Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 12/15 kur. 555-557
  • Kwa Sababu Gani Tuamini Mungu Tusiyeweza Kuona?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Sababu Gani Tuamini Mungu Tusiyeweza Kuona?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • TOFAUTI KUBWA SANA
  • KUAMINI VISIVYOONEKANA
  • UFUNDI WA MUUMBA
  • Mungu
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Kujifunza Juu ya Usichoweza Kuona
    Furaha​—Namna ya Kuipata
  • Imarisha Imani Yako Katika Muumba
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Rekodi ya Kale ya Uumbaji—Je, Unaweza Kuitumaini?
    Je, Kuna Muumba Anayekujali?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 12/15 kur. 555-557

Kwa Sababu Gani Tuamini Mungu Tusiyeweza Kuona?

TUNAISHI katika kizazi chenye ufundi mwingi wa sayansi. Wanasayansi wameyumbua vitu vingi na kufanya matendo ya ajabu, hata wakapeleka wanadamu mwezini.

Kwa sababu ya mambo hayo waliyotimiza, watu wengi wanakubaliana na wanasayansi wakatapo maneno kuhusu mambo mengineyo. Kwa mfano, wanapodai kwamba wanadamu walitokana na wanyama, watu wengi sana wanaamini hivyo. Wakidai kwamba uhai ulijitokeza wenyewe tu katika bahari fulani ya zamani sana, watu wengi wanaamini hivyo.

Kwa sababu ya mafundisho hayo, wakati wanasayansi fulani wanaposema kwamba Mungu hayuko, watu wengi wanakubaliana nao. Tena, wako wengine wanaokata maneno kwamba hayuko kwa sababu hatuwezi kumwona. Kwa hiyo, watu wanaoamini vitu vinavyoonekana tu wanazidi kuwa wengi. Wachache zaidi wanaamini kwamba kuna Muumba asiyeonekana, mwenye kusudi.

Lakini, je! kuna sababu nzuri za kutomwamini Mungu kwa sababu hatuwezi kumwona? Je! inatupasa tuiamini sana sayansi? Je! kunakuwa na tofauti yo yote tukimwamini Mungu au tusipomwamini?

TOFAUTI KUBWA SANA

Kunakuwa na tofauti kubwa sana tusipoamini kwamba kuna Muumba. Ikiwa yuko, bila shaka alikuwa na kusudi fulani la kuiumba dunia hii na kuumba wanadamu ndani yake.

Ni jambo la akili pia kutazamia kwamba Muumba huyo mwenye hekima na uwezo apaswa kuamua jinsi dunia hii na wanadamu watakavyokuwa wakati ujao. Kwa hiyo maoni na matendo yetu juu ya Muumba huyo yanaweza kuleta tofauti kubwa juu ya wakati wetu ujao.

Lakini, ikiwa hakuna Mungu, wanadamu watapatwa na mambo yenye kusikitisha sana wakati ujao. Tukiamua kulingana na mambo ambayo yamekuwa yakitukia, wanadamu wataendelea kuishi katika hali zenye taabu zaidi, ikiwa hakuna Mungu. Ikiwa hakuna Muumba asiyeonekana, aliyekuwa na kusudi la kutuweka hapa, inafaa “tule, na tunywe, maana kesho tutakufa.”​—1 Kor. 15:32.

KUAMINI VISIVYOONEKANA

Je! tunaweza kuamini Mungu tusiyeweza kuona? Je! tunaamini vitu tunavyoona peke yavyo? Hapana, tunaamini sana vitu tusivyoona.

Hasa, maisha yetu yanategemea kitu tusichoweza kuona! Kitu gani? Hewa tunayopumua. Bila hewa, tunaweza kufa baada ya muda mfupi sana. Hatuwezi kuiona hewa hiyo, lakini tuna hakika kwamba iko. Ukifunga pua yako nukta 60, utajua upesi sana kwamba kuna hewa, ingawa huwezi kuiona.

Wala hatuwezi kuona upepo, lakini tunaona miti ikitikiswa na upepo, na mawimbi ya bahari yakitupwa-tupwa na nguvu za upepo. Tunaamini kwamba kuna upepo kwa sababu ya mambo unayofanya.

Hatuwezi kuona nguvu za umeme. Lakini maajabu yafanywayo nao, weee! Zinawasha taa, zinapasha nyumba joto, zinaendesha mashine kubwa sana na kufanyiza kazi vyombo vyetu vya jikoni. Hakuna mtu mwenye kichwa kizuri anayetia shaka akisema hakuna nguvu za umeme kwa sababu haziwezi kuonekana.

Miale ya nuru ya radio, televisheni na radar inapitishwa hewani bila kuonekana. Hata hivyo tunajua kwamba miale hiyo iko kwa sababu vitu hivyo vinatoa sauti au vinaonyesha picha.

Je! tunaweza kuona nguvu za uvutano? Hatuwezi, lakini bila nguvu hizo, vitu vyote ambavyo havikushikamana na dunia, pamoja na watu, vingeelea angani. Nguvu nyingine inayofanana na nguvu za uvutano ni sumaku. Sumaku inavuta chuma, lakini hatuwezi kuziona nguvu hizo zikisafiri zikinase.

Sehemu ya katikati ya atom (kipande kilicho kidogo zaidi sana cha kitu) inakuwa imeshikanishwa pamoja na nguvu nyingi zisizoonekana. Lakini tunajua kwamba nguvu hizo ziko kwa sababu ya mlipuko mkubwa sana unaotokea katika makombora wakati atom inapopasuliwa.

Hatuwezi kuona Eksirei, lakini miale hiyo ya nuru inaweza kupenya miili yetu na kupiga picha za mifupa yetu. Unadhani daktari atasemaje ukimwambia kwamba miale hiyo haiko kwa sababu huwezi kuiona?

Hatuoni harufu kwa macho yetu, lakini pua zetu zinanasa harufu hizo; mbwa wanaokamata watu waliojificha wanawatafuta kwa kunusa harufu isiyoonekana. Wala hatuwezi kuona mawimbi ya sauti, lakini masikio yetu yananasa mawimbi hayo; basi tunajua kwamba yako.

Hivyo, tunaamini vitu vingi tusivyoweza kuona, kwa sababu tunaona ushuhuda au mambo yanayofanywa na vitu hivyo kuonyesha kwamba viko. Vivyo hivyo, tunajua kuna Muumba asiyeonekana kwa sababu tunauona ushuhuda wake au vitu alivyofanya. Biblia inasema hivi: “Kwa sababu mambo yake yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake.”​—Rum. 1:20.

UFUNDI WA MUUMBA

Unapoona nyumba, unasemaje? Unasema kwamba mbao zake, mawe yake na vyuma vyake vilijipanga vyenyewe vikawa nyumba yenye vyumba vya kutosha, yenye taa, mifereji ya maji, nguvu za umeme na viti vya kukalia? Hapana, unasema kwamba ilijengwa na mtu fulani. Hata vitu vidogo kama sanduku au kalamu ya mate havijitokezi vyenyewe.

Lakini, vitu hivyo havihitaji ufundi mwingi sana vikilinganishwa na atom, mti, mwanadamu, sayari, jua, kundi la nyota nyingi sana, ulimwengu wote. Ikiwa vitu visivyohitaji ufundi mwingi sana vinatengenezwa na mtu, namna gani vitu hivyo vilivyo vigumu sana kufahamika?

Mtaalamu wa fizikia, G. E. Davis, anasema hivi: “Hakuna kitu kionekanacho kinachoweza kujiumba.” Kupatana na wazo hilo, Biblia inasema jambo hili lenye busara: “Maana kila nyumba imetengenezwa na mtu; ila yeye aliyevitengeneza vitu vyote ni Mungu.”​—Ebr. 3:4.

Halafu, tena, ukiona orodha ya sheria kama zile zinazofanya katiba ya taifa, hiyo itakuonyesha nini? Ukiona ishara ndogo tu katika pembe ya barabara inayosema, “Simama,” itakuonyesha nini? Sheria zinaonyesha kwamba kuna watunga sheria.

Ulimwengu wote una sheria nyingine zenye kustaajabisha zaidi. Wanaanga wasingaliweza kutua mwezini kama wasingalifuata kabisa sheria zinazoongoza nguvu za uvutano, sheria zinazoongoza miendo ya vitu, za kuongeza mwendo, na vilevile zinazoongoza mzunguko wa dunia na mwezi. Sheria hizo kuu zinaonyesha kwamba kuna Mtunga sheria mkuu, Muumba asiyeonekana.

Basi, si vigumu kufahamu sababu ya Biblia kusema yafuatayo juu ya watu wanaopuza au kukana ushuhuda mwingi unaoonyesha kuna Muumba: “Hata wasiwe na udhuru.”​—Rum. 1:20.

Lakini kwa sababu gani Mungu haonekani kwa macho ya kibinadamu? Je! unadhani unaweza kuokoka ukisafiri kwenda juani? Hapana, utaungua muda mrefu kabla hujafika. Mungu ndiye aliyeliumba jua. Kwa hiyo, yeye ni mwenye uweza mwingi mno asiweze kuonekana na macho ya kibinadamu. Ndiyo sababu Mungu anasema katika Neno lake hivi: “Mwanadamu hataniona akaishi.”​—Kut. 33:20.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki