Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
Ubora mwingi wa Hekima
Urithi ni jambo bora. Lakini unaweza kuwa na ubora gani ikiwa mwenye kuupata hana busara ya kuutumia vizuri? Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Hekima ni njema, mfano wa urithi; naam, nayo ni bora kwao walionao jua. Kwa maana hekima ni ulinzi, kama vile fedha ilivyo ulinzi; na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo.”—Mhu. 7:11, 12.
Basi hekima inaonyeshwa kuwa bora kuliko mali. Mtu asiye na hekima anaweza kuponda mali na kumaliza urithi wake upesi. Ingawa pesa zinalinda mtu kwa njia fulani, na kumwezesha anunue vitu anavyohitaji, zinaweza kupotea au kuibwa. Huenda watu wakamfikiria sana tajiri wakitaka kumnyang’anya mali zake na kumtenda jeuri. Kwa upande mwingine, hekima au uwezo wa kutumia maarifa ili kutatua matatizo au kutimiza miradi fulani inaweza kulinda mtu asifanye mambo ya kipumbavu yanayoweza kuhatirisha maisha yake. Inaweza kuepusha mtu asife mapema, tena inaweza kumwongoza apate uzima wa milele ikiwa anaitumia kumcha Mungu.
Hakika hekima inalinda mtu. Mwenye hekima alisema: “Hekima ni nguvu zake mwenye hekima, zaidi ya wakuu kumi waliomo mjini.” (Mhu. 7:19) Kwa sababu hekima ni ulinzi, inaweza kulinda wakaaji wa mji uliozingirwa hata kuliko “wakuu kumi,” yaani, hesabu kamili ya mashujaa wa vita.
Kwa sababu hakuna mwanadamu mkamilifu, hatuwezi kupatana bila kuwa na uongozi wenye hekima ambao Yehova Mungu ametupa katika Neno lake. Kwa kuwa wanadamu ni watenda dhambi, wanashindwa kufikia ukamilifu wa Mungu. Sulemani alisema: “Hakuna mwanadamu mwenye haki hapa duniani, ambaye afanya mema, asifanye dhambi.” (Mhu. 7:20) Basi, inatupasa tuwe na hekima inayofunuliwa katika Biblia. Halafu tutaweza kufanikisha njia yetu sasa na wakati ujao.
Mambo Ambayo Mwanadamu Hawezi Kubadili
Yako mambo mengi yanayotukia katika ulimwengu huu usio mkamilifu ambayo mwanadamu hawezi kuzuia. Ingawa hayapendezi, hayawezi kubadilishwa. Mfalme Sulemani alisema: “Tafakari vema kazi yake Mungu; kwa sababu ni nani awezaye kukinyosha kitu kile alichokipotosha yeye?” (Mhu. 7:13) Ndiyo kusema, ni mwanadamu yupi anayeweza kunyosha kasoro ambazo Mungu ameruhusu ziwepo? Hakuna anayeweza, kwa maana Aliye Juu Zaidi anafanya mambo yote akiwa na kusudi, tena anakuwa na kusudi fulani anaporuhusu mambo fulani yatukie.
Kwa hiyo Sulemani anapendekeza hivi: “Siku ya kufanikiwa ufurahi, na siku ya mabaya ufikiri. Mungu ameifanya hiyo moja kwenda sambamba na hiyo ya pili, ili mwanadamu asipate kulijua neno lo lote litakalofuata baada yake.” (Mhu. 7:14) Kulingana na shauri hilo, inapasa mtu aonyeshe kwamba amefurahia siku ambayo imekuwa na mambo mazuri kwa kutenda mema, kuonyesha ukarimu, fadhili, na furaha katika maneno na matendo yake mwenyewe. Inapasa aione siku nzuri kama zawadi kutoka kwa Mungu. Lakini namna gani siku hiyo ikileta msiba, shida? Inapasa ‘atafakari’ au ajue kwamba Mungu ameuruhusu msiba huo utukie. Kwa sababu gani akafanya hivyo? Sulemani anasema sababu ni kwamba, “ili mwanadamu asipate kulijua neno lo lote litakalofuata baada yake.”
Tunapata nafasi ya kusitawisha uvumilivu kwa sababu Mungu anaturuhusu tupatwe na mambo yenye kutufurahisha na yenye kutuletea shida pia, tena inatupasa tujue wazi vile Sulemani alivyosema, kwamba hatuwezi kujua mambo ya wakati ujao. Hakuna mwanadamu asiyepatwa na mambo hayo; msiba unaweza kupata wenye haki sawasawa na waovu. Hasa, huenda wenye haki wakawa na shida, huku waovu wakielekea kufanikiwa. Sulemani aliendelea kusema hivi: “Mambo hayo yote nimeyaona mimi katika siku za ubatili wangu, yuko mwenye haki upoteaye katika haki yake, yuko na mtu mwovu azidishaye maisha yake katika udhalimu wake.”—Mhu. 7:15.
Bila shaka, hali hiyo inasumbua watu wengi. Inawafanya hata wamkasirikie Aliye Juu Zaidi. Lakini haitupasi kufanya hivyo. Inatupasa tumtumaini Mungu, tukikumbuka kwamba yeye ni Mungu mwenye upendo. (1 Yohana 4:8) Mambo anayoruhusu yatukie hayataleta madhara ya daima kamwe juu ya mtu ye yote. Kwa kuwa mtu aweza kupatwa na mema na mabaya pia, inatupasa tujulishwe na jambo hilo ubora wa kumtegemea Mungu, badala ya kujitegemea. Ingawa huenda tusifahamu sababu gani mambo fulani yanatukia sasa, tunaweza kuwa na hakika kwamba, jambo likiisha kutendeka na kumalizika kwa ruhusa ya Mungu, litakuwa limetimiza kusudi fulani lenye kufaidi watu wote wanaohusika.
Mtume Petro alieleza jambo hilo wazi alipokuwa akitaja mateso yaliyopata waamini wenzake siku hizo: “Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio kati yenu, unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho. Lakini kama mnavyoyashiriki mateso ya Kristo, furahini; ili na katika ufunuo wa utukufu wake mfurahi kwa shangwe. Mkilaumiwa kwa ajili ya jina la Kristo ni heri yenu; kwa kuwa [roho ya utukufu na ya Mungu inawakalia].” (1 Pet. 4:12-14) “Mkiisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye mwenyewe atawatengeneza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu.”—1 Pet. 5:10.