Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 12/1 kur. 539-543
  • Iweni Wanafunzi wa Kweli wa Kristo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Iweni Wanafunzi wa Kweli wa Kristo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WANADAMU WASIOKAMILIKA WANAWEZA KUMWIGA
  • UTANGAZAJI WA MDOMO HAUTOSHI
  • Je! Utauitikia Upendo wa Yesu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • “Mkafanye Wanafunzi . . . Kuwafundisha”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Upaji wa Kikristo—Ni wa Maana Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 12/1 kur. 539-543

Iweni Wanafunzi wa Kweli wa Kristo

“Hivyo hutukuzwa Baba yangu, kwa vile mzaavyo sana; nanyi mtakuwa wanafunzi wangu.”​—Yohana 15:8.

1. Mwanafunzi ni nini, kwa hiyo ni jambo gani linalofanya mtu awe mwanafunzi wa Yesu Kristo?

MWANAFUNZI ni “mtu anayefunzwa,” “mtu anayejifunza.” Kwa hiyo, wanafunzi wa Yesu Kristo ni watu ambao wamekubali mafundisho yake na wanaishi kupatana na mfano alioweka alipokuwa duniani. Kwa hiyo ili kuwa wanafunzi wa kweli wa Mwana wa Mungu, inafaa tuangalie mambo aliyofanya duniani tujue tunayotakiwa kufanya hasa.

2. Kama inavyoonekana wazi katika Maandiko, kusudi kuu la Yesu Kristo lilikuwa nini?

2 Yesu alifanya utumishi maisha yake yote. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.” (Yohana 4:34) “Kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.” (Mt. 20:28) Alikuwa na maana gani aliponena hivyo?

3. Mazungumzo ya Yesu na mwanamke Msamaria yanaonyeshaje kwamba “chakula” chake kilikuwa kufanya mapenzi ya Baba yake?

3 Yesu alikuwa amechoka, alikuwa na njaa na kiu alipokaa kando ya chemchemi ya Yakobo karibu na Sikari, mji wa Wasamaria. Lakini wakati mwanamke Msamaria alipofika kuchota maji, alitumia nafasi hiyo kutenda wema. Alisahau uchovu wake na njaa yake, akapata furaha na nguvu kwa kufanya kazi ya Baba yake, akamsaidia mwanamke huyo aijue ibada inayokubalika. (Yohana 4:6-34) Naam, kufanya mapenzi ya Baba yake kulikuwa kama chakula kwa Yesu. Kulimtia nguvu. Kusudi lake kuu maishani lilikuwa kusaidia watu kiroho. Aliweka nyuma mahitaji yake mwenyewe ya vitu vya kimwili. Yesu aliishi kupatana kabisa na onyo la upole alilowapa wengine: “Msisumbuke, basi. mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”​—Mt. 6:31-33.

4. Tutayaelewaje maneno ya Yesu kwamba ‘hakuja kutumikiwa, bali kutumika’?

4 Kwa sababu Yesu alikuja kuhudumia watu au kuwatumikia, hiyo haina maana ya kwamba alikataa asitumikiwe hata kidogo. Sivyo alivyofanya, maana tunasoma katika Maandiko habari za wanawake ‘waliomtumikia.’ (Mt. 27:55) Labda utumishi wa wanawake hao ulihusu kupika vyakula, kushona mavazi, kuyatia viraka na kuyafua. Lakini, walifanya utumishi huo kwa kujitolea. Basi, inaposemwa kwamba Yesu Kristo hakuja duniani “kutumikiwa,” maana ni kwamba hakuja kuomba watu wamtumikie. Yeye mwenyewe ndiye aliyetumikia watu zaidi. Aliponya wagonjwa, viwete na walioumbuka mwili, akarudishia vipofu uwezo wa kuona, akafungua vinywa vya mabubu na masikio ya viziwi, na kuondoa mashetani katika watu wengi. Alipotangaza kweli ya Mungu, waliomwitikia walifarijika, wakapona kiroho na kutolewa katika utumwa wa kiroho. Yesu Kristo alitimiza kwa uaminifu kusudi la kutiwa mafuta linalotajwa katika Isaya 61:1: “Roho ya Bwana [Yehova] i juu yangu; kwa sababu [Yehova] amenitia mafuta, niwahubiri wanyekevu habari njema; amenituma ili kuwaganga waliovunjika moyo, kuwatangazia mateka uhuru wao, na hao waliofungwa habari za kufunguliwa kwao.”

5. Yesu alionaje wakati makundi ya watu yalipomsumbua akiwa faraghani?

5 Yesu aliwahurumia ajabu watu aliowatumikia. Hata wakati aliposumbuliwa na makundi ya watu akiwa faraghani, yeye hakuwatolea sauti mbaya, ya hasira. Tunasoma hivi: “Akawahurumia; kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji; akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:34) “Akawakaribisha, akawa akisema nao habari za ufalme wa mungu, akawaponya wale wenye haja ya kuponywa.”​—Luka 9:11. ”‏

6. Yesu alitimizaje maneno ya Isaya 42:3?

6 Yesu Kristo hakudharau kamwe maskini wala wenye taabu. Njia aliyotumia kushughulika na wenye kuonewa ilitimiza maneno ya Isaya 42:3: “Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utokao moshi hatauzima.” (Mt. 12:20) Wenye taabu walikuwa kama mianzi iliyopondwa na kama tambi zilizokaribia kuzimika kwa sababu ya taa kukosa mafuta. Yesu alijua kwamba walikuwa katika hali yenye kusikitisha, basi hakuwatatiza zaidi kwa kuwatenda ukatili. Aliwahurumia, akawapa nguvu mpya na tumaini.

7. Ni jambo gani linalohakikisha kwamba Yesu alikuwa “mnyenyekevu wa moyo”?

7 Ingawa Yesu Kristo alikuwa Bwana, hakuonyesha ukubwa wake alipokuwa kati ya watu aliotumikia. Yeye hakuonyesha watu ukamilifu wake kiasi cha kuwafanya wajione kuwa ovyo tu, na kuogopa-ogopa wakiwa pamoja naye. Yesu alikuwa tofauti kabisa na watu wenye majaliwa mengi, wenye mazoea ya kukasirikia upesi wasio na ujuzi? Ingawa nyakati nyingine wanafunzi wake hawakumtii na walisahau-sahau mambo, Mwana wa Mungu hakuwatolea ukali unaozidi. Kwa sababu alikuwa “mnyenyekevu wa moyo,” alijishusha aweze kufundisha watu waliodharauliwa wakidhaniwa kuwa wajinga.​—Mt. 11:28-30; Yohana 7:47-49.

8. Yesu aliendelea kuwaonaje wananchi wenzake ijapokuwa walikataa kumsikiliza na wakampinga?

8 Hata wakati wananchi wenzake walipokataa kumsikiliza wakampinga, Yesu aliendelea kuwahurumia. Alitaka kuwasaidia wote. Aliuambia Yerusalemu hivi: “Ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka.” (Mt. 23:37) Halafu, alipokuwa akiufikiria uharibifu wa kuogofya ambao ungepata mji huo, Yesu alilia. Aliona uchungu moyoni kwa sababu mateso yote ambayo watu hao wangeletewa na majeshi ya Rumi yangaliweza kuepukwa kama wangalitubu na kukubali kwamba ndiye mtumishi mtiwa mafuta aliyetumwa na Mungu, yaani, Masihi.​—Luka 19:41-44.

9. Ni wakati gani Yesu alipoonyesha upendo ulio mwingi zaidi?

9 Yesu aliweka mfano mzuri kabisa, akaonyesha maana hasa ya kutumikia watu. Lo! jinsi alivyowaonyesha uchangamfu mwingi, fadhili nyingi, na upendo mwingi! Mwishowe, alionyesha upendo mwingi ajabu hata akatoa nafsi au uhai wake uwe ukombozi kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi. Ndiyo sababu alitangulia kuwaambia wanafunzi wake hivi: “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo.”​—Yohana 15:13, 14.

WANADAMU WASIOKAMILIKA WANAWEZA KUMWIGA

10. Kwa sababu gani tunaweza kuwa na hakika kwamba inawezekana kuiga mfano bora wa Yesu?

10 Lakini je! wanadamu wasiokamilika wanaweza kuiga mfano bora wa Yesu Kristo? Hakika wanaweza. Mtume Paulo aliweza, vilevile wanafunzi wengine wengi wa Yesu waliweza kumwiga. Paulo aliwatia moyo Wakristo katika Korintho akawaambia: “Mnifuate mimi kama mimi ninavyomfuata Kristo.”​—1 Kor. 11:1.

11. Mtume Paulo aliwaonaje wananchi wenzake wasioamini?

11 Mtume Paulo alimwiga Yesu Kristo akahurumia watu na kuwapenda kikweli. Aliona uchungu mwingi moyoni wakati wananchi wenzake walipokosa kuamini. Aliwaandikia Warumi hivi: “Nasema kweli katika Kristo, sisemi uongo, dhamiri yangu ikinishuhudia katika [roho takatifu], ya kwamba nina huzuni nyingi na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu. Kwa maana ningeweza kuomba mimi mwenyewe niharimishwe na kutengwa na Kristo kwa ajili ya ndugu zangu, jamaa zangu, kwa jinsi ya mwili.”​—Rum. 9:1-3.

12. Kwa sababu gani ilionekana wazi sana kwamba Paulo aliwafikiria sana Wayahudi?

12 Paulo alichukuliwa na wananchi wenzake kuwa mwasi imani asiyewapenda, kwa sababu ya mambo aliyokuwa akiwahubiri. Lakini, walikuwa wakisema uongo mtupu. Dhamiri yake iliyoelimishwa na roho takatifu ilishuhudia kwamba aliwapenda sana. Alikuwa na nia ya kufanya lo lote asaidie wananchi wenzake wapate wokovu, Tunapokumbuka kwamba wao hasa ndio waliomletea mateso mengi kuliko watu wengineo, tunaona kweli alijitahidi kuwasaidia. Mtume aliwaandikia Wakorintho akawaambia: “Kwa Wayahudi mara tano nalipata mapigo arobaini kasoro moja. Mara tatu nalipigwa kwa bakora; mara moja nalipigwa kwa mawe.”​—2 Kor. 11:

13. Paulo alikuwa na nia ya kusaidia ndugu zake Wayahudi kiasi gani?

13 Sasa angalia kiasi ambacho Paulo alikuwa na nia ya kuwasaidia: “Ningeweza kuomba kwamba mimi mwenyewe niharimishwe na kutengwa na Kristo kwa ajili ya ndugu zangu.” (Rum. 9:3) Hivyo mtume alionyesha alikuwa na nia ya kujitwalia laana ambayo iliwapata wananchi wenzake wasioamini kwa sababu ya kukosa kufuata njia ya Mungu ya wokovu na kutazamia kuishi mbinguni. (Linganisha wagalatia 3:13.) Maneno yake yanaonyesha aliwapenda sana bila kujifikiria mwenyewe. Paulo alikuwa na nia ya kufanya mambo yote aliyoweza ili kusaidia Wayahudi.

14. Inatupasa tuwatendeeje watu wenye ubaridi au wanaopinga “Habari Njema”?

14 Inatupasa sisi tulio wanafunzi wa Yesu Kristo tuhurumie wasioamini kwa njia iyo hiyo. Tusiwachukie kwa sababu wanatupinga na kutuonyesha ubaridi. Watu hao ni washiriki wa jamaa ya kibinadamu iliyofiwa na Kristo. (Rum. 5:6-8) Nayo mapenzi ya Yehova ni kwamba, waendelee kupewa nafasi ya kutubu maadamu wako hai, au mpaka wakati Yehova atakapoharibu uovu wote. (2 Pet. 3:9) Tukithamini jambo hilo kwa mioyo yetu, tutafikiri sana na kusali tuone jinsi ya kusaidia watu kiroho. Hapo tutakuwa tumefuata onyo la upole la Yesu: “Wapendeni adui zenu,,waombeeni wanaowaudhi.”​—Mt. 5:44.

15. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba maisha tunayoishi tukiwa wanafunzi wa Kristo ndiyo bora?

15 Inafaa pia tufikirie jinsi “Habari Njema” zimetusaidia mmoja. Hakika kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo ndiyo njia bora ya maisha. Tunaepushwa tusitumie nguvu na jitihada zetu kuendeleza taratibu za kilimwengu zitakazoangamia bila shaka. Tunalindwa tusijiingize katika ufisadi na uvunjaji sheria wa ulimwengu. Kwa hiyo, hatupatwi na masumbufu na maumivu yanayokuja kwa sababu ya kuvunja amri za Mungu. (Kol. 3:5-10, 12-14) Licha ya kupata faida sasa, tuna tumaini zuri sana la kupata uzima wa milele katika hali zenye haki. (2 Pet. 3:13) Ingekuwa vizuri namna gani kama watu wengi zaidi wangeweza kusaidiwa wapate tumaini hilo kwa kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo!

16. Kwa sababu gani ni jambo la maana watu wapate nafasi ya kuijua kweli upesi iwezekanavyo?

16 Watu wanahitaji “Habari Njema” leo. Huenda kesho ikawa kuchelewa mno. Sababu moja ni kwamba, huenda mtu akajiharibia maisha kwa sababu ya kutozijua “Habari Njema.” Tendo moja la uasherati, kufoka sana kwa hasira kutumia vibaya dawa za kulevya au kufanya mambo kama hayo kunaweza kuleta madhara yasiyoondoleka. Tena siku na saa ambayo Yehova Mungu atauchukulia hatua ulimwengu huu usiomcha haijulikani. (Mt. 24:36-44) Basi inatupasa tutumie wakati uliobaki kwa hekima, tujitahidi kusaidia watu wapate wokovu. (Matendo 18:6) Inatupasa tuwe na maoni kama ya mtume Paulo: “Ole wangu nisipoihubiri Injili!”​—1 Kor. 9:16.

UTANGAZAJI WA MDOMO HAUTOSHI

17. Ili kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo, ni jambo gani tunalohitajiwa tufanye zaidi ya kuhubiri?

17 Lakini, kuzitangaza tu “Habari Njema” hakutoshi ili kuwa wanafunzi wa Kristo. Kunahusu pia kusaidia watu wenye shida nyingi na kuwafadhili hata ikiwa walikuwa wametutenda mabaya. (Rum. 12:17-20) Hata hivyo, kama vile kutimiza mahitaji ya jamaa zetu wenyewe kunavyotangulia kutimiza mahitaji ya watu wengine, ndivyo wajibu wa mtu kwa waamini wenzake unavyotangulia wajibu alio nao kwa wasioamini. (1 Tim. 5:8) Biblia inatushauri hivi: “Kwa hiyo kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.”​—Gal. 6:10.

18. (a) Tuna wajibu gani kwa ndugu zetu wa kiroho walio na shida ya kimwili? (b) Ni wakati gani Mkristo asipokuwa na wajibu wa kumpa mtu mwenye shida msaada wa kimwili?

18 Tunapata nafasi nyingi za kutendea waamini wenzetu mambo mema. Huenda wengine wao wakapatwa na shida kwa sababu ya tukio lisilotazamiwa, msiba wa vitu vya asili au kwa sababu ya mkasa mwingineo. Inatupasa tumwige Yesu Kristo na kujitahidi tuwezavyo tuwasaidie ndugu zetu wa kiroho. Mtume Yohana aliandika hivi: “Katika hili tumelifahamu pendo, kwa kuwa yeye aliutoa uhai wake kwa ajili yetu; imetupasa na sisi kuutoa uhai wetu kwa ajili ya hao ndugu. Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo? Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yohana 3:16-18) Bila shaka, ikiwa mtu haaminiki, ni mvivu tena hataki kufanya kazi ingawa kuna kazi anayoweza kufanya, Mkristo hana wajibu wa kumsaidia kwa kumpa pesa. Kanuni ya Biblia inasema kwamba: “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.”​—2 The. 3:10.

19. Kulingana na aliyoandika mtume Paulo, tunawezaje kusaidia waamini wenzetu kiroho?

19 Mara nyingi sana waamini wenzetu wanakuwa na shida za kiroho. Kulingana na 1 Wathesalonike 5:14, wote walio kundini wana wajibu wa kujitahidi wawezavyo wasaidie wenzao kiroho. Tunasoma hivi: “Waonyeni wale wasiokaa kwa utaratibu; watieni moyo walio dhaifu; watieni nguvu wanyonge; vumilieni na watu wote.” Huenda wengine wakawa wanaachilia wajibu wao wa Kikristo, kwa hiyo wanahitaji kuonywa kwa upole. Kwa mfano huenda ikawapasa wanawake wazee ‘kuwatia wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao; na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe.’ (Tito 2:4, 5) Wanaovunjwa moyo na matatizo au majaribu wanahitaji kutiwa moyo. Je! huwezi kuwajenga kwa kuwaeleza mawazo ya Maandiko ambayo yamekutia nguvu? Je! huwezi kuwatia nguvu kwa kuwaonyesha kwamba unawafikiria? Huenda kukawa na wengine walio na dhamiri dhaifu. Basi wenye dhamiri zenye nguvu wanapaswa kuchukua udhaifu wa ndugu zao kwa kujizuia wasitumie haki zao, (Rum. 15:1-3) Kwa kuwa wote walio kundini ni watu wasiokamilika, lazima tuwe na nia ya kuchukuliana makosa kwa upendo, na kusameheana kwa moyo wa kupenda. (Kol. 3:13) Tukisaidiana kwa njia hizo, hakika vifungo vya upendo vitaimarika.

20. (a) Ni jambo gani hasa linalotutambulisha kuwa wanafunzi wa Kristo? (b) Inakuwaje tunapojitoa tutumikie watu?

20 Tunapoonyesha waamini na wasioamini upendo wa kujinyima, tunaonyesha kwamba sisi ni wanafunzi wa Kristo. (Yohana 13:34, 35) Basi inatupasa tutumie nguvu zetu, wakati wetu, mali zetu na hata nafsi zetu wenyewe tufanye watu wawe na hali bora ya kiroho. Tukitumikia watu hivyo, hatujioni kuwa maskini. Bali, furaha yetu inaendelea kuongezeka, maana “ni heri kutoa kuliko kupokea.” (Matendo 20:35) Basi na tuendelee kuongeza furaha yetu kwa kuzidi kumwiga Yesu Kristo, na kuonyesha sikuzote kwamba sisi ni wanafunzi wake waliojitoa.

​—Kutoka The Watchtower, July 1, 1977.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki