Mwenye Hekima Alikuwa na Maana Gani?
Hakuna Kuruhusiwa Kuondoka katika Vita ya Mauti
Kuna vita ambayo katika hiyo mwanadamu hawezi kuruhusiwa kuondoka. Mfalme Sulemani aliandika juu ya habari hiyo hivi: “Hakuna mwenye uwezo juu ya roho [nguvu ya uzima] aizuie roho; wala hana mamlaka juu ya siku ya kufa; wala hakuna kuruhusiwa katika vita vile; wala uovu hautamwokoa yule aliyeuzoea.”—Mhu. 8:8.
Wakati wa kufa mwanadamu anakuwa hoi (hana nguvu). Hata ajaribu namna gani, hawezi kuizuia roho ili nguvu ya uzima iendelee katika chembe za mwili wake, azidi kuishi. Wanadamu wanaokufa hawana mamlaka juu ya siku ya kufa. Hakuna bidii za kibinadamu zinazoweza kumwondoa mtu katika vita ambayo “Mauti” inapiga juu ya wote. (Rum. 5:14) Hakuna hata uwezekano wa kupanga kuwe na mtu mwingine wa kumwokoa na mauti. Mtunga zaburi aliyeongozwa na Mungu alitangaza hivi: “Hakuna mtu awezaye kumkomboa ndugu yake, wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake, (maana fidia ya nafsi zao ina gharama, wala hana budi kuiacha hata milele); ili aishi sikuzote asilione kaburi.” (Zab. 49:7-9) Huenda wakati wa kuishi kwao watu wabaya wakaweza kuepuka adhabu kwa njia za ujanja na za hila. Walakini, hakuna shauri, hakuna mpango, hakupa njia inayoweza kuwaepusha na mauti.
Kuvumilia Yale ambayo Mtu Anaona katika Ulimwengu Mwovu
Kuna mambo mengi yanayoonwa katika taratibu hii mbaya yanayoweza kutuhangaisha sana. Huenda watu wabaya wakafanikiwa, na huku wenye haki wakipata taabu. Twawezaje kuzuia mambo hayo yasitutie uchungu?
Akitegemea uchunguzi wake wa uangalifu, Mfalme Sulemani alitoa maoni yenye kufaa, akisema kwa kuandika hivi: “Kwa sababu hukumu juu ya tendo baya haitekelezwi upesi, mioyo ya wanadamu huthibitishwa ndani yao ili kutenda mabaya. Ajapokuwa mwenye dhambi amefanya maovu mara mia, akazidisha siku zake; lakini hata hivyo najua hakika ya kwamba itakuwa heri kwao wamchao Mungu, wenye kicho mbele zake; walakini haitakuwa heri kwa mwovu, wala hatazidisha siku zake, zilizo kama kivuli; kwa sababu hana kicho mbele za Mungu.”—Mhu. 8:11-13.
Kama Sulemani anavyoeleza hapa, huenda hukumu za wanadamu zikakawia na baraza za kibinadamu za kuhukumu zikachukua muda mrefu au hata zikaachilia mbali kutekeleza adhabu juu ya matendo mabaya. Kwa sababu waovu hawaadhibiwi kwa uvunjaji wao wa sheria, huenda wakadhani kwamba hawataadhibiwa hata kidogo na kwa hiyo waimarike sana katika njia zao mbaya. Lakini ubaya wao hauleti zawadi yo yote. Uzima wao unapita mbio “kama kivuli,” na hakuna mpango wao unaoweza kurefusha uzima wao. Kwa upande mwingine, wenye haki hawataendelea kupata taabu. Ni kweli kwamba huenda wengine wakawafanyia mbaya. Hata hivyo, mtu anayemwogopa Muumba ana faida. Mwenye haki anatunza dhamiri safi, anafurahia kufanya anayojua kuwa mema, na akifa akiwa mtumishi anayekubaliwa na Mungu, analo tumaini la kufufuliwa katika wafu. Basi mwishowe, kila kitu ‘kinakuwa heri’ kwa wale wanaomwogopa Yehova Mungu,
Akiwa na tumaini hakika kwamba Aliye Juu Zaidi atawalipa wale wanaomwogopa, mtu hataona uchungu akipatwa na yale ambayo Sulemani anaendelea kueleza: “Kuna ubatili unaofanyika juu ya nchi; kwamba wako wenye haki, nao wapatilizwa kama kwa kazi yao waovu; tena wako waovu, nao wapatilizwa kama kwa kazi yao wenye haki. Nami nikasema ya kuwa hayo nayo ni ubatili.” (Mhu. 8:14) Yehova Mungu hawezi kulaumiwa kwa udhalimu huo. Ni “ubatili unaofanyika juu ya nchi”—jambo ambalo wanadamu wenye makosa wanafanya. Mara nyingine inakuwa hivyo kwa sababu ya uovu wa serikali, mara nyingine ni kwa sababu ya kutojua au kutothamini kanuni njema za Mungu zilizoandikwa katika Neno lake.
Mtu anayemwogopa Mungu haruhusu maovu ya ulimwengu yaharibu furaha yake ya maisha. Yeye anafahamu kwamba hawezi kugeuza kitu ambacho mpaka sasa Mungu ameruhusu kati ya wanadamu, naye anafuata maneno ya Sulemani: “Kisha nikaisifu furaha, kwa sababu mwanadamu hana neno lo lote lililo jema chini ya jua, kuliko kula, na kunywa, na kucheka; na ya kuwa hilo likae naye katika amali yake, siku zote za maisha yake alizompa Mungu chini ya jua.” (Mhu. 8:15) Ndiyo, mwendo ulio bora katika maisha ni kuendelea kumwogopa Mungu vya kufaa huku ukifurahia kazi na kufurahia kula na kunywa. Ikiwa mtu anasumbuka na kuhangaika kwa sababu ya mabaya yote yaliyomo katika taratibu hii, anaweza kuvunjika moyo na kukosa furaha ya maisha. Anaweza kuharibu hali yake ya kiroho na furaha yake mwenyewe. Kuhangaika wala kunung’unika hakutaharakisha faraja itakayokuja kwa njia ya kuondoa taratibu ya sasa na kuweka taratibu mpya yenye haki mahali pake.—Zab. 37:5-7.
Zaidi ya hayo, hakuna faida katika kujaribu kuvumbua kanuni au njia fulani ya kueleza sababu gani mambo yanatendeka hivyo katika ulimwengu huu. Zamani sana Mfalme Sulemani pamoja na wengine walichunguza mambo ya wanadamu kwa uangalifu. Hata hivyo hawakuweza kuvumbua kanuni ya kusaidia kujua jambo la kutazamia katika kila hali. Sulemani alieleza hivi: “Mimi nilipotia moyo wangu katika kuijua hekima, na kuuona utumishi uliofanyika juu ya nchi; (maana kuna asiyepata usingizi kwa macho yake mchana wala usiku); basi, niliiona kazi yote ya Mungu, ya kuwa haitafutikani na mwanadamu kazi inayofanyika chini ya jua; kwa sababu mwanadamu na akijisumbua kadiri awezavyo kuitafuta, hata hivyo hataiona; naam, zaidi ya hayo, mwenye hekima ajapodhania ya kuwa ataijua, lakini yeye hataweza kuiona.”—Mhu. 8:16, 17.
Kumbuka kwamba Sulemani alitaja mambo yanayotendeka kati ya wanadamu kama “kazi yote ya Mungu.” Hilo laweza kusema hivyo kwa sababu kila jambo linatukia kwa ruhusa yake, lakini si kwa sababu Mungu anaanzisha, kuunga mkono au kukubali yote yanayotendeka. Hata mtu ajinyime usingizi, hataweza kufahamu kabisa mambo ambayo Mungu anafanya na kuruhusu ili mwishowe atimize kusudi lake kuu. Hiyo ndiyo maana inayotolewa na tafsiri ya Moffatt ya maneno ya Mfalme Sulemani: “Nilipotoa akili zangu ili nijifunze hekima, nijifunze maisha yote ya ulimwengu yenye shughuli, nikaona kwamba mwanadamu hawezi kuifahamu kweli ya mambo yote ambayo Mungu anafanya katika ulimwengu huu; huenda akafanya bidii sana ili aipate, akiitafuta mchana na usiku bila kulala usingizi, lakini hataijua kamwe; huenda mwenye hekima akadhani anavumbua siri, lakini hata hivyo hataijua kamwe.” —Mhu. 8:16, 17.