Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
● Ni nini maana ya unabii wa Amosi unaotajwa kuwahusu “ng’ombe wa Bashani”?
Unabii huo unapatikana katika Amosi 4:1-3 nao unasema hivi: “Lisikieni neno hili, enyi ng’ombe wa Bashani, mnaokaa juu ya mlima wa Samaria, mnaowaonea maskini, na kuwaponda wahitaji; mnaowaambia bwana zao, Haya! leteni, tunywe. Bwana [Yehova] ameapa kwa utakatifu wake, ya kuwa, tazama, siku zitawajilia, watakapowaondoa ninyi kwa kulabu, na mabaki yenu kwa ndoana. Nanyi mtatoka kwenye mahali palipobomolewa, kila mwanamke moja kwa moja mbele yake.”
Hao “ng’ombe wa Bashani” ni wanawake wa Samaria waliochochea waume wao wawapunje na kuwaonea maskini ili wao wenyewe waendelee kuishi katika anasa. Waliwaomba “bwana” zao, au waume wao, wawatafutie vitu walivyotaka ili wawe na maisha ya anasa. Lakini, Aliye Juu Zaidi hakupendelea uovu huo. Yeye ni mtakatifu na ni safi, kwa hiyo aliapa kwa utakatifu wake kwamba angechukua hatua juu ya hao “ng’ombe wa Bashani.” Wangeondolewa Samaria kwa jeuri nyingi kama kwamba wamevutwa kwa kulabu, nao mabaki wenye kuokoka wangeondolewa kama kwamba wamevutwa kwa ndoana. Adui wangewaondoa wanawake hao kwa kuwapitisha mahali palipobomolewa katika kuta za mji ulioshindwa.