Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 9/1 kur. 3-4
  • Kutotii Maonyo ya Mungu Kunaleta Msiba

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutotii Maonyo ya Mungu Kunaleta Msiba
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Habari Zinazolingana
  • Yeriko
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Kitabu Cha Biblia Namba 6—Yoshua
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yoshua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Yoshua na Akusaidie Wewe Umtumikie Yehova kwa Uhodari!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 9/1 kur. 3-4

Kutotii Maonyo ya Mungu Kunaleta Msiba

MUNGU anapotoa onyo, yeye hafanyi hivyo bila sababu nzuri, wala hafanyi hivyo ili aonyeshe tu mamlaka yake. Sikuzote anafanya hivyo kwa faida ya wale wanaolisikia. Litawasaidia wasifanye makosa ambayo yanaweza kuwaletea taabu kubwa sana. Kabla taifa la Israeli halijaingia katika Nchi ya Ahadi, Mungu aliwaonya juu ya kutojali sheria yake, akaongeza hivi: “Kwa maana si jambo lisilofaa kwenu; maana, ni maisha yenu.”​—Kum. 32:46, 47.

Zaidi ya hayo, kwa kusikiliza maonyo ya Yehova tunajifunza vile yeye anavyoona juu ya mambo fulani, kwa hiyo tunajua njia zake. Na hilo ndilo jambo la maana zaidi​—⁠kumjua Yehova sana sana, kwa njia hiyo tunakuwa na uhusiano (urafiki) wa karibu sana naye. Yeye anatuambia tusijisifie mali, hekima au nguvu ambazo huenda tukawa nazo, “bali ajisifuye na ajisifu kwa sababu hii, ya kwamba ananifahamu mimi, na kunijua, ya kuwa mimi ni [Yehova], nitendaye wema, na hukumu, na haki, katika nchi; maana mimi napendezwa na mambo hayo.”​—Yer. 9:23, 24; Yohana 17:3.

Maonyo aliyotoa Mungu mara nyingi yalikuwa katika njia ya unabii, au zilikuwa amri zilizokuwa na maana ya unabii. Mfano wa hili ni jambo lile lililosemwa juu ya Yeriko na Yoshua aliyekuwa mkuu wa jeshi la Israeli aliyechukua mahali pa Yoshua alikuwa na amri kutoka Mungu awamalize Wakanaani wakaaji wa Nchi ya Ahadi, kwa sababu walizoea ibada ya viungo vya uzazi, ibada ya sanamu, pamoja na ibada ya mashetani, na walikuwa wakichafua nchi kwa ufisadi, magonjwa na umwagaji wa damu. (Kum. 20:15-18; Law. 18:24-30) Yeriko ndio uliokuwa mji wa kwanza kutekwa na jeshi la Israeli katika nchi hiyo. Kwa sababu hiyo, ulikuwa “malimbuko” ya nchi hiyo. Kama vile malimbuko ya vitu vyote vya Waisraeli​—nafaka, ng’ombe, na mengineo yalivyoonwa kuwa matakatifu, “wakfu,” ndivyo ungekuwa Yeriko. (Law. 23:10-14; Yos. 6:17) Na kama vile mazao ya kwanza yalivyokuwa “wakfu,” yatolewe kwa Yehova kabla ya mkulima kula mavuno yo yote, ndivyo Yeriko ungekuwa “wakfu” kabisa, bila cho chote kutolewa katika mji huo kwa matumizi ya mtu binafsi. Kwa hiyo Yoshua aliangamiza mji huo kabisa akauteketeza kwa moto, madini yake akayatoa kwa hekalu (hema) la Yehova.

Takwa hili la Yehova lilikuwa kama sheria ambayo baadaye ilitumika juu ya mji wo wote wa Israeli ambao ungefuata ibada ya sanamu. Mji kama huo ‘uliharimishwa,’ au kupigwa marufuku. Wakaaji wake waliuawa na mji wenyewe uliteketezwa kwa moto, usijengwe tena kamwe. Hakuna kitu cho chote kingechukuliwa kutoka mji huo kwa matumizi ya kibinafsi. Ungeonwa na Waisraeli wote kama chukizo. Hata hawangewaza juu ya kutumia vitu kama hivyo.​—Kum. 13:12-17.

Kwa sababu hiyo, Yoshua alipouangamiza mji wa Yeriko, aliapa, akasema: “Laana ya BWANA na ikae juu ya mtu anayejitokeza aujenge tena mji huu wa Yeriko: atafiwa na mwanawe mkubwa kwa kuweka misingi yake, atafiwa na mwanawe aliye mdogo zaidi kwa kuweka malango yake.”​—Yos. 6:26, New English Bible.

Yoshua alimaanisha nini? Bila shaka maneno yake hayakuwa na maana ya kwamba mahali ulipokuwa Yeriko, “mji wa mitende,” hapangekaliwa tena, kwa sababu Yoshua mwenyewe aligawia Wabenjamini ganjo la mji wa Yeriko, na panatajwa baadaye kama pahali panapokaliwa na watu. (Amu. 3:13; 2 Sam. 10:5) Mkazo unatiliwa juu ya “mji” wenye kuta. Maneno ya Yoshua yanaonyesha kwamba alikuwa akitaja juu ya kuujenga tena mji huo. Hii ilitia ndani kujenga ukuta. Kujenga misingi kungekuwa kujenga misingi ya mji wenye kuta. Kujenga malango yake hakungekuwa kuweka milango katika nyumba, bali kungekuwa kuweka malango ya mji, ambayo hayangewekwa bila kuta. Mtu ambaye angefanya hivyo kwa kutojali kiapo cha unabii cha Yoshua angelipa bei ya mwanawe aliyekuwa mzaliwa wa kwanza na aliyekuwa mdogo zaidi. Usemi huu unaweza kuwa na maana ya ‘wana wake wote,’ hivyo yeye hangekuwa na mwana wa kuendeleza jina lake katika Israeli.

Hili lilikuwa onyo zito, hata hivyo lilidharauliwa Waisraeli walipofuata namna mbaya sana ya ibada ya sanamu. Chini ya utawala wa Ahabu juu ya ufalme wa kaskazini wa Israeli wa makabila 10, ibada ya Baali ilikuwa imeingizwa humo. Kuonyesha jinsi Waisraeli walivyokuwa wamepotoka sana ni tendo la Hieli Mbetheli. Habari hiyo inasomwa hivi: “Katika siku zake [Ahabu], Hieli Mbetheli akajenga Yeriko; akatia misingi yake kwa kufiwa na Abiramu mzaliwa wake wa kwanza, na kuyaweka malango yake kwa kufiwa na mwana wake mdogo Segubu; sawasawa na neno la [Yehova] alilolinena kwa Yoshua mwana wa Nuni.”​—1 Fal. 16:34.

Kama vijana hawa walikufa katika misiba iliyotokea wakati wa kujenga kuta, au katika njia nyingine, haisemwi. Hata hivyo, maneno ya Yoshua yalionyeshwa yalikuwa ya unabii.

Maneno yote mengine ya Mungu katika Neno lake vilevile yatatimizwa bila shaka. Kwa hiyo inatupasa tuepuke vitu ambavyo Mungu anasema kwamba ni hatari. Tunaweza kujifunza mambo ambayo yanaonwa na Mungu kuwa mema na yale ayaonayo kuwa chukizo kwa kujifunza sana Biblia. Tunapaswa kuona kama vile anavyoona juu ya mambo anayolaumu; tunapaswa kuzoeza mioyo na dhamiri zetu ili tusielekee hata kidogo mambo anayotoa onyo juu yake na tunayopaswa tukae mbali sana nayo ili tuwe salama. Hatupaswi kukawia, bali tunapaswa kuchukua hatua mara moja tuache kuwa na uhusiano au ushirika na vitu visivyokubaliwa na Mungu. Yesu Kristo alijua sana yale yaliyompendeza na yasiyompendeza Baba yake. (Ebr. 1:9) Yeye alisema: “Nayafanya sikuzote yale yampendezayo.” (Yohana 8:29) Ebu angalia jinsi alivyokataa mara moja shauri lisilofaa la Petro, bila kulifikiria hata kidogo. (Mt. 16:21-23) Yeye alionyesha maneno ya Yehova ni ya kweli: “Mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila [neno] litokalo katika kinywa cha [Yehova].” (Kum. 8:3; Mt. 4:4) Msiba wenye kuhuzunisha uliompata Hieli Mbetheli ni mojawapo mifano mingi ya Biblia inayokazia hatari ya kutojali maonyo ya Mungu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki