Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
Wamo Mikononi mwa Mungu
Ingawa alikuwa mwenye hekima sana, Mfalme Sulemani hangeweza kufahamu ukubwa kazi za Mungu—si mambo yale tu ambayo Aliye Juu Zaidi anafanya, bali vilevile yale anayoachilia yatendeke ili atimize kusudi lake kuu. Hata hivyo kuna kweli ya maana ambayo Sulemani ‘aliiweka moyoni’ baada ya kufanya uchunguzi wa uangalifu wa mambo ya wanadamu. Ilikuwa nini? “Wenye haki, na wenye hekima, pamoja na matendo yao yote, wamo mkononi mwa Mungu.”—Mhu. 9:1.
Ndiyo, kwa hali ya miili yao wenyewe na matendo yao, wenye haki na wenye hekima wamo mikononi au katika uwezo wa Aliye Juu Zaidi. Hata ingawa huenda akaruhusu misiba iwapate, bila shaka wao hawatapoteza zawadi yao. Yehova Mungu “awajua walio wake” na atafanya kazi zake zote ‘ziwafaidi wale wampendao.’ (Rum. 8:28; 2 Tim. 2:19) Hii inaweza kututia moyo na kutufariji tunapoona wenye haki wakitaabika wakati waovu wanasitawi.—Mhu. 8:14.
Wanachuo wa Biblia wa karne za karibuni wameshindwa kujua maana ya maneno ya Sulemani yanayofuata katika Mhubiri 9:1, (NW): “Wanadamu hawajui ama upendo au chuki yote iliyowatangulia.” Huenda ikawa kwamba maneno haya yaliandikwa kwa makusudi ili yaweze kufahamika katika njia mbalimbali. Kwa mfano, hii inaweza kufahamika ikiwa na maana kwamba, kwa kuwa mauti humaliza upendo na chuki za watu, wanaoishi hawajui ni upendo na chuki kiasi gani zilizokuwako kabla ya kuzaliwa kwao, yaani, maishani mwa watu walioishi kabla ya wakati wao.
Au, huenda ikawa kwamba maneno ya Sulemani yapaswa yaonwe katika njia iliyokwisha kutajwa ya Mungu kuwa na uwezo juu ya wenye haki na wenye hekima na kazi zao. Upendo na chuki zinazowapata wao pamoja na wengine wa wanadamu zinawapata kwa sababu Mungu anaziruhusu na kuziachilia. Vilevile, Aliye Juu Zaidi alijua zamani kabla wanadamu hawajazaliwa kwamba wangepatwa na upendo na chuki. Yeye aliruhusu jamii ya kibinadamu yenye dhambi ifokee, ikiwa na upendo na chuki zao. Baada ya uasi wa Adamu na Hawa, Yehova Mungu alisema: “Nami nitaweka uadui kati yako [nyoka wa zamani, Shetani Ibilisi] na huyo mwanamke [si Hawa, bali “mwanamke” wa Mungu (Gal. 4:26-31) ], na kati ya uzao wako na uzao wake.” (Mwa. 3:15) Kwa hiyo, hata ingawa ‘ama upendo au chuki havikuwa vitu visivyojulikana’ na Mungu hili lingekuwa jambo ambalo mwanadamu angejua kwa kupatwa nalo.
Tena, vilevile, maneno ya mwenye hekima katika Mhubiri 9:1 yaweza kuelezwa katika njia hii: Kati ya wanadamu wenye makosa maono ya upendo na chuki mara nyingi yanaonyeshwa bila sababu. Kwa hiyo wanadamu wanakosa ufahamu wa sababu za upendo wote na chuki zilizoonyeshwa kabla ya Wakati wao. Kwa kufahamu hivyo, maneno ya Sulemani yangepatana na mazungumzo yafuatayo juu ya kutokuwa na hakika ya maisha na kutotabirika ambako katika huko mauti inaweza kumaliza kila kitu. Upendo na chuki zinaweza kuwa bila sababu na zisizofahamika namna iyo hiyo.
Kwa sababu wanadamu ni wenye makosa, wawe wenye haki au waovu, huenda wakapatwa na mema na mabaya, yaani, upendo na chuki. Yehova Mungu anaruhusu wote wenye haki na waovu wajifurahishe chakula na vinywaji pamoja na mipango mingine yake ya ukarimu ya kuendeleza maisha. (Mt. 5:45; Matendo 14:16. 17) Zaidi ya hayo, kwa habari ya kufa, hakuna tofauti. Sulemani aliendelea: “Mambo yote yawatukia wote sawasawa; kuna tukio moja kwake mwenye haki na kwake asiye haki; kwa mtu mwema na kwa mtu mwovu; kwa mtu aliye safi na kwa mtu asiye safi; kwake yeye atoaye kafara na kwake asiyetoa kafara; kama alivyo huyo mwema ndivyo alivyo mwenye dhambi; yeye aapaye [kwa vyepesi au bila kufikiri] na yeye aogopaye kiapo.”—Mhu. 9:2.
Kwa kuwa huenda kusionekane tofauti kati ya yale yanayowapata wenye haki na waovu wakati wa maisha yao, na sana sana kwa sababu wote wanakufa, huenda ikaonekana kwamba hakuna faida yo yote ya kuishi maisha manyofu, ya kumwogopa Mungu. Sulemani alionyesha kwamba hii ndiyo sababu kufanya makosa kunaendelea kati ya wanadamu, akisema: “Baa hilo ni katika mambo yote yanayofanyika chini ya jua, ya kuwa wote wanalo tukio moja; naam, zaidi ya hayo, mioyo ya wanadamu imejaa maovu.”—Mhu. 9:3.
Lakini je! kuishi kwao katika uasi kunawafaidi? Hapana, kwa sababu mwenye hekima anasema hivi: “Wazimu umo mioyoni mwao wakati walipo hai, na baadaye huenda kwa wafu.” (Mhu. 9:3) Wanapokuwa hai wanatenda kama kwamba wana wazimu, wakizifuata tamaa zao mbaya na maelekeo mabaya bila kujizuia. Mwishowe, maisha yao ya kujifurahisha na tamaa yanaisha kwa ghafula katika mauti. Hivyo basi, mwendo ulio wa hekima kweli kweli ni gani?
Furahia Maisha Yako katika Njia Inayofaa
Mtu anapaswa kuthamini maisha na kuyatumia vizuri. Sulemani aliandika hivi: “Kwa kuwa liko tumaini kwa yule aliyeambatana na wote walio hai, (maana ni afadhali mbwa aliye hai kuliko simba aliyekufa); kwa sababu walio hai wanajua ya kwamba watakufa [wazo lenye kuamsha fikira ambalo lapaswa kuwasukuma watumie maisha zao katika njia inayofaa]; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena, maana kumbukumbu lao limesahauliwa. Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja; wala hawana sehemu tena katika jambo lo lote lililofanyika chini ya jua.”—Mhu. 9:4-6.
Wakati mtu angali hai ndipo tu kunapoweza kuwa na tumaini. Huo ndio wakati wa kujifanyia jina zuri pamoja na Muumba. Kunapokuwa na uhai, tumaini linaendelea kwamba mambo huenda yakabadilika yawe mema, hata kwa habari ya yule anayeendelea na uasi. Mauti itokeapo inakuwa ni kuchelewa mno. Kwa hiyo, mbwa aliye hai, hata adharauliwe, ni afadhali kuliko simba aliyekufa, ambaye ndiye mfalme wa wanyama. Walio hai bado wanaweza kufanya mambo, lakini wafu hawana sehemu katika utendaji wo wote au katika maono ya upendo, chuki na husuda ambayo ni sehemu kubwa ya maisha ya kidunia ya mwanadamu.
Kwa hiyo, tunapaswa kufurahia kazi za mikono yetu kama watu wanaomwogopa Mungu. Sulemani anashauri hivi: “Wewe nenda zako, ule chakula chako kwa furaha, unywe mvinyo yako kwa moyo wa kuchangamka; kwa kuwa Mungu amekwisha kuzikubali kazi zako. Mavazi yako na yawe meupe sikuzote [yenye kung’aa na safi, yakionyesha, furaha, wala si kilio au huzuni]; wala kichwa chako kisikose marahamu [mafuta, vilevile yakionyesha furaha, kwa kuwa mafuta yanatuliza na kuburudisha]. Uishi kwa furaha pamoja na mke umpendaye, siku zote za maisha yako ya ubatili, ulizopewa chini ya jua; siku zote za ubatili ulizotaabika chini ya jua. Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako, kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu uendako wewe.”—Mhu. 9:7-10.
Kufurahia maisha katika njia inayofaa, kutia na kula na kunywa, ni jambo linalofaa. Ni zawadi ya Mungu, na kwa hiyo, ina kibali yake. Bila shaka hivyo ndivyo alivyomaanisha Sulemani aliposema maneno haya baada ya kuwatia watu moyo wafurahie chakula na vinywaji, “kwa kuwa Mungu amekwisha kuzikubali kazi zako.” Ndiyo, Aliye Juu Zaidi hataki tuishi maisha ya kujinyima mambo kupita kiasi, tukijinyima furaha yote. Kwa kuwa yeye ni Mungu mwenye furaha, yeye anataka watu wawe wenye furaha katika maisha ya kila siku, kutia na maisha yao ya ndoa. (Matendo 14:17) Hii, bila shaka haiungi mkono maisha ya kujifurahisha kupita kiasi na kutafuta anasa tu. Sulemani alifia watu moyo wafanye kazi, watumie vizuri nafasi za kutumia mikono yao wafanye mema kabla mtu hajaondolewa uwezo wote na mauti na kuingia katika Sheol, kaburini.
Kwa hiyo, mwendo ulio wa hekima katika ulimwengu huu ni mtu afurahie maisha wakati awezapo, akifanya hivyo kupatana na sheria za Mungu za mwenendo wa adili. Mauti kumaliza kila kitu kwa haraka sana kwa sababu mara nyingi jambo lisilotazamiwa linatukia. Mwenda mbio mwenye mbio sana huenda akajikwaa akose kushinda mbio. Jeshi lenye nguvu huenda likashindwa vita na jeshi lisilo na nguvu sana. Mtu mwenye hekima huenda akakosa kazi nzuri na kwa sababu hiyo apatwe na njaa. Watu wenye ufahamu mzuri sana wa kusimamia mambo ya biashara huenda wakakosa kutumia ufahamu kwa sababu ya hali fulani na kwa sababu hiyo waingie katika hali ya ufukara. Watu wenye maarifu huenda wakaghadhibikiwa na wenye mamlaka wakakosa kibali. Hili ni jambo ambalo Sulemani aliona kwa kupitia tu, walakini, baada ya kulifikiria kwa uangalifu, aliandika hivi: “Nikarudi ili nione chini ya jua kwamba wenye mbio hawashindi mashindano ya kukimbia, wala walio hodari kushinda vita, wala wenye ufahamu pia hawana mali, wala hata walio na maarifa hawana kibali; kwa sababu wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote. Kwa kuwa pia mwanadamu hajui wakati wake [kwa sababu mauti huenda ikaja bila kutazamiwa]. Kama samaki wanaokamatwa katika wavu mwovu, na kama ndege wanaokamatwa katika mtego, ndivyo wanadamu wenyewe wanavyonaswa wakati wa msiba, unapowapata ghafula.”—Mhu. 9:11, 12, NW.
Kwa hiyo, kama vile samaki wanavyoweza kukamatwa katika wavu na ndege katika mtego, mauti inaweza kuwapata wanadamu ghafula, bila onyo. Ni somo lenye nguvu namna gani alilolitoa Sulemani juu ya kupata furaha inayofaa na yenye kuthawabisha (kutoa zawadi) kutokana na maisha pamoja na faida zake za kweli na nafasi zilizomo wakati tunapoweza!