Watoto Wenye Hekima Wafurahisha Mioyo ya Wazazi Wao
“MWANA mwenye hekima humfurahisha babaye.” (Mit. 15:20) Namna yalivyo kweli maneno hayo yaliyoongozwa na Mungu! Watoto wanapofanya mambo kwa hekima, wanafurahisha mioyo ya wazazi wao.
Lakini, wanahitaji kufundishwa ndipo waweze kufurahisha wazazi wao. Kama ilivyo katika sehemu zote za dunia, katika Burma pia Mashahidi Wakristo wa Yehova wameona kwamba ndivyo inavyokuwa.
Kwa mfano, yuko Joanna mwenye umri wa miaka sita. Msichana huyo amefundishwa vizuri na mama yake. Siku moja, wakati mama yake alipotembelea rafiki zake, Joanna alikwenda naye. Muda mfupi kabla ya kula chakula cha mchana katika nyumba hiyo, Joanna aliwauliza watoto wa nyumba hiyo kama wao walikuwa na desturi ya kusali kabla ya kula. Ndipo alipojua kwamba hata hawakujua namna ya kusali, kisha akamwomba kila mmoja arudie kusema maneno yake huku yeye akisali kwa sauti kubwa. Hata mama ya watoto hao alijiunga nao kurudia maneno ya Joanna. Walipokwisha kula, Joanna alikwenda nje kuwaeleza watoto hao habari za Mungu wake, Yehova. Aliwauliza kama wao walikuwa na Mungu wao. Waliposema hawakuwa naye, aliwauliza tena hivi: “Mungu wenu anaitwa nani?” Walishindwa kumjibu. Basi Joanna akasema hivi kwa kujisikia, “Mungu wangu anaitwa Yehova.”—Zab. 83:18.
Peter mwenye umri wa miaka minane amefundishwa na wazazi wake namna ya kuitumia Biblia kueleza wengine mambo anayoamini. Yeye anaweka vikaratasi katika Biblia yake ili vimkumbushe yanakopatikana maandiko yanayomfaa. Wakati karatasi kimoja kilipoanguka kikatoka katika Biblia yake, Peter alilitaja andiko hilo kutokana na kumbukumbu yake.
Lakini namna gani ikiwa mtu hana wakati wa kuweka alama katika Biblia yake wala kuandika kitu katika kikaratasi? Anaweza kujua la kufanya kutokana na Joshua mwenye umri wa miaka saba. Yeye alikuwa akiendelea kumsikiliza mzee aliyewekwa wa kundi lake akionyesha namna ya kutolea wasioamini mawazo ya Maandiko. Lakini Yoshua hakuwa na karatasi ya kuandikia. Kama angalisimama akaitafute angalikosa mafundisho mazuri. Basi alifanya nini? Aliandika upesi andiko fulani katika kiganja cha mkono wake. Baadaye, aliweza kueleza wengine wazo hilo la Maandiko.
Wazazi wafundishapo watoto wao vizuri, huenda mfano unaowekwa na watoto hao ukatia imani yao nguvu. Ndivyo ilivyokuwa kwa mzee mmoja. Miaka michache iliyopita yeye alifungwa pamoja na mzee mwingine kwa kushtakiwa mambo ya uongo na kwa sababu ya kutoingia katika siasa. Hakukuwa na mzee wala mtumishi mwingine katika kundi hilo. Kwa hiyo, Zami, ambaye ni binti yake mwenye umri wa miaka kumi na miwili, alijichukulia nafasi hiyo kuendesha utendaji fulani mpaka baba yake afunguliwapo. Kila asubuhi ya Jumapili baba yake alikuwa akisimama karibu na tundu dogo la chumba cha gereza, ili kumwona binti yake na wengine wakiendea watu kuwaeleza habari za Biblia.
Bila shaka, kufundisha watoto si kuwafundisha waseme na wengine tu. Wanapaswa pia kufundishwa kusikiliza sana katika mikutano ya kundi na kuyatumia mambo wanayojifunza. Ndivyo walivyofanya wazazi wa Sanju mwenye umri wa miaka minne. Walikuwa wakimwambia asikilize sana mikutanoni. Baadaye, walipofika nyumbani alikuwa akipanda kiti na kutolea wazazi wake hotuba zile zile zilizotolewa kwa njia yake ya kitoto. Wageni walipowatembelea walijua watazisikia hotuba za Sanju. Sasa Sanju ana miaka saba na anatoa hotuba katika Shule ya Kitheokrasi ya kundi.
Mafundisho mazuri yanaweza pia kusaidia watoto wavumilie wanapokazwa wavunje sheria ya Mungu. Ndivyo ilivyokuwa kwa Christine mwenye umri wa miaka sita. Wakati mmoja alikwenda akakae na babu na nyanya wasioamini kwa siku chache. Walipokuwa wameketi mezani kula chakula cha mchana, aliona kwamba nyanya alikuwa ametayarisha wanyama wadogo kwa kuwachoma. Alimwuliza: “Wanyama hawa walichinjwa namna gani?” Christine alipojua kwamba hawakutolewa damu vizuri, alikataa kuwala. Babu na nyanya walishangaa wakamwuliza sababu. “Baba,” kasema Christine, “aliniambia hainipasi kula kitu ambacho hakikuchinjwa vizuri kwa maana mimi ni Mkristo.” (Mwa. 9:3, 4) Akijaribu kumbembeleza, nyanya alimwambia kwamba baba yake asingejua kwamba amekula. Lakini Christine akajibu: “Mimi simwabudu baba. Hata ikiwa hayupo hapa kuniona nikila, Yehova Mungu, ninayeabudu, yupo.” Jambo hilo liliwafungulia wazee hao njia ya kutaka kuujua ujumbe wa Biblia.
Namna yalivyo kweli maneno haya yaliyoongozwa na Mungu: “Toka vinywa vya watoto wachanga nao wanaonyonya [wewe Yehova] umepata sifa”!—Mt. 21:16.