Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w86 10/15 kur. 10-15
  • Uwe Mwenye Furaha Waonyeshe Kibali Walio na Shida

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uwe Mwenye Furaha Waonyeshe Kibali Walio na Shida
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kielelezo Bora kwa Ajili Yetu
  • Kama Baba, Kama Mwana
  • Paulo—Mfano Wenye Furaha
  • Je! Sisi Tutakuwa Wenye Furaha?
  • Fuata Kielelezo Cha Yesu Kwa Kuwahangaikia Maskini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • ‘Wakumbuke Maskini’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Ulimwengu Usio na Umaskini Unakaribia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Mwisho wa Umaskini Wakaribia
    Amkeni!—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
w86 10/15 kur. 10-15

Uwe Mwenye Furaha Waonyeshe Kibali Walio na Shida

“Mwenye kudharau mwanadamu mwenzake anatenda dhambi, lakini mwenye furaha ni yeye anayewaonyesha kibali wenye kusumbuka.”​—Mithali 14:21, NW.

1, 2. Ni jambo gani lililotukia kwa jamaa tatu za Ufilipino, nalo linatuongoza tufikirie maulizo gani?

JAMAA tatu za Ufilipino zilipokuwa zikihudhuria mkutano wa Kikristo katika Mkoa wa Pangasina, moto usiotazamiwa uliteketeza nyumba zao zikawa majivu. Waliporudi nyumbani, walijikuta hawana chakula wala mahali pa kulala. Wakristo wenzao, walipopata habari juu ya msiba huo, walifanya haraka kwenda kule wakiwa na chakula na wakawapangia mahali pa kulala katika nyumba za wengine kundini. Asubuhi iliyofuata, Wakristo walifika wakiwa na mianzi na vifaa vingine vya kujengea. Upendo huo wa kidugu uliwavutia sana jirani. Jamaa zile tatu zilivutwa pia kwa njia njema. Moto ule uliharibu nyumba zao, lakini imani yao na sifa nyingine ya Kikristo ziliokoka zikaongezeka kwa sababu ya itikio hilo lenye upendo.​—Mathayo 6:33; linganisha 1 Wakorintho 3:12-14.

2 Je! mambo yaliyoonwa kama hili hayachangmshi moyo? Yanajenga imani yetu katika fadhili za kibinadamu na hata zaidi ya hivyo katika Ukristo wa kweli. (Matendo 28:2) Ingawa hivyo, Je! tunauthamini msingi wa Kimaandiko wa ‘kuwatendea watu wote mema kwa njia hiyo; na hasa jamaa ya waaminio’? (Wagalatia 6:10) Na ni kwa njia gani sisi binafsi tunaweza kufanya mengi zaidi kuhusu jambo hilo?

Kielelezo Bora kwa Ajili Yetu

3. Tunaweza kuwa na uhakika juu ya nini kuhusu jinsi Yehova anavyotuhangaikia?

3 Mwanafunzi Yakobo anatuambia hivi: “Kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu hutoka juu.” (Yakobo 1:17, NW) Hiyo ni kweli sana kama nini, kwa maana Yehova anatuandalia vitu tele kwa faidi yetu ya kiroho na kimwili! Lakini, yeye anatanguliza mambo gani kati ya hayo. Ni mambo ya kiroho. Kwa mfano, yeye alitupa sisi Biblia ili tuwe na uongozi wa kiroho na tumaini. Tumaini hilo linategemea zawadi ya kumtoa Mwanaye, ambaye dhabihu yake ndiyo msingi wa kusamehewa kwetu na kuwa na taraja la uzima wa milele.​—Yohana 3:16; Mathayo 20:28.

4. Inaonekanaje wazi kwamba Mungu anapendezwa na mahitaji yetu ya kimwili pia?

4 Yehova anapendezwa na masilahi yetu ya kimwili pia. Mtume Paulo alizungumza jambo hilo kwa kuwapa sababu wanaume waliokuwa katika mji wa kale wa Listra. Ingawa wao hawakuwa waabudu wa kweli, hawangeweza kukana kwamba Muumba ‘hakutenda mema, akitupa sisi mvua kutoka mbinguni, na nyakati za mavuno, akitushibisha mioyo yetu chakula na furaha.’ (Matendo 14:15-17) Kwa sababu ya upendo, Yehova anatutolea mahitaji yetu ya kiroho na pia anatufanyia uandalizi kwa ajili ya maisha yetu ya kimwili. Je! wewe hufikiri kwamba kutenda hivyo kunashiriki kumfanya awe ndiye yule “Mungu mwenye furaha”?​—1 Timotheo 1:11, NW.

5. Tunaweza kujifunza nini kutokana na shughuli za Mungu pamoja na Israeli wa kale?

5 Shughuli za Mungu pamoja na Israeli wa kale zinaonyesha jinsi yeye anavyoangalia kwa usawaziko mahitaji ya kiroho na hali ya kimwili ya waabudu wake. Kwanza, yeye alifanya Sheria ipatikane kwa watu wake. Wafalme wake walipaswa watayarishe nakala yao binafsi ya Sheria, na watu walikusanyika pindi kwa pindi wasikie Sheria yake ikisomwa. (Kumbukumbu la Torati 17:18; 31:9-13) Sheria ilifanya uandalizi kuwe na hema takatifu au hekalu na makuhani wa kushughulikia dhabihu ili watu waweze kuwa na kibali cha Mungu. Waisraeli walikusanyika kwa ukawaida kwa ajili ya siku za sherehe za kiroho, ambazo zilikuwa mambo makuu katika ibada yao ya kila mwaka. (Kumbukumbu la Torati 16:1-17) Kwa sababu ya yote hayo, Waisraeli mmoja mmoja wangeweza kuwa matajiri kiroho mbele za Mungu.

6, 7. Katika Sheria Yehova alionyeshaje kuhangaikia mahitaji ya kimwili ya Waisraeli?

6 Ingawa hivyo, Sheria ilionyesha wazi pia jinsi Mungu anavyoangalia hali za kimwili za watumishi wake. Labda wazo linaloingia akilini mwako ni juu ya sheria walizopewa Israeli kuhusu mipango ya afya na hatua za kupunguza kuenea kwa maambukizo. (Kumbukumbu la Torati 14:11-21; 32:10-14) Hata hivyo haitupasi tusahau maandalizi ya pekee ambayo Mungu alifanya asaidie waliokuwa maskini na wenye shida. Afya mbaya au msiba kama kutokea kwa moto au gharika, ni mambo ambayo yangeweza kuingiza Mwisraeli katika umaskini. Yehova alikubali wazi mle mle ndani ya Sheria yake kwamba si watu wote wangekuwa sawa kiuchumi. (Kumbukumbu la Torati 15:11) Lakini yeye hakuwahurumia tu maskini na wenye shida bali alifanya zaidi ya hilo. Alipanga kuwapa msaada.

7 Uhitaji wa mara hiyo kwa watu kama hao ungekuwa chakula. Kwa hiyo Mungu alielekeza kwamba maskini katika Israeli wawe huru kuokota-okota mazao yaliyosalia katika mashamba ya nafaka na mashamba ya mizabibu au kutokana na mizeituni. (Kumbukumbu la Torati 24:19-22; Mambo ya Walawi 19:9, 10; 23:22) Njia ya Mungu haikutia watu moyo wawe wavivu wala waishi kwa kutegemea kupewa-pewa misaada ya umma hali wangeweza kufanya kazi. Mwokotaji Mwisraeli alipaswa kufanya jitihada, labda atumie saa nyingi akichomwa na jua kali ili akusanye chakula cha siku hiyo. Lakini, haitupasi tukose kuangalia kwamba kwa njia hiyo Mungu aliwapa riziki waliokuwa maskini kwa kuifikiria hali yao.​—Linganisha Ruthu 2:2-7; Zaburi 69:33; 102:17.

8. (a) Wayahudi mmoja mmoja walihimizwa wafanye nini kwa ajili ya ndugu zao. (Linganisha Yeremia 5:26, 28) (b) Wewe ungelinganishaje mwelekeo ambao Mungu alihimiza Wayahudi wawe nao na ule wa watu wengi leo?

8 Yehova alizidi kukazia kupendezwa kwake na wenye shida kwa kutoa matangazo rasmi kama lile lililo kwenye Isaya 58:6, 7, NW. Katika wakati ambao Waisraeli fulani wenye kinaya walikuwa wakisingizia tu kwamba wanafunga, nabii wa Mungu alitangaza hivi: “Je! huku siko kufunga ninakochagua mimi? . . . Kuwaacha waliopondwa waende wakiwa huru, na kwamba ninyi watu mvunje katika vipande viwili kila ufito wa nira? Je! si kugawanya mkate wako umpe mwenye njaa, na kwamba uwalete watu wenye kusumbuliwa, wasio na makao ndani ya nyumba yao? Kwamba, ukiona mtu fulani aliye uchi, ni lazima umfunike, na kwamba haikupasi ujifiche kutoka kwa mwili wako mwenyewe?” Watu fulani leo wanalinda kile kinachoweza kuitwa ‘ukanda wa faraja!’ walichojiwekea. Wao wana nia ya kusaidia mtu mwenye uhitaji ikiwa tu kufanya hivyo hakumaanishi kwamba wadhabihu jambo lo lote la kibinafsi au la kuwasumbua. Ni roho tofauti kama nini iliyokaziwa katika maneno ya Mungu kupitia Isaya!—Ona pia Ezekieli 18:5-9.

9. Sheria ilitoa shauri gani juu ya kufanya mikopo, na Mungu alitia moyo juu ya kuwa na mwelekeo gani?

9 Kujali ndugu maskini, Waisraeli kungeweza kuonyeshwa katika kutoa mikopo. Mwisraeli angeweza kutazamia kulipwa riba anapomwazima pesa mtu fulani aliyetaka kuzitumia afanye biashara yake au aipanue. Lakini, Yehova alisema riba isitozwe juu ya pesa alizoazimwa ndugu maskini au sivyo shida yake kubwa ingeweza kumshawishi aingie katika kosa. (Kutoka 22:25; Kumbukumbu la Torati 15:7, 8, 11; 23:19, 20; Mithali 6:30, 31) Mwelekeo wa Mungu juu ya wasiofanikiwa sana ulipasa uwe kiolezo kwa watu wake. Hata tunaahidiwa hivi: “Yeye anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamwazima Yehova, na Yeye atamlipa huyo kwa tendo lake.” (Mithali 19:17, NW) Ebu wazia hilo​—kumwazima Yehova, ukiwa na uhakikisho wake kwamba atakulipa kwa wingi!

10. Baada ya kuufikiria mfano wa Mungu, wewe ungeweza kujiulizaje?

10 Hivyo imetupasa sisi sote tuulize hivi: Maoni ya Mungu na kutendea kwake wenye kusumbuka humaanisha nini kwangu? Je! mimi nimekuwa nikijifunza kutokana na kielelezo chake kikamilifu na kujaribu kukiiga? Je! mimi naweza kufanya maendeleo ya kuwa katika mfano wa Mungu katika jambo hili?​—Mwanzo 1:26.

Kama Baba, Kama Mwana

11. Maoni ya Yesu yalilinganaje na ya Baba yake? (2 Wakorintho 8:9)

11 Yesu Kristo ndiye “mng’ao wa utukufu wake [Yehova] na chapa ya nafsi yake.” (Waebrania 1:3) Kwa hiyo, tungemtazamia yeye aonyeshe anawajali kama Baba yake wale wanaopendezwa na ibada ya kweli. Hivyo ndivyo alivyofanya. Yesu alionyesha kwamba umaskini unaohitaji kuondolewa zaidi ya mwingine wo wote ni umaskini wa kiroho: “Wenye furaha ni wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao.” (Mathayo 5:3, NW; linganisha Luka 6:20.) Kristo alisema hivi pia: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili mimi nimekuja kuingia ndani ya ulimwengu, kwamba nipaswe kutoa ushuhuda kwa ule ukweli.” (Yohana 18:37, NW) Kwa hiyo, yeye hakujulikana kuwa mfanya-miujiza hasa wala mponyaji bali Mwalimu. (Marko 10:17-21; 12:28-33) Kuhusiana na jambo hilo, angalia Marko 6:30-34. Tunasoma juu ya wakati ambao Yesu alikuwa ametafuta wakati fulani wa faragha ili apumzike kidogo. Ndipo “akaona mkutano mkuu . . . [ambao] walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji.” Yeye alitendaje? “Akaanza kuwafundisha mambo mengi.” Ndiyo, Yesu alijipanua kwa kuitikia uhitaji wao uliokuwa mkubwa zaidi: ukweli ambao kwao wangeweza kuishi milele.​—Yohana 4:14; 6:51.

12. Tunaweza kujifunza nini juu ya maoni ya Yesu kutokana na Marko 6:30-34 na Marko 6:35-44?

12 Ingawa Yesu alikaza fikira juu ya mahitaji ya kiroho ya Wayahudi wa hali ya chini, yeye hakupuuza mahitaji yao ya kimwili. Masimulizi ya Marko yanaonyesha kwamba Yesu alikuwa chonjo kuona uhitaji wa chakula halisi. Kwanza mitume walidokeza kwamba umati huo uambiwe waende zao “wakajinunulie chakula.” Yesu hakukubali. Halafu mitume wakautaja uwezekano wa kuchukua nyingine za pesa zilizokuwa za kufanyia kazi yao ambazo walikuwa wakitembea nazo, kisha watumie hizo kununua chakula. Badala ya hivyo, Yesu alitambua kuufanya ule muujiza unaojulikana sana alioutumia kulisha wanaume 5,000, bila kuhesabu wanawake na watoto, kwa kuwapa chakula cha msingi cha mkate na samaki. Watu wengine leo wangeweza kuwa na maoni ya kwamba lilikuwa jambo rahisi Yesu kutosheleza mahitaji ya umati kwa njia ya muujiza. Hata hivyo, tusikose kuuona uhakika wa kwamba yeye alikuwa na hangaikio la kweli, na akachukua hatua.​—Marko 6:35-44; Mathayo 14:21.a

13. Yesu alionyesha ushuhuda gani mwingine wa kwamba alipendezwa na masilahi ya watu?

13 Labda wewe umesoma masimulizi ya vitabu vya Injili yanayothibitisha kwamba hisia za Yesu kwa ajili ya watu wasio na mafanikio zilipanuliwa kwa wengi zaidi ya maskini. Yeye alisaidia wagonjwa na wenye kusumbuka pia. (Luka 6:17-19; 17:12-19; Yohana 5:2-9; 9:1-7) Wala hakuwa akiponya wale waliokuwa karibu na yeye tu. Nyakati nyingine alisafiri mahali alikokuwa mgonjwa ili amsaidie.​—Luka 8:41-55.

14, 15. (a) Kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu alitazamia wafuasi wake waonyeshe wazi mahangaikio kama yake? (b) Ingefaa sisi tujiulize nini?

14 Lakini, Je! waliopaswa kujali mahitaji ya wanafunzi (au watafutaji ukweli) maskini na wenye kusumbuka ni wale tu ambao wangeweza kutoa msaada kwa kufanya miujiza? Hapana. Wanafunzi wote wa Yesu walipaswa wahangaike na kutenda kwa njia yenye kuonyesha hivyo. Kwa mfano, yeye alihimiza mwanamume tajiri aliyetaka uzima wa milele afanye hivi: “Viuze ulivyo navyo vyote, ukawagawanyie maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni.” (Luka 18:18-22) Yesu alishauri hivi pia: “Ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa [mwenye furaha], kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki.”​—Luka 14:13, 14.

15 Mkristo ni mfuasi wa Kristo, kwa hiyo kila mmoja wetu angeweza kuuliza hivi: Ni kwa kadiri gani mimi ninaiga mwelekeo na vitendo vya Yesu kuhusu maskini, wenye kusumbuka, wasiofanikiwa sana? Je! mimi naweza kusema kwa unyofu kama mtume Paulo: “Iweni waigaji wangu mimi, kama mimi ninavyoiga Kristo”?​—1 Wakorintho 11:1, NW.

Paulo—Mfano Wenye Furaha

16. Ni jambo gani lililompendeza mtume Paulo kwa njia ya pekee?

16 Inafaa kumtaja Paulo katika habari hii, kwa maana yeye pia alikuwa mfano mzuri wa kuigwa. Kama vile ambavyo tungetazamia, kazio lake la msingi lilikuwa mahitaji ya kiroho ya wengine. Yeye alikuwa ‘balozi badala ya Kristo, akiomba wengini hivi, “Mpatanishwe kwa Mungu.” ‘ (2 Wakorintho 5:20, NW) Mgawo wa pekee wa Paulo ulikuwa kuhubiri na kujenga makundi kati ya watu wasio Wayahudi. Yeye aliandika hivi: “Nimekabidhiwa injili ya wasiotahiriwa.​—Wagalatia 2:7.

17. Tunajuaje kwamba Paulo alielekeza fikira kwenye mahangaiko ya kimwili pia?

17 Lakini kwa kuwa Paulo alisema alikuwa akiiga Kristo, Je! yeye (kama Yehova na Yesu) aliangalia masumbuko ya kimwili au magumu ya waabudu wenzake? Acheni Paulo mwenyewe ajibu. Katika Wagalatia 2:9, yeye aliendelea kusema ‘Yakobo na Kefa [Petro] na Yohana walinipa mimi na Barnaba mkono wa kuume wa shirika, ili sisi tuende kwa mataifa.’ Halafu katika mstari ule ule unaofuata Paulo akaongeza hivi: “Tuwakumbuke maskini; nami neno lilo hilo nalikuwa na bidii kulifanya.” (Wagalatia 2:10) Kwa hiyo Paulo alithamini jambo la kwamba, ingawa yeye alikuwa mmisionari-mtume mwenye madaraka kwa makundi mengi, yeye hangeweza kuwa mwenye shughuli mno asiweze kupendezwa na masilahi ya kimwili ya ndugu na dada zake.

18. Ni “maskini” gani ambao inaelekea Paulo alikuwa akitaja katika Wagalatia 2:10, na kwa sababu gani wangalipaswa kufikiriwa?

18 Inaelekea kwamba “maskini” aliosema juu yao katika Wagalatia 2:10 walikuwa Wakristo Wayahudi hasa katika Yerusalemu na Yudea. Mapema kabla ya hapo kulikuwa kumekuwa na “manung’uniko . . . kwa upande wa Wayahudi wenye kusema Kigiriki dhidi ya Wayahudi wenye kusema Kiebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa wakikosa kuangaliwa katika ugawaji wa kila siku” wa chakula. (Matendo 6:1, NW) Hivyo, wakati Paulo alipokuwa akitaja kwamba yeye alikuwa mtume kwa mataifa, alieleza wazi kwamba hakuwa akikosa kujali mtu ye yote katika udugu wa Kikristo.(Warumi 11:13) Yeye alithamini kwamba kutunza akina ndugu kimwili kulitiwa ndani ya maneno haya: “Kusiwe na faraka katika mwili, bali viungo vitunzane kila kiungo na mwenziwe. Na kiungo kimoja kikiumia, viungo vyote huumia nacho.”​—1 Wakorintho 12:25, 26.

19. Tuna uthibitisho gani kwamba Paulo alichukua hatua ya kuonyesha kuhangaikia maskini?

19 Wakati Wakristo katika Yerusalemu na Yudea walipotaabika kwa sababu ya umaskini, njaa katika eneo lao, au mateso, makundi fulani ya mbali yalichukua hatua. Bila shaka, ingetazamiwa kwamba walikuwa wakikumbuka ndugu zao wenye uhitaji katika sala za kuomba Mungu awasaidie na kuwafariji. Lakini hawakuachia hapo. Paulo aliandika kwamba “wale katika Makedonia na Akaya wamependezwa kugawana vitu vyao kwa kutoa mchango kwa maskini wa watakatifu katika Yerusalemu.” (Warumi 15:26, 27, NW) Wale waliotolea ndugu zao wenye kusumbuka michango hiyo ya kifedha ‘walikuwa wakitajirishwa katika vitu vyote wapate kuwa na ukarimu wote, umpatiao Mungu shukrani kwa kazi yetu.’ (2 Wakorintho 9:1-13) Je! hicho hakingekuwa kisababishi cha kuwafanya wafurahi?

20. Kwa sababu gani akina ndugu waliotoa michango kusaidia “maskini” wangeweza kuwa wenye furaha?

20 Akina ndugu waliogawana pesa zao na “maskini wa watakatifu katika Yerusalemu” walikuwa na msingi wa ziada wa kupata furaha. Kuwajali wenye kusumbuka kungesaidia wachangaji hao wapate kibali cha Mungu. Tunaweza kuona sababu kwa kuangalia kwamba neno la Kigiriki lililotafsiriwa “mchango” katika Warumi 15:26 na 2 Wakorintho 9:13 lina wazo la “ishara ya ushirika, uthibitisho wa umoja wa kidugu, hata zawadi.” Limetumiwa kwenye Waebrania 13:16, NW linalosema hivi: “Msisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana dhabihu kama hizo Mungu anapendezwa sana nazo.”

Je! Sisi Tutakuwa Wenye Furaha?

21. Tunaweza kukata shauri kwamba ni jambo gani litatutolea msingi wa kupata furaha?

21 Katika mazungumzo haya, tumechunguza ushuhuda wa Kimaandiko wa kuonyesha kwamba Yehova Mungu, Yesu Kristo, na mtume Paulo walijali wenye kusumbuka. Tumeona kwamba wote kati yao walitambua kwamba mahitaji ya kiroho ndiyo yanayopasa kuelekezewa fikira kwanza. Lakini ni kweli pia kwamba wote walionyesha kwa njia zenye mafaa kuwa walipendezwa na maskini; wagonjwa, na wale wenye kukosa kufanikiwa. Wangeweza kupata furaha kwa kutoa msaada wenye mafaa. Je! sisi nasi tusifanye hivyo? Paulo mwenyewe alituhimiza “kukumbuka yale maneno ya Bwana Yesu, wakati yeye mwenyewe aliposema, ‘Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.’”​—Matendo 20:35, NW.

22. Ni mambo gani ya habari hii ambayo bado yanastahili kuelekezewa fikira zako?

22 Ingawa hivyo, huenda wewe ukauliza hivi: “Ni mambo gani hasa ambayo mimi binafsi naweza kufanya? Naweza kujuaje wale walio na uhitaji kikweli? Naweza kutoaje msaada kwa njia isiyotia moyo kuwa na uvivu, ambayo ni ya fadhili na yenye kufaa, inayofikiria hisia za wengine, na yenye usawaziko pamoja na wajibu wangu wa Kikristo wa kuzieneza habari njema? Makala inayofuata itashughulika na mambo hayo, ikuwekee msingi wa kupata furaha ya ziada.

[Maelezo ya Chini]

a Jambo la kupendeza ni kwamba Yesu mwenyewe hakuona haya wala hakuwa mwenye kiburi mno asiweze kukubali msaada wa kimwili kutoka kwa wengine.​—Luka 5:29; 7:36, 37; 8:3.

Je! Wewe Umeona?

◻ Mungu anaonyeshaje ushuhuda wa kwamba anapendezwa na mahitaji yetu ya kiroho na pia mahitaji yetu ya kimwili?

◻ Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Yesu alihangaikia zaidi ya kusaidia watu kwa kuwafundisha ukweli?

◻ Ni mfano wa namna gani ambao Paulo aliweka kuhusu maskini?

◻ Baada ya kuifikiria mifano ya Yehova, Yesu, na mtume Paulo, wewe unaweza kuona uhitaji wa kufanya nini?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wazee Wakristo na wengine wamepaswa kutumia shauri la Yesu katika Luka 14:13, 14

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki