Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 11/1 kur. 5-7
  • Nguvu Zenye Kuchochea za Ukarimu wa Kristo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nguvu Zenye Kuchochea za Ukarimu wa Kristo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Baraka za Ukarimu
  • Ukarimu wa Kikristo Leo
  • Ukarimu Unaleta Thawabu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • ‘Mtihani wa Unyofu wa Upendo Wako’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Watu Wanaotoa kwa Ukarimu Ni Watu Wenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Upaji wa Kikristo—Ni wa Maana Kadiri Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 11/1 kur. 5-7

Nguvu Zenye Kuchochea za Ukarimu wa Kristo

NYAKATI nyingi watu wanapowaona wengine wakiwasaidia wanadamu wenzao wenye shida, wanatiwa moyo waonyeshe ukarimu kama huo. Katika karne ya kwanza, wakati Wakristo katika Makedonia waliposikia juu ya jitihada zenye juhudi za waamini katika Akaya za kusaidia Wakristo maskini katika Yerusalemu, walichochewa washiriki katika jitihada hiyo ya kutoa msaada.​—2 Kor. 9:1, 2.

Hata hivyo, kwa Wakristo, ukarimu wa Bwana yao, Yesu Kristo, umekuwa na nguvu nyingi zaidi za kuchochea. Mtume Paulo alitaja jambo hilo alipowaandikia Wakorintho, akisema hivi: “Maana, ninyi [mnazijua fadhili zisizostahilika za] Bwana wetu Yesu Kristo: yeye, ingawa alikuwa na kila kitu, alijifanya maskini kwa ajili yenu, ili kutokana na umaskini wake awatajirishe.” (2 Kor. 8:9, HNWW) Kwa kufanya kazi pamoja na Baba yake katika kuumba ulimwengu wote, Yesu akiwako kabla ya kuwa mwanadamu alishiriki uenyeji wa vitu vyote, vinavyoonekana na visivyoonekana. Vilevile alikuwa na utukufu wa mwana mzaliwa pekee. Kati ya wana wote wa Mungu wa kimalaika, yeye ndiye aliyekuwa maarufu (mwenye cheo) zaidi.​—Yohana 1:14; Kol. 1:15-18.

Mwana huyo aliacha vyote hivyo kwa hiari ili awe mwanadamu. (Flp. 2:5-8) Kitanda chake cha kwanza kilikuwa hori ya kulishia wanyama. Mama yake, Mariamu, na baba-mlezi wake, Yusufu, walikuwa maskini. Maishani mwake mwote alikuwa na mali chache sana. Pindi moja alimwambia hivi mtu mmoja aliyetaka kuwa mwanafunzi: “Mbweha wana pango, na ndege wa angani wana vioto, lakini Mwana wa Adamu hana pa kujilaza kichwa chake.” (Luka 9:57, 58) Hata hivyo, Yesu mwenyewe aliwaangalia wale waliokuwa na uhitaji mkubwa sana wa vitu vya kimwili. Yeye na mitume wake walikuwa na fedha za shirika za kusaidia Waisraeli maskini.​—Mt. 26:9-11; Marko 14:5-7; Yohana 12:5-8; 13:29.

Aliyofanya Yesu Kristo kwa kuja duniani yaliwezesha wanafunzi wake wapate utajiri mwingi sana. Walipata kuwa wana wa Mungu, warithi wa ufalme wa kimbinguni na wapokeaji wa baraka za kimungu wakati wa maisha yao duniani na kwa umilele wote baada ya kufufuliwa kutoka kwa wafu. (Rum. 8:17) Kama isingekuwa kwa sababu ya ukarimu wa Yesu Kristo, sisi leo tungekuwa tungali chini ya laana ya dhambi na mauti, pasipo taraja la uzima.​—Rum. 6:23.

Kuthamini ukarimu wa Yesu Kristo kuliendeleza roho nzuri ya kutoa kati ya Wakristo wa kwanza. Muda mfupi baada ya kuanzishwa kwa kundi la Kikristo, twaambiwa hivi: “Wala hapakuwa na mtu mmoja miongoni mwao mwenye mahitaji; kwa sababu watu wote waliokuwa na viwanja au nyumba waliviuza, wakaileta thamani ya vitu vile vilivyouzwa, wakaiweka miguuni pa mitume; kila mtu akagawiwa kwa kadiri ya alivyohitaji.”​—Matendo 4:34, 35.

Mpango huo ulifaa sana, sana sana kwa sababu ya hali zilizokuwapo wakati huo. Wayahudi na waongofu wengi walikuwa wamekuja kwenye sikukuu ya Pentekoste katika mwaka 33 W.K. Hawakuwa wamekusudia kukaa sana katika mji huo. Hata hivyo, baada ya kupewa ushuhuda wenye nguvu sana na Petro, na baadaye na wengineo, maelfu walipata kuwa waamini katika Yesu Kristo. Wanafunzi hao wapya walikuwa wangali na mengi ya kujifunza nao walihitaji kutiwa moyo na kutiwa nguvu jambo ambalo lingefanywa na mitume. Kwa njia hiyo ukarimu wa waamini wenzao ukawezesha wakae muda mrefu zaidi katika Yerusalemu wapate kujengwa kiroho.

Roho hiyo nzuri ya kutoa kwa ukarimu vilevile ilionyeshwa na Wakristo katika Filipi. Wakati Lidia alipokuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo, alimwambia Paulo na wenzi wake hivi: “Kama mmeniona kuwa mwaminifu kwa [Yehova], ingieni kwangu mkae.” Mwenzi wa kusafiri wa Paulo, Luka anaongeza hivi: “Akatushurutisha.”​—Matendo 16:15.

Baadaye, wakati Paulo alipokuwa akifanya kazi kwingineko, Wakristo katika Filipi walimtumia michango ya kumsaidia katika kuendeleza “habari njema.” Katika barua yake kwa Wafilipi, twasoma hivi: “Nilipotoka Makedonia, hakuna [kundi] lingine lililoshirikiana nami katika habari hii ya kutoa na kupokea, ila ninyi peke yenu. Kwa kuwa hata huko Thesalonike mliniletea msaada kwa mahitaji yangu, wala si mara moja.” (Flp. 4:15, 16) Alipokuwa akiandika maneno hayo Paulo alikuwa amefungiwa Rumi. Kwa mara nyingine tena Wafilipi walikuwa wamekuja kumsaidia. Si kwamba tu walituma mchango bali pia walimpa mgawo ndugu mwaminifu, Epafrodito, amhudumie mtume huyo. Hiyo ilimaanisha kwamba Epafrodito alipaswa kusafiri katika bahari na juu ya nchi kavu zaidi ya maili 1,000 (kilometres 1,600). Alikuwa mwenye kujinyima sana katika kujitumikisha kwa ajili ya ndugu yake mpendwa Paulo hata akawa mgonjwa mahututi. Hata hivyo, kwa furaha alipata nafuu.​—Flp. 2:25-27; 4:18.

Baraka za Ukarimu

Kama vile Wafilipi, Wakristo wengine katika karne ya kwanza waliipata furaha nyingi sana inayotokana na kutoa. (Matendo 20:35, NW) Walikuwa na furaha ya ndani inayotokana na kusaidia wengine. Vilevile, mtu akitoa kutoka moyoni msaada wa kiroho na wa kimwili jambo hilo linakuwa na thamani kubwa machoni pa Yehova Mungu. Aliye Juu Zaidi analiona jambo hilo kuwa dhabihu inayo kubalika. Angalia maneno ya Waebrania 13:15, 16, NW: “Kupitia kwake sikuzote na tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo linalotangaza waziwazi jina lake. Zaidi ya hayo, msisahau kufanya mema na kushiriki vitu na wengine, kwa kuwa kwa dhabihu hizo Mungu hupendezwa sana.”

Yesu Kristo alitoa uhakikisho kwamba ukarimu haungekosa kuonwa na Baba yake wa kimbinguni. Yeye alisema hivi: “Utoapo [zawadi za rehema], hata mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume; [zawadi yako ya rehema] iwe kwa siri; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.” (Mt. 6:3, 4) Mwana wa Mungu alithawabishwa sana kwa kujinyima utajiri wote na kuwa maskini kwa ajili ya wanadamu. Hivyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Mungu vilevile alimutukuza sana, na kumupa jina lililo juu ya kila jina; hata kwa jina la Yesu kila goti lipigwe . . . na kila ulimi [ukubali waziwazi] ya kuwa Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Flp. 2:9-11, ZSB) Mwana wa Mungu hakupata hasara kwa sababu ya ukarimu wake mwingi mno. Hata sasa, maelfu mengi ya watu wanaweza kushuhudia uhakika wa kwamba kutoa kwao kumebarikiwa sana.

Ukarimu wa Kikristo Leo

Kati ya watumishi wa Yehova leo kwaweza kuonekana tamaa ya unyofu ya kuiga ukarimu wa Yesu Kristo. Wengi pasipo choyo wanatoa wakati wao, nguvu na mali kwa kutembelea watu nyumbani mwao ili wawaletee “habari njema” zenye kufariji ambazo zimeandikwa katika Maandiko. Gharama za kutunza na kuendesha mahali pao pa kukutania zinalipwa kupitia kwa michango ya kujitolea. Kama mtu binafsi au kundi, wanatoa msaada kwa ukarimu kwa watu wenye uhitaji wa kimwili. (Yak. 1:27) Nyakati za misiba inayopata watu wote, watu wenye kutazama wameshangazwa kuona namna Mashahidi wa Yehova wanavyotayarisha misaada.

Mara nyingi watu huuliza namna wanavyoweza kutoa michango kwa ajili ya kuendeleza kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova duniani pote. Zaidi ya kusaidia kundi la mahali pao katika jitihada zake za kueneza “habari njema,” watu mmoja mmoja wanaweza kutoa michango yao moja kwa moja kwa Afisi ya Tawi.

Katika nchi kadha, wakati wa sasa kuna njia nyingine iliyoko sasa ya ‘kumheshimu Yehova kwa mali zako,’ nayo hiyo inakuwa kwa faida ya kiroho ya mtoaji. (Mit. 3:9, 10) Duniani pote, Sosaiti inajitahidi kufanya vifaa na vyombo vyake vya kuchapa na kutangaza “habari njema” kupitia kwa Biblia na vitabu vya Biblia, kutia ndani magazeti, viwe vya kisasa. Tayari, kumekuwa maendeleo fulani kwa habari hiyo, kama ambavyo wasomaji wetu wamekwisha ona bila shaka. Hata hivyo, mashine za kuchapa za kisasa, kwa mfano, za offset, ni ghali (bei kubwa) sana, na kadiri ambavyo tutaweza kufanya vifaa vyetu kuwa bora zaidi itategemea michango itakayopatikana wakati wa mwaka mmoja au miwili ijayo.

Ili kutimiza kusudi hilo, katika nchi zile ambazo mipango ya kujenga viwanda vipya inaendelea, mpango wa kutoa mkopo wa pekee umeanzishwa. Kupitia kwa njia hiyo wanaopendezwa wanaweza kutoa fedha zo zote walizo nazo kwa Sosaiti, ili kwamba Sosaiti itumie fedha hizo katika kufanya kazi ya kulipia gharama za programu ya upanuzi. Baada ya miaka kadha, Sosaiti italipa mkopo wote. Iwapo mpango huo wa kiwanda unaendelea katika nchi yako, waweza kupata habari kamili kutoka kwa tawi la Sosaiti lililoko hapo. Kutegemeza kwa moyo wote mipango hiyo ya ujenzi sikuzote kumetokezea watu wa Mungu furaha nyingi sana, katika nyakati Biblia ilipokuwa ikiandikwa na leo pia.​—Kut. 36:4, 5, 7; 1 Nya. 29:9.

Kweli kweli, kama ilivyokuwa katika wakati uliopita, leo pia mfano wa ukarimu wa Kristo una nguvu zenye kuchochea. Kwa sababu mamia ya maelfu wanathamini sana yale ambayo Mungu Mwenye Nguvu Zote amewafanyia kupitia kwa Mwanawe, wanaendelea kwa juhudi kuzieneza “habari njema” mbali na karibu. Je! wewe binafsi unapata furaha inayoletwa na utendaji huo wa muhimu? Maneno ya mtume Paulo aliyowaandikia Wafilipi na yatimizwe kwako: “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu.”​—Flp. 4:19.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki