Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 11/1 kur. 492-496
  • Ni Nani Anayestahili Kuombolezewa na Kuzikwa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nani Anayestahili Kuombolezewa na Kuzikwa?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUOMBOLEZA WAKATI WETU
  • KWA SABABU GANI MAZIKO AU SHEREHE YA KUMKUMBUKA MTU INAFANYWA?
  • JE! TUTAZIKA WATU WALIOTENGWA NA USHIRIKA?
  • Maoni ya Mkristo Kuhusu Desturi za Mazishi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Je! Wewe Unawaheshimu Wafu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Mazishi ya Kikristo Ni Yenye Heshima, Kiasi, na Yanampendeza Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 11/1 kur. 492-496

Ni Nani Anayestahili Kuombolezewa na Kuzikwa?

IMESEMEKANA kwa njia ya kweli kwamba: “Hakuna kundi la wanadamu . . . linalotupa wafu wao nje tu bila kufanya ibada au sherehe yo yote. Tofauti kabisa na hilo, hakuna mnyama anayezika wanyama wa jamii yake mwenyewe.” “Mwanadamu ndiye kiumbe cha pekee ambacho kimekuwa kikijisikitikia na kusikitishwa na kifo.”a​—Angalia Mwanzo 23:3, 4.

Maneno ya mwanasayansi Mrusi wa siku hizi, Theodosius Dobzhansky, yanaonyesha kwa nini Mfalme Sulemani alitoa shauri lifuatalo karibu miaka elfu tatu iliyopita: “Heri kuiendea nyumba ya matanga, kuliko kuiendea nyumba ya karamu.” Naam, kwa sababu sisi wanadamu tuna hali ya kujisikitikia na kusikitishwa na kifo, kwa kawaida tunapanga mazishi kwa ajili ya rafiki yetu aliyekufa, mwamini mwenzetu au mtu wa ukoo wetu.​—Mhu. 7:2.

Je! ni sawa Wakristo kwenda nyumba yo yote yenye maombolezo na kusikitika pamoja na waliobaki kwa sababu Sulemani anasema ni vizuri zaidi kwenda nyumba yenye maombolezo? Je! ni sawa kuomboleza kifo cha watu wa namna zote? Neno la Mungu, Biblia, linaonyesha nini?

Biblia inatupa mifano mingi ya kuombolezea wafu. Yakobo na Esau waliomboleza kwa njia ya pekee wakati baba yao Isaka alipokufa. Yakobo aliomboleza kwa sababu alidhani mwana wake aliyempenda zaidi ya wengine aliuawa na mnyama-mwitu. Wakati Yakobo mwenyewe, mzee wa ukoo alipokufa, aliombolezewa na Wamisri pia, si nyumba yake peke yake. Waisraeli waliomboleza sana Musa kiongozi wao alipokufa. Ingawa Mfalme Yosia aliuawa katika pigano aliloingia kwa upumbavu, Yeremia na Yuda yote iliomboleza sana mtawala huyo mwema alipokufa. Vipindi vya baadaye watu waliomboleza wakati Lazaro, Yesu Kristo, Stefano na wengine walipokufa.​—Mwa. 27:41; 37:34, 35; 50:1-14; Kum. 34:8; 2 Nya. 35:24, 25; Luka 24:15-24; Yohana 11:17-44; Matendo 8:2; 9:36-42.

Lakini, liko jambo moja tunalopaswa kuangalia juu ya mifano hiyo ya kuomboleza iliyoandikwa katika Maandiko. Watu wote walioombolezewa walikuwa watu wenye kumwogopa Yehova Mungu, tena walikuwa watu wa ukoo wa waliobaki au walikuwa watu wenye kuheshimiwa. Lakini wako wengine ambao hawakuombolezewa walipokufa. Kwa mfano, hakuna jambo lo lote linaloonyesha kwamba Nuhu na jamaa yake waliomboleza wakati kizazi kiovu na chenye jeuri kilipoangamizwa na Gharika. Hakuna jambo lo lote linaloonyesha kwamba Lutu aliomboleza wakati watu waovu sana wa Sodoma na Gomora walipoharibiwa. Wakati Farao na jeshi lake walipozama katika Bahari ya Shamu, badala ya Musa na watu wake kuomboleza, walishangilia kwa kuimba wimbo wa ushindi.​—Kut. 15:1-21; angalia pia Yeremia 22:18, 19.

Kwa sababu gani nyakati zote hizo watumishi wa Mungu hawakupaswa kuombolezea walioangamia? Kwa sababu waliuawa na Yehova Mungu. Kuwaombolezea kungekuwa sawa na kulaumu hukumu za Yehova zenye haki. Kwa hiyo Yeremia aliagizwa asiomboleze msiba ambao ungepata watu wake Waisraeli, wenye kuasi imani. Tena katika kitabu cha Ufunuo tunasoma kwamba ingawa Babeli Mkuu aliombolezewa na baadhi ya hawara zake za kisiasa na kibiashara, makundi ya mbinguni yalishangilia uharibifu wake.​—Yer. 15:4-7; Ufu. 18:9-20.

Kwa hiyo, wakati Mfalme Daudi alipoomboleza sana kifo cha mwanawe Absalomu mwenye kujitakia makuu, mwenye hila na mwasherati, ilifaa sana Yoabu jemadari wake akamkaripia. (2 Sam. 19:1-8) Lakini, kwa upande mwingine, wakati Daudi alipomwombolezea Mfalme Sauli asiye mwaminifu, hakukaripiwa. (2 Sam. 1:17-27) Kwa sababu gani? Kwa sababu Mfalme Sauli alikuwa mtiwa mafuta wa Yehova. Kwa hiyo Daudi alikuwa akimwombolezea kwa sababu ya kuonyesha uaminifu mwingi juu ya cheo cha utiwa mafuta kilichokaliwa na Sauli. (Angalia The Watchtower, Oktoba 1, 1938, uku. 297.) Zaidi ya hilo, Daudi hakutaka kufanya watu wadhani labda alifurahia kifo cha adui yake.​—Mit. 24:17.

Mambo yote hayo yaliandikwa kutufundisha na kutufariji wakati huu wa mwisho wa taratibu mbovu ya mambo. (Rum. 15:4; 1 Kor. 10:11) Karibuni kizazi hiki kitaiona “dhiki kubwa” iliyotabiriwa, itakayokomesha taratibu mbovu hii. (Mt. 24:21) Wakati huo hakuna mmoja wa watumishi waaminifu wa Yehova, ambao ndio watakaookoka peke yao, atakayeomboleza kuharibiwa kwa waovu. Bali, watashangilia, kama vile Musa na watu wake walivyoushangilia uharibifu wa Farao na jeshi lake.

KUOMBOLEZA WAKATI WETU

Lakini namna gani wakati wa sasa? Inatupasa tuwe na maoni gani tunapopata habari za misiba, vifo vya watu wengi vyenye kuletwa na mikasa mibaya, matetemeko ya ardhi, tufani na dhoruba zinazoletwa na maji? Bila shaka inatupasa kuhurumia wenye kupatwa na mambo hayo, hasa waokokaji wenye kuombolezea watu wao, hata ikiwa wamekuwa hawapendi haki. Ingawaje, hawakuuawa na Yehova Mungu kwa sababu ya kuwa waovu. Kwa hiyo wakati watu wa ukoo, watu tunaowafahamu au tunaofanya kazi nao wanapokufa, ni kawaida ya Wakristo kuonyesha fadhili kwa kuwapa pole washiriki wa jamaa iliyofiwa.

Wakati Mkristo mtiwa mafuta aliye mwaminifu anapokufa, tunamwombolezea ingawa tunaamini kabisa kwamba amepokea thawabu yake ya mbinguni. Tunafanya hivyo kwa sababu hatakuwa pamoja nasi tena; lakini hatusikitiki kupita kiasi kama watu wasio na tumaini. (1 The. 4:13-15) Tunaomboleza pia kifo cha walio na tumaini la kuishi duniani ingawa tunatazamia kwamba watafufuliwa mapema. Kama vile Yesu alivyoeleza wazi, “watu wote waliomo makaburini” watafufuliwa.​—Yohana 5:28, 29; angalia pia Matendo 24:15; Ufunuo 20:13.

KWA SABABU GANI MAZIKO AU SHEREHE YA KUMKUMBUKA MTU INAFANYWA?

Wengine wamedhani kwamba maziko yanafanywa ili kumtukuza mtu aliyekufa, ili kumsifu sana na kumpa kinachoitwa “kifo kizuri.” Lakini hayo ni maoni mazuri? Kumbuka kwamba Yehova Mungu aliliruhusu taifa la Israeli liwalilie Nadabu na Abihu na wana wawili wa Haruni, walipoangamia kwa sababu ya kutoa moto usiofaa​—ingawa jamaa zao wenyewe zilikatazwa kuwaombolezea.​—Law. 10:1-7.

Wala haiwezi kusemwa kwamba sherehe ya maziko inafanana kidogo na sakramenti ya kumpa wema mtu aliyekufa. Ni kweli kwamba wanakanisa wengi wa Jumuiya ya Wakristo wangestaajabu sana kuona maziko yasiyo na sherehe ya kanisa. Ndiyo sababu Kanisa Katoliki lina Misa za namna mbalimbali kwa kusudi hilo. Huenda wakampa baraka nyingi mtu aliyekufa na kudai kwamba zinasaidia nafsi katika purgatori. Lakini, mazoea yote hayo hayaungwi mkono na Maandiko, maana Neno la Mungu linaeleza wazi kwamba wafu hawajisikii hata kidogo, na wanaendelea kuwa katika hali hiyo mpaka watakapofufuliwa.​—Mhu. 9:5, 10.

Basi kwa sababu gani mtu aliyekufa afanyiwe maziko au sherehe ya kumkumbuka? Ziko sababu nyingi nzuri. Kwanza, sababu moja ni kuwafariji waliofiwa. Wakristo wanaamriwa wafariji wote wanaoomboleza, kutia na Wakristo wenzao. (Isa. 61:1, 2; 2 Kor. 1:3-5) Kawaida ya kifo ni kuleta maombolezo. Hasa, tunafarijika tunaposikia mazungumzo juu ya sifa nzuri sana za Yehova, hasa upendo mkuu alioonyesha kwa kumtoa Mwanawe kama ukombozi ili wanadamu waweze kuwa na tumaini la kuishi milele. Zaidi ya maneno ya kufariji waliofiwa yanayosemwa na wahudhuriaji, kuhudhuria kwao tu kunawafariji.

Sababu nyingine pia ni kutolea kweli za Biblia ushuhuda. Kwa kawaida maziko yanahudhuriwa na jirani, watu tunaofahamiana, watu tunaofanya kazi nao na watu wa ukoo wetu, ambao huenda wakawa si waamini. Wote hao wanaweza kufaidika kutokana na sherehe ya maziko au ya ukumbusho yenye hotuba inayohusu maoni ya Biblia juu ya hali ya wafu, sababu watu wanakufa na tumaini la ufufuo. Kwa sababu makusudi hayo mema yanatimizwa, mhudumu Mkristo anaweza kuona inafaa kuongoza maziko ya mtu asiyeamini wa ukoo wa Shahidi​—au hata ya mtu aliyejiua kwa kwa sababu ya kuhuzunika sana au kuwa na akili mbaya. Nao Wakristo wale wengine wanaweza kumfariji Shahidi aliyefiwa kwa kuhudhuria maziko.

Tunaelezwa na Sulemani kusudi jingine jema linaloweza kutimizwa na sherehe ya maziko. Kumbuka kwamba alisema: “Heri kuiendea nyumba ya matanga, kuliko kuiendea nyumba ya karamu. Kwa maana huo ndio mwisho wa wanadamu wote, naye aliye hai atautia moyoni mwake.” (Mhu. 7:2) Kifo kinapotokea kinatupa nafasi ya kukumbuka kwamba maisha ni mafupi. Kinapaswa pia kitusaidie kuthamini sana uhai. Mtu afapo hajisikii hata kidogo, hawezi kuongea, hana furaha, hatimizi lo lote.

Kati ya mataifa fulani ya kale maziko yalikuwa na masikitiko ya kupita kiasi, yakawa ishara ya kushindwa. Ndiyo sababu yalifanywa usiku. Ingawa ni kweli kwamba Wakristo hawahuzuniki kama wengine wasio na tumaini, inaonekana kwamba hatupaswi kuwa na vicheko vyenye makelele mengi wala utani tunapokuwa katika nyumba ya waliofiwa au kwenye maziko, kama kwamba tuko kwenye mandari (pikniki) au karamu. Kuna wakati wa kila jambo, nao wakati wa kifo sio wakati wa kicheko kikubwa.​—Mhu. 3:1, 4.

Tena, wakati sherehe inapofanywa kwa ajili ya mtumishi mwaminifu aliyekufa wa Yehova Mungu, wakati huo unaweza kutumiwa kutaja kwamba mtu huyo aliendeleza ukamilifu ajapokuwa alipatwa na vipingamizi vya namna nyingi. (2 Sam. 1:26) Ni kama vile Mark Anthony alivyosema katika hotuba yake ya maziko: “Naja kumzika Kaisari, si kumsifu.” Kwa hiyo kusudi letu si kutukuza viumbe, bali kuona kwamba tunastahili kufuata mfano wao. Ni kama vile mtume Paulo alivyosema: “Msiwe wavivu, bali mkawe wafuasi wa hao wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu.”​—Ebr. 6:12.

JE! TUTAZIKA WATU WALIOTENGWA NA USHIRIKA?

Lakini, tuseme kwamba mtu aliyekufa alitengwa na ushirika, akaondolewa katika kundi la Kikristo kwa sababu fulani. Katika “Maswali kutoka kwa Wasomaji” (The Watchtower, 1961, uku. 544) maoni yalitolewa kwamba haifai kuzika mtu aliyetengwa na ushirika. Maelezo yafuatayo yalitolewa: “Hatutaki kamwe kuwapa watu wa nje maoni ya kwamba mtu aliyetengwa na ushirika alikuwa akikubalika kundini na hali kwa kweli yeye hakuwa akikubalika bali alikuwa ametengwa atoke ndani yake.” Je! hakuna nyakati mtu aliyetengwa na ushirika anapoweza kuzikwa?

Kabla ya kujibu ulizo hilo ingefaa turudie kifupi shauri hilo la kutenga watu na ushirika. Tunaweza kuona kwamba linaungwa mkono na Maandiko katika Wakorintho wa Kwanza sura ya tano, ambamo mtume Paulo anaagiza mwasherati atengwe na ushirika. Lakini, mwaka 1952 ndipo watu wa Yehova wa kisasa walipoanza kuchukua hatua hiyo. Kwa sababu ya kutafuta sana haki na kuchukia yaliyo maovu, waliwekea wenye kuongoza makundi maongozi ya kufuata ili kuyaweka makundi katika hali safi ya kiroho, ya mafundisho na ya adili.

Miaka iliyofuata watu wa Yehova wamelifahamu vizuri zaidi shauri hili la kutenga watu na ushirika. Zaidi ya maelezo mengi zaidi kutolewa, ilizidi kuonekana kwamba hekima na upendo, vilevile haki ya hukumu, zimekuwa zikitumiwa. Wameona uhitaji wa kurehemu wakosaji wenye kutubu kikweli, uhitaji wa kufikiria hali ambazo labda zilikaza sana mtu na uhitaji wa kufikiria kama kuna dalili za kuonyesha mtu anasikitika kikweli. Miaka ya majuzi sana tulionyeshwa kwamba kuna tofauti kati ya jinsi Wakristo wanavyopaswa kutendea mtenda dhambi mbaya sana au mwasi imani mwenye jeuri na jinsi wanavyopaswa kutendea mtu anayeonekana kuwa “mtu wa mataifa”​—ambaye anaweza kupewa salamu ya kiasi.​—Mt. 18:17; 2 Yohana 9, 10.

Inaonekana kwamba tofauti hiyo inaweza kutumiwa hata kuhusu maziko ya mtu aliyetengwa na ushirika. Kundi la Kikristo lisingetaka jina lake zuri liharibiwe kwa kuhusianishwa na mtu ye yote anayetenda kupatana na maelezo ya 2 Yohana 9, 10, hata akifa. Lakini namna gani ikiwa mtu aliyetengwa na ushirika alikuwa akionyesha dalili chache za kutubu kikweli na alikuwa akija mikutanoni na kuonyesha alitaka kurudishwa kundini. Wazee wakiona kwamba amani na mapatano ya kundi yasingeharibiwa wala watu wa Mungu wasingelaumiwa, mzee mmoja anaweza kutoa hotuba. Labda Yehova amekwisha msamehe mtu huyo, kwa sababu kuna dalili fulani za kutubu. Wazee watakuwa wamefanya vizuri kungoja wakitaka kuhakikisha kwamba ametubu kikweli. Ni wazi kwamba kila kisa kinapaswa kuamuliwa kulingana na hali zake chenyewe. Bila shaka, hotuba ya maziko ikitolewa, mwenye kutoa atajiangalia asitaje sana mambo yanayohusu mtu huyo, wala asitaje kwa uhakika kwamba atafufuliwa. Lakini bila shaka hotuba nzuri ya Maandiko na ushuhuda unaweza kutolewa.

Tena, tusisahau sababu zile mbili kubwa za kutenga mkosaji na ushirika. Sababu moja ni kumwamsha aone mambo vizuri ikiwezekana. Ile nyingine ni kulinda kundi na maongozi yake mabaya. Mtu aliyetengwa na ushirika akifa, sababu hizo hazitumiki tena, maana amekufa. Hata ikiwa mtu aliyetengwa na ushirika ameendelea kuwa “mtu wa mataifa” tu, hotuba ya maziko yenye Maandiko inaweza kutimiza makusudi mengi mema, kama ilivyotajwa: Inaweza kufariji waliofiwa na kuwapa watu wa nje ushuhuda. Ushuhuda mzuri ukitolewa unaweza kufariji waliofiwa bila kujali hali za aliyekufa ziko namna gani.

Kati ya viumbe vyote vya dunia, sisi peke yetu ndio tulioumbwa kwa mfano wa Mungu. Ndiyo sababu tuna akili ya kujua habari zote za kifo. Ndiyo sababu pia tuna akili ya kuomboleza kifo cha mwenzetu na kutaka kufariji waliofiwa. Je! Baba yetu wa mbinguni si “Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote”? Hakika! Kwa hiyo tunaacha kanuni zake za hekima, haki ya hukumu na upendo ziongoze mawazo yetu ya ndani na matendo yetu kuhusu maombolezo na maziko, hata katika mambo mengine yote ya maisha.​—2 Kor. 1:3, 4; 1 Kor. 16:14.

[Maelezo ya Chini]

a The Uniqueness of Man, kilichotungwa na J. D. Roslansky.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki