Afya Yetu ya Kiroho na “Figo”
1. Kwa sababu gani tunafurahi figo zetu zinapofanya Kazi vizuri?
AFYA nzuri ya kimwili inategemea sana hali ya figo zetu. Kadiri tunavyoendelea kuishi ndivyo tunavyoendelea kufahamu hivyo. Tunaweza kujua kwamba tuna figo katika miili yetu wakati zikataapo kufanya kazi vizuri na kutuuma sana kwa sababu mbalimbali. Tunaweza kutatizwa kusimama na kutembea wima. Hata hivyo tusingependa kuharibikiwa na yo yote ya figo zetu, maana tunataka miili yetu iwe na afya bora. Figo mojawapo au zote mbili zikiumia au kuharibika tutakufa. Tuna furaha sana kwa kuwa na figo zote mbili na kuzifanya ziendelee kufanya kazi vizuri.
2. Kwa kawaida ni kwa sababu gani inafaa kuchunguzwa figo, nayo Biblia inasema zinaleta afya gani?
2 Kwa kawaida, tukimwendea daktari anaweza kutuchunguza sana aone jinsi figo zetu zinavyoendelea kufanya kazi. Zinasaidia sana kufanya mwili uwe na hali njema, kwa hiyo zinahitaji kuchunguzwa zionekane jinsi zinavyofanya kazi. Figo zimekuwa zikichunguzwa tangu madaktari walipojua jinsi mwili wa kibinadamu ulivyo. Zamani za kale mfalme mmoja mwenye kufikiria mambo ya kisayansi aliandika mithali kadha zenye hekima. Basi, ni wazi kwamba ilifaa ataje habari za moyo, ini, figo na mifupa. Kwa hekima alisema hivi: “Moyo mtulivu ndio uhai wa mwili, lakini wivu ni kuoza kwa mifupa.” (Mit. 14:30, NW) Vilevile anasema kwamba mtu anaweza kuona furaha katika figo. (Mit. 23:16, NW) Hapo kale sana ilisemwa kwamba figo zinatuletea hali njema, ya kimwili na ya kiroho pia. Afya ya mtu ya kiroho ndiyo ya maana zaidi. Inastahili kulindwa.
3. Ni ajabu gani ya mwili wa kibinadamu ambayo mtunga zaburi alitaja katika Zaburi 139:12-14 akimthamini Muumba wake?
3 Figo ni mojawapo maajabu yaliyo katika mwili wa kibinadamu. Zilitajwa kwa njia ya pekee katika wimbo uliotungwa na Mfalme Daudi wa Yerusalemu. Akimthamini Muumba wake aliendelea kusema hivi: “Hata giza lenyewe halikuwa jeusi mno kwako, lakini usiku wenyewe ulikuwa uking’aa kama mchana; hata giza laweza kuwa sawasawa na nuru. Kwa maana wewe mwenyewe ndiwe uliyefanya figo zangu; uliniweka nikiwa nimefichwa katika tumbo la mama yangu. Mimi nitakuhimidi kwa sababu kwa njia ya kutisha nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu. Kazi zako ni za ajabu, kama nafsi yangu ijuavyo sana.”—Zab. 139:12-14, NW.
4. Hapo mtunga zaburi Daudi alizitaja figo akitaka kueleza jambo gani?
4 Sasa, basi, kwa sababu gani Mfalme Daudi akazitaja figo waziwazi? Alitaka kueleza wazi jambo alilokuwa akisema. Alikuwa akionyesha jinsi roho na macho ya Mungu yanavyoweza kuona sana, hata kuona ndani ya Sheoli, kaburi la kawaida la wanadamu. Mungu anaweza kuchungulia ndani kabisa ya mwili wa kibinadamu, naam, ndani mpaka mahali ziliko figo, yaani, chini ya moyo na kiwambo chake (diaphragm) na karibu na sehemu ya chini ya uti wa mgongo. Tena wakati Mungu alipokiumba kiini cha mimba na kukiweka kikiwa kimefichwa katika tumbo la mama ya Daudi, aliweza kuona ndani sana mahali ambamo viungo hivyo vilikuwa. Hakuna kilichomzuia macho wala hakuna kilichozuia lengo la roho yake ya uumbaji. Akionyesha kwamba viungo hivyo vinavyoshtuka upesi vimo ndani sana ya mwili, Ayubu mzee wa ukoo mwenye taabu nyingi alisema hivi: “Figo zangu zimeacha kufanya kazi ndani-ndani mwangu [au, kwa njia halisi, “ndani ya kifua changu”].”—Ayubu 19:27; NW; Leeser.
5. (a) Inaonyeshwaje zaidi kwamba figo zimo ndani sana mahali ambamo haziwezi kuonekana kwa macho ya kibinadamu? (b) Kwa sababu gani figo zilikuwa sehemu ya maana sana katika dhabihu alizotolewa Mungu zamani za kale?
5 Vilevile, na tukumbuke kwamba figo zimo katika kifuko cha mafuta chenye unene wa nusu inchi au zaidi, ikitegemea ukubwa wa mtu. Hiyo inaendelea kuonyesha kwamba viungo hivyo vimo ndani sana, naam, ndani sana mahali ambamo haviwezi kuonekana kwa macho ya kibinadamu. Kwa sababu ya figo kufunikwa na kifuko kinene hivyo cha mafuta, zilikuwa sehemu ya pekee, yenye thamani nyingi, ya dhabihu za wanyama ambazo watu wa Yehova walimtolea hapo kale. Kwa mfano, kwa habari ya dhabihu za wanyama zilizotolewa na Habili ndugu ya Kaini, zinazosemekana ndizo za kwanza alizotolewa Mungu, inatajwa kwamba ‘alileta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona.’ (Mwa. 4:4) Inaelekea kwamba figo zilikuwa kati ya sehemu hizo. Vilevile, kwa habari ya dhabihu ambazo Waisraeli walipaswa kumtolea Yehova, tunasoma mara nyingi kwamba Yehova alipewa “figo zake mbili, na mafuta yaliyoshikamana nazo.” (Law. 3:4, 10, 15; 4:9; 7:4; 8:16) Mafuta ya figo yalichomeka vizuri na kutoa harufu yenye kupendeza. Kwa hiyo figo zilikuwa sehemu ya maana sana ya dhabihu alizotolewa Mungu.
6. Ni viungo gani vinavyozugumzwa hapa vinavyoweza kuwamo katika dhabihu ya Kikristo inayotajwa katika Warumi 12:1?
6 Katika Warumi 12:1 mtume Paulo anawaambia Wakristo waliokuwa wameonyeshwa huruma nyingi na Mungu hivi: “Itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu.” Figo na moyo zinaweza pia kuwa katika dhabihu hiyo. Ingewafaa Wakristo hao kutumia moyo na figo zao katika utumishi wa Mungu.
MOYO NA FIGO ZINAHUSIANISHWA KWA NJIA YA KIROHO
7, 8. Mambo yanayofanywa na figo yanakuwa na matokeo gani juu ya moyo?
7 Katika Maandiko Matakatifu moyo na figo zinahusianishwa (zinatajwa pamoja) kwa ukawaida. Hiyo inaonyesha kwamba katika mwili wa kibinadamu viungo hivyo vinahusiana.
8 Utendaji wa figo unaweza kuonyesha kama moyo unafanya kazi vizuri, maana figo zinaonyesha kama damu haizunguki vizuri sana. Tunajua kwamba figo zinasaidia sana kuiweka damu katika hali ya kutakata, ya usafi, kwa maana hivyo ni viungo vya kuondoa taka. Tunapopata mikazo moyoni na kujisikia vibaya, figo nazo zinafanya kazi yake, maana zinatengeneza hormones (vitu vya umajimaji) zinazopunguza ukubwa au nafasi ya ndani ya mishipa ya damu. Halafu mishipa ya damu inazidi kukazika na kufanya moyo ufanye kazi kwa nguvu zaidi. Biblia inahusianisha moyo na figo kwa njia ya kiroho pia.
9. Yehova anachunguza figo zetu akiwa nini, nayo matokeo ya uchunguzi huo yanahusu mataraja (matumaini) gani ya uzima?
9 Mfano mmoja ni Yeremia 17:10 (NW). Mstari huo unasema hivi: “Mimi, Yehova, naupekua moyo, nikizichunguza figo, hata nimpe kila mtu kulingana na njia zake, kulingana na matunda ya matendo yake.” Yehova hafanyi uchunguzi wake kama vile daktari anavyofanya, bali anaufanya ili kutoa hukumu. Yeye hatazami aone kama viungo hivyo vya mwili ni safi kwa njia halisi, bali aone kama vina usafi wa tabia na wa kiroho. Hiyo ndiyo maana inayoonyeshwa katika Zaburi 7:9 (NW), tunaposoma hivi: “Mungu akiwa ni mwenye haki anaujaribu moyo na figo.” Kama vile uzima wetu wa kimwili unavyotegemea sana hali ya figo zetu, ndivyo uzima wetu wa milele katika makao ya Mungu yanayokuja, yenye haki, amani na afya kamili ya kimwili, unavyotegemea hali ambayo Mungu kama Mwamuzi anasema tunayo katika moyo na figo zetu. Atampa kila mmoja wetu nini kulingana na njia zetu za maisha? Atakuta matunda ya matendo yetu yakiwa namna gani, ili kuona kama atatupa kinachofaa, tunachokistahili? Je! tutapewa uharibifu au uzima wa milele?
10. Yeremia alimlinganisha Yehova na nini wakati Yeye alipokuwa adui ya Israeli, nalo jeraha la figo lingetokeza nini?
10 Hatutaki Yehova Mungu awe adui yetu. (Yak. 4:4; Isa. 63:10) Alipata kuwa adui ya Israeli wa kale. Ndipo nabii Yeremia alipoandika kama kwamba akiwakilisha taifa zima la Israeli, wakati Yerusalemu ulipoharibiwa na majeshi ya Babeli mwaka 607 K.W.K. Alimfananisha Yehova na mpiga upinde (uta) vitani na kusema: “Ameukanyaga upinde wake [autumie], naye aniweka juu niwe shabaha kwa mshale. Yeye ameingiza katika figo zangu wana wa podo lake [kwa kuitupa mishale].” (Omb. 3:12, 13, NW) Wakati mtu mwenye kutoroka alipotupiwa mishale ikajichomeka ndani sana katika figo, mtu huyo alikufa tu. Jeraha hilo baya sana la watu waliowakilishwa na Yeremia lilionyesha kwamba ufalme wa Yuda uliokuwa taifa lenye kujitegemea, lenye mfalme wa ukoo wa Daudi Yerusalemu, ungekufa. Loooo!
11. Ili kuepuka mishale ya Yehova katika “dhiki kubwa” inayokuja, inatupasa tufikirie bila mchezo uchunguzi anaofanya katika sehemu gani yetu?
11 Sasa tunaishi katika “siku za mwisho” za Jumuiya ya Wakristo, iliyofananishwa na Yerusalemu usio mwaminifu na ufalme wa Yuda wa nyakati hizo za kale.Ili sisi sasa tuiepuke mishale ya Yehova ya mfano katika “dhiki kubwa” inayokuja, lazima tuzitii “figo” zetu. Lazima tuufikirie bila mchezo uchunguzi ambao Mchunguzi Yehova anafanya juu ya viungo hivyo vinavyohitajiwa kabisa. Anatuona tukiwa na tabia na hali gani ya kiroho mle ndani kabisa, katika figo za mfano? Ni hali mbaya au ni hali inayoonyesha tunafaa kupata uzima wa milele? Tunataka kuyafanya makao hayo ya mfano, yanayoonyesha jinsi tulivyo hasa, yaendelee kufanya kazi kwa njia nzuri. Ili kufanya hivyo, tunahitaji kuangalia mambo tunayokula na kunywa. Vivyo hivyo na figo halisi. Jambo hilo linahusika kwa njia ya kiroho pia.
12, 13. (a) Ni kitu gani kimoja kinachonywewa na kundi la Kikristo, nalo linapata matokeo gani? (b) Mtume Petro aliwatia moyo Wakristo wa Asia Ndogo watamani kinywaji gani?
12 Katika 1 Wakorintho 12:13 tunasoma hivi: “Kwa maana katika [roho moja] sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa tu watumwa au ikiwa tu huru; nasi sote tulinyweshwa [roho moja].”
13 Hiyo ‘roho moja’ ni roho ya Mungu. Tunatiwa moyo tuiombe tupewe kadiri tunavyoihitaji. (Luka 11:13) Washiriki wote wa kundi la Kikristo wainywapo hiyo ‘roho moja,’ inadumisha mapatano na umoja wa kundi lililo chini ya ukichwa wa Yesu Kristo. Inatuburudisha kama kinywaji. (Rum. 12:11) Mtume Petro aliwaandikia Wakristo katika Asia Ndogo akawaambia: “Kama watoto wachanga waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili yasiyoghoshiwa, ili kwa hayo mpate kuukulia wokovu.” (1 Pet. 2:2) Baadaye, bila shaka watoto wenye kukua wanaachishwa maziwa na kuanza kula chakula kigumu.—Ebr. 5:14.
14. Ili tupate uzima wa milele, lazima tukue tufikie nini na kwa njia gani?
14 Ili tupate wokovu wa milele lazima tukue hata tukomae Kikristo, tufikie utu mzima. Basi lazima tujilishe Neno la Mungu kwa ujumla, wala tusile mafundisho ya Biblia ya msingi tu. Lazima tujilishe mafundisho yake magumu, mashauri yake, maonyo yake ya upole na maagizo inayowapa Wakristo ambao wamekuwa watu wazima. Hapo tutafaidika katika utu wetu wote wa Kikristo. Mfalme Daudi aliyataja mashauri hayo ya kimungu alipoandika hivi: “Kamba za kupima zimeanguka kwa ajili yangu katika mahali pengi papende zapo. Hakika, mali yangu mwenyewe [kati ya kamba hizo za kupimia] imekuwa yenye kunipendeza. Mimi nitamhimidi Yehova, ambaye amenipa mashauri. Hakika, nyakati za usiku figo zangu zimenisahihisha.”—Zab. 16:6, 7, NW.
15. “Mashauri” ya Yehova yalimwingia Daudi mpaka wapi, kwa hiyo ni vitu gani vilivyosemwa kuwa vilimsahihisha makosa yake nyakati za usiku?
15 Hapo tunaona kwamba mtunga zaburi Daudi anaupita moyo na kuzitaja figo, ambazo ziko chini zaidi ya moyo. Figo halisi sizo zilizomsahihisha Daudi. Bali “mashauri” aliyopewa na Mungu ndiyo yaliyomsahihisha. Lakini “mashauri” hayo ya kimungu yaliingia katika sehemu za ndani-ndani kabisa za utu wa Daudi mwabudu wa Yehova. Kwa kuwa “mashauri” hayo yaliingizwa sana ndani yake, yangebaki humo bila shaka. Kwa kuwa yalikuwa yamemwingia sana Daudi na kukazika kikiki, bila shaka yangedumu katika utu wake. Yasingeweza kung’olewa na wanadamu wale wengine.
16. Kwa sababu gani Daudi angeweza kusahihishwa hivyo ‘’nyakati za usiku,” na kwa njia gani?
16 Kwa sababu “mashauri” hayo yalikuwa yamekaa ndani sana, yalihusianishwa na “figo.” Katika maana hiyo, figo zingeweza kumsahihisha Daudi, kumkaripia, kumwonyesha njia iliyo nzuri zaidi au kumpa jibu sahihi. Nyakati za usiku alipokuwa macho kitandani mwake, angeweza kusahihishwa kwa njia hiyo, kwa maana alikuwa peke yake bila kitu cha kumsumbua mawazo yake, nayo roho ya Mungu ingeweza kumkumbusha “mashauri” ambayo Yehova alikuwa amempa wakati wa mchana. Kwa njia hiyo Daudi alijichunguza vizuri, ili kuona jinsi alivyokuwa hasa.
17. Figo zinafananisha makao ya nini, kwa hiyo Yehova anaona nini anapoyachungulia makao hayo?
17 Hivyo, kama vile “moyo” unavyofananisha makao ya utendaji na ya kuthamini mambo, ndivyo “figo” zinavyofananisha makao ya kitu fulani cha mtu mwenyewe. Kitu gani? Zinafananisha utu wa kweli wa mtu. Utu wa ndani wa mtu unaongoza makusudi yake. Wakati Mungu anapochungulia hayo makao ya utu, anaona jinsi mtu alivyo kabisa katika maoni yake makuu. Kwa hiyo “figo” zinakuwa na matokeo fulani juu ya “moyo,” hata kwa njia ya mfano. Tunafaidi afya yetu ya kiroho kwa kutumia “mashauri” ya Yehova. Tunatakaswa barabara.
18, 19. (a) Kwa sababu gani huenda tukaonekana kuwa hivi machoni pa wanadamu lakini tuonekane kuwa vingine machoni pa Mungu? (b) Ni kwa njia gani Yehova alivyokuwa mbali sana na figo za watu fulani waliokuwa karibu naye kwa vinywa vyao?
18 Huenda machoni pa wanadamu tukaonekana kuwa hivi, lakini katika macho ya Mungu yanayotuona ndani mpaka mle chini kabisa, tunaonekana vingine kabisa. Nyakati zote si mali wala cheo kinachoonyesha kwamba mtu ana uhusiano mzuri wa kukaribiana sana na Mungu. Tusipojiangalia, tunaweza kupangwa pamoja na Waisraeli wale walioonekana kupendelewa na kuungwa mkono na Mungu, lakini kwa ndani wakawa wametengana naye. Kwa habari ya watu hao, Yeremia 12:2 (NW) inasema hivi: “Wewe [Mungu] umewapanda; wametia mizizi pia. Wanaendelea kusonga mbele; wamezaa matunda pia. Wewe u karibu katika kinywa chao, lakini u mbali sana na figo zao.”
19 Kwa hiyo, wakati mambo yanapowaendea watu wa namna hiyo kwa uzuri na kwa njia ya kupendeza, hapo huenda wakamtaja-taja Mungu na Neno lake katika vinywa vyao. Lakini, humo ndani yao hawana uhusiano wa karibu na Mungu. Hawana uhusiano halisi naye katika maisha yao ya ndani. Yeye ‘yuko mbali sana na figo zao.’ “Mashauri” yake hayajakwama kabisa ndani yao. Kwa hiyo, wanapotesa Wakristo, “figo” zao haziwasahihishi makosa yao!
UCHUNGUZI NA MAELEZO SAHIHI YA KIDAKTARI
20. Badala ya kuacha mioyo yetu ilionee uchungu tengenezo la Mungu, inatupasa tuache figo zetu zifanye nini?
20 Basi, waacheni wanafiki wote wa kidini wapate ufanisi wa mali na kujulikana na watu wengi maadamu Mungu ameruhusu iwe hivyo. Sisi tusione kamwe kijicho juu ya ufanisi wao na maendeleo yao ya kusonga mbele katika ulimwengu huu. Sisi tunathamini zaidi mambo ya kiroho, mambo yaliyo ya maana zaidi kwa Mungu, yanayoleta upendeleo na kibali yake. Zamani za kale mtunga zaburi aliyeitwa Asafu, aliyekuwa mwimbaji wa hekalu, aliwaza isivyofaa. Alidanganyika alipoona sura za nje za vitu kisha akawa na umaskini wa kiroho. Alisema: “Moyo wangu uliona uchungu na katika figo zangu nikaona maumivu makali, nami sikuwa nikifikiri vizuri wala nisingeweza kujua; nikawa kama wanyama tu kwa maoni yako.” (Zab. 73:21, 22, NW) Badala ya kuona maumivu makali ndani yetu, ni afadhali kuacha figo zetu zitusahihishe makosa. Hatutaki mioyo yetu ilionee uchungu tengenezo la Mungu lionekanalo kama kwamba mioyo yenyewe imeharibika. Hatutaki kuwa kama wanyama wasio na akili kwa maoni ya Mungu.
21. Kulingana na 1 Petro 4:17 na Ufunuo 2:23, sasa sisi Wakristo tunachunguzwa na nani?
21 Na tukumbuke hivi: Sasa tunachunguzwa kwa njia ya pekee. Tangu kundi la Kikristo lilipozaliwa katika sikukuu ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., wakati ambao lilianza kuinywa ‘roho moja’ (yaani, roho ya Mungu iliyomiminwa), nyakati zote tumekuwa tukichunguzwa sana na Yehova. (1 Pet. 4:17) Sasa tunachunguzwa pia na kichwa kilichowekwa cha kundi la Kikristo, Yesu Kristo. Kati ya ujumbe mbalimbali aliopelekea makundi saba ya Asia Ndogo yaliyotajwa kwa majina, Yesu Kristo aliyetukuzwa alitoa onyo hili: “Makundi yote yatajua kwamba mimi ndiye yule apekuaye figo na mioyo, nami nitawapa ninyi mmoja mmoja kulingana na matendo yenu.”—Ufu. 2:23, NW.
22. (a) Kwa kuwa macho ya Yesu ni kama “mwali wa moto,” hiyo inatuonyesha nini? (b) Tunakuwa na uhakika gani wakati tunapochunguzwa na Yehova na Yesu Kristo, kwa hiyo tunatiwa moyo tufanye nini?
22 Tusisahau jambo hili: Yesu Kristo aliyetukuzwa anatupekua sasa tangu moyoni mpaka mle chini mwenye figo. Katika Ufunuo 2:18 anasema kwamba macho yake ni “kama mwali wa moto,” kuonyesha kwamba macho yake yanang’aa sana, na kuona ndani sana. Kwa njia hiyo yeye yu kama Yehova Mungu, ‘anayepekua moyo na kuzichunguza figo.’ (Yer. 17:10, NW) Basi tunajua kwamba hukumu ya haki itafanywa kwa ajili ya wote wale wanaomfunulia Yehova Mungu kesi yao: “Yehova wa majeshi anahukumu kwa haki; anazichunguza figo na moyo.” (Yer. 11:20, NW) Kwa hiyo, tukichunguza makusudi yetu ya moyo na kuona jinsi utu wetu wa Kikristo ulivyo hasa, tunaweza kupiga moyo konde na kumfunulia Yehova “jinsi kesi yetu ilivyo” kisha tumngoje Mwenye Haki huyo atutetee kwamba tu wenye haki.
23. Tunataka nani atutetee kwamba tu wenye haki, na wakati gani?
23 Bila shaka, hatutaki kufanya jambo la maana zaidi liwe kujionyesha kuwa wenye haki. Badala ya kufanya hivyo, sisi kama Ayubu tunamtaka Yehova Mwamuzi mwenye haki ndiye atutetee kwamba tu wenye haki. (Ayubu 19:25-27) Lakini baada ya kujichunguza sana, sana, tukisadiki kwamba hatuna hatia kulingana na Neno la Mungu, tunaweza kumfunulia “jinsi kesi yetu ilivyo” na kuingoja “siku ya kisasi” chake ije. Tukiungama makosa yetu yote, hapo tunaweza kumwambia Mwamuzi Aliye Mkuu Zaidi hivi: “Wewe, Ee Yehova wa majeshi, unamchunguza mwenye haki; wewe unaziona figo na moyo. Uniache nikione kisasi chako juu yao [watesi wetu], kwa maana wewe nimekufunulia jinsi kesi yangu ilivyo.” (Yer. 20:11, 12, NW) Katika hiyo “siku ya kisasi” mishale ya Yehova itajichomeka katika figo za watesi wetu, si katika figo zetu, nayo itawatia jeraha la kifo.—Yer. 46:10; Omb. 3:13.
24. Wenye kuendeleza ukamilifu wanaonaje wanapochunguzwa na Yehova, kama Daudi alivyoonyesha?
24 Wakristo wanaoendelea na ukamilifu wao mbele za Yehova wanafurahi kuchunguzwa naye. Wanamwomba sana awachunguze, sawasawa na mtunga zaburi Daudi, Daudi alisema: “Unihukumu mimi [au, Unitendee haki], Ee Yehova, kwa maana mimi mwenyewe nimetembea katika ukamilifu wangu mwenyewe nikamtumaini Yehova, ili nisije nikayumba-yumba. Unichunguze mimi, Ee Yehova, unitie katika jaribu; uzitakase figo zangu na moyo wangu. Kwa maana fadhili zako zisizostahilika zi mbele ya macho yangu, nami nimetembea katika kweli yako.”—Zab. 26:1-3, NW: Rotherham.
25. Daudi alikuwa akiomba nini kwa kumwambia Yehova atakase figo zake, naye alikuwa na uhakika gani.
25 Daudi alitembea katika ukamilifu wake mwenyewe kisha akatembea katika kweli ya Mungu wakati ule ule, bila kufanya mambo hayo mawili nyakati tofauti tofauti. Hata sisi wenyewe tunahitaji kweli ya Mungu leo ili tuendelee kutembea katika ukamilifu kumwelekea Yeye. Zaidi ya kuchunguzwa na kujaribiwa, Daudi alitaka figo zake zitakaswe. Alitaka Mungu amjaribu aone kama anafaa, kama vile msafisha madini anavyozijaribu dhahabu na fedha katika moto. Daudi alikuwa na hakika kwamba Yehova asingeona vitakataka, uchafu wala ugonjwa wa kiroho ndani yake hata akimchunguza-chunguza mara nyingi sana. Asingemkuta akitaabishwa na mawe katika figo za mfano.
26. Vivyo hivyo, sisi tunaoendeleza ukamilifu leo tunaweza kumwomba Yehova atufanyie nini, na tutakuwa gani ya uzima?
26 Vivyo hivyo, sisi tunaoendelea kuwa na ukamilifu leo tunaweza kumwomba Mungu atuchunguze-chunguze sana hata kwa kutumia moto wa mfano kama msafisha madini. Kwa sababu gani? Kwa sababu tuna hakika kwamba baada ya kuchunguzwa sana hivyo hakuna vitakataka vyenye dhambi vitakavyotokea waziwazi kuhakikisha kwamba humo ndani yetu sana tumechafuka, tuna hali ya kilimwengu, bila ukamilifu wa Kikristo.
27. Wakati Yehova atuchunguzapo, atafurahi sana akiona nini?
27 Basi, Yehova anaona nini anapochunguza “figo” zetu leo? Tunatumaini kwamba anaona hali yenye afya ya kiroho anapotazama jinsi utu wetu ulivyo hasa. Ikiwa ndivyo, hiyo itahakikisha kwamba tumekuwa tukitenda mambo ya hekima, na bila shaka tutapata kibali ya Mungu. Basi Yehova atafurahi sana kwa sababu yetu. Akijitaja kama baba mwenye figo, Yehova anatuambia hivi: “Mwana wangu, ikiwa moyo wako umekuwa wenye hekima, moyo wangu utafurahi, naam, wangu. Nazo figo zangu zitafurahi sana wakati midomo yako inenapo unyofu.”—Mit. 23:15, 16, NW.
28. Kwa hiyo, sisi waabudu na mashahidi wa Yehova tutaangalia unyofu wetu kadiri gani, nasi tutakuwa na matumaini gani ya kuonekana tunafaa tuchunguzwapo?
28 Basi, tutatumia mioyo yetu na figo zetu tumtumikie Yehova ili kumfurahisha sana Baba yetu huyo wa mbinguni. Tunapoendelea kuwa waabudu na mashahidi wake tutakuwa wanyofu mpaka mle ndani-ndani. Halafu hatutakuwa na dhambi zo zote za siri za kumficha. (Zab. 19:13, 14) Hatutaogopa atuchunguzapo mara ya mwisho, hata ikiwa atatuchunguza sana. Kwa msingi huo imara, Yehova atatuona kuwa tunafaa achunguzapo figo zetu, na hapo tutajipatia faida za milele. Yeye atafurahi sana kutuambia kwamba tuna afya bora.
—Kutoka The Watchtower, Nov. 1, 1977.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Figo zinafananisha utu wetu wa kweli, jinsi tulivyo hasa