Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
Mungu Humpa Mwenye Haki na Asiye Haki
Kwa habari ya yale ambayo Mungu humpa mwenye haki na asiye haki, Mhubiri 2:26 lasema hivi: “Humpa yeye aliyemridhia hekima na maarifa na furaha; bali mkosaji humpa taabu, ili kukusanya na kututa, apate kumpa huyo ambaye Mungu amridhia.”
Mtu mwema anakuwa na hekima na kupata maarifa, kwa sababu ya kutumia uongozi unaotolewa na Muumba. Anawezeshwa kutumia mali na uwezo wake kupatana na hekima na maarifa, nalo hilo laongeza furaha yake. Kama hangekuwa na uhusiano na Mungu, yeye hangekuwa na hekima hii ya kweli, maarifa pamoja na furaha. Kwa hiyo yaweza kusemwa kweli kweli kwamba Yehova Mungu amempa “hekima na maarifa na furaha.”
Kwa upande mwingine, asiye haki au mtenda dhambi hupuza shauri la Mungu. Kwa hiyo, Aliye Juu Zaidi humruhusu aendelee na mipango yake ya kichoyo na kupatwa na matokeo yake mabaya. Mtenda dhambi hufanya kazi ngumu na hujitumikisha, akijaribu kujilundikia mali. Walakini yeye haridhiki au kutosheka, kwa kukosa hekima na maarifa ya kufurahia kazi yake yote. Yeye anakosa furaha inayotokana na kutumia mali katika kusaidia walio na uhitaji. (Matendo 20:35) Na zaidi ya hayo, huenda akafikia miradi yake kwa kutumia njia zilizo kinyume cha sheria, na baada ya muda kupita, akashikwa katika hila zake. Mwishowe, yale yote ambayo mtenda dhambi amejipatia huenda yakawa yake mtu mwema. Ndivyo ilivyokuwa kwa Wakanaani. Ijapokuwa walikuwa watu wenye adili zilizopotoka sana, walifanikiwa kwa miaka mingi. Kisha, ndipo, kama vile Yehova alivyokuwa ameamur, mashamba yao ya mizabibu, ya mzeituni, nyumba zao pamoja na mali nyingine, yakaja kuwa urithi wa Waisraeli.—Kum. 6:10, 11.
‘Wakati Uliowekwa kwa Kila Jambo’
Mfalme Sulemani alipata kuona kwamba hapa duniani mambo yanatukia na kutukia tena kwa mfuatano na pia yanabadilika. Kama vile wakati unafika wa mama mjamzito kuzaa mtoto, vivyo hivyo wakati unafika ambapo uzee au ugonjwa huleta mwisho wa uhai. Kama vile kulivyo na wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa, ‘kuna wakati wa kupanda na wa kung’oa yaliyopandwa, wa kuua na wa kupoza, wa kubomoa na wa kujenga, wa kulia na wa kucheka, wa kunyamaza na wa kunena, wa kupenda na wa kuchukia, na wa vita na wa amani.’—Mhu. 3:1-8.
Mara nyingi wakati wa mambo hayo unaletwa na hali zisizoweza kuzuiliwa na mwanadamu. Ndiyo sababu, baada tu ya kuzungumza juu ya mambo haya, Sulemani aliendelea kuuliza ulizo hili: “Je! mtendaji anayo faida gani katika yale anayojishughulisha nayo?” (Mhu. 3:9) Ndiyo, kwa sababu ya uhakika wa kwamba mambo makubwa maishani hutukia ambayo hayawezi kuzuiliwa na mwanadamu, je! ni jambo la hekima kujaribu kupata furaha kutokana na kazi ngumu peke yake? Kwa sababu ya kutokuwa na hakika katika maisha, kazi ngumu ya mtu pamoja na kujitahidi kwake atimize mradi wa mambo ya kimwili huenda upesi ikawa si kitu.—Mt. 6:27.
Sulemani anaendelea hivi: “Nimeiona taabu ambayo Mungu amewapa wanadamu, ili kutaabika ndani yake.” (Mhu. 3:10) Yeye angeweza kujisema kama ‘akiona’ hili kwa sababu alikuwa amechunguza mwenyewe kikamilifu kazi ngumu ya wanadamu. Kwa sababu ya yale aliyokuwa ameona baada ya uchunguzi wake wa makini, Sulemani alifikia uamuzi gani juu ya hali ambazo katika hizo mwanadamu analazimika kufanya utendaji wake? Twasoma hivi: “Kila kitu [Mungu] amekifanya kizuri kwa wakati wake.”—Mhu. 3:11.
Kwa kupatana na hili, Sulemani aliandika hivi katika Mhubiri 7:29: “Tazama, hili tu nimeliona; Mungu amemfanya mwanadamu mnyofu, lakini wamebuni mavumbuzi mengi.” Hili lilifanyika katika wakati unaofaa katika programu ya Mungu ya uumbaji, alipokiumba kiumbe cha kwanza cha kibinadamu kikiwa kikamilifu. Mungu alimpa mwanadamu huyu, Adamu, mke, Hawa, ambaye alikuwa ukamilifu wa uzuri wa kike, alikuwa mzuri kuliko wale mabinti wa Ayubu wenye sifa. (Ayubu 42:15) Baada ya ndoa ya Adamu na Hawa chini ya uzuri wa hali za kiparadiso, siku ya sita ya uumbaji wa Mungu ilifikia mwisho wake, wakati ambapo “Mungu akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.”—Mwa. 1:31.
Katika paradiso ya Edeni Mungu aliweka mbele ya wazazi wa kidunia wa wanadamu taraja la maisha yenye furaha katika ukamilifu “hata milele.” Yeye aliweka mbele yao wakati ujao wa milele kukiwa na masharti ya kwamba wangeendelea kumtii yeye pasipo lawama. Hivyo ‘aliiweka hiyo milele katika mioyo ya wanadamu.’ (Mhu. 3:11; Mwa. 2:16–3:3) Wakati wanadamu hawa wawili wa kwanza walipoanza kutafuta mipango mingi yao wenyewe katika kumwasi Muumba wao, ndipo, katika wakati huo wenye maana sana, Mungu akafanya kitu “kizuri,” kwa kuwa alitoa ahadi yake ya kutokeza uzao ambao ungekiponda kichwa cha yule Nyoka Mkuu katika kumwondolea Mungu lawama na kuwabariki wanadamu. (Mwa. 3:15) Kutokezwa kwa uzao huu kuliwekwa katika wakati ujao usiojulikana. Hivyo, basi, wanaume na wanawake walioonyesha imani katika ahadi ya Mungu waliangalia mbele wakitazamia wakati ujao ulete uzao ulioahidiwa pamoja na baraka ambazo wangepata kutokana na uzao huo. Hivyo Mungu aliweka mbele ya wanadamu wakati ujao wenye matumaini, jambo ambalo wangeishi kwa ajili yake, hata liwe lingekuwa la wakati ujao ulio mbali namna gani.
Baada ya kumwokoa Nuhu na jamaa yake kupitia kwa gharika ya dunia yote, Mungu aliweka mbele ya wanadamu wakati ujao wenye haki, akilipamba agano lake lenye kuleta amani kwa upinde mzuri sana. Akiweka wakati wa matendo yake yenye kusudi baada ya hapo, Mungu alifanya agano lake lenye upendo pamoja na Ibrahimu la kubariki jamaa zote na mataifa yote ya dunia kupitia kwa uzao wake. Agano hili lilithibitisha agano la Edeni la uzao wa “mwanamke” wa Mungu.
Kutoka kwa Ibrahimu na kuendelea katika ukoo huo mpaka kwa ule uzao, alitokea Daudi mfalme wa Israeli katika Yerusalemu kwa wakati uliowekwa. Akiupunguza zaidi ukoo wa Uzao ulioahidiwa, Mungu alifanya kitu “kizuri” kwa kufanya pamoja na Daudi mwaminifu agano la ufalme wa milele katika nyumba yake. Kwa uchaguzi wa pekee wa Mungu, mwana mdogo wa Daudi Sulemani akachukua mahali pa Daudi na kujenga hekalu la Yehova huko Yerusalemu. Katika wakati wa utawala wake wa amani, “Yuda na Israeli wakakaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, tokea Dani mpaka Beer-sheba.” (1 Fal. 4:25) Akiwa na sababu nzuri Sulemani angeweza kuandika hivi: “Tazama, mimi niliyoyaona kuwa ndiyo mema na ya kufaa, ni mtu kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote anayoifanya chini ya jua, siku zote za maisha yake alizopewa na Mungu; maana hilo ndilo fungu lake.”—Mhu. 5:18.
Tukifikiria mambo ‘mazuri’ ambayo Mungu amefanya katika wakati unaofaa, twaweza kufahamu namna maneno haya mengine ya Sulemani kuhusu Yehova Mungu yalivyo ya kweli: “Ameiweka hiyo milele ndani yao [wanadamu]; ila kwa jinsi mwanadamu asivyoweza kuivumbua kazi ya Mungu anayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho.” (Mhu. 3:11) Katika wakati wake Mungu alimtuma Sulemani Mkuu, Yule Mkuu wa Uzao ulioahidiwa, Yesu Kristo. Vilevile Mungu alimtumia Masihi huyu aiweke “hiyo milele” katika mioyo ya wanadamu. Huyu Mwana wa Mungu aliuangaza ufalme wa Kimasihi ambao ungekuwa na utukufu zaidi ya ule wa Sulemani, ambao chini yake wanadamu watiifu watapata uzima wa milele. Ufalme huu utakuwa ndio mojawapo wa vitu vizuri zaidi vya matendo ya Mungu. Uzima wa milele hautakuwa wenye kuchosha, kwa kuwa ufalme huu wenye kuokoa uhai utafungua njia ya kupata wakati usio na mwisho ambao katika huo wanadamu waliokombolewa watapata kuona matendo mengine ambayo Mungu atafanya pasipo wao kufikia mwisho wake. Walakini twaweza kuwa na hakika kwamba kila mojawapo ya matendo haya yasiyofunuliwa bado litakuwa ‘zuri katika wakati wake.’ Lo! namna lilivyo zuri fungu la wakati ujao ambalo wanadamu wamewekewa!
Furahia Yale Anayotoa Mungu
Hivyo, basi, ni mwendo gani unaopendekezwa ambao mtu apaswa kufuata? Sulemani anapendekeza tufurahie maisha katika njia inayofaa tukipata mema katika kazi ngumu, mahali pa kujaribu bure kubadili yale ambayo Mungu ametupatia. Twasoma maneno haya yake: “Mimi najua ya kwamba hakuna jema kwao kupita kufurahi, na kufanya mema maadamu wanaishi. Tena ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote. Najua ya kwamba kila kazi aifanyayo Mungu itadumu milele; haiwezekani kuizidisha kitu, wala kupunguza kitu; nayo Mungu ameifanya ili watu wamche Yeye.”—Mhu. 3:12-14; 5:18.
Mambo ya wanadamu, kutia na kuzaliwa na kufa, yanatukia katika hali ambazo wanadamu hawawezi kugeuza. Maadamu jambo hili latimiza kusudi la Mungu litaendelea kuwa hivyo. Hivyo ilikuwa kwa habari ya kwamba kuna “wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu” kwamba Sulemani alisema hivi: “Najua kwamba kila kazi aifanyayo Mungu itadumu milele.” (Mhu. 3:14) Mwanadamu hawezi kufanya lo lote kuhusu hali ya mambo iliyopo duniani ama kwa kuruhusiwa na Mungu ama kwa kuongozwa naye. Kwa mfano, Mfalme Nebukadreza mwenye nguvu alilazimika kukubali hivi: “Watu wote wanaokaa duniani wamehesabiwa kuwa si kitu; naye hufanya kama atakavyo, katika jeshi la mbinguni, na katika hao wanaokaa duniani; wala hapana awezaye kuuzuia mkono wake, wala kumwuliza, Unafanya nini wewe?” (Dan. 4:35) Hakuna jitihada zo zote za kuzidisha kitu au kupunguza kitu zitafanikiwa, kwa kuwa mpango wote wa maisha duniani unaendelea kwa kuruhusiwa na Mungu na kwa kusudi lake. Uhakika wa kwamba kusudi lote la Mungu kuhusu jambo hili halifahamiki na wanadamu lapaswa kuwafanya wamwogope au wamche.
Wakati ule ule, historia ya wanadamu inaonyesha kwamba katika matukio ya duniani kuna mfuatano unaotokea tena na tena wa kuzaliwa na kufa, kucheka na kulia, na vivyo hivyo. Mfuatano huu unaotokea tena na tena unaunganisha wakati uliopita, wakati uliopo na wakati ujao. Hivyo, Sulemani aliweza kusema: “Yale yaliyoko yamekuwako; na hayo yatakayokuwako yamekwisha kuwako.” Walakini, maneno yake yanayofuata, hayafahamiki sawa-sawa. “Naye Mungu huyatafuta tena mambo yale yaliyopita.” (Mhu. 3:15) Hii yaweza kuonyesha uhakika wa kwamba mara nyingi wenye haki wanatafutwa na waovu. Mungu ‘hutafuta’ kuwafanyia watumishi wake wema, kwa kuwa yeye ana mamlaka juu ya wakati uliopita, wakati uliopo na wakati ujao, aweza kufanya maovu ya waovu yawaangukie naye aweza kuwafanyia hukumu ya haki wale wenye haki. Au, yaweza kumaanisha kwamba, ijapokuwa matukio yanayotukia tena na tena kwa mfuatano yanaendelea na yaelekea kwamba kwa kweli hakuna jambo jipya, hata hivyo, twaweza kuwa na hakika kwamba, Mungu anaendelea kutimiza kusudi lake jema. Hivyo, ijapokuwa huenda mwanadamu asiweze kuzuia hali fulani, sikuzote Aliye Juu Zaidi aweza kufanya mambo yatendeke kwa faida ya watumishi wake watiifu.
Jambo hili linafariji sana, kwa kuwa mtu hawezi kutazamia kwamba wanadamu watatoa hukumu ya haki katika kila jambo katika ulimwengu huu usiokamilika. Sulemani aliieleza sawasawa hali ilivyo: “Zaidi ya hayo, nikaona tena chini ya jua ya kwamba, mahali pa hukumu upo uovu, na mahali pa haki upo udhalimu.” (Mhu. 3:16) Kwa kufaa mtu anatazamia hukumu ya haki kutoka kwa baraza ya hukumu. Walakini rushwa na upendeleo huenda yakaenea, na kufanya watu wengi wasiweze kupata yaliyo haki yao. Udhalimu huu wote waweza kurekebishwaje? Sulemani anajibu hivi: “Mungu atawahukumu wenye haki na wasio haki; kwa kuwa kuna wakati huko kwa kila kusudi na kwa kila kazi.” (Mhu. 3:17) Kwa hiyo mahali pa kufadhaishwa na yale yanayotukia ulimwenguni, mtu mwenye hekima humngojea Mungu, ambaye atatenda katika wakati Wake uliowekwa akifanya hivyo kwa faida ya watu Wake waaminifu.—1 Sam. 26:7-10; Zab. 37:12, 13.