“Figo” na “Moyo” Katika Maandiko
FIGO halisi ziko katika sehemu ya mwili iliyo chini kuliko moyo halisi. Kulingana na moja ya njia za kuzifafanua, figo ndiyo mafao ya maoni ya ndani ya kibinadamu, shauku za upendo na tamaa. Kamusi Webster’s Collegiate Dictionary inahusianisha figo na “hali ya kukasirika au kufurahi”a ya mtu. Kwenye Ufunuo 2:23 (NW ) Yesu Kristo aliyefufuliwa na kutukuzwa anasema: “Mimi ndiye yule anayechunguza-chunguza figo na mioyo, nami nitawapa ninyi kila mtu kulingana na matendo yenu.” (Ona pia Yeremia 11:20, maelezo ya chini, NW, Biblia Yenye Mitajo.) Figo na moyo ni viungo vya mwili vinavyotofautiana na viko katika sehemu zinazotofautiana. Figo halisi ziko katika sehemu ya mwili iliyo chini kuliko moyo wa kimwili. Pia zinaitikia kwa njia tofauti misisimuko ya namna tofauti. Njia hizo za kuitikia zingemaanisha jambo fulani. Hivyo maitikio hayo yangeweza kusomwa au kuonwa kuwa yanamaanisha sifa tofauti zinazoonyesha mtu anayechunguzwa ni wa namna gani. Je! moyo halisi wa mtu unasukumwa kupiga-piga kwa mwendo wa kasi zaidi au, tunaweza kusema, kuwa baridi? Je! figo zake zinachochewa kufanya kazi wakati usio wa kawaida na kwa njia isiyofaa? Mchunguzi wa mioyo na figo anaweza kufasiri maitikio hayo kisha amfahamu mtu kabisa kabisa, kwamba yeye ni figo ya namna gani.
Kwenye Zaburi 16:6-8 (NW ) Daudi mtungaji anaandika hivi: “Kamba za kupimia zenyewe zimeanguka kwa ajili yangu katika mahali pa kupendeza. Kwa kweli, mali yangu mwenyewe imekuwa ya kukubalika kwangu. Mimi nitabariki Yehova, ambaye amenipa shauri. Kwa kweli, wakati wa usiku figo zangu zimenisahihisha. Mimi nimeweka Yehova mbele yangu daima. Kwa sababu yeye yuko mkono wangu wa kuume, sitafanywa nitikisike.” Ni kwa njia gani figo za Daudi zilimsahihisha nyakati za usiku alipokuwa macho? Kama Daudi alikuwa na mashaka yo yote juu ya nia ya Yehova kumwelekea, juu ya yeye alikuwa hasa mtu wa namna gani, figo zake za usemi wa mfano zingempa kadirio sahihi juu ya kusudi la Yehova kumwelekea. Ndiyo sababu Daudi aliendelea kusema: “Kwa maana wewe hutaacha nafsi yangu katika Sheoli. Hutaruhusu mshikamanifu wako aone shimo.”—Zaburi 16:10, NW.
Bila shaka, Daudi atapata ufufuo kutoka kaburini, au Sheoli, katika wakati wake Yehova; lakini, mtume Petro akiwa chini ya uongozi wa roho ya Mungu siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., siku 50 baada ya ufufuo wa Yesu Kristo, alitumia Zaburi 16:10 kumhusu Yesu Kristo, akasema hivi kwenye Matendo 2:25-28, NW: “Kwa maana Daudi anasema kwa habari yake, ‘Yehova alikuwa mbele ya macho yangu daima; kwa sababu yeye yuko mkono wangu wa kuume ili nisipate kamwe kutikiswa. Kwa sababu hiyo moyo wangu ukawa mchangamfu na ulimi wangu ukafurahi sana. Zaidi ya hilo, hata nyama ya mwili wangu itakaa katika tumaini; kwa sababu hutaacha nafsi yangu katika Hadesi, wala hutaruhusu mshikamanifu wako aone uharibifu. Umenijulisha njia za maisha, utanijaza uchangamshi kwa uso wako.’ ”
Moyo mchangamfu ulimtia Daudi mtunga zaburi bidii, na vivyo hivyo moyo mchangamfu ulifanya maisha ya kidunia ya mfananishwa mkubwa wa Daudi, Yesu Kristo, awe mtendaji. Moyo wa asili unaleta matokeo fulani kwenye mwili pia, sawasawa na vile Mithali 14:30 inavyosema: “Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili.” Moyo wa Daudi Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, ungeweza kubaki ukiwa na mpigo mtulivu na mtiririko wa damu usiobadilika-badilika hata, chini ya hali zenye kukoroga fikira, ndiyo chini ya mateso na kutendwa vibaya kimwili, kufikia wakati wa kutundikwa kwake mtini. Hapo tu ndipo alipokufa akiwa na moyo uliovunjika.—Zaburi 69:20.
Kwenye Waebrania 4:12 inasemwa kwamba “Neno la Mungu . . . li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.” Hiyo inamaanisha kwamba “moyo” ndicho kitu kinachosababisha na kutoa msukumo wa kuongoza mawazo na makusudio, ambayo yanafahamiwa na “Neno la Mungu.”
[Maelezo ya chini]
a Kwa habari ya “figo,” ona pia The Compact Edition of the Oxford English Dictionary; The Concise Oxford Dictionary; The Random House Dictionary of the English Language (Unabridged); The American Heritage Dictionary of the English Language; Webster’s New World Dictionary of the American Language.