Kuvumilia Kwa Uaminifu
“Ee [Yehova], macho yako je! hayaangalii uaminifu?”—Yer. 5:3
1. Mwendo uliofuatwa na Yerusalemu ulitofautianaje na wa Yeremia?
YEHOVA aliuliza hivi juu ya Yerusalemu wa kale: “Mbona, basi, watu hawa . . . wamegeuka waende nyuma, wasikome kugeuka hivyo [“mbona . . . ni watu wasioaminika wenye hali ya kutoaminika isiyokwisha,” NW]?” Ni kwa sababu walikuwa wenye shingo ngumu, ‘wakafuata mwendo uliofuatwa na walio wengi, kama farasi aendavyo kasi vitani.’ Nayo maoni yao ya kimwili yalileta mabaya, kwa maana ‘hawakuzijua amri za Yehova.’ (Yer. 8:5-7) Lakini Yeremia alitofautiana sana nao, akavumilia kwa uaminifu. Kwa muda wa miaka 40, aliendelea kutimiza agizo alilopewa kuzihubiri hukumu za Yehova mpaka Yerusalemu ulipoharibiwa na hata baada ya hapo.
2. Kwa habari ya dhiki inayokaribia, hali ya Yeremia ililinganaje na ya watu wa Mungu leo? (Yer. 4:5, 6; 6:1)
2 Inaonekana kwamba Yeremia hakujua mapema siku wala saa ambayo Yerusalemu ungeharibiwa. Lakini alikuwa na habari juu ya “mshindo mkuu kutoka nchi kaskazini,” yaani, Babeli. Alijua kwamba majeshi yenye kuua watu yalikuwa yakikaribia, na kwamba hukumu za Mungu zingetimia bila shaka. Vivyo hivyo, leo watu wa Yehova wanaiona waziwazi “dalili” (alama) ya kukaribia kwa ‘dhiki isiyokuwako tangu mwanzo wa kuumba.’—Yer. 10:22; Marko 13:4, 19.
3. (a) Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakihubiri nini imani wakati za kisasa, na kwa muda gani? (b) Wameongezea imani yao kitu gani?
3 Kwa muda wa miaka karibu 60 sasa, mashahidi Wakristo wa Yehova wamekuwa wakiyatangazia mataifa yaliyo nje na ndani ya Jumuiya ya Wakristo kwamba ulimwengu huu umo katika ‘wakati wake wa mwisho’ tangu mwaka 1914, na kwamba taratibu nzima lazima itoweke karibuni katika “wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo.” (Dan. 12:1, 4) Majeshi ya kishetani yanayakusanya mataifa kuyaelekeza kwenye Har–Magedoni. (Ufu. 16:13-16) Wakati jamii ya kisasa ya Yeremia inapozitangaza habari hizo inavumilia kwa uaminifu. Wanaongezea imani yao uvumilivu.—2 Pet. 1:5, 6.
4. Ni chanzo gani kinachotutia moyo, na jambo hilo linafananishwaje katika Yeremia 17:5-8?
4 Jamii ya Yeremia, pamoja na wote wanaomiminika wakati wa sasa wakawe wahubiri wa Ufalme, wanahitaji kutiwa moyo nyakati zote ili waendelee kusonga mbele kwenye ushindi. Yehova anawapa moyo uo huo wanaouhitaji. Wale waliofananishwa na Yeremia ni tofauti na “mtu yule amtegemeaye mwanadamu, amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake,” maana wao wanamtumaini Yehova na kumtegemea wakiwa na uhakika. ‘Wanakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji,’ hivi kwamba wanaweza kueneza mizizi yao waunywe mpango wote wa Yehova wenye kutoa uzima. Wala “hari” (joto) ya mateso wala “uchache wa mvua” (ukavu) unaotokana na marufuku na mateso hauwezi kuwafanya ‘waache kuzaa matunda.’ Kama mti wenye kuzaa, wao ni ‘wabichi’ (“wanasitawi sana,” NW) katika kumletea Yehova sifa. ‘Wanabarikiwa’ kwa kufanya hivyo.—Yer. 17:5-8.
KULISHINDA JARIBU LA UVUMILIVU
5. Ni mfano gani wa uvumilivu wa Yeremia unaopaswa kututia nguvu?
5 Je! wengine leo wamekaza macho yao juu ya malengo ya kupata vitu vya kimwili, badala ya hazina yenye thamani nyingi sana ya utumishi wa Ufalme? Je! wengine wameona ni vigumu kuvumilia? Basi, kumbuka kwamba nyakati fulani Yeremia aliona ilikuwa vigumu kuvumilia. Hata alitaka kuacha utumishi wake. Lakini ndipo alipojisikia moyoni mwake neno la Yehova likiwa kama ‘moto uwakao, uliofungwa ndani ya mifupa yake.’ Neno hilo lilimsukuma aendelee kufanya vita na kuwashinda adui zake. (Yer. 20:9) Tunapochunguza mengine ya matatizo ambayo Yeremia alishindana nayo akayashinda, hakika inatupasa tuwe na tamaa ya kuvumilia tupate ushindi!
6. (a) Yeremia alipata wapi nguvu za kuvumilia? (b) kupatana na mfano wa Yeremia, inatupasa tuepuke ushirika gani?
6 Yeremia alipingwa vikali na watu waliokuwa wa mji mmoja naye, yaani, Anathothi, wakimwambia hivi: “Hutafanya unabii kwa jina la [Yehova], usije ukafa kwa mkono wetu.” Ndugu zake mwenyewe na jamaa ya baba yake ilimtenda hila. Ilionekana kwamba kila mahali adui walikuwa wakimlaani. (Yer. 11:21; 12:6; 15:10) Lakini Yeremia alipata nguvu za kuvumilia. Wapi? Kwa kumpelekea Yehova sala, na kulikubali pendeleo alilokuwa nalo la kulichukua jina na neno la Yehova:
“Maneno yako yalionekana, nami nikayala; na maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu, na shangwe ya moyo wangu; maana nimeitwa kwa jina lako, Ee [Yehova], Mungu wa majeshi. Sikuketi katika mkutano wao wanaojifurahisha, wala sikufurahi.” (Yer. 15:16, 17)
Yeremia alipata furaha kutokana na maneno ya Yehova na kwa kulichukua jina Lake. Yeye hakufurahia mzaha (utani) usio na maana wa watu wasiomwogopa Mungu, tena alitumia hekima kuepuka kushirikiana nao. Je! haitupasi nasi kufanya hivyo?
7. (a) Ni jambo gani lililomwezesha Yeremia akubali kukaa peke yake bila kulalamika? (b) Yeremia alifanyaje alipotendwa ukatili na Pashuri?
7 Yehova alimwamuru Yeremia asioe ili kumpa ishara ya kumwonyesha kwamba ujumbe wake ungetimia bila shaka. Kwa njia hiyo asingezaa watoto wa uharibifu. Yeye hakulalamika kwa sababu ya kutooa, bali fikira zake zote zilikuwa katika kazi aliyokuwa nayo. Baadaye, Pashuri, mkuu mmoja katika nyumba ya Yehova, aliudhiwa na maneno ya Yeremia, akampiga na kumfunga katika mkatale (ubao wenye matundu) usiku kucha. Lakini alipofunguliwa, Yeremia alimwambia Pashuri tena kwamba nchi yote ya Yuda ingetiwa mkononi mwa mfalme wa Babeli.—Yer. 16:1-4; 20:1-6.
8. Yeremia alionyeshaje kwamba hakuogopa wakati wa utawala wa Yehoyakimu?
8 Wakati Mfalme mwovu Yehoyakimu alipokalia kiti cha ufalme mwaka 628 K.W.K., Yehova alimpa Yeremia unabii mkali autangaze, Naye akamwambia hivi kwa mara nyingine: “Usizuie hata neno moja.” Basi, Yeremia alisimama katika ua wa hekalu la Yehova, akayanena maneno yote aliyoamuru Yehova, naam, ujumbe wa maangamizi kwa Yuda na Yerusalemu. Halafu ikawaje? Maandishi yanajibu hivi:
“Ikawa, Yeremia alipokuwa amekwisha kusema maneno yote [Yehova] aliyomwamuru kuwaambia watu wote, ndipo hao makuhani, na manabii, na watu wote, wakamkamata, wakisema, Bila shaka utakufa. Kwa nini umetabiri kwa jina la [Yehova], ukisema, Nyumba hii itakuwa kama Shilo, na mji huu utakuwa ukiwa, hautakaliwa na mtu? Watu wote wakamkusanyikia Yeremia katika nyumba ya [Yehova].” (Yer. 26:1-9)
Wakuu wa Yuda walifika mahali hapo, nao makuhani na manabii wakaamua ahukumiwe kufa. Lakini Yeremia alitoa hotuba moto-moto na kuonyesha wazi kwamba Yehova ndiye aliyemtuma atoe unabii, kwamba yeye aliitii sauti ya Yehova na kwamba wangemwaga damu isiyo na hatia wakimwua.—Yer. 26:10-15.
9. (a) Ni nani aliyemtetea Yeremia? (b) Jambo hilo linatukumbusha tukio gani la karibuni?
9 Ndipo wakuu na watu wote walipomtetea Yeremia, wakisema: “Amesema nasi katika jina la [Yehova], Mungu wetu.” Wazee fulani walimtetea Yeremia pia, mmoja wao akiwa Ahikamu, baba yake Gedalia. (Yer. 26:16-24) Basi, Yeremia aliendelea kutoa unabii bila kuogopa. Tendo hilo la Wayudea kuacha kumwinda Yeremia linatukumbusha jinsi ndugu zetu wa Malawi waliacha kuteswa kwa muda. Habari fulani za karibuni zimeonyesha kwamba wengi wao wamefunguliwa magerezani, wakaruhusiwa kurudi makwao na kulima mashamba yao. Vijana fulani waliokuwa wakiwatesa hapo kwanza wanasemekana kwamba hata wanajifunza Biblia nao. Lakini, katika sehemu nyingine za nchi, wakuu na watu wa ukoo wanafanya iwe vigumu watu wa Yehova kuishi maisha ya kawaida. Lakini wao wanaendelea kuvumilia katika ukamilifu wao, kama Yeremia.
SHINDANO LA MANABII
10, 11. (a) Ni jambo gani lililofanywa na Yeremia na Hanania lililokuwa mfano wa tukio la wakati ujao? (b) Yeremia alihakikishwaje kuwa nabii wa Kweli?
10 Wakati wa utawala wa Sedekia ndipo pia Yeremia alipofanya jambo lililokuwa mfano wa tukio la wakati ujao. Alifuata agizo la Yehova, akaweka nira ya mbao juu ya shingo yake, akitangaza kwamba Yuda na mataifa jirani walipaswa kujitia chini ya nira ya mfalme wa Babeli, au sivyo wapate adhabu kali. Lakini nabii Hanania aliiondoa nira hiyo ya mbao shingoni pa Yeremia na kuivunja, akitangaza kwamba Yehova angeivunja na kuiondoa nira ya Babeli kwa wepesi hivyo kabla miaka miwili haijamalizika.—Yer. 27:2-15;28: shindano hilo? Ni nani aliyekuwa nabii wa kweli wa Yehova, Yeremia au Hanania? Yehova alionyesha jambo hilo waziwazi kabisa alipomwamuru Yeremia kutabiri kwamba nira ya mbao ingegeuzwa kuwe na nira ya chuma, na kwamba Hanania angekufa tu kabla ya mwaka huo kumalizika. Zaidi ya Hanania kufa mwezi wa saba wa mwaka huo, nira ya Babeli mwishowe ilipata kuwa nira ya chuma kweli kweli.—Yer. 28:12-17.
11 Ni nani kati ya manabii hao wawili angepata ushindi katika shindano hilo? Ni nani aliyekuwa nabii wa kweli wa Yehova, Yeremia au Hanania? Yehova alionyesha jambo hilo waziwazi kabisa alipomwamuru Yeremia kutabiri kwamba nira ya mbao ingegeuzwa kuwe na nira ya chuma, na kwamba Hanania angekufa tu kabla ya mwaka huo kumalizika. Zaidi ya Hanania kufa mwezi wa saba wa mwaka huo, nira ya Babeli mwishowe ilipata kuwa nira ya chuma kweli kweli.—Yer. 28:12-17.
12, 13. (a) Ni kundi gani la kisasa linalotenda mambo kama Hanania, nayo matokeo yatakuwa nini kwao? (b) Ni nini kinachowatia nguvu mashahidi wa kweli wa Mungu?
12 Wale manabii wa uongo wa kisasa wanaojaribu ‘kuibomoa’ kazi ya Mashahidi wa Yehova wakiwa na kusudi ovu wanafanana sana na Hanania. Huenda wengine wao wakawa hata walitembea pamoja na watu wa Mungu kwa muda, lakini wakawa na undani kwa sababu hawakupata makuu waliyotaka, basi wakayarudia mafundisho yale yale waliyokuwa wameyatapika.’Wanahubiri “kwa sababu ya husuda na fitina,” si “kwa nia njema,” kwa maana hawasemi jambo lo lote la kujenga watu. (2 Pet. 2:22; Flp. 1:15) Wao wana matumaini yaliyo tofauti na ya jamii ya Yeremia juu ya kuja kwa “dhiki kubwa.”
13 Lakini, kama vile Yehova alivyoigeuza ile nira ya mbao bila shaka, kisha kukawa na ya chuma, ndivyo ilivyo hakika kwamba “dhiki kubwa” itakuja katika wakati wake Mungu. Na kama vile Hanania alivyohukumiwa na Yehova akafa mwaka uo huo bila shaka, ndivyo ilivyo hakika kwamba makundi hayo yenye unabii wa upinzani yatauawa katika wakati wake. Wao hawana furaha wala hawana roho na “neno” la Yehova linaloweza kuwatia nguvu.—Yer. 23:16-19; 31:1, 12.
YASHIKE SANA MATUMAINI ULIYO NAYO!
14. (a) Kama Yeremia, inatupasa tuonyeshe matumaini gani? (b) Kwa sababu gani Inatupasa tuwe macho nyakati zote?
14 Kama Yeremia, inatupasa tulitumaini “neno” la Yehova la unabii bila kutikisika. Yeremia alionyesha alilitumaini hilo ‘neno la Yehova’ kwa kununua shamba la urithi katika Anathothi, mwaka mmoja tu kabla majeshi ya Babeli hayajaingia kuiharibu nchi! (Yer. 32:8-25) Katika siku hizi za mwisho, inatupasa sisi pia tuwe na matumaini hakika kwamba Yehova atatimiza kila ahadi aliyofanya ya kuwalinda watu wake na kuwasimamisha kabisa. (Yer. 32:38-41) Wakati wa shambulio la majeshi ya mbinguni yenye kuongozwa na Kristo Yesu unakaribia, kwa hiyo kuna hatari! Tunahitajiwa tuwe macho nyakati zote, tukilitangaza “neno” la Mungu.—Marko 13:10, 32-37.
15, 16. (a) Ni nini kilichomtia Yeremia nguvu? (b) Baruku alipatwa na tatizo gani? (c) Onyo ambalo Yehova alimpa Baruku linatutiaje moyo leo? (Ufu. 2:3)
15 Mambo yalikuwa magumu kwa Yeremia. Lakini aliweza kuyavumilia yote kwa sababu alimtumaini Yehova na kushikamana na agizo alilopewa. Aliweza pia kumtia moyo mwenzi wake mwaminifu, mwandishi Baruku, wakati alipopatwa na huzuni. Baada ya Yeremia kuwa akitoa unabii miaka karibu 20 au 30, Baruku alisema hivi kwa nguvu nyingi:
“Ole wangu! kwa maana [Yehova] ameongeza huzuni pamoja na maumivu yangu. Nimechoka kwa ajili ya kuugua kwangu, wala sioni raha.”
Lakini Yehova alimtumia Yeremia kumpelekea maneno haya:
“Tazama, niliyoyajenga nitayabomoa, na niliyoyapanda nitayang’oa; na haya yatakuwa katika nchi yote. Je! unajitafutia mambo makuu? usiyatafute; kwa maana tazama, nitaleta mabaya juu ya wote wenye mwili, asema [Yehova]; lakini [nafsi, NW] yako nitakupa iwe nyara, katika mahali pote utakapokwenda.” (Yer. 45:1-5)
Naam, mtumishi huyo mwaminifu wa Mungu alichoka baada ya muda kupita. Lakini Yehova alimhakikishia Baruku kwamba wakati Wake wa ‘kubomoa na kung’oa,’ wakati Wake wa kuleta dhiki juu ya Yerusalemu na Yuda isiyoaminika ulikuwa karibu. Ingawa “mabaya” hayo yangeweza kuonekana kama yanakawia, yangekuja bila shaka!
16 Yehova alimwonya Baruku asizirudie njia za kilimwengu za Wayudea, za kutafuta vitu vya kimwili, kwa kujitafutia usitawi wake mwenyewe. Hakupaswa kufanya hivyo, bali alipaswa kuendelea kutumikia pamoja na nabii wa Yehova kwa uaminifu. Vivyo hivyo, katika hizi “siku za mwisho” za karne ya 20, huu sio wakati wa ye yote wa watu wa Mungu kuurudia ulimwengu huu uliohukumiwa maangamizi, wenye kutafuta vitu vya kimwili. Jambo linalowafaa ni kutumikia kwa uvumilivu mpaka mwishowe ‘wapokee nafsi yao kama nyara’ katika makao ya ufalme wa Mungu ulio mikononi mwa Kristo Yesu, baada ya Har–Magedoni kupita kwa mshindo.
WENZI WASHIKAMANIFU
17. Warekabu walikuwa kina nani, na ni jambo lililomfanya Yehova awape thawabu?
17 Yeremia alikuwa na rafiki wengine. Walitokea baada ya yeye kutumikia kwa uaminifu muda wa miaka mingi, tena walitokea kwa uongozi wa Yehova. Wakati Yehoyakimu mwovu alipokuwa akiendelea kutawala, Yehova alimwagiza Yeremia awalete hekaluni Warekabu, waliokuwa wazao wa Yonadabu aliyejipanga upande wa Yehova siku za mfalme Yehu, miaka karibu 250 kabla ya hapo. (2 Fal. 10:15-17) Yonadabu alikuwa amewaamuru wazao wake wasinywe divai yo yote “hata milele.” Sasa, Wababeli walipokuja mara ya kwanza, Warekabu walikimbilia Yerusalemu. Ndipo Yeremia alipowaletea divai. Lakini wao wakaikataa kwa sababu ya kuendelea kumtii babu yao, Yonadabu. Ndipo Yehova alipotofautisha kutotii kwa Yuda na Yerusalemu na utii usiokwisha wa Warekabu, kisha akasema hivi nguvu nyingi:
“Yonadabu, mwana wa Rekabu, hatakosa kuwa na mtu wa kusimama mbele zangu hata milele.”
Hivyo wazao wa Yonadabu walipokea thawabu kubwa, wakakombolewa wakati Yerusalemu ulipopatwa na dhiki.—Yer. 35:1-19.
18. Ni nani walio ‘wana wa Yonadabu’ leo, nao wanapata ulinzi wapi?
18 Kuna watu wengine wanaofanana na Warekabu hao leo—watu wenye mioyo minyofu wanaofuata kanuni za haki, ambao labda hata wamejaribu kuziepuka hizi “nyakati za hatari” kwa kuyakimbilia makao ya kidini ya “Jumuiya ya Wakristo” ya kisasa. (2 Tim. 3:1) Lakini kimbilio lao halisi limo katika mpango ambao Yehova amefanya kupitia kwa Kristo. Anaituma jamii ya kisasa ya Yeremia iwapelekee ujumbe wenye kuwaletea wakovu. Usalama wa “Wayonadabu” hao haupatikani katika Jumuiya ya Wakristo iliyobomoka, bali unapatikana upande wa “nabii” wa kisasa wa Yehova peke yake.
19. Msimamo wa Yeremia mbele ya Sedekia unapaswa ututie moyo namna gani?
19 Sedekia, mfalme wa mwisho wa Yuda (aliyetawala kutoka 617 mpaka 607 K.W.K.), ndiye aliyemwomba Yeremia ampelekee Yehova sala kwa ajili ya Yuda. Lakini Yeremia aliendelea kutangaza kwamba uharibifu ulikuwa ukikaribia sana kuupata Yerusalemu. Baadaye, alipokwisha kutendwa ukatili na kufungwa siku nyingi, aliletwa mbele ya mfalme, akamwuliza hivi wakiwa peke yao: “Je! Liko neno lililotoka kwa [Yehova]?” Yeremia alimrudishia jibu moja kwa moja akisema: “Liko. . . . Utatiwa katika mikono ya mfalme wa Babeli.” (Yer. 37:3-17) Vivyo hivyo, leo Mashahidi wa Yehova wanaionyesha hukumu ya kimungu waziwazi. Wao hawataki kuchangamana na dini zile nyingine wala hawataki kupunguza uzito wa ujumbe unaotangazwa juu ya Jumuiya ya Wakristo.
20. (a) Ni jambo gani lililotukia hata Ebed-meleki akamwokoa Yeremia, naye Mwethiopia huyo alipewaje thawabu? (b) Ni nani nyakati za kisasa wametenda kama Ebed-meleki na matokeo yao yatakuwa nini? (Mt. 25:34, 40)
20 Kwa sababu Yeremia aliendelea kuzitangaza hukumu za Yehova juu ya mji huo, alitupwa katika birika kubwa, kisha akazama katika matope yenye majimaji. Alionekana kama kwamba amekufa kimaskini. Lakini towashi Mwethiopia, Ebed-meleki, alimwendea mfalme akamsihi sana amsaidie Yeremia. Ebed-meleki alipewa agizo na mfalme, akachukua wanaume 30, kisha wakatumia matambaa ya zamani kumvuta Yeremia atoke birikani na kumpeleka mahali fulani katika Ua wa Walinzi. Hapo ndipo alipokaa mpaka Yerusalemu ulipoharibiwa, kisha akaachwa huru. Lakini namna gani Ebed-meleki? Wakati Yeremia alipokuwa angali uani, neno la Yehova lilimjia, likisema:
“Kwenda useme na Ebedimeleki, Muethiopia, kusema: [Yehova] wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Tazama, nitaletea muji huu maneno yangu kwa mabaya, wala si kwa mema; nayo yatatimizwa mbele yako katika siku ile. Lakini nitakuokoa wewe katika siku ile, anasema [Yehova]; wala hutatiwa katika mikono ya watu wale unaowaogopa. Kwa maana ni kweli nitakuokoa, wala hutaanguka kwa upanga, lakini nafsi yako itakuwa kama mawindo kwako; kwa sababu uliniamini mimi, anasema [Yehova].”
Hivyo, wakati majeshi ya Babeli yalipotoka kaskazini kwa mshindo, Ebed-meleki aliokoka. Nyakati za kisasa pia kumekuwa na wengi, kutia na wakuu wa serikali na magereza, ambao wamewaonyesha fadhili mashahidi wa Yehova wenye kuteswa. Baadaye wengine wao wamekuwa Mashahidi wenye kutazamia kupata wokovu wakati ambao majeshi ya mbinguni yenye kufisha, ya Kristo Yesu, yatakwenda kufanya kazi penye Har–Magedoni.—Yer. 38:6-13; 39:15-18, ZSB; Ufu. 7:14-17; 16:16.
21. (a) Watumishi wa kisasa wa Yehova wanaonekana kuwa namna gani wanapolinganishwa na watumishi wa wakati wa Yeremia? (b) Ni kwa njia gani wanaonyesha uvumilivu? (Ufu. 14:12)
21 Ni furaha pia kuona kwamba leo kungali kuna watu wa namna ya Yeremia, Baruku, Warekabu na Ebed-meleki duniani. Ripoti ya utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wakati wa mwaka wa utumishi wa 1977 inahakikisha kwamba kunao. Ni kweli kwamba huenda kukawa na wengine waliochoka kama Baruku kisha wakaanza kutafuta faida zao wenyewe kwa muda, lakini inawapasa wakumbuke kwamba ingawa Baruku alijaribiwa aliendelea tu kukaa na nabii wa Mungu. Naam, kuna faida ya kuvumilia kwa kutazamia uzima wa milele baada ya “dhiki kubwa.” Na waendelee kupatikana watu waipendao haki, wenye nia kama ya wana wa Yonadabu na ya Ebed-meleki. Wote wanaoziamini ahadi za Yehova kwa bidii na kuvumilia mpaka mwisho watapata thawabu kubwa weee! Kutoka The Watchtower,—January 1, 1978
[Picha katika ukurasa wa 16]
Baada ya Yeremia kutupwa katika birika lisilo na maji, Ebed-meleki Mwethiopia alimwomba mfalme ruhusa ya kumwokoa; Mungu alimpa thawabu kwa tendo hilo la upendo