“Moyo” Katika Neno la Mungu, Biblia
HAKUNA shaka kwamba moyo wa kibinadamu umekaziwa fikira nyingi zaidi na wanadamu kuliko kiungo kingine cho chote cha mwili. Mashairi na maandishi ya kawaida yana mitajo mingi sana juu ya moyo. Basi si ajabu kwamba moyo unasemwa sana katika Neno la Mungu. Kwa kweli, umetajwa humo karibu mara elfu moja kwa njia fulani. Basi, tufahamu nini kutokana na neno “moyo”?
Katika Biblia, ni jambo la kawaida neno kutumiwa kwa njia za namna mbalimbali likiwa na maana tofauti-tofauti. Kwa mfano, na tuangalie matumizi ya Biblia ya maneno “mbingu” na “roho.” Nyakati nyingine, “mbingu” zinamaanisha upana mkubwa ulio huko juu, au anga, juu ya dunia ambamo ndege wanaruka. (Mwanzo 1:26) Ulimwengu mzima wa kimwili, kutia ndani nyota zinazoonekana na zisizoonekana, nyakati nyingine unatajwa kuwa mbingu. (Zaburi 19:1) Kwenye 2 Petro 3:7 linalomaanishwa linaonekana kuwa ni mbingu za kisiasa. Lakini, nyakati nyingine “mbingu” zinamaanisha makao yenyewe ya tengenezo la Yehova la viumbe wa kiroho. (Ufunuo 12:12) Zinaweza pia kumaanisha Ufalme wa kimbingu, kama vile kwenye 2 Petro 3:13.
Ndivyo ilivyo kwa neno “roho.” Nyakati nyingine Yehova Mungu, Yesu Kristo na malaika wanatajwa kuwa watu wa kiroho. (Yohana 4:24; 1 Wakorintho 15:45; Waebrania 1:13, 14) Kani ya uzima inayotendesha viumbe vyote vilivyo hai inatajwa pia kuwa “roho.” (Mhubiri 12:7) Kani inayochochea utendaji katika mtu nyakati nyingine inaitwa “roho,” kama vile kwenye Mithali 25:28. Na, mara nyingi sana, kani ya utendaji ya Yehova Mungu inatajwa kuwa “roho” au “roho takatifu.”—Mwanzo 1:2; Zekaria 4:6; Marko 13:11.
Namna gani, basi, juu ya “moyo”? Kwenye Kutoka 28:30 neno la Kiebrania la kusema “moyo” linamaanisha kiungo halisi. Hapo Yehova Mungu aliamuru kwamba kitambaa cha kifuani cha hukumu kiwekwe juu ya moyo wa Haruni. Huo ulikuwa ni moyo wa kimwili wa kibinadamu. Na ni wazi kwamba Zaburi 45:5 inataja moyo halisi, ikisema: “Mishale yako ni mikali . . . imo mioyoni mwa adui za mfalme.”
Halafu tena, moyo unatumiwa kumaanisha sehemu ya katikati ya kitu. Kwenye Ezekieli 27:25-27 tunakuta mara tatu maneno ‘moyo wa bahari,’ bila shaka yakiwa na maana ya katikati kabisa ya bahari. Vivyo hivyo, Yesu alitabiri kwamba angekuwa katika “moyo” wa, katikati ya, dunia kwa michana mitatu na siku tatu.—Mathayo 12:40.
Moyo unashirikishwa pia na hisia zetu za furaha na huzuni, au majonzi. Tunasoma kwenye 1 Wafalme 8:66 kwamba wakati hekalu la Sulemani lilipowekwa wakfu, ‘Israeli wote walifurahi na kuchangamka moyoni kwa wema wote Yehova aliomfanyia Daudi mtumishi wake, na Israeli.’ Kwenye Nehemia 2:2 tunakuta Mfalme Artashasta akimuuliza Nehemia sababu gani alionekana mwenye uso wa majonzi sana na hali hakuwa mgonjwa. Alikata maneno kwa kusema, “Nini hii, isipokuwa ni huzuni ya moyo? ”
Moyo unashirikiana na mwelekeo wetu, nia yetu, iwe ni ya kujitukuza, ya kiburi, au ya kujishusha, kujinyenyekeza. Mithali 16:5 inasema kwamba “kila mwenye moyo wa kiburi ni chukizo kwa [Yehova].” Kwa upande mwingine, kwenye Mathayo 11:29, Yesu alisema: “Mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo.”
Sifa za maadili—wema, ustahili, ubaya na uovu—zinasemwa kuwa zinakaa moyoni. Kwa mfano, kwenye Yeremia 7:24 tunasoma juu ya Waisraeli ‘wakienda kwa mashauri yao wenyewe, na kwa ushupavu wa mioyo yao mibaya.’ Yesu anaonyesha kwenye Mathayo 12:34, 35 kwamba mambo mema na hata mabaya yanaweza kupatikana moyoni.
Imani inahusu moyo, kwa maana Paulo anatuambia kwenye Warumi 10:10: “Kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu.”
Moyo ndio makao ya msukumo. Andiko la Kutoka 35:21 linaeleza kwamba wenye kutolea hema takatifu michango ‘walikuja kila mtu ambaye moyo wake ulimhimiza.’ Kulingana na Waebrania 4:12, 13, neno la Yehova ni kama upanga mkali, nalo linaweza “kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.” Ndiyo, moyo wa mtu ndio chanzo cha msukumo, kinachoongoza akili ielekee mema au mabaya. Mfano wa kisa cha moyo ukisukuma watu wa Mungu watende kwa hekima unapatikana kwenye Kutoka 31:6, panaposema hivi: “Nimetia hekima katika mioyo ya wote wenye moyo wa hekima, ili wapate kufanya vyote nilivyokuagiza.”
Lakini, juu ya mambo yote maoni ya ndani ya upendo na chuki yanashirikishwa na moyo. Waisraeli waliamriwa hivi: “Usimchukie ndugu yako moyoni mwako.” (Mambo ya Walawi 19:17) Tunasoma pia juu ya moyo wa Wamisri ukichukia Waisraeli. (Zaburi 105:25) Kwa upande mwingine, Paulo anatuambia hivi: “Walakini mwisho wa agizo hilo ni upendo utokao katika moyo safi.” (1 Timotheo 1:5) Naye Petro anatushauri hivi: “Mkiisha kujitakasa [nafsi] zenu kwa kuitii kweli . . . jitahidini kupendana kwa moyo.”—1 Petro 1:22.
Maandiko yanataja pia matukio yenye ubora mkubwa kuwa yakihifadhiwa moyoni. Hivyo tunasoma kwenye Luka 2:51 kwamba Mariamu, mama ya Yesu, “aliweka kama hazina mambo yote hayo [kuhusu Yesu] katika moyo wake.”—Today’s English Version; New International Version; The New English Bible.
Ni mambo mengi ajabu yanayohesabiwa kuwa yanafanywa na yanaweza kutimizwa na moyo! Je! yote hayo yanakaa katika moyo ule halisi? Haiwezi kuwa hivyo. Hilo linaonyeshwa na lugha zile zinazoonyesha tofauti ya wazi kati ya moyo wa nyama na moyo wa usemi wa mfano. Kuonyesha kisa kimoja, lugha ya Wachina na hata ya Wajapani inatumia Mchoro mbili, zinazomaanisha “moyo-kiungo,” kuhusu moyo halisi. Lakini katika kusimulia sifa zinazotokana na moyo, ni ile Mchoro ya kwanza tu kati ya hizo mbili inayotumiwa, kwa kuunganishwa na mambo mengine, ili kufanyiza sehemu ya Mchoro yenye kusimulia mengi zaidi, katika maneno kama upendo, chuki, kusudio na uvumilivu. (Ona sanduku katika makala hii.) Hivyo tofauti ya wazi inaonyeshwa kati ya kile kiungo cha kimwili na mambo yanayochochea mtu kutenda na sifa zake za kimoyo, ingawa uhusiano wa hivyo viwili unadumishwa.
Ni jambo la kutia maarifa pia kuona namna viungo vingine vya mwili vinavyotajwa katika Maandiko. Hivyo tunakuta kwamba zaidi ya mara 20 figo halisi zinatajwa katika Maandiko ya Kiebrania, sana sana katika vile vitabu vitano vya kwanza. Tunasoma mara nyingi juu ya “figo mbili, na mafuta” kuhusiana na dhabihu za wanyama zilizotakwa chini ya Sheria. (Kutoka 29:13, 22; Mambo ya Walawi 3:4, 10, 15; 4:9; 7:4) Bila shaka mtajo huo unahusu figo halisi. Na pasipo shaka mtunga-zaburi Daudi alikuwa akimaanisha figo halisi wakati alipoandika hivi: “Wewe mwenyewe ulitokeza figo zangu; uliniweka nikiwa nimesitiriwa katika tumbo la mama yangu.”—Zaburi 139: 13, NW.
Lakini, je! nabii Yeremia alikuwa akimaanisha figo halisi aliposema, kwenye Yeremia 11:20 (NW ), kwamba Yehova “anachunguza figo na moyo”? Zaidi ya hilo, je! Daudi angaliweza kuwa alimaanisha figo halisi aliposema hivi: “Kwa kweli, nyakati za usiku figo zangu zimenisahihisha mimi”? (Zaburi 16:7, NW ) Kwa uhakika figo halisi zetu haziwezi kutusahihisha. Alikuwa akimaanisha nini? Je! andiko la Yeremia 12:2 (NW ) halitoi ufahamu juu ya habari hiyo? Linasema: “Wewe umewapanda; wao wametia mizizi pia. Wanaendelea kwenda mbele; wamezaa matunda pia. Wewe u karibu katika kinywa chao, lakini mbali sana na figo zao.” Je! hapa “figo” hazionyeshi maoni ya ndani kabisa ya mtu? Andiko hilo linaelekea kuwa na ufanani pia na lile la Isaya 29:13, ambalo Yesu alitumia maneno yalo, kama yalivyoandikwa kwenye Mathayo 15:7, 8: “Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huni heshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami.” Hapo bila shaka Yesu alikuwa akimaanisha namna watu hao waovu walivyokuwa kwa ndani kabisa.
Mfano mwingine unaoweza kutolewa ni neno la Kigiriki la kusema matumbo, splag’khna. Linatumiwa kwa maana halisi kwenye Matendo 1:18, ambapo tunasoma hivi juu ya Yuda: “Basi mtu huyu alinunua konde kwa ijara ya udhalimu; akaanguka kwa kasi akapasuka, matumbo yake yote yakatoka.” Lakini, ingawa neno hilo linaonekana mara 11 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ni katika kisa hiki peke yake linapomaanisha matumbo halisi. Limetafsiriwa “nyororo” kwenye Luka 1:78 (NW ) na “shauku nyororo za upendo” kwenye 2 Wakorintho 6:12; 7:15; Wafilipi 2:1; Wakolosai 3:12 na kwenye Filemoni 7 (Maandiko hayo yote ni kulingana na New World Translation.) Kwenye Mwanzo 43:30 na 1 Wafalme 3:26 ra·chamimʹ, neno la Kiebrania linalolingana na hilo, limetafsiriwa “matumbo” katika Biblia ya Authorized Version, ingawa kwa kweli linamaanisha “maoni ya ndani,” na ndivyo linavyotafsiriwa na Biblia ya New World Translation.
Ndivyo ilivyo pia kuhusu maneno ya Kiebrania na Kigiriki yaliyotafsiriwa “moyo” katika Biblia zetu. Kuna nyakati, ambazo ni chache kwa kulinganishwa, moyo halisi unapomaanishwa, kwa mfano kwenye Kutoka 28:30 na Zaburi 45:5. Lakini, katika mitajo mingine karibu elfu moja inayosema “moyo” katika Biblia, kwa wazi neno “moyo” linatumiwa katika maana ya mfano. Hiyo si kusema kwamba hakuna uhusiano kati ya moyo wa kimwili na ule wa usemi wa mfano. Kunao. Kwa mfano, mikazo ya maoni ya ndani inaweza kuleta madhara juu ya moyo halisi, kutokeza ugonjwa na hata kifo. Lakini, ni wazi kwamba lazima tofauti ionyeshwe kati ya moyo-kiungo na moyo wa usemi wa mfano. Ni kama vile W. E. Vine anavyosema, “Moyo unatumiwa kwa usemi wa mfano kumaanisha chemchemi zisizoonekana za maisha ya mtu binafsi.”—An Expository Dictionary of New Testament Words, Buku la Pili, kurasa 206-7.
Kutokana na yote yaliyotangulia ni wazi kwamba maneno ya Kiebrania na Kigiriki ya kusema “moyo” yanatumiwa na waandikaji wa Biblia kumaanisha sifa kadha za kindani na za kiadili zinazofanyiza yule mtu wa ndani. Ni wazi kwamba, kwa kutuonya juu ya umaana wa kuangalia tamaa zetu, hamu zetu na mambo yanayotuchochea kutenda, Neno la Mungu linatusaidia ‘tumtumikie kwa moyo kamili.’ Linatutayarisha kwa ajili ya kila kazi njema. (1 Mambo ya Nyakati 28:9, NW; 2 Timotheo 3:17) Kuna mashauri mengi mazuri yanayohusu jambo hilo katika Neno la Mungu.
[Chati katika ukurasa wa 8]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Mchoro za Kichina zinazosimamia moyo
[Mchoro—Herufi ya Kichina] moyo, kwa kawaida ule wa usemi wa mfano
[Mchoro—Herufi ya Kichina] moyo-kiungo, ule halisi
Angalia namna Mchoro ile ya msingi inavyoonekana katika sifa zinazohusiana na moyo:
[Mchoro—Herufi ya Kichina] upendo
[Mchoro—Herufi ya Kichina] chuki
[Mchoro—Herufi ya Kichina] msamaha
[Mchoro—Herufi ya Kichina] huzuni
[Mchoro—Herufi ya Kichina] wasiwasi
[Mchoro—Herufi ya Kichina] kusudio
[Mchoro—Herufi ya Kichina] hasira
[Mchoro—Herufi ya Kichina] uvumilivu
[Picha katika ukurasa wa 7]
Moyo unahusiana na hali za kujisikia, nia, imani, mambo yanayochochea matendo na maoni ya ndani ya kibinadamu