Mahubiri ya Mlimani—Heri 4 na 5
IKIWA ndiyo “heri” ya nne ya Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema: “Heri wenye njaa na kiu ya haki; maana hao watashibishwa.” (Mt. 5:6) Masimulizi ya Luka ya maneno haya yanasema hivi: “Heri ninyi mlio na njaa sasa, kwa sababu mtashiba.”—Luka 6:21.
Kutokana na Injili ya Luka peke yake mtu anaweza kuwazia kwamba Yesu alizungumza juu ya watu wenye njaa ya chakula halisi peke yake. Hata hivyo, Mathayo anafanya iwe wazi kwamba alimaanisha wale wenye tamaa nyingi kwa ajili ya haki. Ingawa hivyo, mawazo yote mawili yanapatana. Watu wasio na chakula na kinywaji halisi ndio mara nyingi wanaoona zaidi sana uonezi unaoenea pote katika taratibu ya mambo iliyopo. Kwa hiyo, njaa, au tamaa yao ya kuona haki ikienea pote inaweza kuwa yenye nguvu zaidi.
Ile “haki” aliotaja Yesu inamaanisha sifa ya unyofu inayopatana kabisa na mapenzi na amri za Mungu. Akitaja wazo kama lile la Yesu, mtunga zaburi alijisema kama kwamba ‘amepondeka kwa kutamani’ maamuzi ya Mungu ya hukumu yenye haki.—Zab. 119:20; linganisha Isaya 26:9, 10.
Tofauti na tangazo hili la furaha, Yesu alisema: “Ole wenu ninyi ambao mmeshiba sasa, kwa kuwa mtaona njaa.” (Luka 6:25) Wale ambao ‘wameshiba’ wametosheka na yanayotolewa na ulimwengu huu. Ingawa pengine wanadai kwamba wanamwamini Mungu, hawaoni wanavyomhitaji sana sana wala hawatamani kanuni zake za haki. (Ufu. 3:17) Hata hivyo, huenda nyakati za misiba zikaamsha kwa muda tu njaa kama hiyo ya uongozi wa Mungu. Hii itakuwa kweli sana sana wakati Mungu aletapo mwisho kwa taratibu ya mambo iliyopo wakati wa “dhiki ile iliyo kuu” inayokuja. (Mt. 24:21; Ufu. 7:14) Watu kama hao ambao hapo kwanza walijitosheleza ‘wataona njaa.’ Vilio vyao vya majonzi wakitaka msaada wa Mungu havitasikuwa. (Linganisha 1 Samweli 28:4-6; Zaburi 18:41; Mithali 1:28-32.) Kwa habari ya kusikiliza neno la Yehova, wataona “njaa na kiu” pasipo tumaini.—Amosi 8:11, 12.
Walakini Yesu anatangaza ‘furaha’ kwa wale wanaoona njaa na kiu sasa kwa ajili ya haki. Kwa sababu gani? Kwa kuwa “watashibishwa,” yaani, watatosheka kabisa. Yesu mwenyewe alifanya mengi kwa ajili ya hilo. Alipokuwa akifunua unafiki wa viongozi waongo wa kidini ambao “walijikinai ya kuwa wao ni wenye haki,” Yesu alifundisha kwamba wote wanaokubali hali yao ya dhambi’ na kutafuta msamaha kwa kutubu wanaweza kupata msimamo wenye haki mbele za Mungu.—Luka l8:1-14; linganisha Mathayo 5:20; 23:23, 24.
Kutosheleza zaidi njaa na kiu kwa ajili ya haki kuliwezeshwa na kifo na ufufuo wa Yesu. Juu ya hili, tunasoma hivi: “Kwa sababu wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu, wanahesabiwa haki bure kwa neema yake, kwa njia ya ukombozi ulio katika Kristo Yesu.”—Rum. 3:23, 24; linganisha Isaya 53:11; Danieli 9:24-27; Ufunuo 7:9-14.
Kutosheleza kwingine njaa na kiu hii ya maana sana kuliwezekana baada ya mwaka 33 W.K., kwa maana ndipo roho takatifu ilipoanza ‘kuhakikishia ulimwengu kwa habari ya . . . haki.’ (Yohana 16:8) Hii ikawa kweli kwa kuwa roho ya Mungu ndiyo iliyotokeza Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, chombo cha lazima “kwa kuwaadibisha [watu] katika haki.” (2 Tim. 3:16) Nguvu ya utendaji iyo hiyo ya Mungu inawezesha watu kuvaa “utu mpya,” unaoleta ‘haki ya kweli’ mahali pa matendo maovu na unafiki. (Efe. 4:24) Kutosheleza kwa mwisho na kwa ukamilifu njaa na kiu ya haki kutaonekana wakati waabudu waaminifu wa Mungu watakapopata uzima wa milele chini ya hali kamilifu na zenye haki.—2 Pet. 3:13; Ufu. 21:1-5.
REHEMA KWA “WENYE REHEMA”
Halafu katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alisema: “Heri wenye rehema; maana hao watapata rehema.”—Mt. 5:7.
Rehema si kufanya matendo ya huruma tu! Kwa sababu mtu anaweza kufanya hivyo kiunafiki. (Mt. 6:1, 2) “Wenye rehema” ni watu wanaosukumwa kikweli na huruma ya upole na maono ya moyo ya kuwahurumia wale wenye hali mbaya na kwa hiyo wanafanya mambo kwa ajili ao. Yesu aliweka mfano mkamilifu katika hili. Maandiko yanasema mara nyingi kwamba kabla ya kufanya miujiza ya kutuliza mateso na taabu za watu, Yesu ‘aliwahurumia.’—Mt. 14:14; 15:32-38; 20:34; Marko 1:40-42; Luka 7:13-15.
Rehema inaonyeshwa wazi kwa njia mbili: (1) Kwa maana ya kuhukumu wakati watu wanaposamehe wale wanaowakosea; (2) Kwa matendo mema ya fadhili, kufikiriana na huruma iletayo faraja kwa watu wanaotaabika.
Wakristo wanaamriwa wawe ‘waigaji wa Mungu’ akiwa wa kwanza kabisa ambaye husamehe wakosaji wanaotubu. (Kut. 34:6, 7; Zab. 103:10; Mit. 28:13; Efe. 4:31-5:2) Katika njia ifaayo watu wanaotaka kumpendeza Mungu lazima watake kutoa msaada wo wote wawezao kwa wale ambao pengine wamepatwa na hali mbaya. (Luka 10:20-37) Njia nzuri ya kuonyesha rehema ni kuishiriki kweli ya Biblia na wengine. Tunaona kwamba wakati mkutano mkubwa wa watu ulipomkuta Yesu alipokuwa akienda kupumzika “akawahurumia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji; akaanza kuwafundisha mambo mengi.”—Marko 6:34.
“Heri” ni wenye rehema kwa sababu “watapata rehema.” Katika maana mojawapo wanaona hili katika kutendeana katika maisha ya kila siku na wanadamu wenzao. Kuwatendea wengine kwa rehema kunawafanya waitikie vivyo hivyo. (Luka 6:38) Lililo la maana zaidi, wenye rehema wataonyeshwa rehema na Mungu. Juu ya hili, Yakobo anaandika hivi: “Maana hukumu haina huruma kwake yeye asiyeona huruma. Huruma hujitukuza juu ya hukumu.” (Yak. 2:13) Watakapoletwa hukumuni na Mungu, wenye huruma kweli kweli wataona kwamba rehema walioionyesha wengine itashinda hukumu yo yote ambayo Mungu angewaletea. (2 Tim. 1:16-18) Nafasi ya kupata msamaha wa dhambi na ya uzima wa milele ni ya watu wenye rehema peke yao. “Msipowasamehe watu makosa yao,” akasema Yesu, “wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu.”—Mt. 6:15; 18:35.