Wakati Mioyo Yetu Inapotusukuma Tufanye Yote Tuwezayo
SIKU ni Nisani 12, mwaka wa 33 W.K.Yesu Kristo anafurahia kula chakula pamoja na watu wengine katika nyumba ya Simoni yule mwenye ukoma wa huko Bethania, karibu na Yerusalemu. Kati ya waliopo yuko mwanafunzi mwaminifu jina lake Mariamu. Yeye anabandua kizungushio kilichofunika chungu alicho nacho na kumimina mafuta ya bei kubwa yenye manukato juu ya kichwa cha Yesu.
‘Hasara hii ya nini?’ wengine wa waliopo wanateta. ‘Mafuta haya yangaliuzwa kisha fedha zenye kupatikana wapewe maskini!’ Lakini Yesu anajibu: ‘Mwacheni mwanamke huyu, kwa maana ninyi mna maskini sikuzote na mnaweza kuwafanyia mema. Lakini mimi hamtakuwa nami sikuzote. Yeye amefanya yote ambayo angeweza kufanya, kutia mafuta yenye manukato juu ya mwili wangu kwa kusudi la maziko yangu.’—Mathayo 26:6-13; Marko 14:3-9; Yohana 12:1-8.
Mariamu wa Bethania hangekuwa na la kufanya apunguze mateso ya Yesu akiisha kutundikwa mtini siku mbili tu baada ya hapo—Nisani 14, mwaka wa 33 W.K. Lakini sasa angeweza kumpaka mafuta ya bei ya juu. Kwa hiyo, kama Yesu alivyosema: “Yeye amefanya yote ambayo angeweza kufanya.” (Marko 14:8, An American Translation) Kwa kweli, moyo wa Mariamu ulimsukuma afanye yote ambayo angeweza kufanya.
Kuchochewa Tufanye Yale Tunayoweza Kufanya
Sisi tulio Mashahidi wa Yehova, au tulio watu mmoja mmoja wanaojifunza kweli ya Mungu, huenda tukawa na bidii ya kutaka kuzieneza habari njema za Ufalme katika hizi “siku za mwisho.” (Mathayo 24:14; 2 Timotheo 3:1-5) Kwa kweli, huenda tukawa tunashiriki sana katika kazi hiyo.
Lakini, madaraka ya kijamaa, matatizo ya kiafya na mambo mengine huenda yasituruhusu kutumikia tukiwa wamisionari katika nchi fulani ya mbali. Huenda tusiweze kuwa washiriki wa makao makuu ya Sosaiti au wafanya kazi wa afisi ya tawi. Huenda ikawa haiwezekani tutumikie tukiwa waangalizi wenye kusafiri, na hivyo hivyo. Hata hivyo, hatuwezi kuzuiwa kutumia mali na nguvu zetu kwa njia itakayoendeleza mbele faida za Ufalme. (Mathayo 6:33) Huenda tukawa tunaweza kweli kweli ‘kumheshimu Yehova kwa mali zetu.’ Tukifanya hivyo tutapata baraka, kwa maana ‘ghala zetu zitajazwa kwa wingi.’—Mithali 3:9, 10.
Wao Walifanya Yale Ambayo Wangeweza
Ndiyo, roho yetu inaweza kuwa kama ile ya Mariamu wa Bethania na watu wengine wenye kumcha Mungu wa nyakati zilizopita. Kwa mfano: Waisraeli wa siku za Musa walipewa pendeleo la kumheshimu Yehova wakati hema takatifu la ibada yake lilipojengwa. Si wote ambao wangeweza kufanya mambo yenye kulingana na yaliyofanywa na wenzao, lakini mioyo yao iliwasukuma wafanye yale ambayo wangeweza kufanya. Kwa mfano, wanawake fulani walisokota nywele za mbuzi zikatumiwa. Wanaume fulani walitumikia wakiwa mafundi wenye kufanya kazi za namna mbalimbali. Namna gani watu wale wengine kwa ujumla? Wao walimheshimu Yehova kwa kutoa dhahabu, fedha, shaba-nyekundu, sufu, kitani na vitu vingine ili hema takatifu liweze kumalizwa. Wenye mioyo ya kupenda walitoa haya “matoleo kwa [Yehova]” kwa furaha, nayo yalikuwa “sadaka ya kumpa [Yehova] kwa moyo wa kupenda.” (Kutoka 35:4-35) Walitoa kiasi gani? Vitu vilivyochangwa “vilikuwa vyatosha kwa kuifanya kazi hiyo yote, kisha vilizidi”! (Kutoka 36:4-7) Ndiyo, wao walifanya yale ambayo wangeweza kuyafanya.
Miaka mingi baadaye Mfalme Daudi alichangia kwa wingi sana hekalu ambalo lingejengwa na Sulemani mwanaye. Daudi hata alitoa ‘hazina yake mwenyewe’ ya pekee ya dhahabu na fedha kwa kusudi hilo. Halafu akawauliza watu wa Israeli: “Yuko wapi anayejitolea kujaza mkono wake leo kwa zawadi ya kumpa Yehova?” (NW) Kwa kuitikia, wana-wafalme na wakuu walitoa, toleo na “mawe yaliyopatikana yakiwa na watu wo wote wakatoa kwenye hazina ya nyumba ya Yehova.” (NW) Hawakufanya hivyo kwa manung’uniko, kwa maana tunaambiwa hivi: “Ndipo hao watu wakafurahi, kwa sababu wametoa kwa hiari yao wenyewe, kwa sababu kwa ukamilifu wa moyo, kwa hiari yao wenyewe, wamemtolea [Yehova]; mfalme Daudi naye akafurahi kwa furaha kuu.” (1 Mambo ya Nyakati 29:3-9) Wote walifanya lile ambalo wangeweza kufanya.
Wakiwa mmoja mmoja, Wakristo wengi wa kwanza walichangia utangazaji wa Ufalme ili usonge mbele. Kwa mfano, yule mtume mzee Yohana alionyesha wazi kwamba washiriki wa kundi la Kikristo walikuwa chini ya wajibu wa kusaidia wajumbe wenye kusafiri waliotumwa, “ili tuwe watenda kazi pamoja na kweli.” Yohana alimsifu Gayo pia kwa ukaribishaji aliowapa “wageni,” yaani, wale ambao hapo kwanza Gayo hakuwajua lakini akawatendea mambo kwa uchangamfu kwa sababu ya utumishi waliokuwa wakilitolea kundi. (3 Yohana 5-8) Mashahidi wa Yehova walio wengi katika eneo fulani hawakuweza kusafiri umbali mkubwa kwa ajili ya zile “habari njema,” lakini walifanya yale ambayo wangeweza kuyafanya.
Makundi mazima-mazima pia yalitumia mali zao kuendeleza mbele kazi ya Ufalme. Kwa mfano, mtume Paulo angeweza kuwaambia hivi waamini Wafilipi: “Hata huko Thesalonike mliniletea msaada kwa mahitaji yangu, wala si mara moja. Si kwamba nakitamani kile kipawa, bali nayatamani mazao yanayozidi kuwa mengi, katika hesabu yenu.” (Wafilipi 4:15-17) Kundi zima halingeweza kusafiri pamoja na mtume, lakini wao walifanya yale ambayo wangeweza kuyafanya.
Maoni Ambayo Wengine Wamekuwa Nayo
Yesu Kristo alisema: “Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.” Kwa hiyo si ajabu kwamba watu wa Mungu walifurahi furaha kuu walipotoa ‘sadaka ya kumpa Yehova kwa moyo wa kupenda’ siku za Mfalme Daudi. (1 Mambo ya Nyakati 29:9; Matendo 20:35, NW) Roho kama iyo hiyo ipo leo.
Shahidi mmoja wa Yehova aliiandikia Sosaiti akasema: “Umri wangu ni miaka 81 na siwezi tena kwenda sana huko nje katika utumishi [huduma ya shambani] kwa sababu ya ugonjwa wa yabisi kavu unaonilemaza, lakini ningependa kufanya kitu kidogo katika uendeshaji wa utumishi. Nitawapelekea ninyi mchango kila mwezi kwa muda ambao nitaweza kufanya hivyo na zaidi sana ningependa kuwasaidia wale wenye kuhitimu [kisomo cha Shule ya Gileadi] wanaoenda nchi za kigeni.” Mwanamke huyo mzee hangeweza yeye mwenyewe kutumikia akiwa misionari, lakini moyo wake ulimsukuma afanye lile ambalo angeweza kulifanya.
Jamaa nzima-nzima zimefanya ushirikiano zishiriki kuchanga kitu kidogo kwa ajili ya mahitaji ya uchapaji na mpango wa Sosaiti wa upanuzi. Jamaa moja iliandika hivi: “Jamaa nzima tulijisikia tukipenda kushiriki katika jambo hili. . . . tulifurahi sana wakati wana wetu wawili walio matineja wadogo walipotufikia wakasema wangetaka hata wao washiriki katika mchango wa jamaa yetu ambao tungepelekea Sosaiti. Ushiriki wao umetokana na pesa ambazo wameokoa kwa kufanya kazi za kibarua za nusu-siku. Sisi tumefurahishwa sana na vichapo vingi vya kupendeza na chakula tele cha kiroho tunacholishwa daima mezani pa Yehova.”
Namna Jambo Hili Linavyoweza Kufanyika
Ni wachache kati ya Mashahidi wa Yehova walio matajiri wa vitu vya kimwili, na wengi leo wanalazimika kupambana na matatizo ya kiuchumi. Lakini wanapotoa pesa za kiasi tu za kuendeleza mbele faida za Ufalme haiwapasi kujisikia kuwa wametoa mchango usiofaa kitu. Yesu alipoona mjane mwenye uhitaji akitumbukiza sarafu mbili ndogo ndani ya sanduku la hazina ya hekalu, yeye hakumdharau. Bali, alisema hivi: “Hakika nawaambia huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote; maana, hao wote walitia sadakani katika mali iliyowazidi, bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo.” (Luka 21:1-4) Ingawa zawadi aliyotoa ilikuwa ya bei ndogo, yeye alifanya lile ambalo angeweza kulifanya.
Ili kuwe na kitu cha kuchanga, kwa kawaida mipango fulani inapasa kufanywa, ama kwa upande wa watu mmoja mmoja na jamaa mbalimbali ama na makundi. Kwa hiyo, wakati uhitaji ulipotokea kati ya Wakristo huko Yudea, waamini wenzao Wakorintho waliotaka kuwasaidia walipokea maoni yenye mafaa kutoka kwa mtume Paulo. Yeye aliandika hivi: “Kwa habari ya ile changizo kwa ajili ya watakatifu, kama vile nilivyoamuru makanisa ya Galatia, nanyi fanyeni vivyo. Siku ya kwanza ya juma kila mtu kwenu na aweke akiba kwake, kwa kadiri ya kufanikiwa kwake; ili kwamba michango isifanyike hapo nitakapokuja.”—1 Wakorintho 16:1, 2.
Sawa na vile mtu anavyoweza kuweka kando akiba ya pesa fulani ili zitumike kukitokea jambo lisilokuwa limetazamiwa, ndivyo Mashahidi mmoja mmoja, jamaa mbalimbali au makundi yanavyoweza kwa ukawaida kuweka kando kitu fulani ili wakitoe kiwe mchango wa kuendelezea ibada ya kweli. Kwa kweli, makundi mazima yanachanga mara kwa mara pesa zinazoyazidi ili kuendeleza mbele kazi ya Ufalme. Yanafanya hivyo kwa kujitayarisha na kupitisha maazimio yanayohusu jambo hilo. Pia watu mmoja mmoja wenye moyo wa kupenda wanaona inawezekana kushiriki kuunga mkono utendaji mbalimbali wa mahubiri ya Kikristo unaofanywa sehemu zote za dunia kwa kutoa upaji wa kibinafsi kwa kusudi hilo. Upaji huo unaofaa unawaongezea furaha yao na kuwapa uradhi wa kujua kwamba wao wanafanya lile ambalo wanaweza kulifanya.
Misaada ya upaji ikiisha kuifikia Sosaiti barua inaandikwa kuonyesha kwamba imepokewa. Watu mmoja mmoja, jamaa mbalimbali au makundi yanayotaka kutoa michango hiyo yanaweza kuituma kwenye afisi ya tawi ya Sosaiti iliyo karibu nao.
Misaada yote ya upaji inayopokewa na Sosaiti inathaminiwa sana na inatumiwa kueneza habari njema za ufalme wa Mungu. Kwa mfano, kwa kutumia misaada hiyo makao ya wamisionari na utendaji wao unaendeshwa katika nchi mbalimbali. Pia, majengo yenye vifaa vya uchapaji, ambavyo ni vya lazima ili kutokeza vitabu vya kusaidia watu waifahamu Biblia, yanaendeshwa kwa njia hiyo na kupanuliwa kunapokuwa na uhitaji. Kwa sababu ya michango hiyo waangalizi wenye kusafiri, wa mizunguko na wilaya, wanawezeshwa kutembelea makundi katika sehemu zote za dunia na kuwapa waamini wenzao usaidizi wa kiroho. (Warumi 1:11, 12) Wengine walio katika huduma ya wakati wote wanasaidiwa hivyo pia.
Waendelezaji wa zamani wa ibada ya kweli walipokea baraka kutoka kwenye mbingu kwa sababu walimheshimu Yehova kwa mali zao. Nao walifurahi weee! Wakati sisi tunapoziunga mkono faida za Ufalme kwa njia iyo hiyo, hata sisi tunabarikiwa kwa wingi. Basi, acheni sisi tuitikie vizuri wakati mioyo yetu inapotusukuma tufanye yote tuwezayo.