Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Kwa nini New World Translation yafasiri neno la Kiebrania ‘a·rumʹ kwenye Mwanzo 3:1 kuwa “mwenye hadhari” kwa kuwa tafsiri nyingine za Biblia husema “mjanja” au “mwerevu”?
Andiko hilo lasomeka hivi: “Sasa nyoka alithibitika kuwa aliye na hadhari zaidi kati ya hayawani-mwitu wote wa uwanja ambao Yehova Mungu alikuwa amefanya. Hivyo basi akaanza kusema hivi kwa mwanamke: ‘Je! kweli ni hivyo kwamba Mungu alisema ni lazima nyinyi msile kutokana na kila mti wa bustani?’”
Kwenye Mithali 12:23 na mahali penginepo, New World Translation hufasiri neno la Kiebrania ‘a·rumʹ kuwa “mwenye utimamu,” ambayo ndiyo maana moja ya msingi ya neno hilo litumiwapo kwa wanadamu. Lakini kama ilivyo kuhusu maneno mengi sana, ‘a·rumʹ lina maana ya namna mbalimbali. Mathalani, Benjamin Davidson afasili ‘a·rumʹ kama ifuatavyo: “I. mwenye mbinu za kiufundi, mjanja, mwenye hila.—II. mmahiri, mwenye hadhari.”—The Analytical Hebrew and Chaldee Lexicon.
Basi, kwa nini New World Translation huchagua ile maana ya pili ya “mwenye hadhari” kwenye Mwanzo 3:1? Chaguo hilo lapatana na tafsiri nyinginezo. Mathalani, Mwanzo 3:1 ilipotafsiriwa kuingizwa katika Kigiriki katika fasiri ya Septuagint ya karne ya tatu K.W.K., neno phroʹni·mos lilitumiwa—neno lile lile lililotumiwa baadaye kwenye Mathayo 10:16: “Ni lazima nyinyi mwe wenye hadhari kama nyoka na wanana kama njiwa.”—Today’s English Version.
Mwanachuo Mwebrania Ludwig Koehler alieleza hivi huko nyuma katika 1945: “Nyoka ni mwenye haya. Hilo laweza kuelezwa vema sana kwa Kigiriki kwa neno phronimos, kwa maana kwa haya au hadhari hii nyoka hudhihirisha ana phrenes na kwamba aizoea.” Hapa phreʹnes yamaanisha aina fulani ya hekima ya kisilika ambayo wanyama wengine pia hudhihirisha.—Linganisha Mithali 30:24.
Hata hivyo, kuna sababu ya maana zaidi kwa utumizi wa neno “mwenye hadhari” badala ya “mwenye utimamu” au “mwerevu” kwenye Mwanzo 3:1. Kumwita nyoka mwerevu hapa, kabla tu hajasimuliwa kuwa akimtongoza Hawa katika dhambi, kungeweza kuongoza wasomaji wengi wakate shauri kwamba Biblia huonyesha nyoka wa kikawaida tu kuwa akipanga njama hii kwa kutumia werevu wake mwenyewe usio wa kikawaida. Fasiri ya jinsi hiyo ingefanya ule usimulizi uwe hadithi ya ubuni tu—tena hadithi ya ujinga kidogo.
Kinyume cha hivyo, Biblia hufundisha kwamba kuna mengi yaliyohusika kuliko nyoka fulani mwerevu kufanya kazi huko katika bustani ya Edeni. Ufunuo 12:9 wamtambulisha Shetani Ibilisi waziwazi na huyo “nyoka wa zamani.” Alikuwa ndiye nguvu isiyoonekana, yenye nguvu zipitazo za kibinadamu iliyokuwa ikimtumia yule mtambaazi sahili kama vile stadi aliye mnenaji-mfumba-midomo hutamka maneno kwa kutumia chombo chake kisicho na sauti. Hadhari ya kiasili ya nyoka ilimfanya awe chaguo zuri kabisa kwa hila hiyo. Ilipokuwa kwamba nyoka hakwenda zake kwa hadhari akiwa mwenye haya kama ilivyokuwa asili yake bali akafungua kinywa chake kwa ujasiri na kuanza kusema kwa Hawa, aliunasa uangalifu wa Hawa kwa matokeo makubwa hata zaidi.
Neno la Mungu lililovuviwa halina hadithi za ubuni, na kwa fasiri sahihi, New World Translation hutusaidia tuthamini uhakika huu.—2 Timotheo 3:16.
◼ Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova wajua kwamba wafu hawana fahamu, kwa nini wao bado huhisi ni jambo la maana kuhudhuria maziko ya waamini wenzao?
Maarifa sahihi kutokana na Biblia juu ya hali ya wafu huwalinda Mashahidi wa Yehova kwenye maziko wasiwe na mitazamo yenye makosa na mwenendo usio wa hekima utokanao na mitazamo hiyo. Pia huwapa sababu ya kuhudhuria maziko ya Kikristo.
Neno la Mungu laonyesha kwamba mtu afapo, haendelei kuishi akiwa nafsi isiyokufa. (Mhubiri 9:5) Baada ya kifo, mwili hurudi kwenye mavumbi, kwa kuoza kiasili ama kupitia kuteketeza maiti. Mfu huwa hayuko hai tena; ataishi tena Mungu akimfufua wakati ujao.—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.
Kwa sababu hiyo, Mashahidi wa Yehova hawafuati mazoea ya maziko yaliyo na msingi wa imani ya kwamba mtu aliyekufa alikuwa na nafsi isiyokufa, ambayo huendelea kuishi mahali fulani. Wao hawashiriki katika makesha, kwa nyimbo za makelele wala mayowe ya kuogopesha “mizimu,” wala katika makesha ya usiku kucha wala kuwa na kihoro cha kupita kiasi kwa kusudi la kuwatuliza wafu.
Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba watu wa Mungu hawaombolezi. Kifo cha mtu wa ukoo au rafiki wa karibu ni tukio lenye kuhuzunisha, hata kwa waabudu wa kweli walio na maarifa sahihi juu ya wafu. Kwa kielelezo, Yakobo alipofikiri kwamba mnyama mwitu alikuwa amemwua Yusufu, huyo mzee wa ukoo “aliendeleza maombolezo juu ya mwana wake kwa siku nyingi.” Twasoma kwamba “wana wake wote na binti zake waliendelea kuinuka wamfariji.” (Mwanzo 37:33-35, NW) Yakobo mwaminifu alipokufa, Yusufu “akawaagiza watumishi wake, waganga, kwamba wampake babaye dawa asioze,” nao “Wamisri wakamlilia siku sabini.” Ingawa familia ya Yakobo haikushikilia maoni bandia ya Wamisri juu ya wafu, kwa wazi waliguswa moyo na kifo cha Yakobo. “Nyumba yote ya Yusufu, na nduguze” walimtaka Yakobo azikwe ifaavyo, na hata watu wa nje waliweza kuona kwamba walikuwa wakiomboleza.—Mwanzo 50:1-11.
Vielelezo vingine vingi sana vya Biblia vyaweza kutajwa ambamo watumishi wa Yehova waliguswa moyo kikweli na kifo cha mwabudu mwenzao au mtu wa ukoo na hivyo basi wakafungulia hisia za maombolezo yafaayo.a Yesu alipokuwa pamoja na wanaukoo wa Lazaro wenye kihoro, Yesu hakuwa bila hisia za kuguswa moyo wala hakuwa mfurahifu isivyofaa. Ingawa alikuwa na uhakika katika uwezo wa ufufuo, Yesu alilia machozi. (Yohana 11:33-35) Baada ya Yesu mwenyewe kufa, wanafunzi wake waliomboleza, hata ingawa alikuwa amewaambia kwamba angeuawa na kuinuliwa tena kwenye uhai.—Mathayo 16:20; Yohana 16:17-20; 20:11.
Watumishi wa Mungu leo waweza kuhisi nao huhisi huzuni ambayo kifo kimeleta. Na bado, uelewevu wao wa Kibiblia husaidia kudhibiti au kusawazisha maombolezo yao, kupatana na 1 Wathesalonike 4:13, 14: “Ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini. Maana, ikiwa twaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye.”
Basi, namna gani kuhudhuria maziko ya Kikristo (au hotuba ya ukumbusho kuhusu mwamini)? Kuna sababu za Kibiblia kwa nini Mashahidi huhisi kuna manufaa kuwa nayo na kuihudhuria.
Kumbuka kwamba wakati ilipoonekana kana kwamba Yakobo alikuwa amefiwa na mwana wake, “wana wake wote na binti zake waliendelea kuinuka wamfariji.” (Mwanzo 37:35, NW) Katika mabara mengi ni desturi watu wa ukoo kukusanyika kwa ajili ya maziko. Hiyo huwaandalia wengine, ambao huenda ikawa hawakuwa na ukaribu wa kadiri ile na hivyo hawakuathirika kihisia-moyo kadiri ile, fursa ya kutoa maneno ya usikitikio na uliwazo. Baada ya Lazaro kufa ‘watu wengi katika Wayahudi walikuja kwa Martha na Mariamu, ili kuwafariji kwa habari ya ndugu yao.’ (Yohana 11:19) Hiyo pia huhusisha Wakristo watakao “kuwafariji wale walio katika dhiki za namna zote.”—2 Wakorintho 1:4.
Waangalizi Wakristo, hata ingawa huenda wakawa wana shughuli sana, wapaswa kuongoza katika kuandaa faraja kwa kundi la kondoo. Wao wakumbuka kwamba kielelezo wao Yesu, yule Mchungaji Mwema, alipewa utume ‘kuwaganga waliovunjika moyo na kuwafariji wote waliao.’ (Isaya 61:1, 2; Yohana 10:14) Yesu hakutoa faraja hiyo wakati tu alipokuwa na fursa nzuri. Alikuwa na nia ya kujiondokea akawe pamoja na wanaukoo waliofiwa wa Lazaro—kushiriki majonzi yao.—Yohana 11:11, 17, 33.
Hata Wakristo ambao huenda wasiweze kusema mengi kwa waliofiwa kwenye maziko waweza kuwa wenye manufa kwa kuwapo kwao tu. Washiriki wa familia yenye kuomboleza waweza kuchota utulizo mwingi kutokana na kuwapo kwa wengi wenye usikitikio—wenye umri mdogo na mkubwa—kutoka kwenye kundi la Kikristo. Kumbuka itikio la Wayahudi fulani wakati Yesu alipowajia dada za Lazaro wenye kihoro: “Angalieni jinsi alivyompenda.” (Yohana 11:36) Watu wa ukoo wasioamini, majirani, au washirika wa kibiashara wenye kuhudhuria maziko ya Mkristo wamevutiwa ifaavyo na hesabu kubwa ya Mashahidi waliopo na hivyo wakawa waitikivu zaidi kwa kweli za Kibiblia zitolewazo.
Mwenendo wa Mashahidi wenye kuhudhuria wapasa ufaane na ile hali. Ingawa wanajua kwamba mfu hateseki, na wana uhakika kwamba ufufuo wawangoja waaminifu-washikamanifu wote, wao wazingatia moyoni lile shauri: ‘Kuna wakati wa kulia, na wakati wa kucheka, wakati wa kuomboleza, na wakati wa kucheza.’ (Mhubiri 3:4) Maziko au pindi ya ukumbusho si wakati wa maneno ya kimchezo yenye sauti kubwa. Ni pindi ya kuwa na hisia-mwenzi, kupatana na ushauri huu: “Furahini pamoja nao wafurahio; lieni pamoja nao waliao.”—Warumi 12:15.
Kuna sababu nyingi kwa nini Mashahidi wa Yehova huhudhuria maziko. Neno la Mungu lasema hivi: “Heri kuiendea nyumba ya matanga, kuliko kuiendea nyumba ya karamu. Kwa maana huo ndio mwisho wa wanadamu wote, naye aliye hai atautia moyoni mwake. . . . Moyo wake mwenye hekima umo nyumbani mwa matanga, bali moyo wake mpumbavu umo nyumbani mwa furaha.”—Mhubiri 7:2-4.
Ingawa Mashahidi wa Yehova wana sababu ya kuwa na tumaini, maneno hayo yalivuviwa na kutiwa katika Biblia kwa manufaa yetu. Maziko yangeweza kulinganishwa na “nyumba ya matanga.” Tuhudhuriapo, mawazo yetu yaweza kugeuzwa kutoka kwenye mahangaiko yetu au utendaji wa kawaida na kukazwa juu ya ufupi wa maisha. Iwe ni kupitia ugonjwa au ‘tukio fulani lisilotazamiwa,’ kifo chaweza kupiga yeyote wetu na kututangua upesi, kwa maana “binadamu pia hajui wakati wake.” (Mhubiri 9:11, 12, NW) Wazazi wenye kuwa pamoja na watoto kwenye maziko ya Kikristo huenda wakaona kwamba hiyo yaweza kuongoza kwenye mazungumzo juu ya uhalisi wa kifo, uhitaji wetu wa ukombozi, na hekima ya kumtumikia “Mungu, awafufuaye wafu.”—2 Wakorintho 1:9, UV; Mhubiri 12:1, 13, NW.
Mashahidi wa Yehova hawayaoni maziko kuwa sakramenti (matendo matakatifu), bali wao hutambua kwamba matukio haya yenye kuhuzunisha hutoa pindi ya kutoa uliwazo. Kwa kuyahudhuria, Wakristo waweza kutoa uthibitisho wa upendo na staha waliyokuwa nayo kwa Mkristo mwenzao. Nao waweza kusukumwa na moyo wafikirie kwa uzito zaidi maana ya uhai, jinsi wapaswavyo kuwa wakitumia uhai wao wenyewe mbele za Mungu.
[Maelezo ya Chini]
a Mwanzo 23:2, 19; Hesabu 20:29; Kumbukumbu 34:7, 8; 2 Samweli 1:11, 12; 3:31-34; 13:32-37; 18:33; 2 Nyakati 35:24, 25; Ayubu 1:18-20; Zaburi 35:14; Yeremia 9:1; Luka 7:12, 13; 8:49-52; Matendo 8:2; 9:39