‘Wakumbuke Maskini’
BARAZA kuu ya wazee katika Yerusalemu ilimpa mtume Paulo, pamoja na Barnaba, “mkono wa kuume wa shirika” wakati Paulo alipokuwa katika mkutano wa baraza huko, na vilevile wakawapa barua yenye maagizo kwa makundi ya Asia. Barua hiyo ilikiondoa kizuizi cha kitaifa kati ya Wayahudi na Mataifa. Walakini, ingawa agizo hilo lilikuwa la maana sana, kuna jambo jingine ambalo wazee walilazimika kulitilia mkazo wakiwaeleza Paulo na Barnaba. Shauri hilo la pekee lilisema kwamba iliwapasa ‘kuwakumbuka maskini.’—Gal. 2:9, 10; Matendo 15:22-29.
Paulo anasema kwamba alijitahidi sana kufanya hivyo, zaidi ya kuhubiri sana. Alijitahidi nyakati zote kutia roho hiyo ya ukarimu katika makundi. Wakati Wakristo wa Yerusalemu walipopatwa na shida, Paulo aliyatia moyo makundi ya Ulaya yawagawie vitu kadiri walivyoweza.—Rum. 15:26; 2 Kor. 8:1-8; 9:1-5.
WAKRISTO WANAONYESHA WATU WOTE UKARIMU
Maandiko yote ya Kikristo yanatia mkazo mwingi yakisema tufikirie maskini. Mtume Yohana alisema: “Mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo?” (1 Yohana 3:17) Ndivyo pia ndugu mzazi mmoja na Yesu alivyoandika: “Ikiwa ndugu mwanamume au ndugu mwanamke yu uchi na kupungukiwa na riziki, na mtu wa kwenu akawaambia, Enendeni zenu kwa amani, mkaote moto na kushiba, lakini asiwape mahitaji ya mwili, yafaa nini?” Yakobo alionyesha kwamba “dini iliyo safi, isiyo na taka mbele za Mungu Baba ni hii, Kwenda kuwatazama yatima na wajane katika dhiki yao, na kujilinda na dunia pasipo mawaa.”—Yak. 2:15, 16; 1:27.
Paulo alimshauri Timotheo, aliyekuwa amemwacha Efeso, awakumbushe matajiri katika kundi uhitaji wa kuwa “matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane” vitu vyao na wengine, kisha akawaambia Wakristo katika Rumi: “Kwa mahitaji ya watakatifu, mkifuata ukarimu; katika kukaribisha wageni, mkijitahidi.” Sifa hizo za ukarimu na ukaribishaji zinahitajiwa sana katika “mema” yanayomwezesha Mkristo ‘aupate uzima ulio kweli kweli.’—1 Tim. 6:18, 19; Rum. 12:13.
Kwa habari ya kutoa msaada wa vitu vya kimwili, mara nyingi Biblia inatutia moyo tugawie Wakristo wenzetu hasa. Lakini ukarimu wa Wakristo wa kweli hauishii hapo tu. Bali, unapasa uonyeshwe nyakati zote, uwe sifa ya daima katika utu wa Kikristo, huku moyo wa mtu ukijitolea kwenda kusaidia wenye shida.
Bila shaka, Mkristo hana mali za kuweza kusaidia kila mtu mwenye shida. Basi, anawezaje kuamua vizuri watu atakaosaidia? Juu ya jambo hilo, mtume alisema hivi: “Na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Gal. 6:10) Kwanza, inawapasa Wakristo wawe wepesi kuona mahitaji ya ndugu zao. Walakini, haiwapasi kusahau watu wengine wanaotaabika.
Mara nyingi Wakristo hawawi na vitu vingi vya kutoa. Lakini wanaweza kutumikia watu kwa upendo, na huenda kufanya hivyo kukafaa hata zaidi. Huenda jirani akawa ni mgonjwa—huenda akawa ni mtu ambaye hakupendezwa na habari njema alipoelezwa na Mkristo. Hata hivyo, Mkristo atapendezwa kutafuta njia ya kumsaidia. Labda mama mwenye kazi za nyumbani ni mgonjwa mno asiweze kujipikia vyakula wala kwenda dukani. Au huenda mgonjwa akahitaji kupelekwa kwa daktari. Huenda akafurahi sana akitembelewa kirafiki tu, au akipelekewa bakuli yenye mchuzi wenye moto. Wazee au watu wenye vizuizi vya mwili wanaweza kusaidiwa kwa njia nyingi.
Matendo hayo ni sehemu ya “mema” ambayo inawapasa Wakristo wayafanye kwa juhudi. (Tito 2:14) Angalia kwamba Biblia inamsifu sana Dorkasi, mwanafunzi Mkristo wa mji wa Yafa, kwa sababu “alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa.” Bila shaka hakuwa na mali nyingi, lakini alifanya utumishi wenye upendo wa kutengenezea wajane maskini mavazi.—Matendo 9:36-40.
Kwa hiyo, inampasa Mkristo aonyeshe ukarimu kwa kutumia busara na akili pia, si kwa kutoa msaada wa kimwili tu. Haimpasi kuwapa wengine vitu kiasi cha kuponda mapato na hali ya jamaa yake mwenyewe. Vilevile, mtu angekuwa mpumbavu akimpa pesa mtu mwingine anayeweza kuziponda au hata kuzitumia katika mazoea mabaya. Vilevile, kusaidia mvivu kunaweza kumharibu, kumsaidia aendelee kujikalia kitako tu na labda hata kumwongezea uzembe. Paulo aliliandikia kundi la Kikristo katika Thesalonike akaliambia hivi: “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula. Maana twasikia kwamba wako watu kwenu waendao bila utaratibu, hawana shughuli zao wenyewe, lakini wanajishughulisha na mambo ya wengine. Basi twawaagiza hao, na kuwaonya katika Bwana Yesu Kristo, watende kazi kwa utulivu na kula chakula chao wenyewe.”—2 The. 3:10-12; linganisha Waefeso 4:28.
Kwa hiyo, Wakristo watawapa msaada wa kimwili wale wanaompenda Mungu hasa, wanaopendezwa na habari njema kikweli, wanaouhitaji msaada huo kikweli. Lakini wawezapo wanasaidia wengine pia walio na shida halisi, na bila shaka nyakati zote wanawapa watu wote msaada wa kiroho. Wao wana roho iliyo kama ya Yesu. Mtume Mathayo, aliyefuatana na Yesu alipokuwa akienda kijiji na kijiji kufanya matendo mema, aliandika hivi: “Alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji.”—Mt. 9:36.
MUNGU ANAMPENDA MKARIMU
Mungu hawasahau wale wanaofikiria wenye shida na kuwasaidia. Anahesabu mambo wanayofanyiwa kama kwamba amefanyiwa yeye. Biblia inasema: “Amhurumiaye maskini humkopesha [Yehova]; naye atamlipa kwa tendo lake jema.” (Mit. 19:17) Mtu mkarimu kweli kweli hana haja ya kuogopa kwamba atakuwa maskini kwa sababu ya kutoa kwa moyo mkunjufu vitu ambavyo labda hata vinaupita uwezo wake wa pesa. Mtume aliyeongozwa na Mungu aliandika hivi: “Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu. Na Mungu aweza kuwajaza kila neema kwa wingi, ili ninyi, mkiwa na riziki za kila namna sikuzote, mpate kuzidi sana katika kila tendo jema; kama ilivyoandikwa, Ametapanya, amewapa maskini, haki yake yakaa milele.” (2 Kor. 9:7-9; Zab. 112:9) Upaji wa Mkristo unamletea Mungu utukufu pamoja na habari njema anazohubiri ikiwa umetolewa kwa upendo, kwa maana “yeye awahurumiaye wahitaji humheshimu [Muumba wake].”—Mit. 14:31.
Biblia inaeleza habari za mke mwema na kusema kwamba, zaidi ya kuwa na sifa njema za bidii na kutumainika, yeye “huwakunjulia maskini mikono yake; naam, huwanyoshea wahitaji mikono yake. . . . Mume wake hujulikana malangoni [yaani, matendo ya mkewe yanamletea heshima mtaani]. . . . Wanawe huondoka na kumwita heri; mumewe naye humsifu.”—Mit. 31:20-28.
UMASKINI UTAMALIZWA
Wakati wa sasa, maneno ya Yesu yanahusu Wakristo pia: “Sikuzote mnao maskini pamoja nanyi.” (Mt. 26:11) Hiyo ni kwa sababu ya hali za uchumi za ulimwengu zinazobadilika nyakati zote, na vilevile kwa sababu ya magonjwa na mateso. Lakini Biblia inaahidi hivi: “Mhitaji hatasahauliwa daima; matumaini ya wanyonge hayatapotea milele.” (Zab. 9:18) Chini ya utawala wa Ufalme wa Mwana wa Mungu, wale wanaonyonya watu na kuonea maskini na wanyonge watakuwa wamemalizwa. “Atawahukumu walioonewa wa watu, atawaokoa wahitaji, atamseta mwenye kuonea.”—Zab. 72:4.
Kama watu wangalitii sheria kamilifu ya Mungu katika Israeli ya kale kusingalikuwa na maskini, na ndivyo itakavyokuwa chini ya utawala wa Kristo juu ya dunia. Mungu aliwaambia Israeli maneno yafuatayo muda mfupi tu kabla hawajaiingia Nchi ya Ahadi: “Hawatakuwako maskini kwenu; (kwa kuwa [Yehova] atakubarikia kweli katika nchi akupayo [Yehova], Mungu wako, uimiliki, iwe urithi wako). (Kum. 15:4) Badala ya kuwa na sheria ya kuandikwa tu, watu watakaokuwa chini ya uongozi wenye haki wa Ufalme wataandikwa sheria ya Mungu katika mioyo yao, kwa maana “hukumu [za Mungu] zikiwapo duniani, watu wakaao duniani hujifunza haki.” (Isa. 26:9) Juu ya wakati huo, nabii aliandika hivi: “Fadhili na kweli zimekutana, haki na amani zimebusiana. Kweli imechipuka katika nchi, haki imechungulia kutoka mbinguni. Naam, [Yehova] atatoa kilicho chema, na nchi yetu itatoa mazao yake.”—Zab. 85:10-12.
Loo! itakuwa vizuri namna gani wakati umaskini utakapokuwa umeng’olewa milele! Hata hivyo, ukarimu hautaondolewa, kwa maana kila mtu ataweza kugawia wenzake ujuzi wake, vipawa vyake na mazao ya bidii yake ili kufaidi mtaa mzima. Tunapotazamia wakati huo, acheni sote tuwe tukitiana moyo, kugawana vitu vya kimwili na mambo ya kiroho, ‘tukihimizana katika upendo na kazi nzuri,’ nayo mojawapo “kazi” hizo ni ‘kuwakumbuka maskini.’—Ebr. 10:24; Gal. 2:10; Rum. 1:12; Matendo 2:42.