi: “Kila mtu kati yenu aliye na moyo wa hekima na aje, na kuyafanya hayo yote ambayo BWANA ameyaagiza.” Naam, kazi hiyo ya ujenzi ilihitaji wafanyakazi wenye ustadi. Kwa kweli, “kazi za werevu kila aina”—kutia ndani useremala, uhunzi, na upambaji kwa vito—zingehitajiwa ili kukamilisha kazi hiyo. Bila shaka, Yehova angeelekeza vipawa vya wafanyakazi hao, na kwa kufaa yeye angepata sifa ambayo ingetokana na kufanikiwa kwa kazi hiyo.—Kutoka 35:10, 30-35; 36:1, 2.

Waisraeli waliitikia kwa hamu mwaliko huo wa kutoa mali zao na ustadi wao. Masimulizi ya Biblia yasema: “Wakaja kila mtu ambaye moyo wake ulimhimiza, na kila mtu ambaye roho yake ilimfanya kuwa apenda, nao wakaleta sadaka [“michango,” NW] za kumpa BWANA, kwa kazi ya hema ya kukutania, na kwa utumishi wake, na kwa hayo mavazi matakatifu. Nao wakaja, waume kwa wake, wote waliokuwa na moyo wa kupenda.”—Kutoka 35:21, 22.

Somo Kwetu

Leo kazi kubwa ya kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu inatimizwa kwa upaji wa hiari. Mara nyingi, upaji huo ni wa kifedha. Katika hali nyinginezo, ndugu na dada Wakristo hutumia ustadi mwingi walio nao kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na majengo ya ofisi za tawi. Kisha kuna kazi ambayo hufanywa katika makao ya Betheli zaidi ya mia moja ulimwenguni kote, ambayo yahusisha ustadi mwingi tofauti-tofauti. Wote wenye moyo wa kupenda ambao wametoa michango hiyo wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova hatasahau kazi yao ngumu!—Waebrania 6:10.

Yehova pia hatasahau kazi ambayo kila mmoja wetu amefanya katika huduma ya Kikristo. Wote wanahimizwa wajinunulie wakati ili kushiriki kwa bidii katika kuhubiri. (Mathayo 24:14; Waefeso 5:15-17) Wengine hufanya hivyo wakiwa waeneza-evanjeli wa wakati wote, au mapainia. Kwa sababu ya hali, wengine hawawezi kutumia wakati mwingi katika huduma kama mapainia. Hata hivyo, wao pia wanampendeza Yehova. Kama ilivyokuwa na michango ya tabenakulo, Yehova haonyeshi kiasi hususa ambacho kila mmoja apaswa kutoa. Lakini, yeye hutaka kila mmoja wetu amtumikie kwa moyo wake wote, nafsi, akili, na nguvu. (Marko 12:30) Ikiwa tutafanya hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba yeye atatuthawabisha kwa sababu ya michango ya hiari tunayotoa ili kuendeleza ibada ya kweli.—Waebrania 11:6.

[Maelezo ya Chini]

a Huo haukuwa wizi. Waisraeli waliomba michango kutoka kwa Wamisri, wakapewa kwa hiari. Isitoshe, kwa kuwa Wamisri hawakuwa na haki ya kuwafanya Waisraeli watumwa, walipaswa kuwalipa watu wa Mungu mishahara kwa kazi ngumu waliyokuwa wamefanya kwa miaka mingi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki