Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 9/1 kur. 21-24
  • Upaji wa Kikristo—Ni wa Maana Kadiri Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Upaji wa Kikristo—Ni wa Maana Kadiri Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MIFANO INAYOFAA KUIGWA
  • SABABU GANI NI WA MAANA SANA?
  • Nguvu Zenye Kuchochea za Ukarimu wa Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Iweni Wanafunzi wa Kweli wa Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Uaminifu Katika Kutumia “Mali ya Udhalimu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • ‘Wakumbuke Maskini’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 9/1 kur. 21-24

Upaji wa Kikristo—Ni wa Maana Kadiri Gani?

NYAKATI zote wanafunzi waaminifu wa Yesu Kristo wameonyesha kuwahangaikia sana wale waliokuwa na mahitaji ya kimwili na ya kiroho. Muda mfupi baada ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., wengi katika Yerusalemu waliuza mali zao kwa hiari wakawapa mitume fedha walizopata ili wagawiwe waamini wenzao waliokuwa na uhitaji. Kati ya hao walikuwa watu waliokuwa wametoka sehemu za mbali ili wahudhurie sikukuu ya Pentekoste kisha wakawa Wakristo. Kupitia kwa ukarimu wa ndugu zao, hawa wapya waliougeukia Ukristo walisaidiwa waendelee kukaa katika Yerusalemu na katika njia hiyo wafaidike na mafundisho bora ya mitume.​—Matendo 2:41-47; 4:34, 35.

MIFANO INAYOFAA KUIGWA

Mmoja aliyethamini sana maana ya kutoa katika njia ya kiroho na ya kimwili alikuwa mtume Paulo. Yeye aliwaandikia hivi waamini wenzake katika Rumi: “Mimi ni mudeni kwa [Wagiriki] na Washenzi [wasio Wagiriki, neno lililotumiwa na Wagiriki kuhusu wageni wote kwa ujumla, sana sana wale waliokuwa wakisema lugha nyingine], kwa wenye akili, na kwa wajinga vilevile. Kwa hivi, kwa upande wangu, mimi ni tayari kuhubiri Habari Njema kwenu munaokaa katika Roma vilevile.”​—Rom. 1:14, 15, ZSB.

Ni kwa sababu gani Paulo alijiona kuwa mdeni kwa watu wa kila namna, kwamba alikuwa na wajibu wa kuwasaidia kiroho? Yeye alijua kwamba ulimwengu wa wanadamu ulikuwa umenunuliwa kwa damu yenye thamani ya Yesu Kristo. Wakiwa mali ya Mungu na Kristo, watu wote wanapaswa bila shaka kufahamishwa ambavyo jambo hilo linavyoweza kumaanisha kwao. Wakati wa Mungu ulikuwa umefika watu wote kila mahali watubu na kuja katika uhusiano wenye kibali pamoja naye kwa msingi wa dhabihu ya Mwanawe. Hali kama hiyo yenye kukubalika ingeyapa maisha yao ubora mwingi na kuwaongoza kwenye uzima wa milele. (Matendo 17:30; 1 Tim. 2:6; Ebr. 2:9) Wakati wa kuwafikia watu wote kwa ujumbe huu ulikuwa mchache sana. Sababu gani? Kwa kuwa muda wa maisha ya wanadamu ni mfupi sana na wenye mashaka. (Yak. 4:13, 14) Hivyo, Paulo alikuwa na bidii ya “kuhubiri Habari Njema” kwa watu wengi iwezekanavyo wakati wa muda wa maisha yake. Kwa kufaa yeye alijiona kuwa na wajibu wa kutoa maarifa hayo yenye kutoa uzima kwa wengine. Alikuwa na deni nao. Kwa kuwa maisha yao yangekoma karibuni, Paulo aliuona uharaka wa kuwafikia watu akiwa na “habari njema” pamoja na nafasi bora sana zilizoambatana nazo. Si mtume Paulo peke yake aliyeona hivyo. Jambo hilo linaonekana wazi kutokana na uhakika wa kwamba miaka inayopungua 30 baada ya kuanzishwa kwa kundi la Kikristo mtume huyo aliweza kuandika hivi: ‘Habari njema zile zilizohubiriwa katika kuumba kote kuliko chini ya mbingu.’ (Kol. 1:23, NW) Hiyo yamaanisha kwamba Wakristo walikuwa wameeneza upaji wao wa Kikristo kufikia sehemu za mbali sana zilizotapakaa za ulimwengu uliojulikana katika wakati huo.

Kwa habari ya kutoa kiroho, bila shaka mtume Paulo pamoja na Wakristo wengine waliojitoa wa karne ya kwanza walitoa mfano bora sana kwetu sisi leo. Na zaidi, wao hawakutoa mahitaji ya kiroho peke yake. Vilevile walikuwa na bidii katika kutoa mahitaji ya kimwili kwa ndugu zao waliopatwa na shida. Kwa mfano, Wakristo katika Makedonia na Akaya, walimkabidhi Paulo fedha zikatumiwe kusaidia waamini wenzao waliokuwa na uhitaji katika Yerusalemu.

Mtume huyo aliiona kazi hiyo ya kuwahudumia wenye mahitaji kwa uzito sana, akiwaomba ndugu katika Rumi wamwombee ili kazi hiyo ipate kufanikiwa. Twasoma hivi: “Ila sasa ninakwenda Yerusalemu, nikiwahudumu watakatifu; maana imewapendeza watu wa Makedonia na Akaya kufanya changizo kwa ajili ya watakatifu huko Yerusalemu walio maskini. Ndugu zangu, nawasihi kwa Bwana wetu Yesu Kristo, na kwa upendo wa Roho, jitahidini pamoja nami katika maombi yenu kwa ajili yangu mbele za Mungu; kwamba niokolewe na wale wasioamini katika Uyahudi, na tena huduma yangu niliyo nayo huko Yerusalemu ikubalike kwao watakatifu.”​—Rum. 15:25, 26 30, 31.

Paulo alipokutana na waamini wenzake katika mahali mbalimbali alipokuwa njiani kuelekea Yerusalemu, roho ya Mungu, ikitenda kazi ama juu yake yeye wenyewe ama juu ya manabii Wakristo ilionyesha kwamba Paulo angefungwa minyororo na kutiwa gerezani huko Yerusalemu. (Matendo 20:23; 21:11) Hata hivyo, mtume huyo hakusita kufanya yale ambayo angeweza kufanya kwa ajili ya ndugu zake waliokuwa na uhitaji huko Yerusalemu. Kwa uhodari yeye aliwaambia waamini wenzake waliokuwa wakitoa machozi hivi: “Mnafanya nini, kulia na kunivunja moyo, kwa maana mimi, licha ya kufungwa, ni tayari hata kuuawa katika Yerusalemu kwa ajili ya jina lake Bwana Yesu.” (Matendo 21:13) Ebu wazia hilo, Paulo alililiona jambo hilo la kuwapelekea ndugu wenye uhitaji msaada wa mambo ya kimwili kuwa jambo la maana sana hivi kwamba, yeye alikuwa na nia si ya kuhatirisha uhuru wake tu kwa kufanya hivyo, bali pia hata na uhai wake.

SABABU GANI NI WA MAANA SANA?

Kwa kweli upaji wa Kikristo huonyesha upendo. Pasipo upendo huo, mtu hawezi kuwa na hali yenye kukubalika mbele za Mungu na Kristo. Watu mmoja mmoja wasiowahangaikia wengine kwa matendo wana hatia ya kujidanganya ikiwa wanajiona wenyewe kuwa wakifuata ibada inayokubalika. Neno la Mungu lasema: “Dini iliyo safi na isiyo na hitilafu mbele ya Mungu Baba ni hii: Kuwasaidia yatima na wajane katika shida zao, na kujilinda mwenyewe usichafuliwe na ulimwengu huu.” (Yak. 1:27, HNWW) ‘Katika hili tumelifahamu pendo, kwa kuwa yeye aliutoa uhai wake kwa ajili yetu; imetupasa na sisi kuutoa uhai wetu kwa ajili ya hao ndugu. Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo? Watoto wadogo, tusipende kwa neno, wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.”​—1 Yohana 3:16-18.

Bwana Yesu Kristo atawahukumu vikali sana wale ambao kwa uchoyo wanawanyima msaada wale wanaouhitaji. Hiyo inaonekana wazi kutokana na mfano wa “kondoo” na “mbuzi.” “Kondoo” ambao Yesu Kristo huwaweka upande wake wa kulia, au upande wenye kibali, ni watu wanaofanyia mema mmojawapo wa hao “walio wadogo” wa ndugu za Kristo. Wanapomwona ye yote wa ndugu za Kristo akiwa na uhitaji, akiwa amekosa chakula, mavazi au nyumba, “kondoo” wanafanya lo lote wawezalo ili kusaidia. Vilevile wanakuwa na nia ya kusaidia wakati ndugu za Kristo wanapoteseka kwa sababu ya magonjwa au ya kutiwa gerezani. Kwa sababu kwa choyo “mbuzi” wanakataa kuitikia mahitaji ya ndugu za Kristo, hawatapata uzima wa milele, wakihukumiwa “adhabu ya milele,” wakikatiliwa mbali milele.​—Mt. 25:34-46.

Hilo lapaswa likazie ndani yetu ubora wa kuwa na maoni yanayofaa juu ya wengine. Tunapowaona wengine wakiwa na shida kwa sababu ya hali wasizoweza kuzuia, je! sisi tunawahurumia? Je! sisi tunaona hali yenye kuhuzunisha sana ya kiroho ya wanadamu wenzetu? Je! jambo hilo linatusukuma tuwe na juhudi katika kutangaza “habari njema”?

Inatupasa sisi kama watu mmoja mmoja tutake kutoa kwa moyo wote mambo ya kiroho na ya kimwili. Ili upaji wa namna hiyo uwe wenye thamani ya kweli machoni pa Mungu, lazima uongozwe na upendo. Si jambo linaloweza kufanywa ili tuvute fikira za watu kwetu sisi wenyewe. Yesu Kristo alionya kwa upole hivi: “Basi, unapomsaidia maskini usitangaze. Usifanye kama wanafiki wafanyavyo katika masunagogi na njiani ili watu wawasifu. Kweli nawaambieni, wamekwisha pata tuzo lao. Lakini wewe unapomsaidia maskini, fanya hivyo kwamba hata rafiki yako asijue ufanyalo. Toa msaada wako kwa siri, na Baba yako aonaye mambo yaliyofichika atakutuza.”​—Mat. 6:2-4, HNWW.

Kama vile ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo watumishi wa Mungu waliojitoa vilevile wanafanya kazi kubwa ya kusaidia wenye shida. Tena, fedha hutumiwa ili kuendeleza mahali pa ibada na vilevile kutoa msaada wa kiroho kwa watu wenye njaa ya kiroho duniani pote. Kati ya Mashahidi wa Yehova, Sosaiti inafanya kazi kubwa ya kusawazisha na kuongoza kazi hiyo ya kusaidia wenye shida na vilevile jitihada za kuwasaidia wengi iwezekanavyo wapate maarifa sahihi ya Neno la Mungu.

Kweli kweli, kutoa msaada wa mambo ya kimwili na ya kiroho kwa wengine ni jambo la maana kwa mtu kuwa Mkristo. Hata hivyo, upaji wa namna hiyo unakubaliwa na Mungu wakati tu unapotolewa kwa hiari na kwa uchangamfu, kwa kuongozwa na upendo wala si kwa kulazimishwa.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Upaji wa mambo ya kimwili na kiroho ni jambo la msingi kwa Ukristo wa kweli.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki